Yehova Hutenda kwa Uaminifu-Mshikamanifu
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA PETER PALLISER
Ilikuwa Desemba mwaka wa 1985. Msisimuko uliongezeka tulipoanza kushuka kuelekea uwanja wa ndege wa kimataifa wa Nairobi, Kenya. Tulipoingia jijini kwa gari, kumbukumbu zilijaa akilini tena, zikiamshwa na mwono na sauti zenye kufahamika.
TULIKUJA Kenya kuhudhuria “Washika Ukamilifu” Mkusanyiko wa Wilaya wa Mashahidi wa Yehova. Miaka 12 mapema, mke wangu nami tulikuwa tumelazimishwa kuondoka Kenya kwa sababu ya marufuku juu ya kazi yetu ya kuhubiri. Tulikuwa tumeishi kwenye Betheli huko, jina linalopewa majengo ya ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova. Ni jambo la kufurahisha kama nini lililotungojea tuliporudi huko kutembelea!
Aliyekuwa akisaidia kutayarisha chakula cha mchana Betheli ni Shahidi mchanga tuliyemjua tangu alipokuwa mwenye umri wa miaka miwili. Angalau washiriki sita wa familia ya Betheli ni watu tuliojua walipokuwa watoto. Ilikuwa ni shangwe kama nini kuwaona sasa wakiwa watu wachanga walio wazima, pamoja na familia zao, wote wakiwa bado watendaji katika huduma! Mungu wetu, Yehova alikuwa amewatunza kwa kupatana na hii ahadi ya Biblia: “Kwa mtu mwenye fadhili [“mwenye uaminifu-mshikamanifu,” NW] utajionyesha kuwa mwenye fadhili [“mwaminifu-mshikamanifu,” NW].” (2 Samweli 22:26) Niliona tofauti iliyoje kati ya maisha yangu ya ujana na maisha yenye kuthawabisha ambayo vijana hao walikuwa wakiishi!
Maisha ya Ujana Yasiyo na Kusudi
Nilizaliwa katika Scarborough, Uingereza, Agosti 14, mwaka wa 1918. Miaka miwili baadaye mama yangu na dada yake wa kambo walihamia Kanada, hivyo nilikaa miaka mitatu iliyofuata na baba yangu, mama yake, na dada yake. Nilipokuwa na umri wa miaka mitano, mama aliniteka nyara na kunipeleka Montreal, Kanada. Miaka minne baadaye alinirudisha Uingereza kuishi na baba tena ili niende shuleni.
Mama yangu na dada wa kambo waliniandikia barua karibu kila miezi sita. Mwishoni mwa barua zao, wangeonyesha tamaa yao kwamba niwe raia mwema, mwenye uaminifu-mshikamanifu kwa Mfalme na nchi. Majibu yangu yaelekea yaliwatamausha kwa sababu niliwaandikia kwamba niliamini kwamba utukuzo wa taifa na vita havikufaa. Hata hivyo, kwa kukosa mwelekezo dhahiri, niliishi maisha yasiyo na kusudi wakati wa miaka yangu ya utineja.
Kisha katika Julai mwaka wa 1939, majuma sita kabla ya Vita ya Ulimwengu ya Pili kuanza, nilisajiliwa katika jeshi la Uingereza. Nilikuwa na umri wa miaka 20 tu. Upesi kikosi changu kilipelekwa kaskazini mwa Ufaransa. Ndege za Ujerumani zilipotushambulia, sisi wanaume vijana tulilenga bunduki zetu na kuzifyatulia risasi. Yalikuwa maisha yenye kuogopesha. Tulirudi nyuma mbele ya majeshi ya Ujerumani yaliyokuwa yakisonga mbele, na nilikuwa miongoni mwa wale waliohamishwa Dunkirk wakati wa juma la kwanza la Juni mwaka wa 1940. Mimi bado hukumbuka kwa kuchukizwa sana ule mwono wa maiti za kikosi kizima zikiwa zimetawanyika ufuoni. Niliokoka jinamizi hilo na kuwasili Harwich katika mashariki mwa Uingereza nikiwa ndani ya meli ndogo ya mizigo.
