Biblia Kitabu cha Pekee
Imeitwa kitabu kinachouzwa sana, na imeitwa hivyo kwa kufaa. Biblia husomwa na kutunzwa kwa upendo mkubwa zaidi ya kitabu kingine chochote. Hadi sasa, ugawanyaji wayo (ikiwa nzima au ikiwa sehemu) wakadiriwa kuwa nakala bilioni nne katika lugha zaidi ya 2,000.
Hata hivyo, lenye kupendeza zaidi ya ugawanyaji wa Biblia, ni dai layo kwamba ilitungwa na Mungu. “Andiko lote limepuliziwa na Mungu,” akaandika mtume Mkristo Paulo. (2 Timotheo 3:16) Hilo lamaanisha nini? Fungu la maneno “limepuliziwa na Mungu” (Kigiriki, the·oʹpneu·stos) lamaanisha kihalisi “lenye kuvuviwa na Mungu.” Neno la Kigiriki linalolingana na hilo pneuʹma, lamaanisha “roho.” Kwa sababu hiyo, yadaiwa kwamba roho takatifu ya Mungu ilisukuma waandikaji wa kibinadamu, ikiwavuvia, kwa kusema kitamathali, ili matokeo ya mwisho yaweze kikweli kuitwa Neno la Mungu, wala si la mwanadamu. Kwa kweli, wengi ambao wameisoma Biblia hustaajabia upatano wayo wa ujumla, usahihi wayo wa kisayansi, ufuatiaji wa haki na uwazi wa waandikaji wayo, na lililo la muhimu zaidi ni unabii wayo mbalimbali uliotimizwa—yote hayo yamewathibitishia mamilioni ya wasomaji wenye kufikiri kwamba kitabu hiki chatokana na chanzo kilicho juu zaidi ya mwanadamu.a
Lakini Mungu aliongozaje kwa ukaribu uandikaji wa Biblia? Watu fulani husema kwamba yeye alitamka kila neno katika Biblia ili wengine waandike. Wengine husema kwamba alipulizia tu mawazo yanayopatikana katika Biblia, si maneno. Hata hivyo, kwa kweli, upulizio hauwezi kuwekewa mipaka uwe ulipitia njia moja, kwa maana Mungu alisema “katika njia nyingi na baba zetu wa zamani kwa njia ya manabii.” (Waebrania 1:1; linganisha 1 Wakorintho 12:6.) Katika makala ifuatayo, tutachunguza njia mbalimbali ambazo kwazo Mungu alisema na waandikaji 40 wa kibinadamu walioiandika Biblia.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa habari zaidi, ona ukurasa wa 53-54, na 98-161 katika kitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu?, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.