Maisha Ambayo Sikuyajutia Kamwe
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA PAUL OBRIST
Katika 1912, nilipokuwa na umri wa miaka sita, mama yangu alikufa alipokuwa akimzaa mtoto wake wa tano. Karibu miaka miwili baadaye, mtunza-nyumba kijana Berta Weibel, alianza kutunza familia yetu. Mwaka uliofuata baba alipomwoa, sisi watoto tulifurahi kuwa na mama tena.
TULIISHI Brugg, mji mdogo katika sehemu ya Uswisi inayozungumza Kijerumani. Berta alikuwa Mkristo kwa kweli, na nilimpenda sana. Alikuwa ameanza kusoma vichapo vya Wanafunzi wa Biblia (Mashahidi wa Yehova) katika 1908, na angeshiriki na wengine yale aliyojifunza.
Katika 1915, muda mfupi baada ya Berta na baba kuoana, nilikwenda pamoja naye katika wonyesho wa “Photo-Drama of Creation.” Wonyesho huo wa slaidi na sinema wa Sosaiti ya Kimataifa ya Wanafunzi wa Biblia Wenye Bidii uliacha wazo lenye kudumu katika akili na moyo wangu. Watu wengine waliohudhuria walivutiwa pia. Ukumbi katika Brugg ulijaa sana kiasi cha kwamba polisi walifunga milango na waliwazuia waliofika baadaye. Kisha wengi walijitahidi kuingia kwa kupitia dirisha lililokuwa wazi kwa kutumia ngazi, na wachache walifanikiwa.
Kielelezo Chema cha Mama
Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilikuwa ikipiganwa katika Ulaya, na watu walikuwa wenye hofu kuhusu wakati ujao. Hivyo, kuhubiri kutoka nyumba hadi nyumba ukiwa na ujumbe wenye kufariji wa Ufalme wa Mungu, kama vile mama yangu wa kambo alivyofanya, lilikuwa jambo gumu sana. Wakati fulani aliniruhusu niandamane naye, na nilifurahia hili sana. Hatimaye, katika 1918, mama aliweza kufananisha wakfu wake kwa Yehova Mungu kwa ubatizo wa maji.
Baba hakuingilia ibada ya mama hadi ubatizo wake, lakini baada ya hapo alianza kumpinga. Siku moja alichukua fasihi zake za Biblia na kuzitupa katika stovu. Mama aliweza kuokoa Biblia yake tu kutoka katika huo moto. Lakini, alilofanya baada ya hapo lilikuwa la kushangaza. Alimwendea baba na kumkumbatia. Hakumwekea kinyongo hata kidogo.
Akiwa ameshangazwa kabisa, baba akatulia. Lakini, mara kwa mara, upinzani wake ulilipuka, nasi tukalazimika kuvumilia mifoko yake ya hasira.
Kazi ya Kuajiriwa na Maendeleo ya Kiroho
Katika 1924, baada ya kumaliza miaka mitatu ya kujifunza kazi nikiwa mtengeneza nywele, niliondoka nyumbani na kupata kazi ya kuajiriwa katika sehemu ya Uswisi inayozungumza Kifaransa. Hii iliandaa fursa ya kuboresha ujuzi wangu wa lugha ya Kifaransa. Ingawa kuhama huko kulizuia maendeleo yangu ya kiroho kwa kiasi fulani, sikupoteza kamwe upendo wangu wa kweli ya Biblia. Hivyo niliporudi nyumbani miaka sita baadaye, nilianza kuhudhuria mikutano ya kutaniko la Kikristo katika Brugg.
Muda mfupi baadaye nilihamia Rheinfelden, mji mdogo ulio umbali wa kilometa 40. Nilifanya kazi hapo katika duka la kutengeneza nywele la dada yangu mkubwa na kuendelea kufanya maendeleo ya kiroho kwa kuhudhuria mikutano na kikundi kidogo cha Wanafunzi wa Biblia. Siku moja wakati wa kumalizia funzo la Biblia la katikati ya juma, Ndugu Soder, mzee msimamizi aliuliza: “Nani apanga kushiriki katika huduma ya shambani siku ya Jumapili?” Nilijitolea, nikidhania kwamba ningeambatana na mtu fulani na kuonyeshwa jinsi ya kufanya hiyo kazi.
Jumapili ilipofika na tukafika eneo letu, Ndugu Soder alisema, “Bw. Obrist atafanya pale.” Ingawa moyo wangu ulidunda zaidi kuliko wakati mwingine wowote, nilianza kuwatembelea watu katika nyumba zao na kuongea nao kuhusu Ufalme wa Mungu. (Matendo 20:20) Kutoka wakati huo na kuendelea, sikurudi nyuma kamwe katika kazi ya kuhubiri ambayo Yesu alisema inapasa kumalizwa kabla ya mwisho wa mfumo huu wa mambo kuja. (Mathayo 24:14) Machi 4, 1934, nilipokuwa na umri wa miaka 28, nilifananisha wakfu wangu kwa Yehova Mungu kwa ubatizo wa maji.
Miaka miwili baadaye nilipata kazi nikiwa mtengeneza nywele katika Lugano, jiji lililo katika sehemu ya Uswisi inayozungumza Kiitalia. Ingawa nilijua Kiitalia kidogo sana, mara moja nilianza kuhubiri habari njema hapo. Hata hivyo, wakati wa Jumapili yangu ya kwanza katika huduma, niliangusha vijitabu 20 ambavyo nilikuwa navyo. Baadaye, nilifanikiwa kukusanya watu wachache waliopendezwa kuunda kikundi ili kujifunza Mnara wa Mlinzi. Hatimaye kadhaa kati yao walibatizwa, na katika Februari 1937 tulianzisha kutaniko la Mashahidi wa Yehova katika Lugano.
Miezi miwili baadaye, katika Aprili 1937, nilipokea barua ambayo ilibadili kabisa maisha yangu. Ulikuwa mwaliko wa kutumikia Betheli, kama ambavyo ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova katika nchi zinavyoitwa. Mara moja nikaukubali huo mwaliko—uamuzi ambao sikuujutia kamwe. Hivyo nilianza kile ambacho kimekuwa kazi-maisha ya miaka 60 katika huduma ya wakati wote.
Utumishi wa Betheli Katika Nyakati za Matatizo
Wakati huo Betheli ya Uswisi ilikuwa katika jiji la Bern, jiji kuu la Uswisi. Hapo tulichapa vitabu, vijitabu, na magazeti katika lugha 14, na hivi vilisafirishwa katika Ulaya yote. Nyakati fulani-fulani, kwa kutumia toroli, nilipeleka kwenye stesheni ya garimoshi fasihi zilizochapwa, kwani katika siku hizo hatukuwa na gari la mizigo. Mgawo wangu wa kwanza Betheli ulikuwa katika Idara ya Kupanga Herufi za Chapa ambapo tulikusanya herufi za risasi zilizotumiwa katika uchapishaji. Baada ya muda mfupi nilianza kufanya kazi katika dawati la mapokezi, na bila shaka, nilitumikia pia nikiwa kinyozi wa familia ya Betheli.
Katika Septemba 1939, Vita ya Ulimwengu ya Pili ililipuka, na mashambulio makali ya Nazi yalieneza hofu kuu katika Ulaya yote. Uswisi ilikuwa nchi isiyokuwamo ikiwa katikati ya mataifa yenye kupigana. Mwanzoni, tuliendelea na kazi yetu ya Kikristo bila ya kuingiliwa. Kisha katika Julai 5, 1940, saa nane adhuhuri, nilipokuwa katika dawati langu katika ukumbi, raia mmoja aliingia, akifuatana na askari-jeshi aliyebeba bunduki iliyo na singe.
“Yuko wapi Zürcher?” yule raia akauliza kwa ukali. Wakati huo Franz Zürcher alikuwa mwangalizi wa tawi wa kazi yetu ya kuhubiri katika Uswisi.
