Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 7/1 kur. 27-30
  • Je, Wewe Ni Rafiki ya Mungu?—kinachofunuliwa na sala zako

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Wewe Ni Rafiki ya Mungu?—kinachofunuliwa na sala zako
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kupata Wakati kwa Ajili ya Sala
  • Kuboresha Sala Zetu
  • Faraja na Uelewevu Katika Nyakati za Uhitaji
  • Mkaribie Mungu Katika Sala
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Jinsi Unavyoweza Kumkaribia Mungu
    Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
  • Zawadi ya Sala
    Biblia Inatufundisha Nini?
  • Sala Zako Ni Zenye Kujaa Maana Kadiri Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 7/1 kur. 27-30

Je, Wewe Ni Rafiki ya Mungu?—kinachofunuliwa na sala zako

JE, UMEPATA kutukia kusikia kiakisdenti watu wawili wakizungumza? Bila shaka haikukuchukua muda mrefu kubainisha asili ya uhusiano wao—kama hao walikuwa wasiri au wasiojuana, wajuani tu au marafiki wenye itibari na ukaribu. Katika njia sawa na hiyo, sala zetu zaweza kufunua uhusiano wetu pamoja na Mungu.

Biblia yatuhakikishia kwamba Mungu “hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.” (Matendo 17:27) Kwa kweli, yeye hutualika tumjue. Twaweza hata kuwa rafiki zake. (Zaburi 34:8; Yakobo 2:23) Twaweza kufurahia ukaribu pamoja naye! (Zaburi 25:14) Kwa wazi, uhusiano wetu pamoja na Mungu ndio kitu chenye thamani zaidi ambacho sisi wanadamu tusio wakamilifu tungeweza kuwa nacho. Na Yehova huthamini urafiki wetu. Hilo ni dhahiri kwa sababu urafiki wetu pamoja naye unategemea imani yetu katika Mwana wake mzaliwa-pekee, aliyetoa uhai wake kwa niaba yetu.—Wakolosai 1:19, 20.

Kwa hiyo sala zetu zapaswa kudhihirisha upendo wa kina na uthamini wetu kwa Yehova. Hata hivyo, je, umepata kuhisi kwamba sala zako, ingawa ni zenye kicho, kwa kiasi fulani zinakosa kuhisiwa moyoni? Hilo ni jambo la kawaida. Je, suluhisho ni nini? Kusitawisha urafiki wako pamoja na Yehova Mungu.

Kupata Wakati kwa Ajili ya Sala

Kwanza kabisa, inachukua muda kukuza na kusitawisha urafiki. Huenda ukasalimia au hata kuzungumza na watu wengi kila siku—majirani, wafanyakazi wenzi, madereva wa basi, na makarani wa duka. Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba kwa kweli una urafiki na watu hao. Urafiki hukua unapozungumza kirefu na mtu fulani, ukianza na mazungumzo ya kijuujuu hadi kueleza hisia na mawazo yako ya ndani.

Katika njia sawa na hiyo, sala hutusaidia kumkaribia Yehova. Lakini lazima wakati wa kutosha utengewe jambo hilo; mengi zaidi yahitajiwa kuliko sala fupi ya shukrani wakati wa chakula. Kadiri uzidivyo kuzungumza na Yehova, ndivyo uwezavyo zaidi kuchanganua hisia, nia, na matendo yako mwenyewe. Utatuzi mbalimbali wa matatizo magumu huanza kujidhihirisha wenyewe roho ya Mungu inapokukumbusha kanuni mbalimbali kutoka Neno lake. (Zaburi 143:10; Yohana 14:26) Zaidi, unaposali, Yehova huwa halisi zaidi kwako, na unapata kujua zaidi upendezi na hangaiko lake kwako.

Hilo huwa hivyo hasa unapopata jibu kwa sala zako. Kumbe, Yehova anaweza “kufanya zaidi kwa wingi uzidio kupita mambo yote tuombayo au tuwazayo”! (Waefeso 3:20) Hilo halimaanishi kwamba Mungu hufanya miujiza kwa niaba yako. Hata hivyo, kupitia Neno lake lililoandikwa, vichapo vya jamii ya mtumwa mwaminifu, au vinywa vya ndugu na dada wenye upendo, huenda akakuandalia shauri na mwelekezo unaohitajiwa. Au huenda akakupatia nguvu unazohitaji ili kuvumilia au kukinza kishawishi. (Mathayo 24:45; 2 Timotheo 4:17) Mambo kama hayo yaliyoonwa hujaza mioyo yetu uthamini kwa Rafiki yetu wa kimbingu!

Kwa hiyo mtu lazima atafute wakati kwa ajili ya sala. Ni kweli, muda ni haba wakati huu wa siku zenye mikazo. Lakini unapojali kikweli mtu fulani, kwa kawaida wewe hutafuta wakati wa kuwa pamoja naye. Ona njia ambayo mtunga-zaburi alijieleza mwenyewe: “Kama ayala aioneavyo shauku mito ya maji. Vivyo hivyo nafsi yangu inakuonea shauku, Ee Mungu. Nafsi yangu imemwonea kiu MUNGU, Mungu aliye hai, lini nitakapokuja nionekane mbele za Mungu?” (Zaburi 42:1, 2) Je, wewe una tamaa sawa na hiyo ya kuzungumza na Mungu? Basi nunua kabisa wakati ili ufanye hivyo!—Linganisha Waefeso 5:16.

Kwa kielelezo, huenda ukajaribu kuamka asubuhi na mapema ili kuwa na wakati wa faragha wa kusali. (Zaburi 119:147) Je, nyakati nyingine wewe hukosa usingizi usiku? Basi, kama mtunga-zaburi, waweza kuziona nyakati hizo zenye masumbufu kuwa fursa ya kumweleza Mungu mahangaiko yako. (Zaburi 63:6) Au huenda likawa tu jambo la kutoa sala kadhaa zilizo fupi wakati wa mchana. Mtunga-zaburi alimwambia Mungu hivi: “Nakulilia Wewe mchana kutwa.”—Zaburi 86:3.

Kuboresha Sala Zetu

Nyakati nyingine utalipata kuwa jambo lenye kusaidia kurefusha sala zako. Wakati wa sala fupi, huenda ukaelekea kusema juu ya masuala ya kijuujuu. Lakini unaposema sala ndefu zaidi na zenye kina zaidi, unaeleza mawazo yako na hisi za ndani kwa urahisi zaidi. Angalau mara moja Yesu alitumia usiku wote katika sala. (Luka 6:12) Hakuna shaka kwamba utapata kwamba sala zako mwenyewe zinakuwa zenye ukaribu zaidi na zenye umaana zaidi ukiepuka kuziharakisha.

Hilo halimaanishi uendelee kusemasema bila mpango unapokuwa na machache ya kusema; wala haimaanishi urejee kurudia-rudia kusiko na maana. Yesu alionya hivi: “Lakini mnaposali, msiseme mambo yaleyale tena na tena, kama vile watu wa mataifa hufanya, kwa maana wao huwazia watapata kusikiwa kwa utumizi wao wa maneno mengi. Kwa hiyo, msijifanye wenyewe kama wao, kwa maana Mungu Baba yenu ajua ni vitu gani mnavyohitaji hata kabla nyinyi hamjamwomba.”—Mathayo 6:7, 8.

Sala inakuwa yenye umaana zaidi unapofikiria kimbele yale ambayo wataka kuzungumzia. Yanayowezekana kuzungumzwa ni mengi—shangwe yetu katika huduma, udhaifu wetu mbalimbali na hali zetu za kutokamilika, mivunjiko yetu ya moyo, mahangaiko yetu ya kiuchumi, misongo kazini au shuleni, hali njema ya familia zetu, na hali ya kiroho ya kutaniko la kwetu, kwa kutaja mambo machache tu.

Je, nyakati nyingine akili yako yaelekea kutangatanga unaposali? Basi weka jitihada zaidi katika kukaza fikira. Kwa vyovyote, Yehova yu tayari ‘kutega sikio lake kwa maombi yetu.’ (Zaburi 17:1) Je, haitupasi kuwa tayari kujitahidi kwa bidii kukazia uangalifu sala zetu wenyewe? Ndiyo, ‘weka akili zako juu ya mambo ya roho,’ na ukatae kuiruhusu itangetange.—Waroma 8:5.

Njia tunayosema na Yehova ni muhimu pia. Ingawa yeye hutaka sisi tumwone kuwa rafiki, lazima tusisahau kamwe kwamba tunazungumza na Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote mzima. Soma na utafakari juu ya mandhari yenye kutia kicho inayoonyeshwa kwenye Ufunuo sura ya 4 na ya 5. Hapo Yohana aliona katika ono fahari ya Yeye ambaye sisi humfikia katika sala. Tuna pendeleo lililoje la kuweza kumwendea na kumfikia “Yeye aketiye juu ya hicho kiti cha ufalme”! Hatutaki kamwe lugha yetu iwe yenye kukosa staha kupita kiasi au isiyo na adhama. Badala ya hivyo, twapaswa kujitahidi sana kufanya ‘maneno ya kinywa chetu, na mawazo ya moyo wetu yapate kibali mbele za BWANA.’—Zaburi 19:14.

Hata hivyo, twapaswa kung’amua kwamba hatumvutii Yehova kwa usemi wenye ufasaha. Yeye hupendezwa na maneno yetu yenye staha, ya kuhisiwa moyoni, hata yawe yanasemwa kwa njia rahisi namna gani.—Zaburi 62:8.

Faraja na Uelewevu Katika Nyakati za Uhitaji

Tunapohitaji msaada na faraja, mara nyingi sisi humwendea rafiki wa karibu kwa ajili ya utegemezo na huruma. Bila shaka, hakuna rafiki anayefikika kwa urahisi zaidi kuliko Yehova. Yeye ni “msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso.” (Zaburi 46:1) Akiwa “Mungu wa faraja yote,” yeye huelewa yale tunayovumilia vizuri zaidi ya mtu mwingine yeyote. (2 Wakorintho 1:3, 4; Zaburi 5:1; 31:7) Naye ana hisia-mwenzi na huruma kwa ajili ya wale walio katika hali zenye kukatisha tamaa. (Isaya 63:9; Luka 1:77, 78) Kwa kumtambua Yehova kuwa rafiki mwenye uelewevu, twajihisi huru kuzungumza naye kwa bidii, kwa hisi zenye kina. Tunasukumwa kusema hofu na mahangaiko yetu yenye kina zaidi. Hivyo sisi hupata kuona moja kwa moja jinsi ‘faraja zake Yehova hufurahisha roho zetu.’—Zaburi 94:18, 19.

Huenda nyakati nyingine tukajihisi wasiofaa kumfikia Mungu kwa sababu ya makosa yetu. Lakini vipi ikiwa rafiki yako alikukosea na kukuomba msamaha? Je, ungesukumwa kumliwaza na kumtuliza mtu huyo? Kwa nini, basi, tusitarajie kwamba Yehova atafanya vivyo hivyo? Yeye husamehe kwa wingi rafiki zake wanaofanya dhambi kwa sababu ya hali ya kutokamilika. (Zaburi 86:5; 103:3, 8-11) Tukijua hilo, hatusiti kuungama kwa uhuru dhambi zetu kwake; twaweza kuwa na uhakika juu ya upendo na rehema yake. (Zaburi 51:17) Ikiwa tumeshuka moyo kwa sababu ya kasoro zetu, twaweza kufarijiwa na maneno ya 1 Yohana 3:19, 20: “Kwa hili tutajua kwamba twatokana na kweli, na tutahakikishia mioyo yetu mbele yake kwa habari ya chochote kile ambacho mioyo yetu huenda ikatulaumu katika hicho, kwa sababu Mungu ni mkubwa zaidi kuliko mioyo yetu na ajua mambo yote.”

Hata hivyo, hatuhitaji kuwa katika hali ngumu, ili kufurahia hangaiko la Mungu lenye upendo. Yehova hupendezwa na chochote kiwezacho kuathiri hali njema yetu ya kiroho na ya kihisia-moyo. Ndiyo, hatuhitaji kamwe kufikiri kwamba hisia zetu, mawazo yetu, na mahangaiko yetu ni yasiyo ya maana sana yasiweze kutajwa katika sala. (Wafilipi 4:6) Unapokuwa na rafiki wa karibu, je, nyinyi huzungumza juu ya matukio makuu tu maishani mwenu? Je, hamshiriki pia mahangaiko madogo kwa kadiri? Katika njia sawa na hiyo, waweza kujihisi huru kuzungumza juu ya sehemu yoyote ya maisha yako pamoja na Yehova, ukijua kwamba ‘yeye hukujali wewe.’—1 Petro 5:7.

Bila shaka, yaelekea urafiki hautadumu muda mrefu ikiwa yote unayozungumza ni juu yako mwenyewe. Hali kadhalika, sala zetu hazipaswi kuwa zenye ubinafsi. Twapaswa kutaja pia upendo wetu na hangaiko letu kwa Yehova na mapendezi yake. (Mathayo 6:9, 10) Sala si fursa ya kuomba msaada kutoka kwa Mungu tu bali pia ni nafasi ya kutoa shukrani na sifa. (Zaburi 34:1; 95:2) “Kuendelea kutwaa ujuzi” kupitia funzo la kawaida la kibinafsi kutatusaidia katika jambo hilo, kwa kuwa hilo hutusaidia kufahamiana zaidi na Yehova na njia zake. (Yohana 17:3) Huenda ukapata kwamba ni jambo lenye kusaidia hasa kusoma kitabu cha Zaburi na kuona jinsi watumishi wengine waaminifu walivyojieleza wenyewe kwa Yehova.

Urafiki wa Yehova kwa kweli ni zawadi yenye thamani. Na tuonyeshe kwamba tunauthamini kwa kufanya sala zetu ziwe za ukaribu, zenye kuhisiwa moyoni, na za kibinafsi hata zaidi. Ndipo tutakaposhiriki furaha iliyoonyeshwa na mtunga-zaburi, aliyetangaza hivi: “Heri mtu yule umchaguaye, na kumkaribisha.”—Zaburi 65:4.

[Picha katika ukurasa wa 28]

Twaweza kusali kwa Mungu mchana kutwa fursa inapotokea

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki