Michael Faraday—Mwanasayansi na Mtu wa Imani
“Baba wa Umeme.” “Mwanasayansi mwenye kufanya majaribio aliye mkubwa kupita wote waliopata kuishi.” Hayo ni mafafanuzi mawili ya Michael Faraday, aliyezaliwa Uingereza katika 1791, ambaye uvumbuzi wake wa mdukizo wa sumakuumeme uliongoza kwenye usitawi wa mota zitumiazo umeme na ufanyizaji wa nguvu.
FARADAY alihadhiri sana juu ya kemia na fizikia kwenye Royal Institution katika London. Mihadhara yake iliyokusudiwa kufanya sayansi ipendwe na watu wengi ilisaidia vijana wengi waelewe dhana zenye utata. Alipokea tuzo kadhaa kutoka vyuo vikuu vingi. Hata hivyo aliepuka kujulikana sana. Alikuwa mtu wa kidini sana, akiwa mwenye furaha zaidi katika faragha ya nyumba yake yenye vyumba vitatu na akiwa pamoja na familia yake na waamini wenzake. Faraday alikuwa wa lile alilofafanua kuwa “farakano la Wakristo lililo dogo sana na lenye kuchukiwa, linaloitwa . . . Sandemanians [Wasandemani].” Walikuwa nani? Waliamini nini? Na mafundisho yao yalimwathirije Faraday?
Wasandemani
“Uhusiano wa kwanza kati ya familia ya Faraday na kanisa la Sandeman ulithibitishwa na babu na nyanya wa Michael Faraday,” asema Geoffrey Cantor, mtungaji wa kitabu Michael Faraday: Sandemanian and Scientist. Wao walishirikiana na wafuasi wa mhudumu fulani mwenye kusafiri asiyefuata kanisa hususa ambaye washiriki wake walifuata itikadi za Wasandemani.
Robert Sandeman (1718-1771) alikuwa mwanafunzi wa chuo kikuu katika Edinburgh, akijifunza hisabati, Kigiriki, na lugha nyinginezo wakati ambapo siku moja alimsikiliza John Glass, aliyekuwa mhudumu wa Kanisa Presbiteri hapo awali, akihubiri. Yale aliyosikia yalimfanya akomeshe masomo ya chuo kikuu, akarudi nyumbani Perth, na kujiunga na Glass pamoja na washiriki wake.
Katika miaka ya 1720, John Glass alikuwa ameanza kutilia shaka mafundisho fulani ya Kanisa la Scotland. Kujifunza kwake Neno la Mungu kulimwongoza akate maneno kwamba taifa la Kibiblia la Israeli lilifananisha taifa la kiroho ambalo raia walo walitoka mataifa mengi. Hakupata popote sababu ya kuwako kwa kanisa tofauti katika kila taifa.
Kwa sababu alikuwa na shaka katika kanisa lake huko Tealing, karibu na Dundee, Scotland, Glass alitoka katika Kanisa la Scotland akapanga mikutano yake mwenyewe. Watu wapatao mia moja walijiunga naye, na tangu mwanzo, walihisi uhitaji wa kudumisha muungano miongoni mwao. Waliamua kufuata maagizo ya Kristo, yaliyorekodiwa kwenye Mathayo sura ya 18, mistari ya 15 hadi 17, ili kusuluhisha mahitilafiano yoyote ambayo huenda wakawa nayo. Baadaye walifanya mikutano ya kila juma ambayo katika hiyo watu wa imani iyo hiyo walikusanyika kwa ajili ya sala na himizo.
Wakati watu wengi vya kutosha walipoanza kuhudhuria kwa kawaida mikutano ya vikundi tofautitofauti, watu wenye kuchukua madaraka walihitajiwa ili kusimamia ibada yao. Lakini ni nani waliokuwa wenye kustahili? John Glass na washiriki wake walikazia fikira hasa yale yaliyoandikwa na mtume Paulo juu ya habari hii. (1 Timotheo 3:1-7; Tito 1:5-9) Wao hawakupata popote mtajo wa elimu ya chuo kikuu wala uhitaji wa kuelewa Kiebrania na Kigiriki. Kwa hiyo baada ya kuifikiria miongozo ya Kimaandiko kwa sala, waliweka rasmi wanaume wenye kustahili kuwa wazee. Wale waliokuwa waaminifu-washikamanifu kwa Kanisa la Scotland waliona “ni kama kukufuru” kwa wanaume wasio na elimu “waliolelewa katika hali za chini” kujifanya kwamba wanaelewa Biblia na kuhubiri ujumbe wayo. Katika 1733, wakati ambapo Glass na waamini wenzake walipojenga jumba lao wenyewe la kukutania katika mji wa Perth, makasisi wa mahali hapo walijaribu kuwasonga mahakimu ili wawaondoshe mjini. Wao hawakufaulu, na harakati hiyo ikaongezeka.
