‘Yehova Hatawatupa Watu Wake’
“Mateso ya mwenye haki ni mengi, lakini BWANA humponya nayo yote.”—ZABURI 34:19.
1, 2. (a) Yehova anawabarikije watu wake leo? (b) Wakristo wengi wanakabili nini, na ni maswali gani yanayozuka?
KWA kutimiza unabii wa Biblia, waabudu wa Yehova hukaa katika paradiso ya kiroho. (2 Wakorintho 12:1-4) Mashahidi wa Yehova ni ushirika wa kimataifa wenye sifa ya upendo na muungano. (Yohana 13:35) Wana ujuzi wenye kina na wenye kufahamika wa kweli za Biblia. (Isaya 54:13) Wanamshukuru Yehova kama nini kwa sababu anawapa pendeleo la kuwa wageni katika hema lake la kiroho!—Zaburi 15:1.
2 Ingawa wote katika tengenezo la Yehova wana ufanisi wa kiroho, baadhi yao wanaonekana kuwa wanaishi katika amani na utulivu wa kadiri huku wengine wakipatwa na taabu za aina moja au nyingine. Wakristo wengi wanajikuta wakiwa katika hali ya kuombolezeka kwa vipindi virefu vya wakati pasipo kitulizo katika wakati ujao ulio karibu. Ni kawaida kuvunjika moyo chini ya hali hizo. (Mithali 13:12) Je, maafa ni uthibitisho wa kuudhika kwa Mungu? Je, Yehova anaandaa kinga ya pekee kwa Wakristo fulani huku akiwatupa wengine?
3. (a) Je, Yehova analaumika kwa sababu ya majanga yanayowapata watu wake? (b) Kwa nini hata waabudu waaminifu wa Yehova hupatwa na kuteseka kwa kibinadamu?
3 Biblia yajibu hivi: “Wakati yuko chini ya jaribu, acheni yeyote asiseme: ‘Mimi ninajaribiwa na Mungu.’ Kwa maana Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote.” (Yakobo 1:13) Yehova ndiye Mkingaji na Mtegemezaji wa watu wake. (Zaburi 91:2-6) “BWANA hatawatupa watu wake.” (Zaburi 94:14) Hilo halimaanishi kwamba waabudu waaminifu hawatateseka. Mfumo wa mambo uliopo wa ulimwengu unaongozwa na watu ambao si wakamilifu kiasili. Wengi wao ni wafisadi, na wachache kati yao ni waovu kabisa. Hakuna yeyote kati yao ambaye humtegemea Yehova ili kupata hekima. Hilo hutokeza kuteseka kwingi kwa kibinadamu. Biblia hutaarifu waziwazi kwamba watu wa Yehova hawawezi kuepuka sikuzote matokeo ya kutokamilika na uovu wa kibinadamu.—Matendo 14:22.
Wakristo Wenye Uaminifu-Mshikamanifu Hutarajia Kuteseka
4. Wakristo wote wanaweza kutarajia nini maadamu wanaishi katika mfumo huu mwovu wa mambo, na kwa nini?
4 Ingawa wafuasi wa Yesu si sehemu ya ulimwengu, wanaishi katikati ya mfumo huu wa mambo. (Yohana 17:15, 16) Biblia yamfunua Shetani kuwa kani inayotawala ambayo inauongoza ulimwengu huu. (1 Yohana 5:19) Kwa sababu hiyo, Wakristo wote waweza kutarajia kukabili matatizo mazito siku moja. Akikumbuka hilo, mtume Petro asema hivi: “Tunzeni akili zenu, iweni wenye kulinda. Mpinzani wenu, Ibilisi, hutembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta sana kunyafua mtu fulani. Lakini chukueni msimamo wenu dhidi yake, mkiwa thabiti katika imani, mkijua kwamba mambo yaleyale kwa njia ya mateso yanatimizwa katika ushirika mzima wa ndugu zenu katika ulimwengu.” (1 Petro 5:8, 9) Ndiyo, ushirika mzima wa Wakristo waweza kutarajia kuteseka.
5. Yesu alielezaje wazi kwamba Wakristo waaminifu watapatwa na mambo yenye kuhuzunisha maishani?
5 Hata ikiwa twampenda sana Yehova na tu wenye uaminifu-mshikamanifu kwa kanuni zake, tutajionea mambo yenye kuhuzunisha maishani. Yesu alieleza hilo wazi katika kielezi kilichorekodiwa kwenye Mathayo 7:24-27, ambapo alitofautisha wanaotii maneno yake na wasiofanya hivyo. Alilinganisha wanafunzi waaminifu na mtu mwenye busara aliyejenga nyumba yake juu ya tungamo-mwamba lililo thabiti. Wasiotii maneno yake aliwafananisha na mwanamume mpumbavu aliyejenga nyumba yake juu ya mchanga. Baada ya dhoruba kali, nyumba tu iliyojengwa juu ya tungamo-mwamba ndiyo inayosalimika. Ona kwamba katika kisa cha nyumba ya mtu mwenye busara, “mvua i[li]mwagika na mafuriko yakaja na pepo zikavuma na kudunda dhidi ya nyumba hiyo, lakini haikuporomoka.” Yesu hakuahidi kwamba mtu mwenye busara angekuwa na amani na utulivu sikuzote. Badala ya hivyo, busara ya mtu huyo ingemtayarisha kukabili dhoruba. Wazo kama hilo lawasilishwa katika kielezi cha mpanzi. Katika hicho Yesu afafanua kwamba hata waabudu watiifu wenye “moyo ulio bora na mwema” ‘wangezaa matunda kwa uvumilivu.’—Luka 8:4-15.
6. Katika kielelezo cha Paulo cha vifaa visivyoshika moto, ni nani wanaotahiniwa kwa moto?
6 Akiwaandikia Wakorintho, mtume Paulo alitumia usemi wa sitiari ili kutolea kielezi uhitaji wa sifa zenye kudumu ziwezazo kutusaidia kukabili majaribu. Vifaa visivyoshika moto kama dhahabu, fedha, na mawe ya thamani hulingana na sifa za kimungu. (Linganisha Mithali 3:13-15; 1 Petro 1:6, 7.) Kwa upande mwingine, vitabia vya kimwili vyafananishwa na vifaa viwezavyo kuwaka. Kisha Paulo asema hivi: “Kazi ya kila mmoja itakuwa dhahiri, kwa maana ile siku itaifichua, kwa sababu itafunuliwa kwa njia ya moto; na moto wenyewe utathibitisha ni ya namna gani kazi ya kila mmoja. Kazi ya yeyote ambayo ameijenga juu ya huo ikibaki, atapokea thawabu.” (1 Wakorintho 3:10-14) Hapa tena, Biblia yafafanua kwamba sisi sote hatuwezi kuepuka kukabili aina fulani ya mitihani iliyo kama moto.
7. Kulingana na Waroma 15:4, Maandiko yaweza kutusaidiaje kuvumilia majaribu?
7 Kuna masimulizi mengi kwenye Biblia juu ya watumishi wa Mungu wenye uaminifu-mshikamanifu ambao walilazimika kuvumilia maafa, nyakati nyingine kwa vipindi virefu. Hata hivyo, Yehova hakuwatupa. Yamkini mtume Paulo alikumbuka vielelezo hivyo aliposema hivi: “Mambo yote yaliyoandikwa wakati wa mbele yaliandikwa kwa kufunzwa kwetu, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tupate kuwa na tumaini.” (Waroma 15:4) Fikiria kwa uangalifu vielelezo vya watu watatu ambao, wakiwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu, walipatwa na maafa mengi.
Tunayojifunza Kutokana na Masimulizi ya Biblia
8. Yehova aliruhusu nini katika kisa cha Yosefu, na kwa muda gani?
8 Yosefu, Mwana wa Yakobo, alipendelewa na Yehova tangu alipokuwa na umri mdogo. Hata hivyo, alipatwa na mfululizo wa maafa, ingawa halikuwa kosa lake. Alitekwa nyara na kutendwa kinyama na ndugu zake mwenyewe. Aliuzwa akiwa mtumwa katika nchi ya kigeni ambapo alishtakiwa kwa uwongo na kuwekwa “gerezani.” (Mwanzo 40:15) Humo, “walimwumiza miguu yake kwa pingu, akatiwa katika minyororo ya chuma.” (Zaburi 105:17, 18) Wakati wa utumwa wake na kifungo chake, bila shaka Yosefu alimwomba Yehova tena na tena ili apate kuachiliwa. Hata hivyo, kwa miaka 13, ingawa aliimarishwa na Yehova katika njia mbalimbali, aliamka kila asubuhi akiwa angali mtumwa na mfungwa.—Mwanzo 37:2; 41:46.
9. Daudi alilazimika kuvumilia nini kwa miaka kadhaa?
9 Kisa kama hicho ni kile cha Daudi. Yehova alipokuwa akichagua mwanamume mwenye sifa za kustahili kutawala Israeli, alisema hivi: “Nimemwona Daudi mwana wa Yese, mwanamume mwenye kukubalika kwa moyo wangu.” (Matendo 13:22) Ujapokuwa wadhifa wake wenye upendeleo machoni pa Yehova, Daudi aliteseka sana. Katika hatari ya kufa, alijificha miaka kadhaa nyikani, katika mapango, katika mianya, na katika nchi ya kigeni. Akiwindwa kama hayawani-mwitu, alivunjika moyo na kupatwa na hofu. Hata hivyo, alivumilia katika nguvu za Yehova. Daudi angeweza kusema hivi kwa usahihi kutokana na mambo aliyojionea mwenyewe: “Mateso ya mwenye haki ni mengi, lakini BWANA humponya nayo yote.”—Zaburi 34:19.
10. Ni maafa gani ya kupita kiasi yaliyompata Nabothi na familia yake?
10 Katika siku ya nabii Eliya, kulikuwa na watu 7,000 tu katika Israeli ambao hawakuwa wamempigia magoti mungu asiye wa kweli Baali. (1 Wafalme 19:18; Waroma 11:4) Nabothi, ambaye yamkini alikuwa mmoja wao, akawa mhasiriwa wa udhalimu mbaya sana. Alipatwa na aibu ya kushtakiwa makufuru. Akiwa amepatikana kuwa na hatia, alifungwa na kuhukumiwa kwa agizo la mfalme auawe kwa kupigwa mawe, na damu yake ilirambwa na mbwa. Hata wana wake waliuawa! Hata hivyo, hakuwa na hatia ya alilokuwa ameshtakiwa. Mashahidi waliokuwa dhidi yake walikuwa wawongo. Tukio hilo lote lilikuwa njama iliyoanzishwa na Malkia Yezebeli ili mfalme aweze kupata shamba la mizabibu la Nabothi.—1 Wafalme 21:1-19; 2 Wafalme 9:26.
11. Mtume Paulo atuambia nini juu ya wanaume na wanawake waaminifu katika historia ya Biblia?
11 Yosefu, Daudi, na Nabothi ni watatu tu kati ya wanaume na wanawake waaminifu walio wengi wanaotajwa katika Biblia ambao walipatwa na maafa. Mtume Paulo aliandika pitio la kihistoria la watumishi wa Yehova katika enzi zilizopita. Katika hiyo alisema juu ya wale ambao “walipokea jaribu lao kwa dhihaka na mapigo kwa mijeledi, kwa kweli, zaidi ya hilo, kwa vifungo na magereza. Walipigwa kwa mawe, walijaribiwa, walikatwa vipande-vipande kwa msumeno, walikufa kwa kuchinjwa kwa upanga, walienda wakizunguka huku na huku katika ngozi za kondoo, katika ngozi za mbuzi, huku wakiwa katika uhitaji, katika dhiki, chini ya kutendwa vibaya; na ulimwengu haukuwafaa. Walizurura huku na huku katika majangwa na milima na mapango na mashimo ya dunia.” (Waebrania 11:36-38) Lakini Yehova hakuwatupa.
Yehova Huwajali Wanaoteseka
12. Ni zipi baadhi ya taabu wanazopata Mashahidi wa Yehova leo?
12 Namna gani watu wa Yehova leo? Tukiwa tengenezo, twaweza kutegemea kinga ya kimungu na kupita salama katika siku za mwisho na dhiki kubwa. (Isaya 54:17; Ufunuo 7:9-17) Hata hivyo, tukiwa watu mmoja-mmoja, twatambua kwamba “wakati na tukio lisilotazamiwa” huwapata wanadamu wote. (Mhubiri 9:11, NW) Leo kuna Wakristo waaminifu wengi wanaopatwa na maafa. Baadhi yao wanavumilia ufukara. Biblia husema juu ya “mayatima na wajane” Wakristo walio na dhiki. (Yakobo 1:27) Wengine wanateseka kwa sababu ya misiba ya kiasili, vita, uhalifu, matumizi mabaya ya nguvu, ugonjwa, na kifo.
13. Ni mambo gani magumu yaliyoonwa ambayo yameripotiwa karibuni?
13 Kwa kielelezo, katika ripoti zao za mwaka wa 1996 kwa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, ofisi za tawi za Watch Tower zilisimulia kwamba baadhi ya ndugu na dada zetu wamefungwa gerezani katika hali mbaya sana kwa sababu ya kushikamana kwao na kanuni za Biblia. Makutaniko matatu katika nchi ya Amerika Kusini yalivunjwa wakati ambapo vikundi vya wapiganaji wa kuvizia viliwalazimisha mamia ya Mashahidi wahame hilo eneo. Katika nchi fulani ya Afrika Magharibi, Mashahidi kadhaa walionaswa katika mapigano ya vita vya wenyewe kwa wenyewe waliuawa. Katika nchi ya Amerika ya Kati, hali ya kiuchumi ya ndugu zetu ambayo tayari ilikuwa yenye hatari ilifanywa kuwa mbaya zaidi na lile shambulio la kimbunga. Katika mahali pengine ambapo labda umaskini na upungufu wa chakula si matatizo mazito, huenda mavutano hasi yakazima shangwe ya watu fulani. Wengine wanalemewa na misongo ya maisha ya siku ya kisasa. Kwa sababu ya ubaridi wa watu, huenda wengine wakahisi kuvunjika moyo wahubiripo habari njema ya Ufalme.
14. (a) Twajifunza nini kutokana na kielelezo cha Ayubu? (b) Badala ya kufikiri kwa njia hasi, twapaswa kufanya nini tupatwapo na taabu?
14 Hali hizo hazipaswi kueleweka kuwa uthibitisho wa kuudhika kwa Mungu. Kumbuka kisa cha Ayubu na majanga mengi yaliyompata. Alikuwa “mtu mkamilifu na mwelekevu.” (Ayubu 1:8) Lazima Ayubu awe alivunjika moyo kama nini Elifazi alipomshtaki kuwa mwenye kosa! (Ayubu, sura ya 4, 5, 22) Hatutaki kufikia mkataa upesi kwamba twapatwa na maafa kwa kuwa tumemtamausha Yehova kwa njia fulani au kwa sababu Yehova ameondoa baraka yake. Kufikiri kwa njia hasi wakati wa dhiki kungeweza kudhoofisha imani yetu. (1 Wathesalonike 3:1-3, 5) Tupatapo taabu, yafaa zaidi kutafakari juu ya jambo la hakika la kwamba Yehova na Yesu wako karibu na wale walio waadilifu haidhuru kinachotukia.
15. Twajuaje kwamba Yehova anahangaishwa sana na maafa yanayowapata watu wake?
15 Mtume Paulo atutumainisha asemapo hivi: “Nani atakayetutenga na upendo wa Kristo? Je, ni dhiki au taabu au mnyanyaso au njaa au uchi au hatari au upanga? . . . Nasadiki kwamba wala kifo wala uhai wala malaika wala serikali wala mambo yaliyo hapa sasa wala mambo yatakayokuja wala nguvu wala kimo wala kina wala kiumbe kingine chochote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.” (Waroma 8:35, 38, 39) Yehova anatuhangaikia sana naye ajua juu ya kuteseka kwetu. Akiwa angali mtoro, Daudi aliandika hivi: “Macho ya BWANA huwaelekea wenye haki, na masikio yake hukielekea kilio chao. BWANA yu karibu nao waliovunjika moyo.” (Zaburi 34:15, 18; Mathayo 18:6, 14) Baba yetu wa kimbingu hutujali na kusikitikia wanaoteseka. (1 Petro 5:6, 7) Yeye huandaa tunachohitaji ili kuvumilia kuteseka kokote tuwezako kupata.
Zawadi za Yehova Hututegemeza
16. Ni uandalizi gani kutoka kwa Yehova ambao hutusaidia kuvumilia, na jinsi gani?
16 Ingawa hatuwezi kutarajia maisha yasiyo na majanga katika mfumo huu wa kale wa mambo, sisi “hatuachwi kabisa bila msaada.” (2 Wakorintho 4:8, 9) Yesu aliahidi kuandalia wafuasi wake msaidiaji. Alisema hivi: “Nitamwomba Baba naye atawapa nyinyi msaidiaji mwingine awe pamoja nanyi milele, roho ya ile kweli.” (Yohana 14:16, 17) Kwenye Pentekoste 33 W.K., mtume Petro aliwaambia wasikilizaji wake kwamba wangeweza kupokea “zawadi ya bure ya roho takatifu.” (Matendo 2:38) Je, roho takatifu yatusaidia leo? Ndiyo! Kani ya utendaji ya Yehova hutupa matunda ya ajabu: “Upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujidhibiti.” (Wagalatia 5:22, 23) Yote hayo ni sifa zenye thamani kubwa ambazo hutusaidia kuvumilia.
17. Ni zipi baadhi ya kweli za Biblia ambazo huimarisha imani na azimio letu la kumngojea Yehova kwa subira?
17 Roho takatifu pia hutusaidia kuelewa kwamba dhiki zilizopo ni za “dakika na ni nyepesi” zilinganishwapo na thawabu ya uhai udumuo milele. (2 Wakorintho 4:16-18) Twasadikishwa kwamba Mungu hatasahau kazi zetu na upendo tunaomwonyesha. (Waebrania 6:9-12) Tusomapo maneno yaliyopuliziwa ya Biblia, twafarijiwa na vielelezo vya watumishi waaminifu wa kale ambao walivumilia maafa mengi lakini waliotamkwa kuwa wenye furaha. Yakobo aandika hivi: “Akina ndugu, watwaeni kama kiolezo cha kuvumilia uovu na kudhihirisha subira wale manabii, waliosema katika jina la Yehova. Tazameni! Twawatamka kuwa wenye furaha wale ambao wamevumilia.” (Yakobo 5:10, 11) Biblia huahidi “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida” ili kutusaidia kuvumilia majaribu. Yehova pia hutubariki kwa tumaini la ufufuo. (2 Wakorintho 1:8-10; 4:7) Kwa kusoma Biblia kila siku na kutafakari juu ya ahadi hizo, tutaimarisha imani yetu na azimio letu la kumngojea Mungu kwa subira.—Zaburi 42:5.
18. (a) Kwenye 2 Wakorintho 1:3, 4, twatiwa moyo kufanya nini? (b) Waangalizi Wakristo waweza kuthibitikaje kuwa vyanzo vya faraja na burudisho?
18 Kwa kuongezea, Yehova ametupatia paradiso ya kiroho ambamo twaweza kuufurahia upendo wa kweli wa ndugu na dada zetu Wakristo. Sisi sote tuna daraka la kufarijiana. (2 Wakorintho 1:3, 4) Waangalizi Wakristo mahususi waweza kuwa chanzo kikuu cha faraja na burudisho. (Isaya 32:2) Kwa kuwa wao ni “zawadi zikiwa wanadamu,” wana utume wa kujenga wengine wanaoteseka, “[kusema] kwa kuliwaza nafsi zilizoshuka moyo,” na “[kutegemeza] walio dhaifu.” (Waefeso 4:8, 11, 12; 1 Wathesalonike 5:14) Wazee wanatiwa moyo kutumia vizuri magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, na vichapo vingine vilevile vinavyoandaliwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45-47) Hivyo vina mashauri mengi yenye kutegemea Biblia ambayo yaweza kutusaidia kusuluhisha—na hata kuzuia—baadhi ya matatizo yanayotuhangaisha. Na tumwige Yehova kwa kufarijiana na kutiana moyo katika nyakati ngumu!
19. (a) Ni nini hutusaidia kuepuka baadhi ya majanga? (b) Zaidi ya wote, twapaswa kumtumaini nani, na ni nini kitakachotusaidia kukabili majaribu?
19 Tuzidipo kuingia katika siku za mwisho na hali katika mfumo wa mambo uliopo zizidipo kuwa mbaya, Wakristo hufanya yote wawezayo ili kuepuka maafa. (Mithali 22:3) Busara, utimamu wa akili, na ujuzi wa kanuni za Biblia zaweza kutusaidia kufanya maamuzi yenye hekima. (Mithali 3:21, 22) Twasikiliza Neno la Yehova na kulitii ili kuepuka kufanya makosa isivyo lazima. (Zaburi 38:4) Hata hivyo, twang’amua kwamba hakuna kiasi chochote cha jitihada kwa upande wetu kiwezacho kuondosha kuteseka maishani mwetu. Katika mfumo huu wa mambo, watu waadilifu wengi hukabili majanga makali. Hata hivyo, twaweza kukabili majaribu yetu tukiwa na uhakika kamili kwamba “BWANA hatawatupa watu wake.” (Zaburi 94:14) Nasi twajua kwamba mfumo huu wa mambo utatoweka karibuni pamoja na taabu zao. Kwa hiyo, na tuazimie “tusife moyo katika kufanya lililo bora, kwa maana katika majira yapasayo tutavuna ikiwa hatuchoki kabisa.”—Wagalatia 6:9.
Tulijifunza Nini?
◻ Ushirika mzima wa Wakristo hupatwa na majaribu gani?
◻ Ni vielelezo vipi vya Biblia ambavyo hutusaidia kuelewa kwamba maafa si uthibitisho wa kuudhika kwa Yehova?
◻ Yehova anahisije juu ya majanga yanayowapata watu wake?
◻ Ni zipi baadhi ya zawadi kutoka kwa Yehova ambazo hutusaidia kuvumilia majaribu?
[Picha katika ukurasa wa 10]
Daudi, Nabothi, na Yosefu ni watu watatu waliopatwa na maafa