Jinsi Biblia Ilivyotufikia—Sehemu ya Kwanza
Sehemu ya 2 na ya 3 zitatokea katika toleo la Septemba 15 na la Oktoba 15.
NDANI ya karakana ndogo, mchapaji na wanagenzi wake vijana wafanya kazi kwa kufuatana wakitumia matbaa yao yenye fremu ya mbao, wakiwekelea kwa uangalifu karatasi zisizoandikwa kitu juu ya herufi za kupigia chapa. Watoapo kurasa hizo, wanachunguza maandishi yaliyochapwa. Wanaanika kurasa zilizokunjwa kwenye nyuzi zilizofungwa toka ukuta mmoja hadi mwingine, ili zikauke.
Kwa ghafula, mlango wagongwa kwa ujeuri. Wakiwa wameshtushwa kwa hofu, mchapaji aufungua mlango, na kikosi cha askari wenye silaha chaingia ghafula na kwa vishindo. Wanaanza kupekua aina ya fasihi isiyo halali ambayo yashutumiwa zaidi—Biblia katika lugha ya watu wa kawaida!
Wamechelewa sana. Wakiwa wameonywa juu ya hiyo hatari, mtafsiri na msaidizi mmoja tayari wamepiga mbio hadi kwenye karakana, wakachukua kurasa nyingi mkononi, nao sasa watorokea upande wa juu wa Mto Rhine. Angalau wameokoa sehemu ya kazi yao.
Mtafsiri huyo alikuwa William Tyndale, aliyekuwa Cologne, Ujerumani, mwaka wa 1525, akijaribu kutokeza “Agano [lake] Jipya” la Kiingereza lililopigwa marufuku. Jambo lililompata likawa la kawaida sana. Kotekote katika ile miaka ipatayo 1,900 tangu kumalizika kwa kuandikwa kwa Biblia, wanaume na wanawake wengi wamehatarisha kila kitu ili walitafsiri na kuligawanya Neno la Mungu. Sisi leo tungali twanufaishwa na kazi yao. Walifanya nini? Biblia tulizo nazo mikononi mwetu sasa zilitufikiaje?
Kunakiliwa na Kutafsiriwa kwa Biblia kwa Mapema
Sikuzote watumishi wa kweli wa Mungu wameliona Neno lake kuwa lenye kuheshimika sana. Kichapo New Catholic Encyclopedia chakiri hivi: “Sawa na mababu zao Wayahudi, Wakristo wa mapema walithamini kusoma Vitabu Vitakatifu. Wakifuatia kielelezo cha Yesu (Mt 4.4; 5.18; Lu 24.44; Yn 5.39), Mitume walizoelea A[gano] la K[ale] jambo ambalo lilidokeza kusoma na kujifunza kulikorefushwa na kwa makini, nao waliwahimiza sana wanafunzi juu ya hilo (Rom 15.4; 2 Tm 3.15-17).”
Ilikuwa lazima nakala za Biblia zifanyizwe kwa kusudi hilo. Katika nyakati za kabla ya Ukristo, sehemu kubwa ya kazi hiyo ilifanywa na ‘wanakiliji stadi’ waliokuwa wataalamu sana ambao walihofu kufanya makosa. (Ezra 7:6, 11, 12, NW) Wakijitahidi kutokeza nakala kamilifu, waliwekea wanakiliji wote wa Biblia wa baadaye kiwango cha juu.
Hata hivyo, katika karne ya nne K.W.K., tatizo lilizuka. Aleksanda Mkubwa alitaka watu wote wa ulimwengu waelimishwe utamaduni wa Kigiriki. Ushindi wake mbalimbali ulithibitisha Kigiriki cha kawaida, au Kikoine, kuwa lugha iliyotumika kotekote katika Mashariki ya Kati. Tokeo ni kwamba, Wayahudi wengi walikua bila kujifunza kusoma Kiebrania na kwa hiyo hawakuweza kusoma Maandiko. Kwa hiyo, wapata mwaka wa 280 K.W.K., kikundi cha wasomi Waebrania kilikusanyika Aleksandria, Misri, ili kutafsiri Biblia ya Kiebrania katika lugha ya watu wengi ya Kikoine. Tafsiri yao ikaja kujulikana kuwa Septuagint, neno la Kilatini linalomaanisha “Sabini,” likirejezea idadi takriban ya watafsiri walioaminika kuwa walihusika. Ilimalizwa wapata mwaka wa 150 K.W.K.