Mwaka uliofuata, katika Machi 1941, nilipelekwa India. Huko nilipokea mazoezi ya kuwa mekanika wa kutengeneza vifaa vya ndege. Baada ya kipindi fulani hospitalini kwa sababu ya maradhi fulani, nilihamishwa kupelekwa kwenye kikundi cha jeshi kilichokuwa Delhi, jiji kuu la India. Nikiwa mbali na nyumbani na nikiwa bado mgonjwa, nilianza kufikiria wakati ujao. Hasa nilifikiria juu ya nini hutendeka tunapokufa.
Kudhihirisha Uaminifu-Mshikamanifu Mpya
Mwingereza mwenzangu, Bert Gale, alikuwa mshiriki wangu wa chumba huko Delhi. Siku moja alisema kwamba “dini ilikuwa ya Ibilisi,” maoni yaliyoamsha upendezi wangu. Mke wake alikuwa amekuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, na pindi kwa pindi, alimpelekea vichapo vya Biblia. Kimojawapo cha hivyo, kijitabu Hope, kilinasa upendezi wangu. Mazungumzo yacho juu ya tumaini la ufufuo yaliniandalia hali halisi ya utulivu.
Wakati fulani mapema mwaka wa 1943, Bert alizungumza na raia mmoja ambaye mzazi mmoja alikuwa Mhindi na yule mwingine Mwingereza, Teddy Grubert, aliyefanya kazi nasi katika kituo cha jeshi. Tulishangaa kujua kwamba Teddy alikuwa Shahidi. Ijapokuwa katika mwaka wa 1941 vichapo vya Mashahidi wa Yehova vilikuwa vimepigwa marufuku, alitupeleka kwenye mikutano iliyofanywa na Mashahidi wa Yehova katika Delhi. Katika kutaniko hilo dogo, nilipata uandamani wa kweli na wenye uchangamfu kwa mara ya kwanza maishani mwangu. Basil Tsatos, ndugu Mkristo mzee kutoka Ugiriki alipendezwa nami kibinafsi na alinijibu maswali yangu. Aliandaa majibu ya Biblia juu ya ni kwa nini tunazeeka na kufa, juu ya ufufuo, na juu ya ulimwengu mpya wenye uadilifu ulioahidiwa na Mungu.—Matendo 24:15; Waroma 5:12; 2 Petro 3:13; Ufunuo 21:3, 4.
Kijitabu Peace—Can It Last?, kilichochapishwa katika mwaka wa 1942, hasa kilinasa upendezi wangu. Kilitambulisha Ushirika wa Mataifa kuwa yule “hayawani-mwitu mwenye rangi-nyekundu-nyangavu.” (Ufunuo 17:3) Kikinukuu sura ya 17, mstari wa 11, wa Ufunuo, hicho kijitabu kilisema hivi: “Yaweza kusemwa sasa kwamba Ushirika ‘ulikuweko, na haupo.’” Kiliendelea kusema hivi: “Ushirika wa mataifa ya kilimwengu utainuka tena.” Katika mwaka wa 1945, zaidi ya miaka mitatu baadaye, hivyo ndivyo ilivyotokea wakati Ushirika wa Mataifa ulipofanyizwa!
Wakati wa marufuku juu ya fasihi za Mashahidi, niliweza kuwasaidia marafiki wangu wapya. Wakati katoni la vijitabu Peace—Can It Last? lingefika, kutaniko lingenipatia ili nihifadhi. Nani angefikiria kutafuta fasihi iliyopigwa marufuku kambini mwa jeshi? Kila nilipohudhuria mikutano, nilibeba vijitabu vichache ili ndugu waendelee kupata ugavi. Hata nilificha fasihi zao za kibinafsi za Biblia walipohofia msako wa nyumba zao. Hatimaye, Desemba 11, mwaka wa 1944, marufuku iliondolewa.
