Wapiga-Mbiu wa Ufalme Waripoti
Kuachana na Uvutano wa Roho Waovu
ZOEA la uwasiliani-roho limetawala maisha ya mamilioni ya watu. Lakini inawezekana kuachana nalo! Hilo ndilo lililotukia kwa wengi katika mji wa kale wa Efeso. Kulingana na maelezo ya Biblia, “idadi kubwa ya wale waliozoea kufanya ufundi wa kimzungu wakaleta pamoja vitabu vyao wakavichoma kabisa . . . Hivyo katika njia yenye uweza neno la Yehova likafuliza kukua na kuweza.”—Matendo 19:19, 20.
Hali kadhalika kutaniko la Kikristo leo linapata ukuzi. Kama ilivyokuwa katika Efeso, miongoni mwa wale wanaokuwa waamini ni wale ambao awali walizoea kuabudu roho waovu. Jambo hili lililoonwa kutoka Zimbabwe latoa kielezi.
Gogo (nyanya) Mthupha alijulikana sana kwa sababu ya nguvu zake za roho waovu. Watu walitoka sehemu za mbali kama vile Zambia, Botswana, na Afrika Kusini ili awatibu kwa kutumia dawa za miti shamba. Gogo Mthupha pia alifundisha wengine jinsi ya kuwa n’anga, au mganga. Na nyakati nyingine alikuwa akiroga!
Jumapili moja asubuhi Gogo Mthupha alitembelewa na Mashahidi wa Yehova ambao walikuwa katika huduma ya nyumba hadi nyumba. Alifurahia sana mazungumzo pamoja nao kuhusu ahadi ya Biblia ya ulimwengu mpya wenye uadilifu, ulimwengu usio na uvutano wowote mwovu. Alipokea kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniania na alikubali kuwa na funzo la Biblia nyumbani. Baada ya kujifunza mara tatu tu, alianza kuhudhuria mikutano.
Kupitia funzo lake la Biblia, Gogo Mthupha alijifunza kwamba nguvu zake za kipekee zilitoka kwa viumbe walio roho waovu ambao walikuwa wameasi dhidi ya enzi kuu ya Yehova. (2 Petro 2:4; Yuda 6) Pia alijifunza kwamba hawa roho waovu wanaazimia kugeuza kila mtu wanayeweza dhidi ya Yehova na dhidi ya ibada safi. Kwa vile maisha yake yalitegemea kufanya mizungu pamoja na hivi viumbe walio roho waovu, angefanya nini?
Gogo Mthupha alieleza tamaa yake ya kuachana kabisa na hirizi na vitu vingine vya kibinafsi vya kiuchawi. Hivi vilitia ndani kilemba chake maalumu na “pembe ya fahali inayoongea,” ambayo aliitumia katika uponyaji wake wa n’anga. Gogo Mthupha alitaka kuachana kabisa na vitu vyote kama hivyo ili aweze kumtumikia Mungu wa pekee anayeishi, Yehova.
Lakini baadhi ya jamaa zake walipinga kwa sababu alikuwa akiwategemeza kifedha. Walimsihi awape vitu hivyo, pamoja na nguvu zake zisizo za kawaida ili kwamba waweze kuendelea kujifaidi. Gogo Mthupha alikataa.
Kupitia msaada wa kutaniko la mahali hapo la Mashahidi wa Yehova, alikusanya mifuko mitatu mikubwa ya vitu vyote vya kuwasiliana na roho waovu na kuvichoma vyote. Moto ulipokuwa ukivichoma vitu vyake vya ibada ya roho waovu, Gogo Mthupha alisema kwa mkazo: “Angalia! Ile pembe, haiwezi kujiokoa.”
Baadaye, Gogo Mthupha alifananisha wakfu wake kwa Yehova kwa ubatizo wa maji. Sasa anajipatiaje riziki? Kwa kuuza mboga. Ndiyo, kupitia nguvu za Neno la Mungu, mtu aweza kuachana na ibada ya roho waovu. Asema Gogo Mthupha: “Sijapata kamwe kuhisi nikiwa huru namna hii.”
[Maelezo ya Chini]
a Huchapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.y