Robert Sandeman alimwoa binti mkubwa wa Glass na, alipofikia umri wa miaka 26, akawa mzee katika kutaniko la Perth la Waglassi. Yeye alilemewa sana na wajibu wake mbalimbali akiwa mzee hivi kwamba aliamua kutoa wakati wake wote ili kufanya kazi ya uchungaji. Baadaye, baada ya mke wake kufa, Robert “alikubali kwa uchangamfu kumtumikia Bwana popote pale alipohitajiwa,” wasema muhtasari fulani wa maisha yake.
Usandemani Waenea
Sandeman alipanua huduma yake kwa bidii kutoka Scotland hadi kuingia Uingereza, ambako vikundi vipya vya waamini wenzake viliongezeka. Wakati huo, kulikuwa na ubishi mwingi miongoni mwa Wakalvini Waingereza. Baadhi yao waliamini kwamba wokovu wao ulikuwa umeamuliwa kimbele. Kwa upande mwingine, Sandeman aliwaunga mkono wale walioamini kwamba imani ilikuwa takwa la lazima. Ili kuunga mkono maoni hayo, alitangaza kitabu kilichochapwa upya mara nne na kilichotokea pia katika chapa mbili za Kimarekani. Kulingana na Geoffrey Cantor, kutangazwa kwa buku hilo kulikuwa “ndiko jambo moja la maana zaidi lililolipanua hilo farakano [la Sandemani] kutoka vyanzo vyalo vidogo sana katika Scotland.”
Katika 1764, Sandeman, akiwa ameandamana na wazee wengine Waglassi, walisafiri kwenda Marekani, ziara iliyochochea ubishi na upinzani mwingi. Hata hivyo, matokeo yayo yalikuwa kuanzishwa kwa kikundi cha Wakristo wenye maoni yaleyale katika Danbury, Connecticut.a Sandeman alikufa huko 1771.
Itikadi za Kidini za Faraday
Michael mchanga aliyashika kabisa mafundisho ya Wasandemani ya wazazi wake. Alijifunza kwamba Wasandemani walijitenga wenyewe na wale ambao hawakuzoea yale yaliyofundishwa na Biblia. Kwa kielelezo, walikataa kushiriki katika sherehe ya ndoa ya Kianglikana, wakipendelea kufunga ndoa yao kwa njia ya kisheria tu.
Ujitiisho kwa serikali, na bado kutokuwamo katika siasa, ni jambo lililowatambulisha Wasandemani. Ingawa walikuwa washiriki wenye kustahiwa katika jumuiya, mara nyingi wao hawakukubali nyadhifa za kiserikali. Hata hivyo katika vile visa vichache walipokubali, waliepuka siasa za vyama. Kudumisha msimamo huo kuliwaletea suto. (Linganisha Yohana 17:14.) Wasandemani waliamini kwamba Ufalme wa kimbingu wa Mungu ndio mpango mkamilifu wa serikali. Waliona siasa kuwa “hila chafu, isiyo na maana na maadili yoyote,” asema Cantor.
Ingawa walijitenga na wengine, hawakuwa na mitazamo ya Kifarisayo. Walitangaza hivi: “Twaamua kwamba ni lazima kabisa kuepuka Roho na Zoea la Mafarisayo wa kale, kwa hiyo tutaepuka kuyaita [mambo mengi zaidi kuwa] Dhambi na Wajibu kuliko yale ambayo Andiko limeita; na tutaepuka kubatilisha Mawazo ya kimungu kwa Mapokeo ya kibinadamu au Kuepuka mambo kwa kuyachanganua.”