Uaminifu-mshikamanifu wangu kwa mafundisho ya Kikristo ulitahiniwa wakati wa sherehe za Krismasi ya mwaka wa 1943 zilizopangwa kwa ajili ya kikosi chetu. Nilikataa kushiriki, kwa kuwa nilikuwa nimejifunza kwamba Yesu hakuzaliwa katika majira ya baridi ya mwezi wa Desemba na Wakristo wa kwanza hawakusherehekea Krismasi.—Linganisha Luka 2:8-12.
Kusanyiko “Watangazaji Wenye Muungano” lilipofanywa katika Jubbulpore Desemba 27 hadi 31, mwaka wa 1944, nilikuwa miongoni mwa wahudhuriaji 150. Wajumbe wengi wa mkusanyiko walisafiri kwa gari-moshi kutoka Delhi, safari ya zaidi ya kilometa 600. Sitasahau kamwe hali yenye kupendeza katika kikao hicho cha nje, ambako niliona tengenezo la Yehova likiwa katika kutenda.
Wajumbe wa mkusanyiko walikaa kwenye nyumba za kulala za shule, ambako tuliimba nyimbo za Ufalme na kufurahia ushirika wa Kikristo. Wakati huo wa kusanyiko nilianza kushiriki katika kazi ya kuhubiri peupe, kazi ambayo tangu wakati huo imebaki yenye kupendwa sana na moyo wangu.
Huduma ya Wakati Wote Katika Uingereza
Nilirudi Uingereza katika mwaka wa 1946 na upesi nikaanza kushirikiana na Kutaniko la Wolverton. Ijapokuwa tulikuwa na watangazaji wa Ufalme wapatao kumi, hao walinifanya nijihisi nimestarehe, na nilipata uradhi uleule niliopata miongoni mwa ndugu zangu huko India. Vera Clifton alijitokeza kutanikoni kuwa mtu wa kweli, mwenye moyo mchangamfu. Nilipojua kwamba alikuwa na tamaa sawa na yangu ya kuwa painia, kama vile watumishi wa wakati wote wanavyoitwa, tulioana Mei 24, mwaka wa 1947. Nilitengeneza gari kuwa makao, au makao yatembeayo, na mwaka uliofuata, tulipokea mgawo wetu wa kwanza wa upainia, mji wa mashambani wa Huntingdon.
Katika siku hizo tuliondoka kwa baiskeli asubuhi na mapema kwenda eneo la vijijini. Mahubiri yetu ya siku nzima yalikatizwa kwa muda mfupi tu ili tule chakula chetu cha mchana. Haidhuru tuliendesha baiskeli kwenda nyumbani kupitia upepo wa mbisho wenye nguvu jinsi gani au mvua nyingi jinsi gani, tulifurahi na kuridhika katika kazi ya Bwana.
Baada ya muda tulitamani sana kupanua huduma yetu na kushiriki “habari njema” na watu wa nchi nyingine. (Mathayo 24:14) Hivyo tulipeleka ombi la kuhudhuria shule ya mishonari ya Gileadi katika South Lansing, New York, Marekani. Hatimaye, tulikubaliwa kuhudhuria darasa la 26 la Gileadi lililohitimu katika Februari mwaka wa 1956.
Huduma Iliyopanuka Katika Afrika
Mgawo wetu wa umishonari ulikuwa Northern Rhodesia (sasa ni Zambia) katika Afrika. Upesi baada ya kuwasili, tulialikwa kutumikia katika Betheli ya nchi hiyo. Ikiwa sehemu ya kazi yangu ya Betheli, nilishughulikia barua za Afrika Mashariki. Katika mwaka wa 1956, Kenya—mojawapo ya nchi hizo za Afrika Mashariki—ilikuwa na Mashahidi wanne tu, huku kukiwa na Mashahidi zaidi ya 24,000 katika Northern Rhodesia. Vera nami tulianza kufikiria jinsi ingekuwa vizuri kutumikia mahali palipokuwa na uhitaji mkubwa zaidi.
