Shule ya Gileadi Yatuma Darasa Layo la 100
SHULE ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower imetimiza fungu la maana katika upigaji-mbiu wa tufeni pote wa Ufalme wa Mungu katika nyakati za kisasa. Tangu Shule ya Gileadi ilipoanza kuzoeza wamishonari katika 1943, wahitimu wayo wametumikia katika nchi zaidi ya 200. Katika Machi 2, 1996, darasa la 100 lilihitimu.
Wanafunzi walikuwa wamehudhuria shule katika kipindi ambacho zaidi ya meta mbili za theluji zilikuwa zimeanguka katika hilo eneo la Kitovu cha Kielimu cha Watchtower katika Patterson, New York. Haishangazi kwamba theluji ilikuwa ikianguka siku ya kuhitimu. Hata hivyo, ukumbi ulikuwa umejaa, na wasikilizaji wenye kufurika walisikiliza wakiwa Patterson, Wallkill, na Brooklyn—kwa ujumla watu 2,878.
Theodore Jaracz, mshiriki wa Halmashauri ya Kufundisha ya Baraza Linaloongoza, alitumikia akiwa mwenyekiti. Baada ya kuwakaribisha kwa shauku wageni kutoka nchi nyingi waliokuwapo, aliwaalika wote kusimama na kuimba wimbo namba 52. Huo ukumbi ulinguruma na sifa kwa Yehova walipokuwa wakiimba “Jina la Baba Yetu,” kutoka kitabu Mwimbieni Yehova Sifa. Wimbo huo, pamoja na maelezo ya mwenyekiti juu ya kutumia elimu ili kumsifu Yehova, ulitayarisha watu kwa ajili ya programu ambayo ilifuata.
Shauri la Kimaandiko Kutoka kwa Wanaume Wazee
Sehemu ya kwanza ya programu ilifanyizwa kwa hotuba fupifupi zilizotolewa na watumishi wa Yehova wa muda mrefu kwa darasa lililokuwa likihitimu. Richard Abrahamson, mshiriki wa familia ya Betheli ya makao makuu, aliyeanza utumishi wake wa wakati wote katika 1940, alilisihi sana darasa: “Endeleeni Kurekebishwa Upya.” Aliwakumbusha kwamba tayari walikuwa wamejionea vipindi mbalimbali vya kurekebishwa upya maishani mwao wakiwa Wakristo, kutia ndani miezi mitano ya mazoezi katika Gileadi. Hivyo, ni kwa nini wao wapaswa kuendelea kurekebishwa upya?
Msemaji alieleza kwamba usemi uliotumiwa na Mtume Paulo kwenye 2 Wakorintho 13:11 (NW) “hudokeza hatua yenye kuendelea, ujitiisho wenye kuendelea kwa Yehova, mfanyizo na usafisho wa mtu, marekebisho madogo-madogo, ili mtu aweze kufikia viwango vya juu zaidi vya Yehova.” Katika migawo yao ya kigeni, darasa lenye kuhitimu litakabili magumu mapya katika imani yao. Watahitaji kujifunza lugha mpya, wabadilikane ili kufaana na utamaduni tofauti na hali za kuishi zilizo tofauti, na kubadilikana kulingana na aina mbalimbali za eneo. Pia watakuwa wakishughulika na nyutu tofauti-tofauti katika makao ya wamishonari na katika makutaniko yao mapya. Ikiwa watatumia kwa uangalifu kanuni za Biblia katika hali zote hizo, wakiwa tayari kurekebishwa upya, basi, kama alivyoandika mtume Paulo, wataweza pia ‘kuendelea kushangilia.’
