Sikukuu za Furaha
“Uwe katika kufurahi kabisa.”—Kum. 16:15.
1. Ni nani leo wanaojionyesha kuwa watu wenye furaha zaidi, na sababu gani?
NI NANI asiyefurahia sikukuu? Katika karne zote watu duniani wamefurahia sikukuu. Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa watu wale waliopata sheria zao za taifa kutoka kwa Muumba wa wanadamu kupitia kwa nabii wake Musa. Walakini sikukuu zao zilikuwa tofauti; zilikuwa za kiunabii za mambo mazuri yatakayokuja. Vivyo hivyo furaha ni fungu la walio mfano wa kisasa wa washerehekeaji wale wa kale katika Mashariki ya Kati, kwa kuwa wao wanaingia kwenye utimizo wa sikukuu hizo za kiunabii. Kwa maoni ya Biblia Takatifu, washerehekeaji hao wa kisasa ni Waisraeli wa kiroho, nao wanajionyesha kuwa watu wenye furaha zaidi duniani.
2. Katika Kumbukumbu la Torati 16:16, ni sikukuu ngapi zilizoamriwa zifanywe, nazo zilikuwa sikukuu gani?
2 Katika vitabu vilivyoongozwa kwa roho vilivyoandikwa na Musa, sikukuu tatu ziliamrishwa. Katika kitabu hiki cha tano, kinachoitwa Kumbukumbu la Torati, sura ya 16, mstari wa 16, twasoma hivi: “Mara tatu kwa mwaka na watokee wanaume wako wote mbele za [Yehova], Mungu wako, mahali atakapochagua; katika [siku-kuu] ya mikate isiyotiwa chachu, na katika [sikukuu] ya majuma, na katika [siku-kuu] ya vibanda; wala wasitokee mbele za [Yehova] mikono mitupu.”
3. Wakati maneno yaliyoongezewa ya Kumbukumbu la Torati 16:17 yalipotajwa, hali ya Waisraeli wa halisi ilikuwa gani?
3 Kum 16 Mstari wa 17 unasema hivi: “Kila mtu na atoe kama awezavyo, kwa kadiri ya baraka ya [Yehova], Mungu wako, alivyokupa.” Wakati maneno hayo yaliposemwa, Waisraeli walikuwa wakiishi katika hema, wakiwa njiani kuelekea Nchi ya Ahadi ya Kanaani.
SIKUKUU YA MIKATE ISIYOTIWA CHACHU
4. Sikukuu ya kwanza ilikuwa sikukuu gani, na katika siku yake ya pili, kuhani mkuu alimtolea Yehova nini?
4 Ya kwanza ya zile sikukuu za kila mwaka, ile ya mikate isiyotiwa chachu, iliadhimishwa mara tu baada ya kuadhimisha kijio cha Sikukuu ya Kupitwa katika Abibu au Nisani 14. Sikukuu mikate isiyotiwa chachu iliadhimishia kwa muda wa siku saba, tangu Nisani 15 mpaka na kutia Nisani 21. Siku ya kwanza za sikukuu hiyo ilikuwa siku ya Sabato iliyofuata kuadhimisha kijio cha Sikukuu ya Kupitwa. Katika siku ya pili ya sikukuu hiyo, au Nisani 16, kuhani mkuu wa Kiisraeli katika hekalu la Yehova katika Yerusalemu angemtolea Yeye mganda kutoka kwa shayiri iliyokuwa imekuwa tayari karibuni.—Law. 23:11-16.
5. Sababu gani Yesu hakusherehekea sikukuu hiyo katika Nisani 15. 33 W.K., nao ni wakati gani wanafunzi wake walipoingia kwenye furaha isiyolinganika?
5 Kuna masimulizi ya kweli ya mwana wa kiume mwenye umri wa miaka 12 ambaye alipelekwa Yerusalemu kutoka Nazareti ili aisherehekee Sikukuu ya Kupitwa. Mvulana huyo alikuwa Yesu, mwana wa Mariamu. Miaka kumi na minane baadaye, katika mwaka 29 W.K., Mwisraeli huyo wa kiume, sasa akiwa Bwana Yesu Kristo, akawa “Mwana-Kondoo wa Mungu,” jambo lililofananishwa na mwana-kondoo wa Sikukuu ya Kupitwa. (Luka 2:41-52; Yohana 1:29-37) Miaka mitatu u nusu baadaye alitolewa dhabihu kwa halisi juu ya mti huko Kalvari, nje ya Yerusalemu, siku ya Ijumaa, Nisani 14, 33 W.K. Usiku huo wa Nisani 15 ulianza, pamoja na sikukuu ya mikate isiyotiwa chachu, walakini Yesu mwenyewe hakushiriki katika kufurahi kulikofuatana na pindi hiyo. Yeye alikuwa amekufa na kuzikwa. Huku Wayahudi kwa ujumla kule Yerusalemu wakifurahia kuanza kwa sikukuu yao, wanafunzi wa Yesu hawakufanya hivyo. Walikuwa wakihuzunikia jambo lililokuwa likionekana kwao kuwa kumpoteza Kiongozi wao milele. Lakini katika siku iliyofuata, Jumapili, Nisani 16, huzuni yao iligeuzwa kuwa furaha kubwa kuliko ile ya Wayahudi wenye kusherehekea sikukuu.
6. Kukulingana na 1 Wakorintho 15:20, suke la nafaka ya shayiri lililotikiswa na kuhani mkuu katika Nisani 16 lilifananisha nini, na sababu gani?
6 Sababu gani hivyo? Kwa sababu Kiongozi wao, Yesu Kristo, alifufuliwa kutoka kwa wafu kwa uwezo wenye nguvu zote wa Babaye wa kimbinguni, Yehova. Akifasiri yale ambayo jambo hilo lilimaanisha, mtume Mkristo Paulo, alipokuwa akiandika juu ya ufufuo, alisema hivi: “Sasa Kristo amefufuka katika wafu, limbuko lao waliolala [katika mauti].” (1 Kor. 15:20) Kwa hiyo mganda wa malimbuko ya mavuno ya shayari ambao kuhani mkuu wa Kiyahudi hekaluni alipunga mbele za Yehova siku ya Jumapili, Nisani 16, ulifananisha mtu mmoja, Bwana Yesu Kristo aliyefufuliwa, wa kwanza kufufuliwa kabisa kutoka katika mauti kuingia kwenye uzima wa milele. Kwa hiyo yeye peke yake ndiye angeweza kuitwa “Limbuko lao waliolala [katika mauti].” Mwujiza huo ulikuwa katika siku ya pili ya sikukuu hiyo.
7. Sababu gani chachu ilikatazwa isiwe katika makao ya Wayahudi wakati wa sikukuu hiyo ya siku saba, nalo jambo hilo lilikuwa ukumbusho wa nini?
7 Wakati wa zile siku saba za sikukuu hiyo, hakuna chachu ambayo ingeweza kupatikana katika makao ya Wayahudi, kwa sababu chachu ilifananisha kitu kisichopatana na Mungu, dhambi. Kwa kweli sikukuu hiyo ilikumbusha jambo hilo, kwa sababu ya kulazimika kuondoka Misri kwa haraka, Waisraeli hawakuwa na wakati wa kutosha kuacha unga wao uliookwa uchachuke. Hivyo, walilazimika kula mkate usiotiwa chachu, kama vile walivyokuwa wamefanya siku ya Sikukuu ya Kupitwa.—Kut. 12:11-34; Kum. 16:2-4.
8, 9. Kwa kulingana na mfano huo, sikukuu ya mfano ya mikate isiyotiwa chachu ingepaswa kufuata mpango gani, naye Paulo anathibitishaje jambo hilo?
8 Kama vile sikukuu ya mikate isiyotiwa chachu ilivyofuata Sikukuu ya Kupitwa na kuchukua muda wa siku saba, ndivyo na mfano wa sikukuu hiyo unavyopaswa kufuata baada ya dhabihu ya “Mwana-Kondoo wa Mungu,” Yesu Kristo, siku ya Ijumaa, Nisani 14, 33 W.K. Kwa kuwa hesabu ya siku za sikukuu hiyo, saba, inafananisha ukamilifu, basi sikukuu hiyo ya mfano imeendelea katika karne zote mpaka wakati huu, na Wakristo wale walio Waisraeli wa kiroho, Wayahudi kwa ndani, wana lazima ya kuiadhimisha. Katika 1 Wakorintho 5:6-8, mtume Paulo anataja juu ya sikukuu hiyo ya mfano anapoandika hivi:
9 “Hamjui kwamba chachu kidogo hulichachusha donge zima? Basi, jisafisheni, mkatoe ile chachu ya kale, mpate kuwa donge jipya, kama vile mlivyo hamkutiwa chachu. Kwa maana [sikukuu wetu wa kupitwa] amekwisha kutolewa kuwa sadaka, yaani, Kristo; basi na tuifanye karamu, si kwa chachu ya kale, wala kwa chachu ya uovu na ubaya, bali kwa yasiyochachika, ndio weupe wa moyo na kweli.”
10. Sababu gani na kwa namna gani sikukuu ya mfano inapaswa kusherehekewa leo, na sababu gani washerehekeaji wanaweza ‘kuwa katika kufurahi kabisa’?
10 Hayo yaliandikwa wapata mwaka 55 W.K., au miaka 22 baada ya kifo cha dhabihu cha Kristo. Leo, zaidi ya karne 19 baadaye Waisraeli wa kiroho wanaosoma maneno hayo ya mtume Paulo wana wajibu wa kuiadhimisha sikukuu hiyo ya mfano, yaani, kwa unyofu wa moyo na kweli. Mabaki watiwa mafuta wa Waisraeli wa kiroho wanapofanya hivyo, wanaweza kuwa na roho ile ya sikukuu ya halisi ya kale na kuwa “katika kufurahi kabisa.” Sababu gani? Kwa sababu kuadhimisha kwa uaminifu sikukuu hiyo ya mfano ilitokeza tengenezo la kitheokrasi lililo safi ambalo Yehova aweza kulikubali.
SIKUKUU YA MAJUMA
11. Ya pili ya sikukuu za lazima ilikuwa nini, na sababu gani iliitwa hivyo?
11 Ya pili ya sikukuu za lazima za Israeli wa kale ilikuwa sikukuu ya majuma. Sababu gani iliitwa hivyo? Kwa sababu Waisraeli walipaswa kuhesabu majuma saba toka Nisani 16, siku iliyofuata kuhani mkuu kumtolea Yehova mganda wa nafaka iliyokuwa tayari karibuni kama malimbuko ya mavuno ya shayiri. Siku 49 zingehesabiwa, na katika siku ya 50 walipaswa kusherehekea sikukuu ya majuma. Katika lugha ya Kigiriki ambayo katika hiyo kikundi cha Wayahudi kilitafsiri Biblia yao, neno linalotumiwa kwa (siku) ya 50 ni pentecostēʹ. Hivyo, Wayahudi wenye kusema Kigiriki waliita sikukuu ya majuma Pentekoste. Ni mambo gani yangefanywa katika siku hiyo?
12. Kulingana na Mambo ya Walawi 23:15-21, ni mambo gani yaliyopaswa kuwa katika siku hiyo ya sikukuu?
12 Katika kujibu, Mambo ya Walawi 23:15-21 yasema hivi: “Nanyi mtajihesabia tangu siku ya pili baada ya sabato, tangu siku hiyo mliyouleta mganda wa sadaka ya kutikiswa; zitatimia sabato saba; hata siku ya pili ya hiyo sabato ya saba mtahesabu siku hamsini; nanyi mtamsongezea [Yehova] sadaka ya unga mpya. Mtatoa katika makao yenu mikate miwili ya kutikiswa, itakuwa ya sehemu za kumi mbili za efa; itakuwa ya unga mwembamba. . . . Kisha kuhani atawatikisa pamoja na hiyo mikate ya malimbuko kuwa sadaka ya kutikiswa mbele za [Yehova], pamoja na wale wana-kondoo wawili; watakuwa watakatifu kwa [Yehova], wawe wa huyo kuhani. Nanyi mtapiga mbiu siku iyo hiyo; kutakuwa na kusanyiko takatifu kwenu; msifanye kazi yo yote ya utumishi; ni amri ya milele katika makao yenu yote, katika vizazi vyenu.”
13. Pentekoste ya mfano ilianza kufanya kazi wakati gani, nalo tukio hilo lilifuatwa na mambo gani?
13 Sikukuu hiyo ya majuma ya kiunabii, au Pentekoste, ilitimizwa juu ya kundi la wanafunzi wa Yesu katika Yerusalemu katika siku ya 50 kuhesabu tangu kufufuliwa kwake kutoka kwa wafu. Kwa hiyo sikukuu ya majuma ya mfano, au Pentekoste, ilianza kutenda kazi katika siku ya sita ya mwezi wa tatu, yaani, katika Siwani 6, wa mwaka 33 W.K. Wakati huo Yesu Kristo aliyetukuzwa alikuwa katika Patakatifu Zaidi pa hekalu kuu la kiroho la Yehova, yaani, akiwa na Yehova mwenyewe mbinguni, ambako alikuwa amepaa katika siku ya 40 tangu kufufuliwa kwake. Huku Wayahudi wakisherehekea sikukuu ya majuma ya halisi, au Pentekoste, kwenye hekalu la Herode katika Yerusalemu, wanafunzi wapata 120 wa Kuhani Mkuu wa kiroho, Yesu Kristo, walikutanika pamoja katika chumba cha orofani katika mji huo. Kisha, kabla ya saa ya tatu ya siku hiyo (saa 3 asubuhi), Bwana Yesu Kristo aliimimina roho takatifu kutoka Patakatifu Zaidi pa hekalu la kiroho la Yehova. Matokeo yake yakawa kuzaliwa kwao kwa kiroho na Baba yao wa kimbinguni, Yehova, na kutiwa kwao mafuta kwa roho takatifu kupitia kwa Kuhani Mkuu wao, Yesu Kristo. (Matendo 2:1-36) Hivyo mikate miwili ya unga mwembamba ya mfano ilitambuliwa na Yehova mbinguni, katika Patakatifu Zaidi pake.—Ebr. 9:24.
14. (a) Uhakika wa kwamba mikate hiyo miwili ya ngano Ilikuwa na chachu ulifananisha nini? (b) Ni sababu gani zinazoweza kutolewa juu ya kuwapo kwa mikate miwili?
14 Katika sikukuu ya majuma ya halisi, au Pentekoste, sababu gani mikate miwili iliyotengezwa kwa nafaka ya mavuno ya ngano iliyokuwa imekuwa tayari karibuni ilitolewa kwa Yehova? Ilionyesha kwamba zaidi ya mtu moja angehusika katika utimizo wa jambo hilo. Mikate miwili hiyo ya ngano iliokwa pamoja na chachu. Jambo hilo linaonyesha kwamba wale wanaotimiza sikukuu hiyo wamechachishwa kwa dhambi, kwa kuzaliwa kiasili, kama vile walivyokuwa wale wanafunzi 120 wa Yesu asiyekuwa na dhambi, waliokuwa wakingojea Yerusalemu siku ya Jumapili Siwani 6, 33 W.K. Kuwapo kwa mikate miwili kwaweza kuonyesha pia kwamba wale wanaozaliwa kwa roho, wanafunzi waliotiwa mafuta wa Masihi Yesu wangetwaliwa kutoka kwa vikundi viwili duniani, kwanza kutoka kwa Wayahudi wa asili waliotahiriwa na baadaye kutoka kwa mataifa mengine yote ya ulimwengu, Watu wa Mataifa. Vikundi hivyo viwili, vyote pamoja, vilikuwa washiriki wa sadaka moja ya mfano ya kutikisiwa Yehova.—Efe. 2:13-18.
15. Mkate uliofananisha mkate wa Wayahudi ulitolewa kwa Yehova wakati gani, nako kuukubali kwake kulionyeshwaje?
15 Jambo hilo likiangaliwa kwa maoni hayo ya pili, wa kwanza wa mikate hiyo ya mfano, ukimaanisha Waisraeli waliotahiriwa, ulitolewa na Kuhani Mkuu Yesu kwa Yehova Mungu wakati ufaao kabisa, katika Siwani 6, ambayo ilikuwa siku ile ile ambayo katika hiyo kuhani mkuu wa Kiyahudi alitikisa mikate miwili ya halisi mbele za Yehova katika hekalu la Herode katika Yerusalemu. Kwa kuwa mikate hiyo miwili ya ngano haikuwa tena ya lazima kama mfano, Yehova hakuikubali na kwa hiyo Wayahudi waliokuwa wakisherehekea katika hekalu la Herode hawakupata zawadi ya roho takatifu. Wayahudi wale waliotaka kuona utimizo wa Yoeli 2:28, 29 juu yao walipaswa kuondoka katika hekalu hilo la halisi na kushirikiana na wanafunzi 120 wa Kristo ambao tayari walikuwa wametimiziwa unabii huo. Hivyo wapata 3,000 wao wakawa sehemu ya mkate wa mfano wa kutikiswa katika siku hiyo ya Pentekoste yenye sehemu mbili, 33 W.K.
16. Mkate wa pili wa mfano ulitolewa kwa Yehova wakati gani, na ni mpaka wakati gani mikate hiyo ya mfano imekuwa ikitimizwa?
16 Mkate wa pili wa mfano, ukimaanisha Watu wa Mataifa, au watu wasiokuwa Wayahudi, ulianza kutikiswa mbele za Yehova baadaye kwa kuruhusiwa kwa Wasamaria wenye kuamini kwenye kundi la Kikristo na baadaye kuruhusiwa kwa Mataifa wasiotahiriwa au watu wa mataifa kwa ujumla. Jambo hilo linafahamika baadaye kuwa lilitokea katika vuli ya mwaka 36 W.K. (Matendo, sura 8 na 10) Hiyo mikate miwili ya mfano imekuwa ikitimilizwa wakati wa karne 19 zilizopita. Mambo ya hakika yanaonyesha kwamba wengine wameongezwa wawe sehemu ya “mikate” hiyo katika nyakati za karibuni, hao wakiwa walifananishwa na Ruthu Mmoabi aliyepata kuwa nyanya wa Yesu Kristo na Malkia Esta, binamu wa Myahudi Mordekai aliyekuwa waziri mkuu wa Milki ya Uajemi.—Tazama kitabu Preservation, kilichochapwa katika mwaka 1932 na kuchapisha tena habari hiyo katika mfululizo wa makala zilizotokea katika matoleo ya Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) ya 1931 na 1932.
17. (a) Tendo la kutimiza wenye kushiriki mikate hiyo miwili ya mfano limekuwa sababu ya nini kwa washerehekeaji wa sikukuu hiyo? (b) Ni kwa sababu gani washiriki wa hiyo mikate ya mfano ni namna ya “malimbuko”?
17 Kukamilishwa kwa ile mikate miwili ya mfano ya Kipentekoste wakati wa zaidi ya miaka 1,900 sasa kumekuwa sababu ya kufurahi sana kwa Waisraeli wa kiroho wanaosherehekea sikukuu ya mfano ya majuma. Kama vile mikate miwili ya mfano ilivyofananisha malimbuko katika mwezi wa mavuno wa Siwani, ndivyo walio washiriki wa mikate hiyo miwili ya mfano yalivyo malimbuko kwa Yehova Mungu kupitia kwa Yesu Kristo, kwa kuwa wanatangulia wengine wa ulimwenguni wa wanadamu, wakipata urithi wa kimbinguni kama wenye kufaidika kwanza na dhabihu ya “Mwana-Kondoo wa Mungu.”—Yak. 1:18; Ufu. 14:4.
SIKUKUU YA VIBANDA
18. Sikukuu ya mwisho wa mwaka mtakatifu wa Kiyahudi ilikuwa ikiitwaje, na ilifanywa lini, nao ni nani waliopaswa kuishiriki?
18 Sikukuu ya mwisho ya mwaka mtakatifu wa Kiyahudi ilifanywa katika mwezi wa saba, mwezi wa Ethanimu, au Tishri. (1 Fal. 8:2) Ilikuwa na sherehe fulani fulani zenye kutokeza. Mara nyingi iliitwa sikukuu ya vibanda, walakini mara mbili inaitwa sikukuu ya kukusanya. (Kut. 23:16; 34:22) Kwa mfano, Kutoka 23:16, 17 lasema hivi: “Tena, sikukuu ya mavuno, hayo malimbuko ya kazi zako za kupanda mashambani; tena, sikukuu ya kukusanya, mwisho wa mwaka, hapo utakapokusanya hayo uliyoyataabikia shambani. Mara tatu katika mwaka watu waume wako wote watahudhuria mbele za [Yehova] Mungu.” Vilevile, Kutoka 34:22 lasema juu ya ‘sikukuu ya kukusanya vitu mwisho wa mwaka.’ Kumbukumbu la Torati 16:13-15 linaitaja kama sikukuu ya vibanda na kusema hivi: “Fanya [sikukuu] ya vibanda siku saba, utakapokwisha kuyakusanya yatokayo katika sakafu yako ya nafaka, na katika kinu chako cha divai; nawe utafurahi katika [sikukuu] yako, wewe, na mwanao, na binti yako, na mtumwa wako, na mjakazi wako, na Mlawi, na mgeni, na yatima, na mjane aliyefiwa na mumewe, walio ndani ya malango yako. Siku saba mfanyie [sikukuu Yehova], Mungu wako, mahali atakapochagua [Yehova]; kwa kuwa [Yehova], Mungu wako, atakubarikia katika maongeo yako yote, na katika kazi zote za mikono yako, nawe uwe katika kufurahi kabisa.”
19. (a) Ni kwa nini sikukuu hiyo ililingana na jina lake kwa namna ilivyosherehekewa? (b) Ni kwa sababu gani wakati wa kufanywa kwayo uliwafaa washerehekeaje?
19 Kwa sehemu kubwa, sikukuu hiyo inaitwa ‘sikukuu ya vibanda.’ Wakati wa siku zake saba Wayahudi wale waliokuwa wamekutanika Yerusalemu walifanya makao katika vibanda au hema, kwa kulingana na jina la sherehe hiyo. Ilianza siku tano baada ya Siku ya Upatanisho, ambayo ilifanyika kila mwaka katika Tishri 10 na ambayo kupitia kwayo taifa la Israeli lilirudishwa kwenye uhusiano wenye amani pamoja na Yehova Mungu. Kwa hiyo sikukuu ya vibanda ilianza wakati wenye pendeleo sana, nayo iliendelea kuanzia Tishri 15 mpaka Tishri 21, hesabu kamili ya siku.
20. Kulingana na maandishi ya kihistoria yasiyokuwamo ndani ya Biblia, kuhani alifanya nini kila asubuhi ya sikukuu hiyo?
20 Furaha yake haikuwa na mfano. Kulingana na maandishi ya kihistoria, kila siku ya sikukuu ilipoanza kuhani angechukua gudulia (mtungi) la dhahabu ambalo lingeweza kuchukua kipimo cha painti mbili (litre 1) za umajimaji naye angetelemka toka Yerusalemu mpaka mahali pale palipokuja kuitwa Birika la Siloamu. Wasomaji wetu ambao wamezuru Yerusalemu wa leo wanaweza kukumbuka namna walivyofika mahali palipoitwa Kisima cha Bikira, au Kisima cha Gihoni, walipotoka katika mji huo kupitia kwa Lango la Mavi katika pembe yake ya mashariki-kusini Kutoka kwa kisima hicho, Mfalme Hezekia alichimba mtaro mrefu wa chini ya ardhi wakati wa tisho la kushambuliwa na Waashuru. Watembezi waliopiga moyo konde wanaweza kukumbuka namna walivyotokea kwenye Birika la Siloamu, baada ya kuupitia mtaro huo.
21. (a) Kuhani aliendaje katika Birika la Siloamu, naye alifanya nini kwa kutumia maji ya Siloamu? (b) Kufurahi katika wakati huo kungekumbusha Wayahudi juu ya maneno gani ya unabii wa Isaya?
21 Si kwa kupitia mtaro mrefu wa chini ya ardhi wa Hezekia, bali akifuatwa na msafara mkubwa, kutia ndani kikundi cha wacheza muziki, kuhani huyo mwenye gudulia la dhahabu alikwenda kwenye Birika la Siloamu. Baada ya kulijaza gudulia hilo maji, kuhani huyo alirudi kwenye mji na kwenda kwenye ua mahali ambapo madhabahu ya Yehova ya dhabihu ilikuwa. Upande wa kusini wa madhabahu hiyo zilikuwapo bakuli mbali, kila moja ikiwa na shimo upande wa chini. Birika iliyokuwa katika upande wa magharibi-kusini ilikuwa ya maji yaliyotekwa katika Birika la Siloamu. Wakati kuhani alipoyamwaga ndani maji hayo, yalitiririka ndani na kumwagika kwenye sakafu ya madhabahu. Katika pindi hiyo Wayahudi waliokuwa wakiadhimisha walifurahi sana. Huenda hilo likawa lilikumbusha washerehekeaji hao wenye furaha juu ya Isaya, sura ya 12, inayosimulia furaha waliyopata Waisraeli baada ya kutolewa utumwani katika Babeli katika mwaka 537 K.W.K. Isaya 12:3 lasema hivi: “Basi, kwa furaha mtateka maji katika visima vya wokovu.”
22. Yehova alikuwaje Chanzo cha maji ya wokovu kwa babu za washerehekeaji Wayahudi?
22 Yehova Mungu ndiye aliyekuwa Chanzo cha kimbinguni cha wokovu wao. Ndiye Ambaye aliokoa babu zao kutoka uhamisho wa miaka 70 katika Babeli ya kipagani ambako walikuwa wamekuwa na kiu ya kupata wokovu baada ya kupinduliwa kwa Babeli katika mwaka 539 K.W.K. (Isa. 44:28 mpaka 45:7; Yer. 2:13) Kukumbuka wokovu huo kulikuwa sababu ya kufurahi wakati wa sikukuu ya vibanda.
[Picha katika ukurasa wa 8]
Suke la malimbuko ya mavuno ya shayiri linamfananisha Yesu aliyefufuliwa
[Picha katika ukurasa wa 9]
Mikate miwili inakubaliwa na Yehova mbinguni tangu Pentekoste