Walikubali kufuata zoea la Kimaandiko la kutenga na ushirika mshiriki yeyote aliyekuwa mlevi, mnyang’anyi, mwasherati, au aliyezoea dhambi nyinginezo nzito. Ikiwa mtenda-dhambi alitubu kikweli, walijaribu kumrudisha. Ama sivyo, walifuata agizo la Kimaandiko la ‘kumwondoa yule mbaya.’—1 Wakorintho 5:5, 11, 13.
Wasandemani walitii amri ya Kibiblia ya kuepukana na damu. (Matendo 15:29) John Glass alikuwa amebisha kwamba watu wa Mungu walikuwa na wajibu wa kutii kile kizuizi juu ya damu sawa na vile Mungu alivyokuwa amewaamuru wale wanadamu wa kwanza waepuke kula tunda la mti wa ujuzi wa mema na mabaya. (Mwanzo 2:16, 17) Kutotii ile amri kuhusu damu kulikuwa sawa na kukataa matumizi yafaayo ya damu ya Kristo, yaani ufuniko wa dhambi. Glass alikata maneno hivi: “Sikuzote katazo hili la kula damu lilikuwa lenye maana kubwa sana, na lingali hivyo.”
Kufikiria Maandiko kwa Wasandemani kuliwasaidia waepuke mitego mingi. Kwa kielelezo, kuhusiana na vitumbuizo, wao waliyaona maagizo ya Kristo kuwa miongozo. “Tusithubutu kufanya Sheria ambapo Kristo hakufanya zozote,” wao wakasema, “wala kutupilia mbali zozote ambazo ametupa sisi. Kwa hiyo, kwa kuwa hatuwezi kupata mahali ambapo Tafrija, ya hadharani au ya faraghani, imekatazwa; twaona Tafrija yoyote kuwa halali, maadamu haihusiani na Hali ambazo kwa kweli ni zenye dhambi.”
Ingawa kwa njia hiyo Wasandemani walikuwa na maoni mengi yaliyotegemea Andiko kwa usahihi, wao hawakuelewa umaana wa ule utendaji wenyewe ambao huwatambulisha Wakristo wa kweli leo, yaani, kwamba kila mmoja apaswa kuhubiri kwa wengine habari njema ya Ufalme. (Mathayo 24:14) Hata hivyo, watu wote waliweza kuihudhuria mikutano yao, na huko walijitahidi kuwapa wote waliowaomba sababu ya tumaini lao.—1 Petro 3:15.
Kigezo hicho cha itikadi kilimwathirije mwanasayansi Michael Faraday?
Faraday Msandemani
Michael Faraday mwenye kuheshimiwa, aliyestahiwa sana kwa msherehekeo, ambaye alisifiwa sana kwa sababu ya uvumbuzi wake mbalimbali wenye kutokeza, aliishi maisha sahili. Watu maarufu walipokufa na wale wenye umashuhuri walitazamiwa kuhudhuria maziko yao, Faraday mashuhuri hakuwapo, akiwa haruhusiwi na dhamiri yake kuhusika katika ibada ya Kanisa la Uingereza.
Akiwa mwanasayansi Faraday alishikamana sana na yale aliyoweza kuonyesha kuwa mambo ya hakika. Kwa njia hiyo aliepuka ushirikiano wa karibu pamoja na watu wenye elimu walioendeleza udhani wao wenyewe na waliounga mkono pande mbalimbali za masuala. Kama alivyowaambia wasikilizaji fulani wakati mmoja, ‘jambo la msingi lililo la hakika huthibitika kuwa kweli sikuzote.’ Alionyesha sayansi kuwa yenye kutegemea ‘mambo ya hakika yaliyochunguzwa kwa uangalifu.’ Alipokuwa akitoa umalizio wa wonyesho mmoja juu ya kani za msingi za asili, Faraday aliwatia moyo wasikilizaji wake watafakari juu ya “Yeye aliyekuwa ameziumba.” Kisha akamnukuu mtume Mkristo Paulo: “Mambo yake yasiyoonekana tangu kuumbwa ulimwengu yanaonekana, na kufahamika kwa kazi zake; yaani, uweza wake wa milele na Uungu wake.”—Warumi 1:20.
Jambo lililomfanya Faraday awe tofauti sana na wanasayansi wengine wengi lilikuwa tamaa yake ya kujifunza kutokana na Kitabu cha Mungu kilichopuliziwa na pia kujifunza kutokana na uumbaji. “Kupitia dini yake ya Usandemani yeye alivumbua njia ya kuishi kwa kutii sheria ya adili ya Mungu na akiwa na ahadi ya uhai wa milele,” aonelea Cantor. “Kupitia sayansi yake alishughulika kwa ukaribu na sheria za maumbile ambazo Mungu alikuwa ameamua ziongoze ulimwengu wote mzima.” Faraday aliamini kwamba “mamlaka kamili ya Biblia isingeweza kudhoofishwa na sayansi, lakini ikiwa sayansi inazoewa katika njia ambayo ni ya Kikristo kikweli, yaweza kufafanua kile kitabu kingine cha Mungu [yaani, uumbaji].”
Faraday alikataa kwa unyenyekevu heshima nyingi ambazo wengine walitaka kumpa. Alionyesha daima kutopendezwa kwake na kupewa cheo cha ubwana mashuhuri. Alitaka kuendelea kuitwa ‘Bwana Michael Faraday wa kawaida.’ Alitumia wakati mwingi ili kufanya utendaji wake mbalimbali akiwa mzee, kutia na kusafiri kwa kawaida kutoka jiji kuu hadi kijiji cha Norfolk ili kutunza kikundi kidogo cha waamini wenye maoni yaleyale waliokuwa wakiishi huko.
Michael Faraday alikufa Agosti 25, 1867, akazikwa katika kaburi huko Highgate London kaskazini. Mtungaji wa kitabu chenye usimulizi wa maisha yake, John Thomas atuambia kwamba Faraday “aliachia vizazi vya wakati ujao kusanyiko kubwa la kazi halisi za kisayansi kuliko mwanasayansi mwingine yeyote wa maumbile, na matokeo yenye kutumika ya uvumbuzi wake yamekuwa na uvutano mkubwa sana juu ya hali ya maisha yenye ustaarabu.” Sara, mjane wa Faraday, aliandika hivi: “Naweza kuelekezea tu Agano Jipya kuwa mwongozo na kanuni yake; kwani aliliona kuwa Neno la Mungu . . . lililopaswa kufuatwa na Wakristo wa siku ya kisasa sawasawa na vile lilivyofuatwa lilipoandikwa”—huo ni ushuhuda wenye ufasaha kuhusu mwanasayansi mashuhuri aliyeishi kwa kujitoa kulingana na imani yake.
[Maelezo ya Chini]
a Kikundi cha mwisho kusalia cha Wasandemani, au Waglassi katika Marekani kilikoma kuwako yapata mapema katika karne hii.
[Sanduku katika ukurasa wa 29]
Alipowekwa kuwa mhadhiri kwenye Royal Institution ya Uingereza, Michael Faraday alikusudia kufanya sayansi ipendwe na watu wengi katika njia ambayo hata vijana wangeweza kuelewa. Shauri lake kwa wahadhiri wenzake lina madokezo yenye kutumika ambayo Wakristo wa kisasa wanaofundisha hadharani wanahitaji kufikiria.
◻ “Usemi haupaswi uwe wa upesi na wa haraka, na hivyo usieleweke, bali wapaswa uwe wa polepole na wa utaratibu.”
◻ Msemaji apaswa ajitahidi kuamsha kupendezwa kwa wasikilizaji wake “mwanzoni mwa mhadhara na kwa mfululizo wa hatua ndogo-ndogo zisizodhahiri kwa wasikilizaji, adumishe hali hiyo maadamu habari yahitaji hiyo.”
◻ “Mhadhiri hujishusha adhama sana anapogeuza usemi wake ili apate kupigiwa makofi na anapoomba pongezi.”
◻ Juu ya matumizi ya muhtasari: “Sikuzote mimi huona ni lazima . . . niandike mpango wa [habari] kwenye karatasi na kujazia sehemu-sehemu kwa kuzikumbuka, ama kwa njia ya kulinganisha mambo mbalimbali au vingine. . . . Ninakuwa na mfululizo wa vichwa vikubwa na vidogo vilivyopangwa kwa utaratibu, nami huvitumia kujua ni mambo gani nitakayozungumzia.”
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 26]
Picha zote mbili: Kwa hisani ya Royal Institution