John Barr, mmojawapo wa wale washiriki watano wa Baraza Linaloongoza walioshiriki katika hiyo programu, alichukua kichwa cha hotuba yake kutoka 1 Wakorintho 4:9. Aliwakumbusha wasikilizaji wake kwamba Wakristo ni tamasha kwa malaika na kwa wanadamu. “Kujua hilo,” akasema, “huongezea sana umuhimu wa mwendo wa maisha wa Mkristo, hasa atambuapo kwamba kupitia asemayo na afanyayo, aweza kuwa na matokeo yenye kuonekana si na watazamaji wa kibinadamu tu bali pia na malaika. Naamini kwamba kukumbuka hilo mwendapo kwenye miisho ya dunia kutakuwa na matokeo mazuri sana kwenu ninyi nyote ndugu na dada wapendwa wa darasa la 100 la Gileadi.”
Ndugu Barr aliwasihi sana wale wanafunzi 48 wakumbuke kwamba, wasaidiapo wenye mfano wa kondoo kujifunza kweli, “kuna furaha mbele ya malaika wa Mungu kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja atubuye.” (Luka 15:10) Akirejezea 1 Wakorintho 11:10, alionyesha kwamba mtazamo wa mtu kuelekea mipango ya kitheokrasi huathiri si ndugu na dada zetu tu tuwaonao bali pia malaika tusiowaona. Jinsi ifaidivyo kuwa na maoni haya mazuri akilini!
Mshiriki mwingine wa Baraza Linaloongoza, Gerrit Lösch, yeye mwenyewe akiwa mhitimu wa Shule ya Gileadi, alizungumzia maandiko kama vile Zaburi 125:1, 2; Zekaria 2:4, 5; na Zaburi 71:21 (NW) ili kuonyesha kwamba Yehova ‘huwazunguka watu wake.’ Yeye huwaandalia ulinzi kila upande. Je, Mungu ataandaa ulinzi kama huo wakati wa dhiki kubwa tu? “La,” akajibu msemaji, “kwa kuwa tayari Yehova ni ‘ukuta wa moto,’ ulinzi kwa watu wake. Mwaka uliofuata vita wa 1919 uliyapata mabaki ya Israeli la kiroho yakisubiri kwa hamu kuhubiri habari njema za Ufalme ulimwenguni pote kuwa ushuhuda kwa mataifa yote. Wao walikuwa wawakilishi wa Yerusalemu la mfano katika mbingu. Yehova huhakikisha ulinzi wa kimungu kwa hao wawakilishi wakiwa kikundi wakati wa mwisho. Basi ni nani awezaye kuwazuia kwa kufanikiwa? Hakuna.” Jinsi iwapavyo uhakikisho wao na wale ambao hushirikiana nao kwa ukaribu katika kufanya mapenzi ya kimungu!
Ulysses Glass, mwalimu wa muda mrefu wa hiyo shule, alilitia moyo hilo darasa ‘limalizie kujichongea kishubaka katika tengenezo la ulimwenguni pote la Yehova.’ Kishubaka hicho ni hali au utendaji ufaao kipekee uwezo mbalimbali wa mtu au utu wake. “Ninyi mtakaokuwa wamishonari mmepata kishubaka chenu katika tengenezo la ulimwenguni pote la Mashahidi wa Yehova,” akatangaza. “Lakini, ingawa ni chenye thamani sasa, huu ndio mwanzo tu wa maisha yenu mkiwa wamishonari.” Watahitaji kujitoa kwa bidii kutumia uwezo wao mbalimbali na kufaana na migawo ya pekee ambayo wamepata kutoka kwa Yehova na tengenezo lake.