Kisha, bila kutazamia, nikapokea mwaliko mwingine wa kwenda Shule ya Gileadi, wakati huu kwa ajili ya mtaala wa waangalizi wa miezi kumi. Huku nikimwacha Vera katika Northern Rhodesia, nilisafiri kwenda New York City, ambako Shule ya Gileadi ilikuwa wakati huo. Baada ya kumaliza mtaala huo katika Novemba mwaka wa 1962, nilipewa mgawo wa kwenda Kenya kuanzisha ofisi ya tawi huko. Kufikia wakati huo Kenya ilikuwa na Mashahidi zaidi ya mia moja.
Nilipokuwa nikirudi Northern Rhodesia kuonana na Vera, nilipaswa kupitia Nairobi, Kenya, kwa muda mfupi. Lakini nilipowasili, Bill Nisbet, mhitimu wa Gileadi wa darasa la 25, aliniambia kwamba kulikuwa na fursa ya kupata kibali cha kuingia Kenya mara moja. Tuliwafikia wenye mamlaka katika idara ya uhamiaji, na katika muda wa dakika chache, nilikuwa nimepata hati za kuturuhusu kukaa Kenya kwa miaka mitano. Hivyo sikurudi tena Northern Rhodesia; badala ya hivyo, Vera aliungana nami Nairobi.
Baada ya kuhudhuria mtaala wa lugha ya Kiswahili uliotayarishwa kwa ajili yetu, tuliungana katika huduma na kutaniko dogo lililokuwa Nairobi. Nyakati nyingine baada ya kusoma utoaji wetu wa mahubiri kwa Kiswahili, mwenye nyumba angesema kwa mshangao, “Sielewi Kiingereza!” Licha ya hayo, tulivumilia na hatua kwa hatua tukashinda hicho kizuizi cha lugha.
Eneo letu lilitia ndani, eneo kubwa lenye nyumba nyingi za kukaa lililokuwa na majina ya Biblia kama Jerusalem na Jericho. Kupendezwa kulisitawishwa, na watu wengi kutoka maeneo hayo wakawa watangazaji wa Ufalme. Kweli ya Biblia ilikuwa na matokeo kama nini juu ya watu hao! Hisi za ubora wa kikabila ziliisha pale uaminifu-mshikamanifu wa Ufalme ulipoleta muungano miongoni mwa watu wa Yehova. Hata ndoa baina ya makabila mbalimbali zilifanyika, jambo ambalo si la kawaida sana miongoni mwa wasio Mashahidi.
Wapiga-mbiu wapya wa Ufalme walifuata kweli kwa bidii. Kwa kielelezo, Samson, alikuwa na hamu sana kweli ya Biblia ipenye eneo lake la nyumbani hivi kwamba alifuliza kuomba mapainia wapelekwe huko. Kwa hakika, alipanua nyumba yake iliyokuwa katika eneo la Ukambani ili kuwaandalia makao. Upesi kutaniko jipya la wapiga-mbiu wa Ufalme lilianzishwa huko.
Mara kadhaa nilitembelea ndugu zetu katika nchi ya Afrika Mashariki ya Ethiopia. Walikuwa wakitumia wastani wa saa 20 kila mwezi katika huduma, licha ya vifungo mbalimbali, kuchapwa, na kupelelezwa daima. Wakati mmoja ndugu na dada wa Ethiopia waliojaa basi mbili walisafiri kwa muda wa juma moja, wakivuka vijia hatari vya milima, ili kuhudhuria mkusanyiko wa wilaya katika Kenya. Werevu wao katika kupanga fasihi za Ufalme ipatikane nchini mwao ulikuwa wenye kusifika. Sisi tuliokuwa Kenya tulifurahia kuwapelekea.
Katika mwaka wa 1973 marufuku rasmi iliwekwa juu ya kazi yetu katika Kenya, na wamishonari walilazimishwa kuondoka. Kufikia wakati huo tulikuwa na Mashahidi zaidi ya 1,200 katika Kenya, na wengi wao walikuwa kwenye uwanja wa ndege kutuaga jambo ambalo hatutasahau. Kuwapo kwao kulimsukuma msafiri mwenzetu kutuuliza ikiwa sisi tulikuwa watu maarufu wa aina fulani. Vera nami tulirudi Uingereza na tulipewa mgawo huko, lakini tulitamani sana kurudi Afrika.
