Furaha ya Kweli Yaweza Kupatikana Wapi?
WATU wengi huhisi kwamba furaha yaweza kupatikana kwa kujipatia mali za kimwili. Namna gani wewe? Ingawa mali za kimwili zaweza kuchangia furaha yetu kwa hakika, hazihakikishi furaha; wala starehe za kimwili hazijengi imani wala kujaza mahitaji ya kiroho.
Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu Kristo alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wenye kuona uhitaji wao wa kiroho, kwa kuwa ufalme wa mbingu ni wao.” (Mathayo 5:3) Yesu pia alisema hivi: “Fulizeni kufungua macho yenu na mlinde dhidi ya kila namna ya tamaa, kwa sababu hata wakati mtu ana wingi uhai wake hautokani na vitu alivyo navyo.”—Luka 12:15.
Watu wengi hutafuta furaha kwa kushiriki katika ngono haramu na “kazi [nyingine] za mwili.” (Wagalatia 5:19-21) Hata hivyo, kujiruhusu kushiriki katika raha za kimwili hakuleti furaha ya kweli na idumuyo. Kwa hakika, wale wanaozoea mambo hayo hawatarithi Ufalme wa Mungu.—1 Wakorintho 6:9, 10.
Wengine hugeukia utu wa ndani katika kutafuta kwao furaha kwa kujaribu kujenga heshima yao wenyewe. Maktaba na duka za vitabu zimejaa vitabu vyenye kutoa mwongozo wa kufanya maendeleo ya kibinafsi, lakini vichapo hivyo haviwaletei watu furaha idumuyo. Hivyo, basi, ni wapi tuwezapo kupata furaha halisi?
Ili kuwa wenye furaha kikweli, twapaswa kutambua uhitaji wetu wa kiroho tuliozaliwa nao. Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale wenye kuona uhitaji wao wa kiroho.” Bila shaka, haingetunufaisha kama tungeufahamu uhitaji huo kisha tushindwe kufanya jambo lolote juu yao. Kwa kutoa kielezo: Ni nini kingempata mkimbiaji wa shindano la mbio la mwendo mrefu ambaye baada ya shindano angeshindwa kuitikia uhitaji wa mwili wake wa kupata maji? Je, asingekabili upesi upungufu wa maji mwilini na matokeo mengine mazito? Hali kadhalika, tukishindwa kuitikia uhitaji wetu wa kupata lishe la kiroho, hatimaye tutanyauka kiroho. Hilo litaongoza kwenye hali ya kupoteza shangwe na furaha.
Yesu alitambua kikamili uhitaji wake wa kiroho, akijifunza na kutafakari juu ya Neno la Mungu kwa ukawaida. Yeye aliweza kupata na kusoma sehemu za Maandiko Matakatifu kwa urahisi, na alifundisha wengine kufanya vivyo hivyo. (Luka 4:16-21; linganisha Waefeso 4:20, 21.) Yesu pia alifananisha kule kufanya mapenzi ya Baba yake wa kimbingu na chakula. Kufanya mapenzi ya Mungu kulimletea furaha nyingi.—Yohana 4:34.
Ndiyo, furaha ya kweli haiwezi kupatikana kwa kujipatia vitu vya kimwili; wala furaha haitokani na kuuandalia mwili wenye dhambi. Furaha ya kweli ni hali ya moyoni, inayotegemea imani ya kweli na uhusiano mzuri pamoja na Yehova Mungu. Kwa kufaa, basi, mtunga-zaburi Daudi aliimba hivi: “Heri watu wenye BWANA kuwa Mungu wao.”—Zaburi 144:15b.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Imani na uhusiano mzuri pamoja na Mungu utakuletea furaha ya kweli