Hotuba ya mwisho katika sehemu hiyo ya programu ilitolewa na Wallace Liverance, mwalimu wa Gileadi aliyetumikia kwa miaka 17 katika Bolivia. “Je, mtamjaribu Mungu?” aliliuliza darasa lote la wanafunzi. Wao wapaswa kufanyaje hivyo? Taifa la Israeli lilimjaribu Mungu katika njia isiyofaa. (Kumbukumbu la Torati 6:16) “Ni wazi kwamba ni kosa kumjaribu Mungu kwa kulalamika au kunung’unika au labda kwa kuonyesha ukosefu wa imani katika njia yake ya kushughulikia mambo,” akasema msemaji. “Mfikapo katika mgawo wenu mpya, kinzeni mwelekeo huo,” akasihi sana. Basi, ni njia ipi iliyo sawa ya kumjaribu Mungu? “Ni kwa kuamini asemayo, kwa kufanya yale tu asemayo, kisha kuacha matokeo mikononi mwake,” Ndugu Liverance akaeleza. Kama ionwavyo kwenye Malaki 3:10, Yehova huwaalika watu wake: “Mkanijaribu.” Aliahidi kwamba ikiwa wangeleta sehemu yao ya kumi kwa uaminifu katika ghala la hekalu, angewabariki. “Mbona usiuone mgawo wako wa umishonari kwa njia iyo hiyo?” msemaji akauliza. “Yehova hutaka ufanikiwe katika huo, kwa hiyo mjaribu. Baki katika mgawo wako. Fanya marekebisho atakayo uyafanye. Vumilia. Uone ikiwa hatakubariki.” Ni shauri zuri kama nini kwa wote wamtumikiao Yehova!
Baada ya wimbo programu ilibadilika kutoka hotuba na kuwa mfululizo wa mahoji yenye kupendeza.
Maelezo Yenye Kutumika Kutoka Shambani
Mark Noumair, mwalimu mpya wa Gileadi, aliwaalika wanafunzi waeleze mambo yaliyoonwa waliyokuwa wamepata shambani huku wakihudhuria hiyo shule. Hayo yalionyesha wazi umuhimu wa ujianzilishi katika huduma na yaliwapa wasikilizaji mawazo yenye kutumika ambayo wangeweza kutumia.
Wakati wa muhula wao wa shule, wanafunzi katika darasa hilo la Gileadi walifaidika hasa kwa kushirikiana na washiriki wa Halmashauri ya Tawi kutoka nchi 42, ambao pia walikuwa kwenye Kitovu cha Kielimu cha Patterson kwa ajili ya mazoezi ya pekee. Wengi wao walikuwa wamehitimu shule ya Gileadi miaka mingi mapema. Kwenye programu, mahoji yalifanywa pamoja na wawakilishi kutoka madarasa ya 3, 5, 51, na 92, pamoja na wale waliotoka Tanzu la Shule ya Gileadi katika Ujerumani. Jinsi maelezo yao yalivyokuwa na faida!
Walieleza jinsi wamishonari wamehisi waonapo idadi za wasifaji wa Yehova ikiongezeka katika migawo yao kutoka idadi ndogo kufikia makumi ya maelfu. Walieleza juu ya fungu lao katika kupeleka habari njema hadi makao yaliyotapakaa katika Milima Andes na vijiji katika vyanzo vya Mto Amazon. Walizungumza juu ya kutolea ushahidi watu wasiojua kusoma na kuandika. Walieleza juu ya kujitahidi kwao wenyewe kujifunza lugha mpya na yale ambayo wahitimu wapaswa kutarajia kihalisi kuhusu ni upesi kadiri gani wataweza kutoa ushahidi na hotuba katika lugha kama vile Kichina. Hata walionyesha utoaji wa mfano katika Kihispania na Kichina. Walikazia kwamba wamishonari huwa na matokea zaidi wajifunzapo si lugha tu bali pia kufikiri kwa watu. Walieleza juu ya hali za kuishi ambazo mara nyingi huwa ngumu katika nchi maskini na kusema: “Wamishonari wapaswa kutambua kwamba hali hiyo mara nyingi huwa ni kwa sababu watu wametumiwa vibaya. Mishonari hufanya vema ahisipo kama Yesu alivyohisi—aliwahurumia watu, waliokuwa kama kondoo wasio na mchungaji.”