“Nimwambie nani anamwita?” nikauliza. Walininyakua mara moja na kuniburuta juu ya ngazi, wakidai kwamba niwapeleke kwenye ofisi ya Zürcher.
Familia yote ya Betheli—wakati huo tulikuwa karibu 40—iliamuriwa ikusanyike katika chumba cha chakula. Bombomu nne ziliwekwa nje ya jengo ili kuzuia mtu yeyote asijaribu kutoroka. Ndani, karibu askari-jeshi 50 walianza kulipekua jengo. Kinyume cha matarajio, hakuna ushahidi uliopatikana kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa wakijishughulisha na kuendeleza upinzani dhidi ya utumishi wa kijeshi. Hata hivyo, kiasi kikubwa cha fasihi kilitwaliwa na kuchukuliwa na malori matano ya kijeshi.
Tulipokataa kuruhusu Mnara wa Mlinzi kuchujwa na mamlaka za kiserikali, uchapishaji walo ulizuiwa katika Uswisi. Hii ilimaanisha kwamba watu wachache walihitajika kwa kazi katika Betheli, na washiriki wachanga wa familia walitiwa moyo kuondoka na kuwa mapainia, kama ambavyo Mashahidi wa Yehova ambao hushiriki katika kazi ya kuhubiri wakati wote wanavyoitwa.
Kupainia Wakati wa Vita
Katika Julai 1940, nilirudi katika sehemu ya Uswisi inayozungumza Kiitalia karibu na Lugano, ambapo niliishi kabla ya kuja Betheli. Eneo hili lililodhibitiwa sana na Ukatoliki, ambalo wakati huo lilikuwa pia chini ya uvutano mkubwa wa Ufashisti, likawa mgawo wangu wa upainia.
Karibu kila siku nilisimamishwa na polisi ambao walidai kwamba niache kazi yangu ya kuhubiri. Siku moja nilipokuwa nikiongea na mwanamke mmoja kwenye lango la bustani, mwanamume mmoja akiwa na mavazi ya kiraia alinishika kutoka nyuma, akaniongoza hadi gari la doria, akanipeleka Lugano. Hapo alinikabidhi kwa polisi. Nilipoulizwa maswali, nilieleza kwamba Yehova Mungu alikuwa ametuamuru tuhubiri.
“Hapa duniani, ni sisi tunaoamuru,” huyo ofisa akajibu kwa kiburi. “Mungu aweza kuamuru mbinguni!”
Wakati wa vita, ilikuwa muhimu hasa kwamba tutii shauri la Yesu la kuwa “wenye hadhari kama nyoka na bado kuwa wasio na hatia kama njiwa.” (Mathayo 10:16) Hivyo, nilificha karibu vitabu vyangu vyote katika mifuko ya ndani ya shati langu. Na ili kuhakikisha kwamba sipotezi chochote, nilivaa kaboka ambazo zilibana sana chini ya magoti.
Baadaye, nilipata maagizo nihamie bonde la Engadine, ambapo mchezo wa paka na panya uliendelea pamoja na polisi. Hili ni bonde lenye kuvutia sana mashariki mwa milima ya Alps ya Uswisi, ambapo wakati wa kipupwe hufunikwa chini ya matungamano ya theluji, hivyo niliomba nipelekewe skii zangu ili niweze kusafiri katika eneo hilo.
Glavu za kuzuia baridi ni muhimu sana wakati wa kusafiri kwa skii wakati wa majira ya baridi kali. Kwa sababu ya kutumika sikuzote, upesi glavu zangu zilianza kuchakaa. Nilikuwa mwenye shukrani kama nini siku moja kupokea kifurushi ambacho sikutarajia kilichotumwa kwa posta chenye sweta iliyofumwa kwa mkono na pia glavu za kuzuia baridi! Dada mmoja wa Kikristo katika kutaniko langu la zamani la Bern alikuwa amenitengenezea. Hata sasa nifikiriapo kukihusu, mimi hushukuru sana.
Mapendeleo Mengi ya Shangwe
Katika 1943, hali katika Uswisi ilianza kuwa nzuri, na niliitwa tena kutumikia Betheli. Kwa sababu ya matatizo fulani katika kutaniko linalozungumza Kifaransa katika Lausanne, umbali wa kilometa 100 hivi, nilipewa mgawo wa kutembelea mji huo kwa ukawaida ili kusaidia watangazaji kupata maoni sahihi ya tengenezo la Mungu.
Baadaye nilitumika kwa muda fulani nikiwa mwangalizi wa mzunguko kwa makutaniko yote ya Kifaransa katika Uswisi. Mwanzoni katika juma nilifanya kazi Betheli, lakini nilitumia Ijumaa, Jumamosi, na Jumapili kutembelea makutaniko tofauti-tofauti kila juma katika jitihada za kusaidia kiroho. Kwa kuongezea, wakati kutaniko linalozungumza Kifaransa lilipoanzishwa katika Bern mwaka 1960, nilikuwa mwangalizi-msimamizi walo. Nilitumikia wadhifa huo hadi 1970, wakati Betheli ilipohamishwa kutoka Bern hadi sehemu nzuri sana ilipo kwa sasa katika mji wa Thun.
Katika Thun nilifurahi kupata kikundi kidogo cha Mashahidi kilichozungumza Kiitalia, na nilianza kufanya kazi pamoja nacho. Baadaye kutaniko lilianzishwa, na nilitumikia nikiwa mwangalizi-msimamizi kwa miaka kadhaa hadi ndugu vijana wakawa na sifa zenye kustahili kubeba daraka hilo.
Kile nimeona kimahususi kuwa pendeleo la shangwe ni kuhudhuria makusanyiko ya kimataifa ya watu wa Yehova. Kwa kielelezo, katika 1950, kulikuwa na lile Kusanyiko la Ongezeko la Kitheokrasi lenye kukumbukwa sana katika Yankee Stadium, New York. Kutembelea makao makuu ya Mashahidi wa Yehova katika Brooklyn, New York, kuliacha wazo la kudumu kwangu. Pia sitasahau kamwe hotuba ya Ndugu Milton G. Henschel mwaka uliofuata katika Kusanyiko la Ibada Safi katika London, Uingereza, ambalo lilikazia maneno ya Yesu, “Mimi nawaambia nyinyi, Kama hawa wangekaa kimya, mawe yangepaaza kilio.” (Luka 19:40) Ndugu Henschel aliuliza, “Je, mwafikiri mawe yatapaswa kupaaza kilio?” Bado ninaweza kusikia katika masikio yangu mngurumo, “Hapana!” ambao ulitoka kwa makumi ya maelfu ya sauti.
Niliporudi Betheli katika 1937, baba yangu, ambaye alijua kwamba sisi hupokea posho kidogo tu, kwa hofu aliuliza, “Mwana, utaishije katika umri wa uzee?” Nilijibu kwa kunukuu maneno ya mtunga-zaburi Daudi: “Sijamwona mwenye haki ameachwa wala mzao wake akiomba chakula.” (Zaburi 37:25) Katika kisa changu, maneno hayo yametimia bila shaka.
Mimi ni mwenye shukrani kama nini kwamba zaidi ya miaka 80 iliyopita, Berta Weibel aliolewa na baba yangu na kwamba kupitia kielelezo chake na uongozi wake nilikuja kumjua Yehova na sifa zake! Ingawa washiriki wengine wa familia walimdhihaki, kwa uaminifu alimtumikia Yehova hadi wakati wa kifo chake katika 1983. Hakujuta kamwe kumtumikia Mungu wake, Yehova; wala sikupata kujuta kamwe kubaki mseja na kutoa maisha yangu yote katika utumishi wa Yehova.
[Picha katika ukurasa wa 25]
Nikifanya kazi Betheli