Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 6/1 kur. 4-7
  • Wakati Ambapo Ubaguzi Hautakuwapo Tena!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wakati Ambapo Ubaguzi Hautakuwapo Tena!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mungu Hana Upendeleo
  • Uvutano wa Biblia
  • Kuvunja Vizuizi vya Ubaguzi
  • Jinsi ya Kukabili Hali
  • “Hawatadhuru”
  • Ubaguzi Utakwisha Lini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • Ubaguzi Tatizo la Ulimwenguni Pote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • Je, Wewe ni Mhasiriwa wa Ubaguzi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Mwisho wa Ubaguzi
    Amkeni!—2004
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 6/1 kur. 4-7

Wakati Ambapo Ubaguzi Hautakuwapo Tena!

KULINGANA na ripoti moja, mwanasayansi Albert Einstein alisema wakati mmoja kwamba katika ulimwengu huu wenye huzuni, ni vigumu zaidi kushinda ubaguzi kuliko kupasua atomu. Vivyo hivyo, Edward R. Murrow, mwandishi wa habari aliyejulikana sana wakati wa Vita ya Ulimwengu 2 na aliyekuwa baadaye mkurugenzi wa Shirika la Kutoa Habari la Serikali ya Marekani, alisema kwamba “hakuna mtu awezaye kuondoa ubaguzi—wao wanaweza kuutambua tu.”

Je, taarifa hizi zaonekana kuwa kweli? Je, haiwezekani kuondoa upendeleo na ubaguzi wa jamii? Mungu huhisije juu ya ubaguzi?

Mungu Hana Upendeleo

Biblia hupinga upendeleo. (Mithali 24:23; 28:21) Hiyo hutaarifu kwamba “hekima itokayo juu, kwanza ni safi, tena ni ya amani, ya upole, tayari kusikiliza maneno ya watu, imejaa rehema na matunda mema, haina fitina [“isiyofanya tofauti zenye upendeleo,” New World Translation], haina unafiki.” (Yakobo 3:17) Hekima hiyo ilikaziwa kwa mahakimu katika Israeli ya kale. “Msitende yasiyo haki katika hukumu,” wao waliagizwa. “Usimpendelee mtu maskini, wala kumstahi mwenye nguvu; bali utamhukumu jirani yako kwa haki.”—Mambo ya Walawi 19:15.

Msimamo thabiti wa Biblia dhidi ya upendeleo na ubaguzi ulikaziwa na Yesu Kristo na mitume wake Petro na Paulo. Yesu hakuwa na upendeleo kuelekea wale waliokuwa “wamechoka na kutawanyika kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mathayo 9:36) Yeye alifundisha: “Msihukumu hukumu ya macho tu, bali ifanyeni hukumu iliyo ya haki.”—Yohana 7:24.

Petro na Paulo wanatuhakikishia kwamba Yehova Mungu mwenyewe hana upendeleo. Petro alitaarifu hivi: “Hakika natambua ya kuwa Mungu hana upendeleo; bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye.” (Matendo 10:34, 35) Mtume Paulo atuambia: “Kwa maana hakuna upendeleo kwa Mungu.”—Warumi 2:11.

Uvutano wa Biblia

Biblia ina uwezo wa kubadili nyutu za wale wanoongozwa nayo. Waebrania 4:12 husema: “Neno la Mungu li hai, tena lina nguvu.” Kwa msaada wa Yehova mtu mwenye ubaguzi aweza hata kubadili njia yake ya kufikiri na kuwa bila upendeleo katika shughuli zake pamoja na wengine.