Baada ya wimbo programu iliendelea na hotuba ya A. D. Schroeder, mshiriki wa Baraza Linaloongoza. Alikuwa na pendeleo la kuwa mmoja wa wafunzi wa awali kwenye Shule ya Gileadi ilipoanzishwa katika 1943. Ukiwa mwisho ufaao wa programu, alizungumzia habari yenye kichwa “Kumsifu Yehova Akiwa Bwana Mwenye Enzi Kuu.” Mazungumzo ya Ndugu Schroeder ya Zaburi ya 24 yenye kuvutia yaliwakumbusha wote waliokuwapo jinsi lilivyo tukufu pendeleo la kumsifu Yehova akiwa Bwana Mwenye Enzi Kuu.
Baada ya diploma kutolewa, na wimbo wa mwisho, Karl Klein wa Baraza Linaloongoza alimalizia kwa sala yenye kuhisiwa moyoni. Ilikuwa programu yenye kutumika na yenye kuburudisha kiroho jinsi gani!
Katika siku za baada ya kuhitimu, wale washiriki 48 wa darasa la 100 wakaanza kuondoka na kwenda kwenye migawo ya mishonari katika nchi 17. Lakini hawakuwa wakianza tu huduma yao. Tayari walikuwa na rekodi ndefu ya huduma ya Kikristo ya wakati wote. Waliposajiliwa katika Gileadi, kwa wastani, walikuwa na umri wa miaka 33 na walikuwa wametumia zaidi ya miaka 12 katika huduma ya wakati wote. Baadhi yao walikuwa wale ambao wamekuwa washiriki wa familia ya Betheli ya tufeni pote ya Watch Tower Society. Wengine walikuwa wametumikia wakiwa waangalizi wasafirio. Wanafunzi kadhaa tayari walikuwa wameshiriki katika aina moja au nyingine ya utumishi wa kigeni—katika Afrika, Ulaya, Amerika Kusini, visiwa vya baharini, na kati ya vikundi vyenye kuzungumza lugha za kigeni katika nchi zao. Lakini sasa wanajiunga na wamishonari wengine ambao wamefurahi kuweza kusema, ‘Tutatumikia kokote ulimwenguni ambako twahitajiwa.’ Tamaa yao ya moyoni ni kutumia maisha yao kumtukuza Yehova.
[Sanduku katika ukurasa wa 27]
Takwimu za Darasa:
Idadi ya nchi zilizowakilishwa: 8
Idadi ya nchi walikogawiwa: 17
Idadi ya wanafunzi: 48
Wastani wa umri: 33.75
Wastani wa miaka katika kweli: 17.31
Wastani wa miaka katika huduma ya wakati wote: 12.06
[Picha katika ukurasa wa 26]
Darasa la 100 Lililohitimu la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower
Katika orodha iliyo chini, safu zimepewa nambari kutoka mbele kuelekea nyuma, na majina yameorodheshwa kuanzia kushoto kuelekea kulia katika kila safu.
(1) Shirley, M.; Grundström, M.; Genardini, D.; Giaimo, J.; Shood, W.; Phair, P.; Buchanan, C.; Robinson, D. (2) Pine, C.; Kraus, B.; Racicot, T.; Hansen, A.; Beets, T.; Berg, J.; Garcia, N.; Fleming, K. (3) Whinery, L.; Whinery, L.; Harps, C.; Giaimo, C.; Berg, T.; Mann, C.; Berrios, V.; Pfeifer, C. (4) Randall, L.; Genardini, S.; Kraus, H.; Fleming, R.; D’Abadie, S.; Shirley, T.; Stevenson, G.; Buchanan, B. (5) Robinson, T.; Garcia, J.; Harps, P.; Racicot, D.; D’Abadie, F.; Phair, M.; Stevenson, G.; Shood, D. (6) Beets, L.; Pfeifer, A.; Berrios, M.; Pine, J.; Mann, L.; Randall, P.; Grundström, J.; Hansen, G.