Ripoti ya Watangazaji wa Ufalme
Ukweli wa Biblia Unaweka Huru na Uwasilianaji na Ulimwengu wa Roho
MAONI ya Yehova juu ya kuwasiliana na ulimwengu wa roho yalielezwa wazi kwa Israeli kwa maneno haya: “Haiwapasi kamwe kutafuta viashirio vya matukio ya wakati ujao, na haiwapasi ninyi kamwe kuzoea miujiza-uchawi.” (Walawi 19:26, NW) Lakini mtu anayehusika katika miujiza-uchawi na uwasilianaji na ulimwengu wa roho anaweza kukombolewaje kutoka uwezo wa mashetani? Yesu alisema: “Mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.” (Yohana 8:32) Jambo hilo lilithibitishwa kuwa kweli, kama linavyoonwa katika kituko kifuatacho cha Shahidi mmoja katika Ufaransa.
“Nilipohamia kao langu jipya, nilikuwa ndiyo sasa tu nimeanza kutulia wakati jirani mwenye urafiki alipokuja akajitolea kunitabiria nyota yangu. Bila kukawia niliamua nisiwe tena na uhusiano pamoja na mwanamke huyo. Hiyo haikuwa shughuli ndogo kwa maana yeye alikuwa mtu mwenye maumbile ya urafiki sana.
“Katika Novemba 1980 nikawa mgonjwa, naye akaja kunisaidia. Nilikuja kuthamini kwamba alikuwa na moyo wenye fadhili. Nilivutwa zaidi kwake aliponieleza siri ya kwamba angeamka mara kwa mara akiwa na maumivu makali kutokana na kukabwa koo. Ndipo nilipotambua kwamba hakuwa mwenye furaha kama nilivyokuwa nimewazia. Lakini tatizo hili la kuwasiliana na ulimwengu wa roho lingeweza kushughulikiwaje? Kwa kuhisi kwamba singeweza tena kungojea, nikaazimia kusema naye juu ya ukweli.
“Tulianza kwa kuzungumzia matatizo ya kipesa yaliyo mageni kwetu wanawake waseja. Ndipo yeye akasema: ‘Mimi nina utatuzi. Ninachuma pesa kwa kusoma kadi za utabiri.’ Kwa hiyo nikatoa Biblia yangu na kumwonyesha jinsi ilivyo hatari kuhusika na kani mbovu zenye nguvu nyingi.
“Jambo hilo lilianzisha zungumzo zito juu ya kuwasiliana na ulimwengu wa roho. Yeye alieleza kwamba kila jambo alilotabiri lilitukia. Nikajaribu kumsaidia afikirie mambo kwa kuona sababu zayo. Nikaendelea kumwonyesha maneno ya Musa kwenye Kumbukumbu 18:10, 11: ‘Hakupasi kupatikana katika wewe mtu ye yote . . . anayetumia uaguzi, mzoeaji wa miujiza-uchawi au mtu ye yote anayetafuta viashirio vya matukio ya wakati ujao . . . au mtu ye yote anayeomba habari kutoka kwa chombo cha kuwasiliana na ulimwengu wa roho au mtaalamu wa kutabiri matukio au mtu ye yote anayeomba apewe habari juu ya wafu.’ Nilipokuwa nikiondoka, yeye alisema: ‘Lo, ni ajabu kwamba nimepata utatuzi kwa matatizo yangu.’ Maneno hayo yalinitia moyo kama nini, kwa maana baada ya zungumzo moja tu, alikuwa sasa akiutaja uwasilianaji na ulimwengu wa roho kama jambo la zamani! Kwangu mimi ilimaanisha kwamba alikuwa ameishika maana ya jambo lile kwa ndani sana.
“Kwa sababu ya kuwa na hamu isiyotosheleka ya chakula cha kiroho, akawa akisoma Biblia mpaka saa tisa au kumi ya asubuhi. Kwanza, tulijifunza mara mbili kwa juma. Yeye alihudhuria mikutano na akafanya maendeleo ya haraka sana. Bila shaka, tulipekua sana habari ya kuwasiliana na ulimwengu wa roho, kwa kutumia Biblia na vichapo vya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi, naye akafanya uamuzi wa kibinafsi kuchoma kila kitu alichokuwa nacho chenye uhusiano na ushetani.
“Bibi huyo alivumilia na baada ya muda mfupi akawa nje akiwahubiri wengine ‘habari njema.’ Mara kwa mara alipokea simu kutoka kwa waliokuwa wateja wake, na baada ya kuwaeleza kwamba ameacha utendaji wake wa kuwasiliana na ulimwengu wa roho, akawaalika waje kusikia juu ya jambo lenye kupendeza zaidi ya hilo. Alibatizwa na sasa ni dada yetu.”