Kurudi Afrika
Hivyo, miezi michache baadaye, tulipokea mgawo wetu mpya, wa kwenda Betheli katika Accra, jiji kuu la nchi ya Afrika magharibi ya Ghana. Mmojawapo ya migawo yangu hapa ulinileta uso kwa uso na shida ambazo ndugu zetu walikabiliwa nazo. Niliposhughulikia ununuzi wa chakula na vifaa kwa ajili ya familia ya Betheli, nilishangazwa na bei ya kupita kiasi ya vyakula. Mara nyingi mtu hangeweza kununua vitu vilivyohitajiwa. Upungufu wa petroli na uhaba wa speapati uliongezea matatizo.
Nilijifunza umuhimu wa subira, jambo ambalo ndugu zetu wa Ghana walikuwa wamesitawisha. Ilitia moyo sana kuona mtazamo mchangamfu walioudumisha huku wakikataa kishawishi cha kupata mahitaji ya lazima ya maisha kwa njia ya hongo. Tokeo ni kwamba watu wa Yehova katika Ghana walijulikana sana kwa ufuatiaji wao wa haki na walikuja kujipatia sifa nzuri pamoja na maofisa wengi.
Hata hivyo, licha ya upungufu wa vitu vya kimwili, kulikuwa na usitawi wa hali ya kiroho. Nchini mwote, vichapo vyetu vya Biblia vilipatikana karibu kila nyumba. Na tuliona idadi ya wapiga-mbiu wa Ufalme katika Ghana ikikua kutoka watu 17,156 katika mwaka wa 1973 tulipofika hadi zaidi ya watu 23,000 katika mwaka wa 1981. Katika mwaka huo milipuko yangu ya kansa ya ngozi, ambayo bila shaka ilikuwa imefanywa iwe mibaya zaidi na kuchomwa na jua miaka mingi katika India na Afrika, ilitulazimisha kuondoka Ghana na kurudi Uingereza kwa ajili ya matibabu ya kawaida.
Hali Mpya Katika Uingereza
Kwa upande wangu kurudi kwetu kulimaanisha marekebisho makubwa katika huduma yangu. Nilikuwa nimezoea kuzungumza kwa uhuru na watu walioheshimu Mungu na Biblia. Lakini katika London, ni mara chache ninapouona mtazamo kama huo. Mimi hustaajabia uvumilivu wa ndugu katika Uingereza. Hilo limenifanya kuona uhitaji wa kusitawisha hisia-mwenzi kwa watu ambao ‘wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku’ kiroho.—Mathayo 9:36.
Baada ya kurudi kutoka Afrika, Vera nami tulitumikia kwenye Betheli ya London hadi alipokufa katika Septemba mwaka wa 1991 akiwa na umri wa miaka 73. Halijakuwa jambo rahisi kumpoteza mwandamani mwaminifu hivyo ambaye alifanya kazi pamoja nami bega kwa bega katika huduma kwa miaka mingi hivyo. Ninamkosa sana. Lakini ninafurahia kitia moyo ninachopata kutoka kwa washiriki 250 wa familia ya Betheli.
Kwa kweli naliona kuwa pendeleo kuona tengenezo la Yehova likisonga mbele na kuwaona wengi hivyo wakifanya huduma ya wakati wote kuwa njia yao ya maisha. Ninaweza kuwahakikishia kwamba, hakuna njia nyingine ya maisha iliyo nzuri kupita hii, kwa maana “BWANA . . . hawaachi watauwa [“waaminifu-washikamanifu,” NW] wake.”—Zaburi 37:28.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Tulipainia katika Uingereza kuanzia mwaka wa 1947 hadi mwaka wa 1955
[Picha katika ukurasa wa 23]
Mara yangu ya kwanza katika huduma wakati wa mkusanyiko katika India
[Picha katika ukurasa wa 23]
Tulipokuwa wamishonari katika Northern Rhodesia
[Picha katika ukurasa wa 23]
Katika mwaka wa 1985, tukiwa na marafiki ambao hatukuwa tumewaona kwa muda wa miaka 12