Je, Misherehekeo ya Mavuno Humpendeza Mungu?
MATUNDA matamu sana, mboga zenye kupendeza sana, na miganda ya mahindi mazuri ikiwa imerundamana hutokeza picha yenye kuvutia. Wakati wa mavuno maonyesho hayo hurembesha madhabahu na mimbari ya makanisa kotekote katika Uingereza. Katika Ulaya, kama ilivyo kwingineko, shughuli nyingi za misherehekeo hutia alama mwanzo na mwisho wa msimu wa mavuno.
Wale ambao riziki yao hutegemea udongo ni wenye shukrani hasa kwa ajili ya mazao ya nchi. Kwa kweli, Mungu aliagiza taifa la kale la Israeli lisherehekee misherehekeo mitatu ya kila mwaka ambayo ilishirikishwa kwa ukaribu na mavuno. Mapema wakati wa masika, wakati wa Msherehekeo wa Keki Zisizotiwa Chachu, Waisraeli walimtolea Mungu mganda wa matunda ya kwanza wa mavuno ya shayiri. Kwenye Msherehekeo wa Majuma (au, Pentekoste) mwishoni mwa masika, walitoa mikate iliyotengenezwa kwa matunda ya kwanza ya mavuno ya ngano. Wakati wa vuli, Msherehekeo wa Kukusanya ulifanywa, ambao ulitia alama mwisho wa mwaka wa kilimo wa Waisraeli. (Kutoka 23:14-17) Misherehekeo hiyo ilikuwa “makusanyiko matakatifu” na nyakati za kushangilia.—Mambo ya Walawi 23:2; Kumbukumbu la Torati 16:16.
Basi, namna gani sherehe za mavuno za siku ya kisasa? Je, hizo humpendeza Mungu?
Viunganishi vya Kipagani
Akiwa amevurugwa na hali ya kilimwengu ya karamu ya kidesturi ya wakati wa mavuno na ulevi ambao hushirikishwa na hiyo sherehe, kasisi Mwanglikana katika Cornwall, Uingereza, aliamua katika 1843 kurudisha desturi ya mavuno ya enzi za kati. Alichukua nafaka ya kwanza kuvunwa na kutokana nayo akatengeneza mkate kwa ajili ya sherehe ya ushirika katika kanisa lake. Kwa kufanya hivyo, aliendeleza msherehekeo wa Lammas—sherehe ya “Kikristo” ambayo watu fulani husema kwamba ilitokana na ibada ya kale ya mungu wa Waselti, Lugh.a Hivyo, msherehekeo wa kisasa wa mavuno wa Kianglikana una asili ya kipagani.
Namna gani sherehe nyingine ambazo hufanyika mwishoni mwa msimu wa mavuno? Kulingana na Encyclopædia Britannica, asili ya nyingi za desturi ambazo hutia alama misherehekeo hiyo ni “ile itikadi katika roho ya mahindi [nafaka] au mama ya mahindi.” Katika maeneo fulani wakulima waliamini kwamba roho fulani ilikaa ndani ya mganda wa mwisho wa nafaka iliyovunwa. Ili kufukuza hiyo roho, walitoa hiyo nafaka yote kwa kuupiga mganda huo kwa vijiti. Kwingineko walifuma baadhi ya majani ya nafaka ili kutengeneza “kipambo cha mahindi” walichotunza salama hadi upandaji-mbegu wa mwaka uliofuata ili kupata “bahati.” Kisha walilima kwa plau wakiweka hayo masuke ndani ya udongo kwa matumaini ya kwamba, kufanya hivyo kungebariki hayo mazao mapya.
Hekaya fulani hushirikisha wakati wa mavuno na ibada ya mungu wa Kibabiloni, Tamuzi, mume wa mungu wa kike wa uzazi, Ishta. Kukata suke la nafaka lililokomaa kulifananisha kifo cha mapema cha Tamuzi. Hekaya nyingine hata huhusianisha wakati wa mavuno na dhabihu ya kibinadamu—zoea ambalo Yehova Mungu huchukia sana.—Mambo ya Walawi 20:2; Yeremia 7:30, 31.
Maoni ya Mungu Ni Nini?
Kushughulika kwa Mungu na Israeli la kale kwa wazi hufunua kwamba Yehova, Muumba na Chanzo cha uhai, alidai kutoka kwa waabudu wake ujitoaji usiohusisha wengine. (Zaburi 36:9; Nahumu 1:2) Siku ya nabii Ezekieli, zoea la kutoa machozi kwa ajili ya mungu Tamuzi lilikuwa ‘chukizo kubwa’ machoni pa Yehova. Jambo hilo, pamoja na sherehe nyingine za ibada, zilimfanya Mungu afunge masikio yake asisikie sala za waabudu hao wasio wa kweli.—Ezekieli 8:6, 13, 14, 18.
Tofautisha hilo na yale ambayo Yehova Mungu aliagiza Israeli kuadhimisha kuhusiana na mavuno. Kwenye Msherehekeo wa Kukusanya, Waisraeli walifanya kusanyiko rasmi wakati ambapo wachanga kwa wazee, matajiri kwa maskini, waliishi katika makao ya muda yaliyorembeshwa kwa matawi yenye majani mabichi ya miti yenye kuvutia. Huo ulikuwa wakati wa shangilio kuu kwao, lakini ulikuwa pia wakati wa kukumbuka ule ukombozi ambao Mungu alikuwa amewatolea baba zao wa zamani wakati wa kule Kutoka Misri.—Mambo ya Walawi 23:40-43.
Wakati wa misherehekeo ya Waisraeli, matoleo yalitolewa kwa Yehova, Mungu wa pekee wa kweli. (Kumbukumbu la Torati 8:10-20) Kwa habari ya zile itikadi zilizotangulia kutajwa, za kuwako kwa roho katika vitu vyote, Biblia haisemi mahali popote kwamba mazao, kama vile miganda ya ngano, kuwa na nafsi.b Na Maandiko huonyesha wazi kwamba sanamu hubaki bila uhai, zisizoweza kusema, kuona, kusikia, kunusa, kuhisi, au kuwatolea waabudu wake msaada wowote.—Zaburi 115:5-8; Waroma 1:23-25.
Wakristo leo hawako chini ya agano la Sheria ambalo Mungu alifanya na taifa la kale la Israeli. Kwa kweli, Mungu ‘aliiondoa njiani kwa kuipigilia misumari kwenye mti wa mateso wa Yesu.’ (Wakolosai 2:13, 14) Watumishi wa Yehova wa siku ya kisasa huishi kwa “sheria ya Kristo” na huitikia kwa uthamini yale yote ambayo Mungu huandaa.—Wagalatia 6:2.
Mtume Paulo alitaarifu waziwazi kwamba misherehekeo ya Kiyahudi ilikuwa “kivuli cha mambo yajayo,” akiongeza, “bali uhalisi ni wa Kristo.” (Wakolosai 2:16, 17) Kwa sababu hiyo, Wakristo hukubali kusababu huku kwa Kimaandiko: “Vitu ambavyo mataifa huvidhabihu huwa wavidhabihu kwa roho waovu, na si kwa Mungu . . . Hamwezi kuwa mkinywa kikombe cha Yehova na kikombe cha roho waovu.” (1 Wakorintho 10:20, 21) Isitoshe, Wakristo husikiza lile agizo la ‘kukoma kugusa kitu kisicho safi.’ Je, misheherekeo ya mavuno ujiranini mwako, ina vidokezo vya kipagani au vya dini isiyo ya kweli? Ikiwa ndivyo, Wakristo wa kweli waweza kuepuka kutompendeza Yehova kwa kukataa kujihusisha kokote katika ibada iliyochafuliwa.—2 Wakorintho 6:17.
Mtoto mwenye uthamini apokeapo zawadi kutoka kwa baba yake, yeye humshukuru nani? Mtu asiyemjua kabisa au mzazi wake? Kwa sala ya kuhisiwa moyoni waabudu wa Mungu humshukuru Yehova, Baba yao wa kimbingu kila siku, kwa ukarimu wake mwingi.—2 Wakorintho 6:18; 1 Wathesalonike 5:17, 18.
[Maelezo ya Chini]
a Neno “Lammas” latokana na neno la Kiingereza cha Kale linalomaanisha “misa ya mkate.”
b Kichapo Insight on the Scriptures chataarifu hivi: “Neno neʹphesh (nafsi) halitumiwi kurejezea kuumbwa kwa uhai wa mimea ‘siku’ ya tatu ya uumbaji (Mwa 1:11-13) au baada ya hapo, kwa kuwa mimea haina damu.”—Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.