Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 1/1 kur. 23-25
  • Kuacha Mengi kwa Ajili ya Kitu Bora Zaidi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuacha Mengi kwa Ajili ya Kitu Bora Zaidi
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Jinsi Nilivyopata Kuwa Mwaladura
  • Uwasiliano wa Mapema Pamoja na Mashahidi wa Yehova
  • Umashuhuri Wenye Kuongezeka Pamoja na Mzinduko
  • Uamuzi wa Kumtumikia Yehova
  • Jitihada za Kunifanya Nibaki Kanisani
  • Kushikamana na Mke Mmoja
  • Kufurahia Baraka za Yehova
  • Biblia Inabadili Maisha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Kanisa La Kweli na Msingi Wake
    Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele
  • Katika Masikio ya Kitoto
    Amkeni!—1997
  • Sababu kwa Nini Watu wa Namna Zote Wanakuwa Mashahidi wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 1/1 kur. 23-25

Kuacha Mengi kwa Ajili ya Kitu Bora Zaidi

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA JULIUS OWO BELLO

Kwa miaka 32 nilikuwa Niliaminia kwamba kuponya kwa imani na sala zingetatua matatizo yangu yote na kuponya magonjwa yote. Sikununua madawa yoyote kamwe, hata yale ya kutuliza maumivu. Katika miaka hiyo, hakuna yeyote katika familia yangu aliyelazwa hospitalini wakati wowote. Wakati wowote yeyote wa watoto wangu aliposhikwa na ugonjwa, nilisali kwa ajili yao mchana na usiku hadi walipopata nafuu. Niliamini kwamba Mungu alikuwa akijibu sala zangu na kunibariki.

NILIKUWA wa Egbe Jolly, klabu mashuhuri zaidi cha kijamii katika Akure, mji ulioko magharibi mwa Nigeria. Marafiki wangu walikuwa watu matajiri zaidi na wenye mamlaka zaidi katika jumuiya yetu. Mfalme wa Akure, Deji, alinitembelea mara nyingi nyumbani kwangu.

Nilikuwa na wake wengi pia, nikiwa na wake sita na masuria wengi. Biashara yangu ilisitawi. Mambo yote yalikuwa yakiendelea vizuri upande wangu. Hata hivyo, kama yule mfanya-biashara msafiri katika kielezi cha Yesu juu ya lulu, nilipata kitu chenye thamani sana hivi kwamba niliwaacha watano kati ya wake zangu, masuria wangu, kanisa, klabu cha kijamii, na umashuhuri wa kilimwengu ili kubadilishana nacho.—Mathayo 13:45, 46.

Jinsi Nilivyopata Kuwa Mwaladura

Nilisikia mara ya kwanza juu ya Waaladura katika mwaka wa 1936, nilipokuwa na umri wa miaka 13. Rafiki aitwaye Gabriel aliniambia hivi: Ukitembelea Kanisa la Kimitume la Kristo, utamsikia Mungu akiongea.”

“Mungu huongeaje?” Nikamwuliza.

Akasema: “Njoo, ukaone.”

Nilikuwa na hamu ya kumsikiliza Mungu. Kwa hiyo usiku huo, nikaenda pamoja na Gabriel kanisani. Hilo jengo dogo lilikuwa limejaa waabudu. Kutaniko lilianza kuimba-imba: “Njooni, enyi watu! Hapa ndipo alipo Yesu!”

Katika kuimba-imba huko, mtu fulani alipiga kelele hivi: “Shuka chini, roho takatifu!” Mtu mwingine akapiga kengele, na kutaniko likanyamaza. Halafu, mwanamke fulani akaanza kupayuka-payuka kwa msisimko katika lugha isiyojulikana. Kwa ghafula akalia kwa sauti: “Usikilizeni ujumbe wa Mungu, Ee enyi watu! Hili ndilo Mungu amesema: “Salini kwa niaba ya wawindaji ili wasipate kuwaua wanadamu!’” Hali ilijaa hisia-moyo.

Niliamini kwamba Mungu alikuwa amesema kupitia yeye, kwa hiyo mwaka uliofuata nikabatizwa kuwa mshiriki wa Kanisa la Kimitume la Kristo.

Uwasiliano wa Mapema Pamoja na Mashahidi wa Yehova

Katika mwaka wa 1951, nilikubali nakala ya gazeti Mnara wa Mlinzi kutoka kwa Shahidi mmoja aitwaye Adedeji Boboye. Hilo gazeti lilikuwa lenye kupendeza, kwa hiyo nilijipatia andikisho la gazeti hilo na kulisoma kwa ukawaida. Katika mwaka wa 1952, nilihudhuria mkusanyiko wa wilaya wa siku nne wa Mashahidi wa Yehova katika Ado Ekiti.

