Je, Maponyo ya Kimuujiza Bado Hutukia?
“MKUBALI Yesu na utaponywa!” Wito mbalimbali kama huo uliongoza Alexandre, mshiriki wa kanisa la Kievanjeli, aamini kwamba kunywa dawa kwa ajili ya ugonjwa wake kungeonyesha ukosefu wa imani. Alisadikishwa kwamba imani yake pekee ingemletea ponyo la kimuujiza alilohitaji. Benedita, Mkatoliki mwenye bidii, aliguswa sana kihisia-moyo aliposikia juu ya miujiza yenye kuponya katika patakatifu pa Aparecida do Norte, katika jimbo la São Paulo, Brazili. Kwa kutumia maneno ya kimuujiza ambayo shangazi yake alikuwa amemfunza, Benedita alisali kwa sanamu ya Our Lady of Aparecida, “Mtakatifu” Anthony, na “watakatifu” wengine ili kupata nguvu ya kuponya wagonjwa.
Yaonekana, hata mwishoni-mwishoni mwa karne ya 20, watu wengi bado huamini maponyo ya kimuujiza—lakini kwa nini? Yamkini, wengine wanavunjika moyo madaktari wanaposhindwa kufanya mengi kutuliza ugonjwa, maumivu, na kuteseka kwa wapendwa wao, hasa watoto wao. Huenda wale wanaosumbuliwa na ugonjwa wa kudumu sana wakahisi kwamba kwa sababu ya gharama za juu za dawa za kisasa, halingekuwa jambo lenye kudhuru wakitafuta uponyaji kwa imani. Wengine huona kwenye televisheni makanisa mbalimbali na watu mmoja-mmoja wakiwatolea maponyo ya UKIMWI, mshuko-moyo, kansa, kichaa, msongo mkubwa wa damu, na magonjwa mengine mengi. Kama wao wana imani yoyote katika madai hayo au la, huenda wakageukia hao likiwa jambo la mwisho. Hata hivyo huenda wengine ambao huamini kwamba ugonjwa wao unasababishwa na roho waovu wakahisi kwamba dawa za kawaida hazina uwezo wa kuwasaidia.
Kwa upande ule mwingine, kuna wale wanaopinga vikali, hata kushutumu, wazo la kuponywa kwa muujiza na “watakatifu” waliokufa au waponyaji walio hai. Kulingana na gazeti la habari la Jornal da Tarde, mtaalamu wa kinga-maradhi Dráusio Varella ahisi kwamba imani katika maponyo ya muujiza “hudhihaki imani ya wasio na hadhari na wenye kukata tumaini.” Yeye aongeza hivi: “Kwa kutumaini miujiza, huenda wengi wakaacha matibabu ya maana ya kitiba kwa sababu ya wadanganyifu hao.” Kichapo The New Encyclopædia Britannica chaeleza hivi: “Maponyo yasiyo ya kawaida yamefungamanishwa na mahali mbalimbali patakatifu na sherehe za ibada za kidini, na sayansi ya kitiba ina mwelekeo wa kuona kwamba utaratibu wa kawaida wa kupumbaza akili ukifanya kazi chini ya hali zifaazo ndio sababu ya maponyo hayo yote.” Hata hivyo, kuna wengi wanaoamini kwamba wao kwa kweli waliponywa kwa muujiza. Kwao, huo uponyaji ulikuwa wenye matokeo!
Wale wanaoijua Biblia wana habari kwamba Yesu Kristo aliponya wagonjwa katika pindi nyingi, akifanya hivi kwa “nguvu ya Mungu.” (Luka 9:42, 43) Hivyo huenda wakauliza hivi, ‘Je, nguvu ya Mungu bado inatenda kazi, na kusababisha maponyo ya kimuujiza leo?’ Ikiwa ndivyo, kwa nini majaribio ya kuponya hushindwa kuleta matokeo yaliyoahidiwa? Je, hilo ni kwa sababu mgonjwa hana imani ya kutosha au upaji wake si mkubwa vya kutosha? Je, ni jambo lifaalo kwa Mkristo kutafuta ponyo la kimuujiza anapougua maradhi yenye maumivu au yasiyoponyeka? Na je, maponyo ya kimuujiza yasiyoshindwa kama yale Yesu aliyofanya yatatokea tena wakati wowote? Waweza kupata majibu kwa maswali haya muhimu katika makala ifuatayo.