Wakati wa Yesu, Kiebrania kilikuwa kingali kikisemwa katika Palestina. Lakini Kikoine ndicho kilichoenea sana huko na katika ile mikoa mingine ya mbali ya ulimwengu wa Roma. Kwa hiyo, waandikaji Wakristo wa Biblia, walitumia aina hiyo ya kawaida ya Kigiriki ili kufikia watu wengi iwezekanavyo wa mataifa. Pia, walinukuu sana kutoka katika Septuagint na kutumia mengi ya maneno yake.
Kwa kuwa Wakristo wa mapema walikuwa wamishonari wenye bidii, upesi wakawa stadi wa kutumia Septuagint ili kuthibitisha kwamba Yesu alikuwa Mesiya aliyekuwa amengojewa kwa muda mrefu. Hilo liliwafadhaisha Wayahudi na kuwachochea watokeze tafsiri kadhaa mpya katika Kigiriki, zilizokusudiwa kuwanyima Wakristo majibizano yao kwa kufanyia marekebisho maandiko yao ya ithibati waliyopenda sana. Kwa kielelezo, kwenye Isaya 7:14 Septuagint ilitumia neno la Kigiriki linalomaanisha “bikira,” ikirejezea kiunabii mama ya Mesiya. Hizo tafsiri mpya zilitumia neno tofauti la Kigiriki, linalomaanisha “mwanamke mchanga.” Kuendelea kwa hao Wakristo kuitumia Septuagint hatimaye kulisukuma Wayahudi waache mbinu zao zote na kuunga mkono kurudia maandishi ya Kiebrania. Mwishowe, tendo hilo likawa baraka kwa tafsiri za Biblia za baadaye kwa sababu ilisaidia kudumisha lugha ya Kiebrania.
Wachapishaji wa Kwanza wa Vitabu vya Kikristo
Wakristo wenye bidii wa karne ya kwanza walianza kutokeza nakala nyingi za Biblia kadiri walivyoweza, zote zikiwa zimenakiliwa kwa mkono. Pia walianzisha matumizi ya kodeksi, ambayo ilikuwa na kurasa kama kitabu cha kisasa, badala ya kuendelea kutumia hatikunjo. Mbali na kuwa yenye kufaa zaidi ili kupata maandiko upesi, kodeksi ingeweza kuwa na maandiko mengi zaidi katika buku moja kuliko ambavyo ingeweza kurekodiwa katika hatikunjo moja—kwa kielelezo, Maandiko ya Kigiriki yote au hata Biblia nzima.
Maandiko yaliyokubalika ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yalikamilishwa wapata mwaka wa 98 W.K. pamoja na vitabu vya mwisho vya mtume wa mwisho ambaye bado alikuwako, Yohana. Kuna kipande cha nakala ya Gospeli ya Yohana, kiitwacho Rylands Papyrus 457 (P52), chenye tarehe ya kurudi nyuma hadi kabla ya mwaka wa 125 W.K. Mapema kama mwaka wa 150 hadi 170 W.K., Tatian, mwanafunzi wa Justin Martyr, alitokeza Diatessaron, simulizi la maisha ya Yesu lenye sehemu nyingi kutokana na Gospeli zilezile nne zipatikanazo katika Biblia zetu za sasa.a Hilo lilionyesha kwamba alizoona kuwa asilia ni Gospeli hizo tu na kwamba tayari zilikuwa zikigawanywa. Wapata mwaka wa 170 W.K., katalogi ya mapema zaidi inayojulikana ya vitabu vya “Agano Jipya,” iitwayo Kipande cha Muratori, ilitokezwa. Yaorodhesha vingi vya vitabu vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.
Kuenea kwa itikadi za Kikristo upesi kulitokeza uhitaji wa tafsiri za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo na pia Maandiko ya Kiebrania. Tafsiri kadha wa kadha katika lugha kama vile Kiarmenia, Kikoptiki, Kigeorgia, na Kisiria zilifanyizwa hatimaye. Mara nyingi ilikuwa lazima kubuni alfabeti kwa kusudi hilo tu. Mathalani, Ulfilas, askofu wa karne ya nne wa Kanisa la Kiroma, alisemwa kuwa alibuni alfabeti ya Kigothi ili kuitafsiri Biblia. Lakini aliacha vitabu vya Wafalme kwa sababu alifikiri kwamba hivyo vingetia moyo yale maelekeo ya kivita ya Wagothi. Hata hivyo, tendo hilo halikuwazuia Wagothi “Waliofanywa Wakristo” wasiteke nyara Roma mwaka wa 410 W.K.!
Biblia ya Kilatini na ya Kislavoni
Wakati uleule, Kilatini kikapata umaana, na tafsiri kadhaa za Kilatini cha Kale zikatokea. Lakini zilitofautiana katika mtindo na usahihi. Kwa hiyo mwaka wa 382 W.K., Papa Damasus alimpa mwandishi wake, Jerome, utume wa kutayarisha Biblia ya Kilatini yenye mamlaka.
Jerome alianza kwa kufanyia marekebisho tafsiri za Kilatini za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Hata hivyo, alisisitiza kutafsiri Maandiko ya Kiebrania kutoka katika Kiebrania cha awali. Hivyo, mwaka wa 386 W.K., alihamia Bethlehemu ili kujifunza Kiebrania na kutafuta msaada wa rabi. Kwa tendo hilo, aliamsha ubishi mkubwa miongoni mwa makanisa. Wengine, kutia na Augustine, aliyeishi wakati uleule na Jerome, waliamini kwamba Septuagint ilikuwa imepuliziwa, nao walimshtaki Jerome kuwa “alikosa uaminifu-mshikamanifu kwa kuwaendea Wayahudi ili kupata msaada.” Akisonga mbele, Jerome alimaliza kazi yake wapata mwaka wa 400 W.K. Kwa kukaribia chanzo cha lugha na hati za awali na kwa kuzitafsiri katika lugha zilizosemwa wakati huo, Jerome alizitangulia kwa miaka elfu moja njia za kisasa za kutafsiri. Biblia yake ikaja kujulikana kuwa Vulgate, au Tafsiri ya Kawaida, nayo iliwanufaisha watu kwa karne kadhaa.
Katika Jumuiya ya Wakristo ya mashariki bado wengi wangeweza kusoma Septuagint na yale Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Hata hivyo, lugha na lahaja za Kislavoni, au Kislavi, zikaja kutumiwa kwa ukawaida katika sehemu za mashariki za Ulaya. Mwaka wa 863 W.K., ndugu wawili wenye kusema Kigiriki, Cyril na Methodius, walienda Moravia, ambayo sasa iko katika Jamhuri ya Cheki. Walianza kuitafsiri Biblia katika Kislavoni cha Kale. Ili kufanya hivyo, walibuni alfabeti ya Kiglagoliti, ambayo baadaye ilipitwa na alfabeti ya Kisirili, iliyopata jina kutokana na Cyril. Hiyo ndiyo iliyokuwa chanzo cha maandishi ya lugha ya kisasa ya Kirusi, ya Kiukrainia, ya Kiserbia, na ya Kibulgaria. Biblia ya Kislavoni ilitumiwa na watu wa eneo hilo kwa vizazi kadhaa. Ingawa hivyo, punde si punde, lugha zilipokuwa zikibadilika, ikawa isiyofahamika kwa mtu wa kawaida.
Biblia ya Kiebrania Yaokoka
Wakati wa kipindi hicho, tangu karne ya sita hivi hadi ya kumi W.K., kikundi cha Wayahudi kilichojulikana kuwa Wamasora kilikuza njia za hatua kwa hatua za kunakili ili kuhifadhi maandishi ya Andiko la Kiebrania. Hata walijitahidi kuhesabu mistari yote na hata kila herufi, wakiandika tofauti zilizokuwako miongoni mwa hati, yote hayo katika jitihada za kuhifadhi maandiko asilia. Jitihada zao hazikuwa kazi bure. Kwa kielelezo kimoja, kulinganishwa kwa maandiko ya kisasa ya Kimasora na Hatikunjo za Bahari Iliyokufa, zilizoandikwa kati ya mwaka wa 250 K.W.K. na mwaka wa 50 W.K., hakuonyeshi badiliko lolote la kimafundisho kwa kipindi kinachozidi miaka 1,000.b
Katika Ulaya Enzi za Kati zilifanana sana na Enzi za Giza. Kiwango cha kusoma na kujifunza cha watu wa kawaida kilikuwa cha chini. Hatimaye, hata makasisi, kwa sehemu kubwa wakawa hawawezi kusoma Kilatini cha kanisa na mara nyingi hawangeweza hata kusoma lugha yao wenyewe. Huo pia ndio uliokuwa wakati ambapo Wayahudi walikusanywa pamoja na mitaa yao ikaanzishwa Ulaya. Kiebrania cha Biblia kilihifadhiwa kwa kiasi fulani kwa sababu ya kutengwa huko. Hata hivyo, kwa sababu ya upendeleo na kutoaminiana, mara nyingi ujuzi wa Wayahudi haukupatikana nje ya mitaa yao. Mashariki mwa Ulaya, ujuzi wa Kigiriki ulikuwa pia ukipungua. Hiyo hali ilifanywa kuwa mbaya zaidi na kule kuitolea Vulgate ya Kilatini ya Jerome heshima ya kuzidi, kulikofanywa na Kanisa la Magharibi. Kwa kawaida ilionwa kuwa ndiyo tafsiri pekee yenye mamlaka, ingawaje kufikia mwishoni mwa kipindi cha Kimasora, Kilatini kilikuwa lugha isiyotumika katika kuwasiliana kila siku. Hivyo, tamaa ya kuijua Biblia ilipoanza kuchipuka polepole, mandhari iliwekwa kwa ajili ya bishano kubwa.
Kutafsiriwa kwa Biblia Kwakabili Upinzani
Mwaka wa 1079, Papa Gregory wa Saba alitoa ya kwanza kati ya zile amri nyingi za kanisa la enzi za kati za kupiga marufuku kutokezwa na nyakati nyingine hata kuwa na tafsiri za lugha za kienyeji. Aliondoa ruhusa ya Misa kusherehekewa katika Kislavoni kwa sababu kufanya hivyo kungetaka visehemu vya Andiko Takatifu vitafsiriwe. Tofauti kabisa na msimamo wa Wakristo wa mapema, aliandika hivi: “I[me]mpendeza Mungu Mweza-Yote kwamba andiko takatifu lapaswa kuwa siri katika mahali fulani-fulani.” Huo ukiwa ndio msimamo rasmi wa kanisa, waendelezaji wa usomaji wa Biblia walionwa kuwa hatari zaidi na zaidi.
Zijapokuwa hali zisizopendeza, kule kunakili na kutafsiri Biblia katika lugha za kawaida kuliendelea. Tafsiri za lugha nyingi zilienea kisiri katika Ulaya. Zote hizo zilinakiliwa kwa mkono, kwa kuwa kupiga chapa hakukubuniwa Ulaya mpaka miaka ya katikati ya 1400. Lakini kwa kuwa nakala zilikuwa za bei ghali na chache, mwananchi wa kawaida angeweza kujiona kuwa mwenye furaha kumiliki kisehemu tu cha kitabu kimoja cha Biblia au kurasa chache tu. Watu fulani walikariri moyoni sehemu kubwa-kubwa, hata Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yote!
Hata hivyo, baada ya muda fulani kulikuwa na harakati zenye kushtusha zilizoenea sana za marekebisho ya kanisa. Kwa sehemu zilichochewa na ufahamu uliofanywa upya kuhusu umaana wa Neno la Mungu katika maisha ya kila siku. Harakati hizo na maendeleo ya uchapaji yangeiathirije Biblia? Na ni nini kilichompata William Tyndale na tafsiri yake, iliyotajwa mwanzoni? Tutaendeleza simulizi hili lenye kuvutia sana hadi nyakati zetu wenyewe katika matoleo ya wakati ujao.
[Maelezo ya Chini]
a Kitabu Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc., ni kielelezo cha kisasa cha upatano wa zile Gospeli nne.
b Ona Insight on the Scriptures, Buku la 2, ukurasa wa 315, lililochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Chati katika ukurasa wa 8, 9]
Tarehe Muhimu Katika Kupitishwa kwa Biblia
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
KABLA YA WAKATI WA KAWAIDA (K.W.K.)
Maandiko ya Kiebrania yakamilishwa karibu 443 K.W.K.
400 K.W.K.
Aleksanda Mkubwa (alikufa 323 K.W.K.)
300 K.W.K.
Septuagint ilianza karibu 280 K.W.K.
200 K.W.K.
100 K.W.K. Nyingi za Hatikunjo za Bahari Iliyokufa karibu 100 K.W.K. hadi 68 W.K.
WAKATI WA KAWAIDA (W.K.)
Yerusalemu laharibiwa 70 W.K.
Maandiko ya Kigiriki yakamilishwa 98 W.K.
100 W.K.
Mafunjo ya Rylands ya Yohana (kabla ya 125 W.K.)
200 W.K.
300 W.K.
400 W.K. Vulgate ya Kilatini ya Jerome karibu 400 W.K.
500 W.K.
600 W.K.
Maandishi ya Kimasora Yatayarishwa
700 W.K.
800 W.K.
Cyril akiwa Moravia 863 W.K.
900 W.K.
1000 W.K.
Amri dhidi ya Biblia ya kienyeji 1079 W.K.
1100 W.K.
1200 W.K.
1300 W.K.
[Picha katika ukurasa wa 9]
Wakristo wa mapema walianzisha matumizi ya kodeksi
[Picha katika ukurasa wa 10]
Jerome alienda Bethlehemu kujifunza Kiebrania