Niliyoyaona katika huo mkusanyiko yalinivutia. Nilifikiria kwa uzito juu ya kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova lakini nikapuuza hilo wazo. Tatizo langu lilikuwa kwamba nilikuwa na wake watatu na suria mmoja wakati huo. Nilifikiri nisingeweza kamwe kuishi na mke mmoja tu.

Niliporudi Akure, nilimwambia Adedeji aache kunitembelea, na sikufanya upya andikisho langu la Mnara wa Mlinzi. Nikawa mtendaji zaidi katika kanisa langu. Nilisababu kwamba, iwayo yote, Mungu alikuwa amenibariki tangu nilipojiunga na Kanisa la Kimitume la Kristo. Nilikuwa nimeoa wake watatu na kupata watoto wengi. Nilikuwa nimejenga nyumba yangu mwenyewe. Sikuwa nimepata kamwe kulazwa hospitalini. Kwa kuwa ilionekana kwamba Mungu alikuwa akijibu sala zangu, sababu gani nibadili dini yangu?

Umashuhuri Wenye Kuongezeka Pamoja na Mzinduko

Nilianza kuchanga fedha nyingi kwa kanisa langu. Upesi wakanifanya mzee wa kanisa, wadhifa ulioniwezesha kuona matendo ya ndani zaidi ya kanisa. Niliyoona yalinisumbua. Pasta na “manabii” walipenda fedha; pupa yao ilinifadhaisha.

Kwa kielelezo, katika Machi 1967 nilipata kuwa baba ya watoto watatu kupitia wake mbalimbali. Ilikuwa ni desturi kanisani kuwa na sherehe ya kumpa mtoto jina. Kwa hiyo nikapeleka zawadi—samaki, maji ya limau, na vinywaji vya chupani visivyolewesha—kwa pasta katika kuandaa hiyo sherehe.

Katika siku ya mahubiri ya kanisani, pasta alisema mbele ya kutaniko lote hivi: “Matajiri katika kanisa hili wamenishangaza. Wanataka kuwa na sherehe ya kumpa mtoto jina, na kile wanacholeta ni vinywaji visivyolewesha na samaki tu. Hakuna nyama! Hakuna mbuzi! Ebu wazieni hilo! Kaini alimtolea Mungu dhabihu ya viazi vikuu vikubwa, lakini Mungu hakukubali dhabihu hiyo kwa kuwa haikuwa na damu. Mungu hutaka vitu vilivyo na damu. Abeli alitoa mnyama, na dhabihu yake ikakubalika.”

Baada ya hayo, nilisimama na kutoka nje kwa hasira. Hata hivyo, bado nilienda kanisani. Kwa kuzidi nilitumia wakati mwingi zaidi pamoja na marafiki na kuhudhuria mikutano ya klabu changu. Mara kwa mara nilihudhuria mikutano katika Jumba la Ufalme, nami nikafanya upya andikisho langu la Mnara wa Mlinzi. Hata hivyo, bado sikuwa tayari kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.

Uamuzi wa Kumtumikia Yehova

Badiliko la maana kwangu lilitokea mwaka wa 1968. Siku moja nilianza kusoma makala katika Mnara wa Mlinzi iliyofafanua mnyanyaso wenye ukatili wa Mashahidi wa Yehova katika Malawi. Ilisimulia juu ya msichana wa miaka 15 aliyefungwa kwenye mti na kubakwa mara sita kwa sababu alikataa kuridhiana imani yake. Kwa kushtuka sana, niliacha kusoma hilo gazeti, lakini nikaendelea kulifikiria. Niling’amua kwamba hakuna msichana kanisani mwangu ambaye angeonyesha imani kama hiyo. Baadaye jioni hiyo nilichukua hilo gazeti nikasoma huo ukurasa tena.

Nilianza kujifunza Biblia kwa bidii. Nilipokua katika ujuzi, nilianza kuona kadiri ambavyo kanisa lilikuwa limetupotosha. Kama ilivyokuwa kweli nyakati za kale, makasisi wetu walikuwa ‘wakitenda mambo maovu sana.’ (Hosea 6:9) Wanaume kama hao walikuwa miongoni mwa manabii wa uwongo ambao Yesu alionya juu yao! (Mathayo 24:24) Sikuweka imani tena katika maono yao na kazi zao zenye nguvu. Niliamua kujiweka huru na dini isiyo ya kweli na kusaidia wengine wafanye vivyo hivyo.

Jitihada za Kunifanya Nibaki Kanisani

Wazee wa kanisa walipong’amua kwamba niliazimia kuacha kanisa, walituma wajumbe ili kunisihi. Hawakutaka kupoteza chanzo muhimu cha mapato. Walinitolea wadhifa wa kuwa Baba Egbe, mfadhili wa mojawapo ya makanisa ya Kimitume ya Kristo katika Akure.

