Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 9/1 kur. 4-7
  • Thawabu za Kuwaheshimu Wazazi Wazee-Wazee

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Thawabu za Kuwaheshimu Wazazi Wazee-Wazee
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kutoa Kimwili
  • Kutoa Kihisia-Moyo
  • Kutoa Kiroho
  • Mwenendo Mzuri Huvuta Watu kwa Mungu
  • Kuwaheshimu Wazazi Wetu Wazee-Wazee
    Siri ya Furaha ya Familia
  • Kwa Nini Niwajue Vyema Babu na Nyanya?
    Amkeni!—2001
  • Ninawezaje Kusitawisha Uhusiano wa Karibu Pamoja na Babu na Nyanya?
    Amkeni!—2001
  • Kuishi Pamoja kwa Upendo
    Amkeni!—1995
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 9/1 kur. 4-7

Thawabu za Kuwaheshimu Wazazi Wazee-Wazee

WAABUDU wa kweli wa Mungu hustahi, huheshimu, na hutunza wazazi wao wazee-wazee kwa sababu wanawapenda. Ni sehemu ya ibada yao. Biblia hutaarifu hivi: “Acha [watoto au wajukuu] wajifunze kwanza kuzoea ujitoaji-kimungu kwa watu wa nyumbani mwao wenyewe na kufuliza kulipa wazazi na babu na nyanya zao fidia ipasayo, kwa maana hili ni lenye kukubalika machoni pa Mungu.” (1 Timotheo 5:4) Tuwe wachanga au wazee, yafaa kwamba tuwatolee wazazi wetu na babu na nyanya zetu “fidia ipasayo.” Kwa njia hiyo twaonyesha kuthamini upendo wao, kufanya kwao kazi kwa bidii, na kututunza kwa miaka mingi. Kwani, twaishi kwa sababu ya wazazi wetu!

Tambua kwamba kuwalipa wazazi na babu na nyanya fidia ipasayo “[kwa]kubalika machoni pa Mungu.” Kwahusianishwa na “ujitoaji-kimungu” wetu. Hivyo, kwa kutekeleza shauri hilo, twathawabishwa, tukijua kwamba tunafanya limpendezalo Mungu. Hilo hutuletea shangwe.

Kuna shangwe katika kutoa kwa wengine, hasa tunapowatolea wale ambao wametutolea kwa ukarimu. (Matendo 20:35) Basi, inathawabisha kama nini kutenda kupatana na ile kanuni ya Biblia: “Wafurahishe baba na mama yako; mama aliyekuzaa na afurahi”!—Mithali 23:25, Biblia Habari Njema.

Twaweza kuwatoleaje fidia iwapasayo wazazi wetu na babu na nyanya zetu? Katika njia tatu: kimwili, kihisia-moyo, na kiroho. Kila njia huleta thawabu zake.

Kutoa Kimwili

Wanaomtumikia Mungu wanajua kwamba ni jambo la maana kuandalia kimwili washiriki wa karibu wa familia. Mtume Paulo alionya hivi kwa upole: “Ikiwa yeyote hawaandalii kitu wale walio wake mwenyewe, na hasa kwa ajili ya wale walio washiriki wa nyumbani mwake, ameikana imani naye ni mbaya zaidi kuliko mtu asiye na imani.”—1 Timotheo 5:8.

Tunji na Joy wanaishi Afrika Magharibi. Ingawa wamebanwa sana kifedha, waliwaalika wazazi wa Joy walio wazee-wazee waishi pamoja nao. Baba alikuwa mgonjwa na hatimaye akafa. Tunji akumbuka hivi: “Papa [baba-mkwe] alipokufa, Mama [mama-mkwe] alimkumbatia mke wangu na kusema hivi: ‘Mlifanya yote mwezayo kufanya kibinadamu. Msihisi hatia kwa njia yoyote kwa sababu ya kifo cha Papa.’ Ingawa twamkosa Papa, twajua tulimnunulia dawa bora kabisa na sikuzote tulijaribu kumfanya ahisi kwamba alitakikana na kuhitajiwa; tulifanya yote tuwezayo ili kutimiza daraka letu lenye kupewa na Mungu. Uradhi huo upo.”

Bila shaka, si kila mtu anayeweza kusaidia wengine kimwili. Mwanamume aishiye Nigeria alisema hivi: “Ikiwa mtu hawezi kujitegemea, awezaje basi kutegemeza mtu mwingine?” Katika nchi nyingi huenda hata hali ikawa mbaya zaidi miaka ijayo. Kulingana na utabiri wa Umoja wa Mataifa, karibuni nusu ya wakazi wa Afrika iliyo sehemu ya kusini ya Sahara watakuwa wakiishi katika ufukara.

Ukijikuta katika hali mbaya kiuchumi, waweza kufarijiwa na hadithi ya kweli ya mjane mwenye uhitaji. Yesu alipokuwa duniani, alimchunguza kwa makini mjane fulani akitoa upaji mdogo kwenye sanduku la hazina la hekalu. Alitoa “sarafu ndogo mbili za thamani ndogo sana.” Hata hivyo, akijua hali yake, Yesu alisema hivi: “Nawaambia nyinyi kwa kweli, Mjane huyu, ijapokuwa ni maskini, alitumbukiza nyingi kuliko wao wote. Kwa maana wote hawa walizitumbukiza ndani zawadi kutokana na ziada yao, lakini mwanamke huyu kutokana na uhitaji wake alitumbukiza ndani njia yote ya kujipatia riziki aliyokuwa nayo.”—Luka 21:1-4.

Vivyo hivyo, tukifanya yote tuwezayo katika kuwatunza kimwili wazazi wetu au babu na nyanya zetu, ingawa huenda likawa jambo dogo, Yehova huchunguza kwa makini na huthamini hilo. Hatarajii tufanye zaidi ya yale tuwezayo kufanya. Yamkini wazazi wetu au babu na nyanya zetu watahisi vivyo hivyo.

Kutoa Kihisia-Moyo

Kuwaandalia wazazi wetu na babu na nyanya zetu kwahusisha mengi zaidi ya kuwaandalia mahitaji yao ya kimwili tu. Sisi sote tuna mahitaji ya kihisia-moyo. Kila mmoja, kutia na wenye umri mkubwa zaidi, ana tamaa ya kupendwa, ya kuhisi kwamba anahitajiwa na anatakikana, na ya kuwa mshiriki wa familia anayethaminiwa.

Mary, anayeishi Kenya, amemtunza mama-mkwe wake aliye mzee-mzee kwa miaka mitatu. Mary asema hivi: “Zaidi ya kuandaa mahitaji yake ya kimwili, sikuzote sisi huzungumza naye. Mama hawezi kufanya mengi nyumbani, lakini sisi huzungumza na tumekuwa marafiki wa karibu. Nyakati nyingine sisi huzungumza juu ya Mungu, nyakati nyingine juu ya watu huko nyumbani. Ingawa ana umri unaozidi miaka 90, kumbukumbu lake ni zuri sana. Yeye hukumbuka na kuzungumzia jinsi maisha yalivyokuwa alipokuwa msichana mdogo, siku za kabla ya mwaka wa 1914.”

Mary aendelea kusema hivi: “Si rahisi kumtunza mtu mzee, lakini kuwa na mama pamoja nasi kumetuletea thawabu zenye thamani. Tuna amani na upatano katika familia. Kutoa kwangu kumewachochea wengine katika familia wawe na roho ya kutoa. Mume wangu ananiheshimu zaidi. Na mama akisikia yeyote akisema nami kwa ukali, yeye hunitetea upesi. Hakuna awezaye kuniambia neno lenye kuumiza mama akiwepo!”

Kutoa Kiroho

Kama vile kutoa kimwili na kihisia-moyo humthawabisha atoaye, ndivyo ilivyo na mambo ya kiroho. Mtume Paulo aliandikia kutaniko la Kikristo katika Roma hivi: “Nina hamu sana ya kuwaona nyinyi, ili nipate kuwapa baadhi ya zawadi ya kiroho kusudi mfanywe imara; au, badala ya hivyo, kwamba kupate kuwa na badilishano la kitia-moyo miongoni mwenu, kwa kila mmoja kupitia imani ya mwingine, yenu na yangu pia.”—Waroma 1:11, 12.

Katika njia hiyohiyo, kwa habari ya kuwatolea kiroho wazee-wazee wanaomtumikia Mungu, mara nyingi kitia-moyo huwa kutoka pande zote mbili. Osondu, anayeishi Nigeria, asimulia hivi: “Linalonipendeza zaidi juu ya babu yangu na nyanya yangu ni fursa ambayo wao hunipa ya kupata kuona kidogo wakati uliopita. Babu yangu, akiwa na macho mangavu, atasema kuhusu eneo alilohubiri akiwa mhudumu wa wakati wote katika miaka ya 1950 na ya 1960. Yeye hulinganisha muundo wa sasa wa kutaniko na jinsi ulivyokuwa alipopata kuwa Shahidi. Mambo hayo yaliyoonwa hunisaidia katika utumishi wangu nikiwa painia.”

Wengine pia katika kutaniko la Kikristo waweza kusaidia katika kutolea wenye umri mkubwa zaidi. Tunji, aliyetajwa mwanzoni, alieleza lililotukia kutanikoni mwake: “Ndugu painia aliye kijana ambaye alipewa mgawo wa kutoa hotuba ya watu wote alimletea Papa [baba-mkwe] muhtasari wake ili wautayarishe pamoja. Kiongozi wa Funzo la Mnara wa Mlinzi alikuja na kumwambia Papa hivi: ‘Wewe una uzoefu. Waweza kusema nini ili kunisaidia nifanye maendeleo.’ Papa aliweza kumpa mzee huyo shauri lenye kutumika. Akina ndugu walitaja jina la Papa katika sala za kutaniko mara kadha wa kadha. Yote hayo yalimfanya ahisi anatakikana.”

Mwenendo Mzuri Huvuta Watu kwa Mungu

Nyakati nyingine, tuonyeshapo upendo na heshima kwa wazazi wetu na babu na nyanya zetu, twawavuta watu kwa Mungu. Mtume Petro aliandika hivi: “Dumisheni mwenendo wenu ukiwa bora miongoni mwa mataifa, ili, katika jambo ambalo katika hilo wao wanasema dhidi yenu kuwa watenda-maovu, likiwa tokeo la kazi zenu bora ambazo wamekuwa mashahidi wa kujionea wapate kumtukuza Mungu.”—1 Petro 2:12.

Andrew, mzee Mkristo huko Afrika Magharibi, alisafiri kilometa 95 mara mbili kwa juma ili kumtunza baba yake mgonjwa, ambaye hakuwa mwamini. Yeye asimulia hivi: “Nilipopata kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, baba yangu alipinga kwa nguvu. Lakini alipoona jinsi nilivyokuwa nikimtunza alipokuwa mgonjwa, aliendelea kuwahimiza ndugu na dada zangu wachanga hivi, ‘Lazima mjiunge na dini ya ndugu yenu!’ Hilo liliwachochea, na sasa watoto wote tisa wa baba yangu ni Mashahidi wa Yehova.”

Kuwaheshimu na kuwatunza wazazi wetu wazee-wazee kwaweza kuwa jambo gumu, hasa katika nyakati zilizo ngumu kiuchumi. Lakini Wakristo wajitahidipo kufanya hivyo, wanapata thawabu nyingi. Zaidi ya yote, wanapata shangwe ya kutoa, pamoja na uradhi wa kujua kwamba wanampendeza Yehova Mungu, aliye “Baba wa watu wote.”—Waefeso 4:6.

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

Shauri la Kimungu kwa Wale Wanaotunzwa na kwa Wale Wanaotunza

Uwe Mwenye Kutia Moyo: “Acheni kila mmoja wetu ampendeze jirani yake katika lililo jema kwa ajili ya kujengwa kwake.”—Waroma 15:2.

Uwe Imara: “Acheni tusife moyo katika kufanya lililo bora, kwa maana katika majira yapasayo tutavuna ikiwa hatuchoki kabisa.”—Wagalatia 6:9.

Uwe Mnyenyekevu: ‘Msifanye jambo lolote kwa ugomvi au kwa majisifu ya bure, bali kwa hali ya akili ya kujishusha chini mkifikiria kwamba wengine ni wakubwa kuliko nyinyi.’—Wafilipi 2:3.

Uwe Mtenda-Mema: “Acheni kila mmoja afulize kutafuta sana, si faida yake mwenyewe, bali ya mtu yule mwingine.”—1 Wakorintho 10:24.

Uwe Mwenye Kukubali Sababu: “Hali yenu ya kukubali sababu na ijulikane kwa watu wote.”—Wafilipi 4:5.

Uwe Mwenye Huruma: “Iweni wenye fadhili nyinyi kwa nyinyi, wenye huruma kwa njia nyororo, mkisameheana kwa hiari mtu na mwenzake.”—Waefeso 4:32.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Wazee wa kutaniko wenye umri mdogo zaidi waweza kunufaishwa na uzoefu wa wale wenye umri mkubwa zaidi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki