Kurudi Mavumbini—Jinsi Gani?
“UMAVUMBI wewe, nawe mavumbini utarudi.” Mtu wa kwanza, Adamu, aliposikia maneno hayo, alijua jambo la kutazamia. Alikuwa amefanyizwa kwa mavumbi ya ardhi na angerudi kwenye mavumbi tu. Angekufa kwa sababu alikuwa amekosa kumtii Muumba wake, Yehova Mungu.—Mwanzo 2:7, 15-17; 3:17-19.
Biblia huonyesha kwamba wanadamu wote wamefanyizwa kwa mavumbi. Hiyo pia husema hivi: “Roho [“nafsi,” NW] ile itendayo dhambi itakufa.” (Ezekieli 18:4; Zaburi 103:14) Kifo kimeletea mamilioni ya watu huzuni nacho mara kwa mara kimezusha maswali juu ya jinsi ya kuondolea mbali maiti.
Mazoea ya Wakati Uliopita na ya Sasa
Maiti ziliondolewaje mbali miongoni mwa watu wa Mungu wa nyakati za kale? Katika kurasa zayo za mapema, Biblia inataja njia tofauti-tofauti za kushughulikia maiti, kutia na kuzika ardhini. (Mwanzo 35:8) Mzee wa ukoo, Abrahamu, na mkeye, Sara, na pia mwana wao Isaka na mjukuu wao Yakobo walizikwa katika pango la Makpela. (Mwanzo 23:2, 19; 25:9; 49:30, 31; 50:13) Waamuzi Waisraeli Gideoni na Samsoni walizikwa ‘katika viwanja vya kuzikia vya baba zao.’ (Waamuzi 8:32; 16:31) Hilo ladokeza kwamba kuwa na viwanja vya kuzikia vya familia kulipendelewa miongoni mwa watu wa Mungu wa kale. Yesu Kristo alipokufa katika karne ya kwanza W.K., mwili wake uliwekwa katika kaburi jipya lililokuwa limechongwa mwambani. (Mathayo 27:57-60) Kwa ujumla, basi, maiti zilizikwa ardhini au zikawekwa makaburini. Hilo lingali zoea katika sehemu zilizo nyingi duniani pote.
Hata hivyo, katika sehemu fulani-fulani ulimwenguni leo, ukosefu mkubwa wa nafasi na gharama ya juu ya ardhi inafanya izidi kuwa vigumu kupata mahali pa kuzikia. Kwa hiyo, watu fulani wanafikiria njia nyinginezo za kuondolea mbali maiti.
Kutapanya majivu baada ya kuteketeza maiti kunakuwa jambo la kawaida zaidi. Huko Uingereza yapata asilimia 40 ya maiti zinashughulikiwa kwa njia hiyo. Katika Sweden, ambapo zaidi ya asilimia 80 ya waliokufa katika maeneo ya mijini huteketezwa, misitu fulani imechaguliwa kwa ajili ya kutapanywa kwa majivu. Na katika Shanghai na miji mingineyo michache ya pwani ya China, serikali za majiji hudhamini kutapanya kwingi mbalimbali baharini mara kadhaa kwa mwaka.
Majivu yaweza kutapanywa wapi? Si popote tu. Wengine huenda wakahofu kuwa kutapanya majivu kwaweza kudhuru mazingira. Kwa kweli, hatari yoyote iwezekanayo ya kuambukizwa kwa watu wengi huzuiwa na kule kuteketezwa kwa maiti. Makaburi fulani Uingereza na bustani za ukumbusho huko Marekani hutenga maeneo yenye nyasi au bustani za maua ziwe mahali pa kutapanya majivu. Bila shaka, Wakristo huhangaikia hasa maoni ya Kimaandiko juu ya kuteketeza maiti na kutapanywa kwa majivu.
Maoni ya Kimaandiko Ni Nini?
Katika hukumu dhidi ya “mfalme wa Babeli,” nabii Isaya alisema hivi: “Umetupwa mbali na kaburi lako.” (Isaya 14:4, 19) Je, kutapanywa kwa majivu kulinganishwe na kisa hicho cha kufedheheshwa? La, kwa kuwa hakuna rejezo lolote la kuteketeza maiti na kuhifadhi au kutapanya majivu yaliyotokea.
Yesu Kristo alisema juu ya ufufuo wa kidunia wa wafu utakaotokea wakati wa Utawala wake wa Mileani aliposema hivi: “Watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti [yangu]. Nao watatoka.” (Yohana 5:28, 29) Hata hivyo, jambo la kwamba kaburi hususa halihitajiwi ili kufufua mtu laonekana katika ufafanuzi mwingine wa kiunabii wa ufufuo. Ufunuo 20:13 lataarifu hivi: “Bahari ikawatoa wafu waliokuwamo ndani yake; na Mauti na kuzimu zikawatoa wafu waliokuwamo ndani yake.” Kwa hiyo jambo la maana si mahali au jinsi ambavyo mtu ‘hurudi mavumbini.’ Badala ya hivyo, ni kama anakumbukwa na Mungu na anafufuliwa. (Ayubu 14:13-15; linganisha Luka 23:42, 43.) Bila shaka Yehova hahitaji maziara yenye kupendeza ili yamsaidie kukumbuka watu. Kuteketeza maiti hakuzuii kufufuliwa kwa mtu. Na ikiwa kutapanywa kwa majivu kunafanywa kukiwa na kusudio lifaalo na bila sherehe za kidini zisizo za kweli, huko hakungepingana na Maandiko.
Wanaoamua kwa kupendelea kutapanywa kwa majivu watahitaji kukazia uangalifu sheria za nchi. Ingefaa pia wafikirie hisia za waliofiwa na wengineo. Watumishi wa Yehova watafanya vema kuwa waangalifu kwamba kutumia uhuru wao wa Kimaandiko katika jambo hili hakuletei suto jina zuri walilo nalo Wakristo. Hilo ni la maana hasa katika nchi ambapo kuteketeza maiti na kutapanywa kwa majivu kunakubaliwa kisheria lakini bado hakujakubaliwa kabisa katika jamii. Bila shaka, Mkristo ataepuka sherehe zozote za ibada au desturi zenye msingi katika itikadi ya kutokufa kwa nafsi ya kibinadamu.
Uhuru Kamili Kutoka Katika Makaburi!
Watu fulani wanaotetea kutapanywa kwa majivu husema kwamba huko humaanisha uhuru kutoka katika kuzika makaburini. Hata hivyo, utakaoleta kitulizo kikubwa kupita vyote utakuwa utimizo wa ahadi ya Biblia kwamba “adui wa mwisho atakayebatilishwa ni mauti.”—1 Wakorintho 15:24-28.
Hilo lamaanisha kwamba makaburi, maziara, hata kuteketezwa kwa maiti na kutapanywa kwa majivu, yatakuwa mambo ya wakati uliopita. Ndiyo, kifo hakitakuwapo tena. Chini ya upulizio mtume Yohana aliandika hivi: “Nikasikia sauti kubwa kutoka katika kile kiti cha enzi ikisema, Tazama, maskani ya Mungu ni pamoja na wanadamu, naye atafanya maskani yake pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Naye Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufunuo 21:3, 4.
Yote hayo yatatokea wakati kifo cha kibinadamu kitokanacho na dhambi ya Adamu kinapoondolewa mbali kabisa chini ya Ufalme wa Mungu. Wakati huo wanadamu watiifu hawatakabiliwa na taraja la kurudi mavumbini.
[Picha katika ukurasa wa 29]
Njia za kawaida za kushughulikia maiti
[Picha katika ukurasa wa 31]
Kutapanywa kwa majivu katika Ghuba la Sagami, Japani
[Hisani]
Hisani ya Koueisha, Tokyo