Nilikataa toleo lao nikawaambia sababu ya kufanya hivyo. “Kanisa limekuwa likitudanganya,” nikasema. “Wao husema kwamba watu wote wazuri wataenda mbinguni. Lakini nimeisoma Biblia, na ninasadiki kwamba watu 144,000 tu ndio watakaoenda mbinguni. Watu wengine waadilifu wataishi katika dunia iliyo paradiso.”—Mathayo 5:5; Ufunuo 14:1, 3.

Pasta wa hilo kanisa alijaribu kuwafanya wake zangu wanipinge. Aliwaambia wazuie Mashahidi wa Yehova wasije nyumbani kwetu. Mmoja wa wake zangu alitia sumu katika chakula changu. Wawili wao walinionya juu ya ono walilokuwa wameona kanisani. Hilo ono lilionyesha kwamba ningekufa kama ningeacha kanisa. Licha ya hayo, niliendelea kuwatolea wake zangu ushahidi, nikiwaalika waje kwenye mikutano pamoja nami. “Mtapata waume wengine huko,” nikasema. Hata hivyo hakuna yeyote kati yao aliyeonyesha upendezi wowote, nao wakaendelea kujaribu kunivunja moyo.

Hatimaye, Februari 2, 1970, niliporudi nyumbani kutoka safari ya kwenda mji ulio karibu, nilikuta kwamba nyumba haikuwa na watu. Wake zangu wote walikuwa wametoroka pamoja na watoto.

Kushikamana na Mke Mmoja

‘Sasa naweza kurekebisha hali yangu ya ndoa,’ nikawaza. Nilimwalika mke wangu mkubwa, Janet, arudi nyumbani. Akakubali. Hata hivyo, familia yake ilipinga vikali hilo wazo. Wakati wake zangu wengine walipopata kujua kwamba nilikuwa nimemwomba Janet arudi nyumbani, walienda nyumbani kwa baba yake wakajaribu kumpiga. Ndipo familia yake ikaniita kwenye mkutano.

Watu karibu 80 walikuwapo kwenye huo mkutano. Mjombake Janet, aliyekuwa kichwa cha familia, alisema hivi: “Ikiwa wataka kumwoa tena binti yetu, basi itakupasa uwachukue tena wale wanawake wengine. Lakini ikiwa wataka kuzoea dini yako mpya na kukaa na mke mmoja, basi ni lazima utafute mwanamke mwingine. Ukimchukua Janet tena, wale wake zako wengine watamwua, na hatutaki binti yetu afe.”

Baada ya maongezi mengi, hiyo familia iling’amua kwamba nilikuwa nimeazimia kuwa na mke mmoja tu. Hatimaye wakatulia. Huyo mjomba akasema: “Hatutamchukua mke wako kutoka kwako. Waweza kwenda pamoja naye.”

Mei 21, 1970, Janet nami tulioana kisheria. Siku tisa baadaye nikabatizwa kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Desemba ya mwaka huohuo, Janet akabatizwa pia.

Kufurahia Baraka za Yehova

Waliokuwa washiriki wa kanisa letu hapo awali walikuwa wametabiri kwamba kama tungekuwa Mashahidi, tungekufa. Hiyo ilikuwa karibu miaka 30 iliyopita. Hata nikifa sasa, je, ingekuwa ni kwa sababu nilipata kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova? Mke wangu akifa sasa, je, mtu yeyote aweza kusema kwamba ni kwa sababu alipata kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova? Nimejitahidi kuonyesha watoto wangu 17 njia ya kweli. Ingawa wengi wao walikuwa watu wazima wakati nilipopata kuwa Shahidi, niliwatia moyo wajifunze Biblia, nikawapeleka kwenye mikutano na mikusanyiko. Ni furaha yangu kuwa na watano wao wanaomtumikia Yehova pamoja nami. Mmoja hutumikia pamoja nami akiwa mzee kutanikoni. Mwingine ni mtumishi wa huduma katika kutaniko lililo karibu. Wawili wa watoto wangu hutumikia wakiwa mapainia wa kawaida.

Nikumbukapo ya nyuma, nastaajabia fadhili isiyostahiliwa ya Yehova katika kunisaidia kuwa mtumishi wake. Jinsi maneno ya Yesu yalivyo ya kweli: “Hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute yeye”!—Yohana 6:44.

[Maelezo ya Chini]

a Kutokana na neno la Kiyoruba linalomaanisha “mtu asaliye.” Larejezea mshiriki wa kanisa la Kiafrika ambalo lina mazoea ya kuponya kiroho.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki