Mungu, Serikali, na Wewe
“Kanisa na Serikali Zakabiliana Katika Mahoji ya Watu Juu Ya Talaka Katika Ireland.”
KICHWA hicho kikuu katika The New York Times chaonyesha jinsi watu leo wawezavyo kukabiliwa na chaguo baina ya matakwa ya Serikali na mafundisho ya kanisa lao.
Makala hiyo ilisema hivi: “Huku kukibakia muda unaopungua mwezi mmoja kabla ya mahoji ya watu juu ya suala la kuondoa marufuku iliyowekwa na katiba juu ya talaka, Ireland yenye Wakatoliki wa Kiroma wengi sana inapata mgongano ulio nadra sana kati ya viongozi wa Serikali na wale wa kanisa.” Serikali ilipendekeza kuondolewa kwa marufuku juu ya talaka, huku Kanisa Katoliki likipinga vikali talaka na kufunga ndoa nyingine. Iliwapasa Wakatoliki wa Ireland wachague kati ya Kanisa na Serikali. Matokeo yakawa kwamba Serikali ilishinda kwa kiasi kidogo sana.
Jambo la kutazamisha zaidi ni kwamba kwa miaka mingi watu katika Ireland Kaskazini walikuwa wamekabiliwa na pambano kali juu ya utawala wa taifa. Wengi wameuawa. Wakatoliki wa Kiroma na Waprotestanti walikuwa wamekuwa na maoni yenye kutofautiana juu ya kujitiisha kwa Serikali ipi: kuendelezwa kwa utawala wa Uingereza katika Ireland Kaskazini au serikali kuu ya kutawala Ireland nzima.
Vivyo hivyo, katika ile iliyokuwa Yugoslavia, wenye mamlaka wametaka washiriki wa dini tofauti-tofauti, kutia ndani Wakatoliki na Waothodoksi, waende katika vita ya kung’ang’ania eneo. Kwa raia wa kawaida, wajibu wao wa kwanza ulikuwa upi? Je, walipaswa kufuata wale waliodai kuwakilisha Serikali, au walipaswa kumtii Mungu, asemaye: “Usiue . . . Mpende jirani yako kama nafsi yako”?—Warumi 13:9.
Waweza kufikiri kwamba hali ya aina hii haiwezi kukupata. Lakini inaweza. Hata inaweza kukuhusu sasa. Katika kitabu chake The State in the New Testament, mwanatheolojia Oscar Cullmann asema juu ya “maamuzi ya uhai au kifo ambayo Wakristo wa kisasa ni lazima wafanye au waweza kutakikana wafanye katika hali zenye hatari wanapotishwa na serikali za kimabavu.” Hata hivyo, yeye asema pia juu ya “daraka ambalo pia ni halisi na muhimu kwa kila Mkristo—pia Mkristo anayeishi chini ya zile hali ziitwazo ‘za kawaida,’ ‘za kila siku’—kukabiliana na kusuluhisha tatizo zito kwa sababu tu yeye ni Mkristo.”
Basi, je, uhusiano kati ya dini na Serikali upendeze Wakristo leo? Hakika wapaswa kuwapendeza. Tangu nyakati za mapema zaidi, Wakristo wamejaribu kusitawisha maoni yaliyosawazika juu ya mamlaka za kilimwengu. Kiongozi wao, Yesu Kristo, alijaribiwa, akahukumiwa, na kufishwa na Serikali ya Roma. Wanafunzi wake walipaswa kupatanisha wajibu wao wa Kikristo na madaraka yao kwa Milki ya Roma. Hivyo, pitio la uhusiano wao pamoja na mamlaka laandaa miongozo kwa Wakristo leo.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]
Tom Haley/Sipa Press