Kwa kielelezo, chukua kisa cha Sauli wa Tarso. Kulingana na simulizi la Biblia wakati mmoja yeye alipinga kwa jeuri kutaniko la Kikristo kwa sababu alifuata mapokeo ya kidini yasiyonyumbulika. (Matendo 8:1-3) Yeye alikuwa amesadikishwa kabisa na mapokeo ya Kiyahudi kwamba Wakristo wote walikuwa waasi-imani na maadui wa ibada ya kweli. Ubaguzi wake ulimwongoza kuunga mkono mauaji ya Wakristo. Biblia husema kwamba alikuwa “akizidi kutisha na kuwaza kuwaua wanafunzi wa Bwana.” (Matendo 9:1) Alipokuwa akifanya hivyo aliwaza kwamba alikuwa akitoa utumishi mtakatifu kwa Mungu.—Linganisha Yohana 16:2.

Hata hivyo, Sauli wa Tarso aliweza kuondosha ubaguzi wake wa kupita kiasi. Yeye mwenyewe hata akawa Mkristo! Baadaye, akiwa Paulo, mtume wa Yesu Kristo, aliandika hivi: “Ingawa hapo kwanza nalikuwa mtukanaji, mwenye kuudhi watu, mwenye jeuri, lakini nalipata rehema kwa kuwa nalitenda hivyo kwa ujinga, na kwa kutokuwa na imani.”—1 Timotheo 1:13.

Si Paulo peke yake aliyefanya mabadiliko hayo makubwa katika njia yake ya kufikiri. Katika barua yake kwa Tito, mweneza evanjeli mwenzake, Paulo aliwaonya Wakristo “wasimtukane mtu ye yote [“wasiseme kwa ubaya juu ya yeyote,” NW], wasiwe wagomvi, wawe wema, wakionyesha upole wote kwa watu wote. Maana hapo zamani sisi nasi tulikuwa hatuna akili, tulikuwa waasi, tumedanganywa, huku tukitumikia tamaa na anasa za namna nyingi, tukiishi katika uovu na husuda, tukichukiza na kuchukiana.”—Tito 3:2, 3.

Kuvunja Vizuizi vya Ubaguzi

Leo, Wakristo wa kweli hujitahidi kufuata shauri hilo. Wanataka kuepuka kuhukumu watu kwa msingi wa maonyesho ya kijuu-juu. Mtazamo huo huwazuia “wasiseme kwa ubaya,” juu ya wengine. Wao hufurahia udugu wa kimataifa ambao huvuka mipaka yote ya kitaifa, kikabila, na kijamii ya ulimwengu huu.

Fikiria kisa cha Henrique, Mbrazili mweusi. Mwenyewe akiwa mhasiriwa wa ubaguzi wa kijamii, alisitawisha chuki ya kina kirefu dhidi ya watu weupe. Yeye aeleza: “Mashahidi wawili weupe walikuja nyumbani kwangu kuzungumza nami juu ya jina la Mungu. Mwanzoni sikutaka kusikiliza kwa sababu sikuwatumaini watu weupe. Lakini mara nikaona kwamba ujumbe wao ulionekana kuwa kweli. Nilikubali funzo la Biblia. Swali la kwanza nililokuwa nalo lilikuwa, ‘Je, kuna watu weusi wengi katika kanisa lenu?’ Wao walijibu, ‘Ndiyo.’ Kisha wakanionyesha picha ya mwisho katika kitabu Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia,a inayoonyesha vijana wa jamii mbalimbali. Miongoni mwao mlikuwa mvulana mweusi, hili lilinitia moyo. Baadaye nilizuru Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova, ambapo niliona watu wa jamii mbalimbali wakitendeana kwa staha. Hilo lilikuwa la maana sana kwangu.”

Sasa, akiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, Henrique anafurahi kuwa sehemu ya udugu wa kweli wa Kikristo. Yeye afahamu kwamba sifa haiendi kwa binadamu yeyote. Yeye asema: “Leo namshukuru Yehova na Yesu kwa kila kitu ambacho wamenifanyia. Nafanya kazi pamoja na mamilioni ya watumishi wa Yehova waaminifu-washikamanifu kutoka jamii zote, rangi, na malezi, wakiunganika kwa kusudi moja.”

Alipokuwa akikua, Dario alikuwa mhasiriwa mwingine wa ubaguzi. Alipokuwa na umri wa miaka 16, yeye alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Yeye alionelea hivi: “Miongoni mwa Mashahidi, nimepata kwamba hakuna hisia za kuwa wa jamii bora.” Yeye alivutiwa na mazingira ya upendo wa kweli. Aliona hasa kwamba watu wa jamii mbalimbali walitumikia katika vyeo vya madaraka kutanikoni. Wakati wowote anapopatwa na aina fulani ya ubaguzi au upendeleo na watu wa nje ya kutaniko, Dario hukumbuka kwamba Yehova hupenda watu wa mataifa, makabila, na lugha zote.

Jinsi ya Kukabili Hali

Sote hupenda kutendewa kwa heshima na staha. Ndiyo sababu kuwa mhasiriwa wa ubaguzi ni jaribu gumu sana kuvumilia. Kutaniko la Kikristo halitulindi kutokana na hatari za mitazamo yote ya ubaguzi ya ulimwengu huu mwovu. Mradi Shetani Ibilisi anaongoza mambo ya ulimwengu, kutakuwa na ukosefu wa haki. (1 Yohana 5:19) Ufunuo 12:12 hutuonya: “Ole wa nchi na bahari! kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.” Nia yake si kuvuruga starehe tu. Yeye alinganishwa na mnyama mwindaji. Mtume Petro atuambia: “Mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze.”—1 Petro 5:8.

Biblia hutuambia pia: “Basi mtiini Mungu. Mpingeni Shetani, naye atawakimbia.” (Yakobo 4:7) Msaada bora wa kupambana na ubaguzi ni kumtegemea Mungu kwa ajili ya ulinzi, kama alivyofanya Mfalme Daudi: “Ee Mungu wangu, uniopoe mkononi mwa mkorofi, katika mkono wake mwovu, mdhalimu.” (Zaburi 71:4) Hata twaweza kusali kama alivyosali mtunga-zaburi: “Mungu, unirehemu, maana yuko atakaye kunimeza, mchana kutwa amenionea akileta vita.”—Zaburi 56:1.

Mungu ataitikiaje sala kama hizo? Biblia hujibu: “Atamkomboa mhitaji aliapo, na mtu aliyeonewa iwapo hana msaidizi. Atamhurumia aliye dhaifu na maskini, na nafsi za wahitaji ataziokoa.” (Zaburi 72:12, 13) Ni vema kama nini kujua kwamba kwa wakati ufaao Yehova ataleta kitulizo kwa wote walio wahasiriwa wa ukosefu wa haki!

“Hawatadhuru”

Huenda serikali za ulimwengu huu zikaendelea kupambana na ubaguzi kupitia sheria na programu zazo. Huenda zikaendelea kuahidi usawa na haki. Lakini haziwezi kufaulu. (Zaburi 146:3) Ni Mungu tu awezaye na ndiye atakayeondoa matendo yote ya ubaguzi. Yeye atabadili wanadamu wote kuwa familia moja iliyounganika. “Mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha,” wataokoka mwisho wa mfumo huu mwovu na kufurahia kuishi katika amani.—Ufunuo 7:9, 10.

Yehova ataondoa madhara yoyote yaliyosababishwa na ubaguzi wa jamii na kijamii. Wazia, hakuna mtu atakayetendewa kwa ukosefu wa haki! “Wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu.” (Mika 4:4) Na Isaya 11:9 husema: “Hawatadhuru.”

Ikiwa wewe ni mhasiriwa wa ubaguzi sasa, tumaini hili zuri ajabu la wakati ujao litaimarisha uhusiano wako pamoja na Yehova. Litakusaidia kuvumilia ukosefu wa haki wa mfumo huu mwovu. Unapokabiliana na ubaguzi na kutazama mbele, fuata shauri lenye hekima la Biblia: “Iweni hodari, mpige moyo konde, ninyi nyote mnaomngoja BWANA.”—Zaburi 31:24.

[Maelezo ya Chini]

a Kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 4]

U.S. National Archives photo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki