Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 6/1 kur. 24-27
  • Udhaifu wa Kibinadamu Hutukuza Nguvu za Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Udhaifu wa Kibinadamu Hutukuza Nguvu za Yehova
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kukabiliana na Majaribu
  • Kukabiliana na Hali ya Kutokamilika
  • Nguvu za Kuhubiri
  • Kukabiliana na “Mwiba Katika Mwili”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Je, Una “Mwiba Katika Mwili”?
    Huduma Yetu ya Ufalme—1998
  • “Mwiba Katika Mwili” wa Paulo
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2019
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 6/1 kur. 24-27

Udhaifu wa Kibinadamu Hutukuza Nguvu za Yehova

“Kila mmoja alinifikiria kuwa mhudumu wa wakati wote mwenye furaha na uchangamfu. Sikuzote mimi ndiye niliyewasaidia wengine na matatizo yao. Hata hivyo, wakati huohuo, nilijihisi kindani kana kwamba nilikuwa nikifa. Mawazo yenye kusumbua na maumivu makali ya kiakili yalikuwa na matokeo yenye kudhuru. Nilianza kujihisi mwenye kujitenga na watu. Nilitaka tu kukaa nyumbani nikiwa kitandani. Kwa miezi mingi, nilimwomba Yehova aniache nife.”—Vanessa.

KAMA ilivyo katika mfano uliotajwa hapo juu, ni jambo la kutazamiwa tu kwamba nyakati nyingine watumishi wa Yehova watahisi matokeo ya kuishi katika “nyakati [hizi] za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Huenda wengine hata wakashuka moyo. (Wafilipi 2:25-27) Hali ya kuvunjika moyo izidipo, yaweza kutunyang’anya nguvu zetu, kwa maana Biblia hutaarifu hivi: “Ukizimia siku ya taabu, nguvu zako ni chache.” (Mithali 24:10) Ndiyo, tunapovunjika moyo, twahitaji nguvu—labda hata ile ambayo mtume Paulo aliiita “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida.”—2 Wakorintho 4:7.

Yehova Mungu ndiye chanzo cha nguvu nyingi. Hili ni dhahiri tuchunguzapo uumbaji wake. (Waroma 1:20) Kwa kielelezo, chunguza jua. Dunia hupokea mtiririko usiobadilika wa nguvufarasi zipatazo trilioni 240 kutoka kwa jua. Hata hivyo, tarakimu hiyo yaonyesha karibu nusu ya sehemu ya bilioni tu ya nishati ambazo jua hutoa. Na jua ni dogo lilinganishwapo na nyota zijulikanazo kama nyota zilizo kubwa mno. Miongoni mwazo ni Rigel, nyota iliyo katika kundinyota la Orion ambayo ina ukubwa mara 50 zaidi ya jua letu na hutoa nishati mara 150,000 zaidi!

Muumba wa vyanzo hivyo vya nguvu lazima yeye mwenyewe awe na “ukuu wa uweza.” (Isaya 40:26; Zaburi 8:3, 4) Kwa kweli, nabii Isaya alitaarifu kwamba Yehova “hazimii wala hachoki.” Na Mungu yuko tayari kushiriki hizo nguvu zake pamoja na wowote ambao, kwa sababu ya udhaifu wa kibinadamu, wajihisi kwamba wanachoka. (Isaya 40:28, 29) Jinsi afanyavyo hivyo hutolewa kielezi katika kisa cha mtume Mkristo Paulo.

Kukabiliana na Majaribu

Paulo aliwaambia Wakorintho juu ya kizuizi ambacho alilazimika kuvumilia. Alikiita “mwiba katika mwili.” (2 Wakorintho 12:7) Huenda ikawa “mwiba” huo ulikuwa tatizo la kiafya, labda uwezo wa kuona uliokuwa umedhoofika. (Wagalatia 4:15; 6:11) Au huenda Paulo alikuwa akirejezea mitume wasio wa kweli na wasumbuaji wengine waliopinga utume na kazi yake. (2 Wakorintho 11:5, 6, 12-15; Wagalatia 1:6-9; 5:12) Hata uwe ulikuwa nini, ‘mwiba huo katika mwili’ ulimsononesha sana Paulo, na alisali tena na tena kwamba uondolewe.—2 Wakorintho 12:8.

Hata hivyo, Yehova hakukubali ombi la Paulo. Badala ya hivyo, alimwambia Paulo hivi: “Fadhili yangu isiyostahiliwa yakutosha wewe.” (2 Wakorintho 12:9) Yehova alimaanisha nini kwa kusema hivyo? Bila shaka, tufikiriapo mwendo wa zamani wa Paulo wa kuwanyanyasa Wakristo, ilikuwa tu ni kwa fadhili isiyostahiliwa kwamba angeweza kuwa na uhusiano pamoja na Mungu kwa vyovyote—wacha hata kutumikia akiwa mtume!a (Linganisha Zekaria 2:8; Ufunuo 16:5, 6.) Huenda ikawa Yehova alikuwa akimwambia Paulo kwamba pendeleo la kuwa mwanafunzi “lilitosha.” Halingeandamanishwa na uondoshaji kimuujiza wa matatizo ya kibinafsi ya maisha. Kwa kweli, huenda shida fulani zikaja kama tokeo la mapendeleo yaliyoongezeka. (2 Wakorintho 11:24-27; 2 Timotheo 3:12) Kwa vyovyote vile, Paulo angelazimika kuvumilia tu ‘mwiba wake katika mwili.’

Hata hivyo, kwa hakika Yehova hakuwa akimwacha Paulo pekee pasipo huruma. Badala ya hivyo, alimwambia hivi: “Nguvu yangu inafanywa kamilifu katika udhaifu.” (2 Wakorintho 12:9) Ndiyo, Yehova kwa upendo angemwongezea Paulo nguvu za kukabiliana na hali yake. Hivyo, “mwiba katika mwili” wa Paulo ukawa kielelezo chenye kutumika. Ulimfundisha kutegemea nguvu za Yehova badala ya nguvu zake mwenyewe. Kwa wazi Paulo alijifunza kikamili somo hilo, kwa maana miaka kadhaa baadaye aliandikia Wafilipi hivi: “Nimejifunza, kuwa mwenye ujitoshelevu, mwenyewe katika hali zozote nilimo. Kwa mambo yote ninayo nguvu kwa njia ya yeye anipaye nguvu.”—Wafilipi 4:11, 13.

Namna gani wewe? Je, unavumilia namna fulani ya “mwiba katika mwili,” labda ugonjwa au hali maishani inayosababisha wasiwasi mwingi? Ikiwa ndivyo, jipe moyo. Ingawa huenda ikawa Yehova hatakuondolea hicho kizuizi kimuujiza, yeye aweza kukupatia hekima na uvumilivu wa kukabiliana nacho uendeleapo kuweka masilahi ya Ufalme kwanza maishani.—Mathayo 6:33.

Ikiwa ugonjwa au umri unaoongezeka wakuzuia kutimiza mengi katika utendaji wa Kikristo kama vile ungependa, usikate tumaini. Badala ya kuona jaribu lako kuwa linawekea mipaka utumishi wako kwa Yehova, lione kuwa fursa ya kuongeza utegemeo wako kwake. Kumbuka pia, kwamba thamani ya Mkristo haipimwi kwa kiwango chake cha utendaji, bali kwa imani na kina cha upendo wake. (Linganisha Marko 12:41-44.) Kumpenda Yehova kwa nafsi yako yote kwamaanisha kwamba unamtumikia kwa uwezo wako wote—si kwa uwezo wa mtu mwingine.—Mathayo 22:37; Wagalatia 6:4, 5.

Ikiwa “mwiba [wako] katika mwili” wahusisha hali yenye kusononesha maishani, kama vile kufiwa na mpendwa, fuata hili shauri la upole la Biblia: “Umtwike BWANA mzigo wako naye atakutegemeza. Hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele.” (Zaburi 55:22) Mwanamke Mkristo aitwaye Sylvia alifanya hivyo. Katika muda wa miaka michache tu, alifiwa na mume wake baada ya miaka 50 ya ndoa na pia washiriki wengine tisa wa familia—wakitia ndani wajukuu wawili wachanga. “Kama asingekuwa Yehova,” Sylvia asema, “ningehuzunika bila kujizuia. Lakini mimi hupata faraja kubwa katika sala. Mimi hudumisha mazungumzo yasiyokoma pamoja na Yehova. Ninajua yeye hunipa nguvu za kufaulu.”

Latumainisha kama nini kujua kwamba “Mungu wa faraja yote” aweza kuwapa wale wanaohuzunika nguvu za kuvumilia! (2 Wakorintho 1:3; 1 Wathesalonike 4:13) Kwa kung’amua jambo hilo, twaweza kuelewa mkataa wa Paulo juu yalo. Yeye aliandika hivi: “Napendezwa na udhaifu, katika matusi, katika visa vya uhitaji, katika minyanyaso na magumu, kwa ajili ya Kristo. Kwa maana niwapo dhaifu, ndipo niwapo mwenye nguvu.”—2 Wakorintho 12:10.

Kukabiliana na Hali ya Kutokamilika

Sisi sote tumerithi hali ya kutokamilika kutoka kwa wazazi wetu wa kwanza wa kibinadamu. (Waroma 5:12) Tokeo ni kwamba, tumo katika pigano dhidi ya tamaa za mwili wenye dhambi. Laweza kuwa jambo la kuvunja moyo kama nini kutambua kwamba vitabia vya “utu wa hapo zamani” vinatushika kwa nguvu zaidi ya tulivyofikiria! (Waefeso 4:22-24) Huenda katika nyakati hizo tukahisi kama alivyohisi mtume Paulo, aliyeandika hivi: “Kwa kweli napendezwa na sheria ya Mungu kulingana na mtu niliye kwa ndani, lakini mimi naona katika viungo vyangu sheria nyingine ikifanya vita dhidi ya sheria ya akili yangu na kunichukua mateka kwa sheria ya dhambi iliyo katika viungo vyangu.”—Waroma 7:22, 23.

Hapa, pia, twaweza kujinufaisha na nguvu kutoka kwa Yehova. Unapong’ang’ana na udhaifu wa kibinafsi, usiache kamwe kumwendea yeye katika sala, ukitafuta kwa bidii msamaha wake hata ikiwa walazimika kumfikia mara nyingi jinsi gani juu ya tatizo lilelile. Kwa sababu ya fadhili zake zisizostahiliwa, Yehova, ambaye “hupima mioyo” na awezaye kuona kina cha weupe wa moyo wako, atakupa dhamiri iliyosafishwa. (Mithali 21:2) Kwa njia ya roho yake takatifu, Yehova aweza kukuandalia nguvu za kuanza tena pigano dhidi ya udhaifu wa kimwili.—Luka 11:13.

Twahitaji pia nguvu kutoka kwa Yehova tunaposhughulika na hali ya kutokamilika ya wengine. Kwa kielelezo, huenda Mkristo mwenzetu akazungumza nasi “bila kufikiri, kama kuchoma kwa upanga.” (Mithali 12:18) Jambo hili laweza kutuumiza sana, hasa ikiwa latokana na mtu ambaye twahisi apaswa kujua zaidi mwenendo wake ni wenye makosa. Huenda tukasumbuka sana. Watu fulani hata wametumia kukosewa huko kuwa sababu ya kumwacha Yehova—kosa lililo kubwa zaidi ya yote!

Hata hivyo, mtazamo wenye usawaziko utatusaidia kuona udhaifu wa wengine katika njia ifaayo. Hatuwezi kutazamia ukamilifu kutoka kwa wanadamu wasio wakamilifu. “Hakuna mtu asiyetenda dhambi,” Solomoni atukumbusha. (1 Wafalme 8:46) Arthur, Mkristo mtiwa-mafuta aliyemtumikia Yehova kwa uaminifu-mshikamanifu kwa miongo saba, alisema hivi: “Udhaifu katika watumishi wenzetu hutokeza fursa ya kuthibitisha uaminifu-maadili wetu, ukitahini sifa zetu za Kikristo. Tukiruhusu yale ambayo wanadamu husema au hufanya ili yazuie utumishi wetu kwa Yehova, tunatumikia wanadamu. Zaidi ya hayo, ndugu zetu wahitajika kumpenda Yehova pia. Ikiwa twatafuta lililo jema kwao, karibuni tutaona kwamba wao si watu wabaya hivyo.”

Nguvu za Kuhubiri

Kabla hajapaa kwenda mbinguni, Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Mtapokea nguvu wakati roho takatifu iwasilipo juu yenu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu na pia katika Yudea yote na Samaria na hadi sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.”—Matendo 1:8.

Kwa utimizo wa maneno ya Yesu, kazi hii sasa inaendelezwa na Mashahidi wa Yehova katika nchi 233 tufeni lote. Kwa ujumla, wao hutumia zaidi ya saa bilioni moja kila mwaka wakisaidia wengine kupata ujuzi juu ya Yehova. Haiwi rahisi sikuzote kutimiza kazi hii. Katika nchi fulani kazi ya kuhubiri Ufalme imepigwa marufuku au imezuiwa. Fikiria, pia, wanaofanya kazi hiyo—wanadamu dhaifu, wasio wakamilifu, ambao kila mmoja wao ana fungu lake la matatizo na mahangaiko. Hata hivyo, kazi yaendelea, na tokeo ni kwamba, katika miaka mitatu iliyopita, watu zaidi ya milioni moja wameweka maisha yao wakfu kwa Yehova na kuonyesha wakfu wao kwa ubatizo wa maji. (Mathayo 28:18-20) Kwa kweli, kazi hii inatimizwa kwa nguvu za Mungu tu. Yehova alisema kupitia nabii Zekaria hivi: “Si kwa uwezo, wala si kwa nguvu, bali ni kwa roho yangu.”—Zekaria 4:6.

Ikiwa wewe ni mtangazaji wa habari njema, unashiriki—hata iwe yaonekana ni kidogo jinsi gani—katika huo utimizo mtukufu. Bila kujali ‘miiba’ ambayo lazima uvumilie, waweza kuwa na hakika kwamba Yehova hatasahau ‘kazi yako na upendo ulioonyesha kwa ajili ya jina lake.’ (Waebrania 6:10) Hivyo endelea kutegemea Chanzo cha nishati yenye msukumo kwa ajili ya utegemezo. Kumbuka, ni kwa nguvu tu za Yehova kwamba twaweza kuvumilia; nguvu zake hufanywa kamilifu na udhaifu wetu mbalimbali.

[Maelezo ya Chini]

a Bila shaka, kwa kuwa “wote wamefanya dhambi na hupungukiwa na utukufu wa Mungu” ni udhihirisho wa rehema ya Mungu kwamba wanadamu wowote waweza kuingia katika uhusiano pamoja naye kwa vyovyote.—Waroma 3:23.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Kazi ya kuhubiri hutimizwa tu kwa nguvu za Yehova

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki