Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w80 8/1 kur. 13-19
  • Mwangaza wa Sikukuu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mwangaza wa Sikukuu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • SIKUKUU YA VIBANDA ILIYOFANANISHWA
  • WASHEREHEKEAJI WALIOCHUKUA MATAWI
  • Sikukuu Itakayosherehekewa na Mabilioni
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Misherehekeo ya Matukio Muhimu Katika Historia ya Israeli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Sikukuu za Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Ushindi wa Ibada ya Kweli Wakaribia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
w80 8/1 kur. 13-19

Mwangaza wa Sikukuu

1. Wakati wa sikukuu ya vibanda Yerusalemu ulimulikiwaje kipekee, nao Wayahudi walitendaje chini ya mwangaza huo?

WAKATI wa sikukuu ya vibanda ulikuwa wakati wa mwangaza wa pekee kwa “mji wa Mfalme mkuu,” Yehova. (Mt. 5:35) Kila siku katika hekalu la Herode, katika Ua wa Wanawake uliokuwa upande wa mashariki wa madhabahu, kulikuwako wonyesho wa kipekee. Taa nne kubwa ziliwekwa hapo. Kila mojawapo ilikuwa na bakuli nne kubwa. Ili kuzijaza bakuli hizo mafuta, ilikuwa lazima kutumia ngazi ili kuzifikia. Nguo kuukuu za makuhani zisizotumiwa tena zilitumika kama tambi kwa bakuli hizo za mafuta. Mwangaza uliotoka kwenye bakuli hizo 16 zenye mafuta yenye kuwaka ulikuwa na nguvu ya kutosha kumulikia Yerusalemu wote wakati wa usiku. Chini ya mwangaza huu mkubwa, wanaume Waisraeli waliokuwa ndani ya ule Ua wa Wanawake walicheza dansi au michezo ya kutumia viungo vya mwili, huku wanawake wakitazama chini kwenye tamasha hiyo wakiwa roshani (jukwaani) mwao. Waimbaji waliziimba zile Zaburi 15 za Kupanda huku Walawi wakicheza muziki. Hali hii ya kufurahi iliendelea usiku kucha.

2. Mataifa waliohudhuria sikukuu hiyo walikaa wapi wakati huo?

2 Mataifa wasiotahiriwa waliohudhuria sikukuu hiyo waliruhusiwa wakae kwenye Ua wa Mataifa peke yake, uliotenganishwa na Ua wa Israeli kwa Ukuta wa Mawe pamoja na Ua wa Nje.​—Angalia Matendo 21:28, 29, kuonyesha vizuizi walivyowekewa Mataifa hekaluni.

3, 4. (a) Wakati wa vuli ya mwaka 32 W.K., Yesu alihudhuriaje sikukuu hiyo, naye alisema jambo gani wakati huo ambalo lingewakumbusha Wayahudi juu ya maji ya Siloamu? (b) Kulingana na Yohana 7:39, Yesu alikuwa akisema juu ya nini?

3 Kwa sababu ya mambo yenye kutokeza yaliyoongezewa kwenye mwadhimisho wa sikukuu ya vibanda, twaweza kuthamini maneno fulani yenye kufaa yaliyosemwa na Yesu Kristo kuhusiana na sikukuu hiyo. Yeye aliadhimisha sikukuu hii kwa mara ya mwisho katika vuli ya mwaka wa 32 W.K. Kwa kuwa Wayahudi walikuwa wakitafuta kumwua, Yesu aliondoka Galilaya akiwa peke yake akakwea kwenda kwenye sikukuu hiyo kwa siri. Karibu na wakati wa katikati wa sikukuu hiyo, yaani, kama Tishri 18 hivi, alisimama mbele ya watu wote akaanza kuwafundisha, makutano waliokuwa wakisherehekea humo hekaluni.

4 Siku ya mwisho ya sikukuu hiyo, Tishri 21, ilikuwa ikiitwa “siku ile kubwa ya sikukuu.” Huenda katika siku hiyo Yesu aliwakumbusha watu juu ya kumwagwa kwa maji ya Siloamu aliposema hivi: “Mtu akiona kiu, na aje kwangu anywe. Aniaminiye mimi, kama vile maandiko yalivyonena, mito ya maji yaliyo hai itatoka ndani yake.” Mtume Yohana anatoa maelezo juu ya yale ambayo Yesu alisema wakati huo hivi: ‘Na neno hilo alilisema katika habari ya roho, ambayo wale wamwaminio wataipokea baadaye; kwa maana roho ilikuwa haijaja, kwa sababu Yesu alikuwa hajatukuzwa.’​—Yohana 7:37-39.

5. Maneno hayo yenye kustaajabisha yalianza kutimizwa wakati gani, na namna gani?

5 Maneno hayo yenye kustaajabisha yalianza kutimia katika siku ya Pentekoste ya mwaka uliofuata, wakati wanafunzi 120 hivi, waliokuwa wamekusanyika katika chumba cha orofa huko Yerusalemu, walipopokea roho takatifu waliyomiminiwa. Kwa hakika, tangu siku hiyo, mito yenye maji ya uhai ilianza kutiririka, waliponena kwa lugha nyingi walizopewa kimwujiza “matendo makuu ya Mungu” kwa Wayahudi elfu nyingi waliokuwa wamekusanyika kwa mshangao washuhudie tukio hilo.​—Matendo 2:1-41.

6. Yesu alisema jambo gani katika siku ya mwisho ambalo huenda likawa liliwakumbusha wanafunzi wake juu ya mwangaza wa pekee wa hekalu?

6 Katika siku ya saba na ya mwisho ya sikukuu ya vibanda, Yesu alisema jambo jingine ambalo huenda liliwakumbusha wanafunzi wake ule mwangaza wa pekee uliokuwa sehemu ya mwadhimisho huo, yaani, zile taa nne ndefu zilizowekwa kwenye Ua wa Wanawake wa hekalu. Yesu alisema hivi: “Mimi ndimi nuru ya ulimwengu, yeye anifuataye hatakwenda gizani kamwe, bali atakuwa na nuru ya uzima.”​—Yohana 8:12.

7. Ni kwa sababu gani lilikuwa jambo lenye kufaa sana kwamba Yesu ajiite “nuru ya ulimwengu” wakati wa sikukuu ya vibanda?

7 Ilifaa sana Yesu ajiite “nuru ya ulimwengu” katika sikukuu hii ya vibanda, kwa kuwa sikukuu hiyo ilikuwa kama sikukuu ya ulimwengu wote. Namna gani hivyo? Kwa kuwa “mgeni” aliyekuwamo ndani ya malango ya Israeli alisemekana kuwa alikuwa na haki ya kushiriki katika sherehe hiyo, akifurahi pamoja na watu wa Mungu walioteuliwa.​—Kum. 16:14.

8. (a) Ni Jambo gani lililokuwa la pekee sana kuhusiana na kutolewa dhabihu kwa ng’ombe dume katika siku kuu ya vibanda? (b) Kwa habari ya hesabu, hii inapatanaje na yale yaliyoandikwa katika Mwanzo sura ya 10, ikionyesha nini?

8 Kulingana na Hesabu 29:12-34, hesabu kubwa ya ng’ombe dume ilitolewa dhabihu. Katika siku ya kwanza ng’ombe dume 13 walitolewa, na katika siku sita zilizofuata hesabu ya ng’ombe dume waliotolewa ilipunguzwa kwa moja kila siku, kufikia siku ya saba na ya mwisho walipotolewa ng’ombe dume saba, siku ambayo katika hiyo Yesu alisema hivi: “Mimi ndimi nuru ya ulimwengu.” Hivyo, kufikia siku ya mwisho ya sikukuu hiyo ng’ombe dume 70 walikuwa wamekwisha tolewa. Hesabu 70 ni jumla ya 7 kujumlisha na 10, namba hizi mbili zikifananisha ukamilifu, 7 ikifananisha ukamilifu wa kiroho nayo 10, ikifananisha ukamilifu wa kilimwengu. Katika Tishri 10, ile Siku ya Upatanisho, ng’ombe dume mmoja tu ndiye aliyekuwa ametolewa kuwa dhabihu ya upatanisho. Walakini wakati wa siku saba za sikukuu ya vibanda, Tishri 15-21, ng’ombe dume 70 walitolewa. Kama mfano, hao wangeweza kutoa damu ya kutosha kusafisha na kuokoa ulimwengu mzima wa wanadamu. Hii inalingana na yale yaliyoandikwa katika Mwanzo sura ya 10. Humo majina ya kibinafsi ya vichwa vya jamaa na mataifa yanatolewa, kuanzia na Nuhu kupitia kwa wana wake watatu kufikia majina Mesha na Sefari. Jumla yake inakuwa majina 70, nayo yanaonekana yakihusu idadi yote ya watu waliokuwako katika kipindi hicho cha baada ya Gharika.

9. Yesu alijisema kuwa alikuwa “nuru” ya nani, nacho ni nini wanachohitaji wanadamu ili wapate uzima?

9 Kwa hiyo, katika wakati wenye kufaa, ilifaa sana kwamba Yesu Kristo atangaze, “Mimi ndimi nuru ya ulimwengu,” wala si nuru ya wafuasi wake watiwa mafuta peke yao. Kwa habari ya faida ya nuru, twakumbuka kwamba Mungu aliumba wanyama na mwishowe mwanamume na mwanamke wakamilifu, ili waifurahie nuru ya uzima, baada ya Mungu kusema, “Na iwe nuru,” na baada ya yeye kuumba jua, mwezi na nyota na kuziwezesha kuangaza dunia yetu. Leo, katika ulimwengu huu uliotiwa giza na dhambi na uliotenganishwa na Mungu, watu wote wanaweza kufaidika kutokana na nuru itokayo kwa Yesu Kristo, aliye “nuru ya ulimwengu.” Wote wanahitaji hiyo “nuru ya uzima.”​—Yohana 8:12; Mwa. 1:3.

SIKUKUU YA VIBANDA ILIYOFANANISHWA

10. Ni katika njia siku kuu ya vibanda inafanana na zile sikukuu nyingine mbili zilizotangulia, nayo ni mambo gani ya hakika tunayohitaji kufikiria hapa.

10 Kama vile ilivyokuwa kwa habari ya sikukuu mbili zilizotangulia zilizoamriwa na Mungu kwa watu wake walioteuliwa, vivyo hivyo sikukuu ya vibanda yapaswa kuwa na maana iliyofananishwa katika siku zetu. Kwa furaha ina utimizo uliofananishwa. Hivyo, basi, utimizo huo ulianza wakati gani? Sisi twaweza kuujuaje wakati huo? Kwa mambo ya mfano, pamoja na yale yaliyofananishwa, yaliyotukia kweli kweli.

11. Matukio ya hakika yaliyotukia kweli kweli yanaonyeshaje kama “mavuno” yanayotajwa katika Mathayo 13:39 yalianza katika mwaka 1914, au hapana?

11 Katika Mathayo, sura ya 13, Yesu Kristo alitutolea mfano ambao katika huo alizungumza juu ya kukusanywa kwa mazao ya shamba. Huu ulikuwa ule mfano wa ngano na magugu. Akieleza sehemu mbalimbali za mfano huo, Yesu alisema hivi: “Mavuno ni mwisho wa taratibu ya mambo.” (Mt. 13:39, NW) Unabii wa Biblia pamoja na hesabu ya nyakati, na vilevile matukio ya kihistoria, huthibitisha kwamba mwisho wa taratibu ya mambo ya leo ulianza katika mwaka 1914 W.K., wakati ambapo katika vuli ya mwaka huo “nyakati saba” za Mataifa kuitawala dunia pasipo kuingiliwa na ufalme wa Mungu wa Kimasihi zilikoma. (Dan. 4:23-25) Je! “mavuno” au kukusanywa kwa jamii ya “ngano” ya Wakristo wa kweli yalianza wakati huo? Hapana, kwa kuwa historia yaonyesha kwamba Wakristo waabudu wa Yehova walio wakf walitapanywa wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza iliyoanza katika mwaka 1914. Tengenezo lao la ulimwenguni pote lilivunjwa-vunjwa na adui za ufalme wa Kimasihi wa Yehova, ule ufalme wa kimbinguni uliokuwa ukitangazwa kwa bidii na hao wanafunzi watiwa mafuta, waliozaliwa kwa roho wa Mfalme anayetawala, Yesu Kristo. Kuvunjwa-vunjwa huko kwa tengenezo mwishowe kulifika mpaka kwenye makao makuu ya watu wa Yehova walio wakf, huko Brooklyn, New York, U.S.A., katika mwaka 1918.

12. Kazi ya kukusanya iliyotabiriwa na Yesu katika Mathayo 24:31 ilianza wakati gani, nayo ilionyesha mwanzo wa sikukuu gani?

12 Katika unabii wa Yesu juu ya “ishara” ya kuwapo kwake na ya mwisho wa taratibu hii ya mambo, yeye alisema hivi, katika Mathayo 24:31: “Naye atawatuma malaika zake pamoja na sauti kuu ya parapanda, nao watawakusanya wateule wake toka pepo nne, toka mwisho huu wa mbingu mpaka mwisho huu.” Maneno hayo yalitabiri juu ya kukusanywa pamoja kwa “wateule” wa Kristo kutoka sehemu zote ambako walikuwa wametawanywa. Kukusanywa huko kulianza katika mwaka 1919 uliofuata baada ya vita kumalizika, mara tu baada ya washiriki wa wafanya kazi wa makao makuu katika Brooklyn kufunguliwa, baada ya kutumikia kifungo cha miezi tisa katika gereza ya serikali kuu huko Atlanta, Georgia, U.S.A., Machi 25, 1919. Hivyo, ilikuwa katika mwaka huo wenye kukumbukwa sana kwamba sikukuu ya kukusanya, au ya vibanda iliyofananishwa ilipoanza kutimizwa. Tukio hilo lilionyeshwa na furaha kuu waliyokuwa nayo mabaki watiwa mafuta wa “wateule” wa Kristo ulimwenguni pote.

13. (a) Yesu alipozungumza juu ya mavuno katika Mathayo 13:39, yeye alikuwa akisema juu ya kuvunwa kwa watu gani? (b) Ni akina nani wa hao ambao walivunwa baada ya mwaka 1919?

13 Ili kuthibitisha jambo hili, lazima tukumbuke mambo fulani yaliyo mazito. Yesu aliposema, “Mavuno ni mwisho wa taratibu ya mambo,” yeye alikuwa akizungumza juu ya nini? Juu ya kukusanywa kwa “wana wa ufalme,” yaani, wale warithi waliozaliwa kwa roho wa ufalme wa kimbinguni. Hiyo ilikuwa jamii ya kiroho iliyotiwa mafuta, iliyofananishwa na ngano, nako kukusanywa kwao kulianza kweli kweli katika masika ya mwaka 1919. Kadiri wakati ulivyokuwa ukipita wengine zaidi walikusanywa pamoja zaidi ya wale warithi wa Ufalme waliokuwa wametawanywa na matukio ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Katika kipindi kilichofuata tangu mwaka 1919 na kuendelea wengine elfu nyingi walisimama upande wa ufalme wa Mungu uliosimamishwa wakajiweka wenyewe wakfu kwa Yehova, wakabatizwa, wakazaliwa kwa roho na kutiwa mafuta kwa roho ya Mungu, nao hao waliongezwa kwenye jamii ya kwanza ya mabaki. Hawa wapya walioongezwa, kama kikundi, walifananishwa na watu waliokuwa mashuhuri katika maigizo ya Biblia ya nyakati za kabla ya Ukristo. Watu hawa mashuhuri walikuwa Ruthu Mmoabi, aliyepata kuwa mwenzi mshikamanifu wa Naomi Myahudi, mama mkwewe, na vilevile Malkia Esta, ambaye Mordekai Myahudi, aliyepata kuwa waziri mkuu ya Milki ya Waajemi chini ya Mfalme Ahasuero, au Artashasta, alikuwa binamu yake.

14. Hivyo, ni jambo gani linaloonyesha mwanzo wa sikukuu ya kukusanya au ya vibanda iliyofananishwa?

14 Wote wawili Ruthu na Esta walipata kuwa na uhusiano na nasaba ya kifalme ya Daudi pamoja na kuhifadhiwa kwayo mpaka kufikia kuja kwa mara ya kwanza kwa Yesu, “mwana wa Daudi.” (Mt. 1:1, 5; Ruthu 4:18-22; Esta 4:13, 14) Kukusanywa kwa jamii ya Ruthu na Esta, pamoja na mabaki watiwa mafuta wa kwanza, kwaonyesha mwanzo wa kufunguliwa kwa sikukuu ya kukusanya au ya vibanda iliyofananishwa.

15. Sikukuu hiyo iliyofanywa majira ya vuli ilikuwa sikukuu ya nani, nao ni akina nani walioamriwa wakae katika vibanda wakati wa sherehe hiyo?

15 Jambo jingine: Katika nyakati za kabla ya Ukristo Wayahudi wa asili ndio walioadhimisha sikukuu ya mfano ya vibanda. Ndio walioamriwa na Yehova kupitia kwa Musa waiadhimishe. Kwa hiyo, katika wakati huo wa kukusanya wa vuli walimiminika Yerusalemu wakakaa katika vibanda huko. Hata wakaaji wa daima wa Yerusalemu walifanya vivyo hivyo. Sikukuu hiyo ya vibanda ilikuwa kumbukumbu la jambo lililokuwa limefanyika mapema. Jambo gani? Mambo ya Walawi 23:42, 43 hujibu likisema hivi: “Mtaketi katika vibanda muda wa siku saba; wazalia wote wa Israeli wataketi katika vibanda; ili vizazi vyenu vipate kujua ya kuwa niliwaketisha wana wa Israeli katika vibanda, hapo nilipowaleta kutoka nchi ya Misri; mimi ndimi [Yehova], Mungu wenu.” Wayahudi wazalia walifanya hivyo.

16. (a) Walipokuwa wakielekea katika Nchi ya Ahadi, lile ‘kundi kubwa lililochangamana’ Iiliishi namna gani pamoja na Waisraeli? (b) Katika hekalu la Herode katika siku za Yesu, Mataifa waliendelea kutenganishwaje na Waisraeli?

16 Bila shaka, “kundi kubwa la watu waliochangamana nao” wasiokuwa Waisraeli ‘waliokwea pamoja nao’ walilazimika kukaa hemani pia walipokuwa wakielekea kwenye Nchi ya Ahadi. (Kut. 12:38) Walakini amri ya kusherehekea sikukuu ya vibanda haikuelekezwa kwenye ‘kundi kubwa lililochangamana’ bali walipewa Israeli. Wala ‘kundi kubwa lililochangamana’ si ndilo lililopewa Nchi ya Ahadi bali iligawanywa kati ya yale makabila 12 ya Israeli wasiokuwa Walawi, nayo sheria ya Yubile ya kurudisha mashamba iliwahusu Waisraeli. Kwa hiyo sikukuu ya kukusanya sana sana ingewahusu Waisraeli. Kwa kuwafadhili, “wageni” waliruhusiwa washiriki. Wakati wa sherehe katika siku za Yesu Kristo, wale wasio Wayahudi, au Mataifa, waliruhusiwa wakae tu kwenye Ua wa Mataifa, Ukuta wa Mawe na Ua wa Nje ukiwatenganisha na Ua wa Israeli. Mahali pao palikuwa sehemu ya chini kabisa katika jengo hilo lote la hekalu ya Herode.

WASHEREHEKEAJI WALIOCHUKUA MATAWI

17, 18. Ni akina nani walioichukua ile “lulab”, nalo wazo lake lasemekana kuwa lilitokana na andiko gani?

17 Wakati wenyewe wa kusherehekea, Waisraeli ndio waliochukua lulabs (matawi) na ethrog (balungi). Ili kupata kiwazo kidogo cha kujulisha namna ilivyokuwa katika siku za Yesu, twaweza kusoma maelezo ya sherehe ya Kiyahudi kama vile yalivyoandikwa katika Nehemia 8:14-18. Ile lulab ilikuwa fungu la matawi ya miti mbalimbali nayo ilichukuliwa mkononi mwa msherehekeaji Myahudi. Inasemekana kwamba wazo lake linatokana na Mambo ya Walawi 23:40:

18 “Nanyi siku ya kwanza mtajipatia matunda ya miti mizuri, na makuti ya mitende, na matawi ya miti minene, na mierebi ya vijitoni; nanyi mtafurahi mbele za [Yehova], Mungu wenu, muda wa siku saba.”

19. (a) Hiyo “lulab” ilifanyizwa kwa vitu gani? (b) Waisraeli walifuata utaratibu gani kuichukua hiyo lulab, huku wakirudia-rudia kuimba wimbo gani?

19 Lulab ilifanyizwa kwa (1) chipukizi la mtende katika hali yake iliyokunjwa, (2) vitawi vitatu vya mhadasi vikiwa na majani yake, na (3) matawi mawili ya mwerebi, ambao mti wake ni mwekundu na ambao matawi yake ni marefu. Waisraeli walioichukua hiyo lulab waliitikisa-tikisa na kisha wakaitupa baada ya sikukuu kumalizika. Ile lulab pamoja na ethrog (tunda la namna ya balungi linalofanana na limau walakini halina kinundu kama vile limau katika upande mmoja) vilichukuliwa kwa maandamano kuizunguka madhabahu iliyokuwa katika Ua wa Makuhani, kuizunguka mara moja katika kila mojawapo ya zile siku sita za kwanza na mara saba katika siku ya saba na ya mwisho. Baada ya hapo lile tunda la ethrog, au balungi, lililiwa. Wakati wa maandamano, Zaburi 118:25 iliimbwa kwa kurudia-rudia maneno haya: “Ee [Yehova], utufanikishe, twakusihi”! Mataifa, wakiwa uani mwao hawakushiriki katika hayo yote.

20. Katika siku za Liwali Nehemia yeye aliwaambia Waisraeli katika Yerusalemu wawe na roho gani wakati sikukuu yao ya vibanda?

20 Wakati wa sikukuu ya vibanda katika siku za Nehemia, yeye akiwa liwali aliwaambia hivi Waisraeli waliokuwa wamerudi kutoka uhamishoni Babeli: “Siku hii ni takatifu kwa [Bwana] wetu; wala msihuzunike; kwa kuwa furaha ya [Yehova] ni nguvu zenu.” (Neh. 8:10) Waisraeli wa kiroho wa leo wapaswa wawe na maoni kama hayo tangu wakombolewe kutoka Babeli Mkuu katika mwaka 1919 W.K.

21. (a) Ni kwa sababu gani mabaki ya Waisraeli wa kiroho walifurahi katika masika ya mwaka 1919? (b) Wao walifikiria kwamba ni kazi ya namna gani iliyokuwa mbele yao, walakini ilionekana kuwa kazi ya namna gani?

21 Ni wazi kwamba utimizo wa sikukuu ya vibanda ulianza katika mwaka huo uliofuata baada ya vita. Kwa sababu ya matazamio yao ya mapema kabla ya mwaka huo, “wana wa ufalme” wa kiroho walitatizwa kidogo walipoingizwa katika kipindi hicho kilichofuata baada ya vita kumalizika. Walakini walifurahi sana walipokombolewa kutoka kwa Babeli Mkuu katika masika ya mwaka 1919. Mara hiyo wakaingia kwenye kazi ya kukusanya ambayo sasa ilikuwa mbele yao. Mwanzoni walifikiria kwamba ingekuwa ‘kazi ya kuokota-okota tu mavuno.’ Kuhusu jambo hili, angalia Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) wa Mei 1, 1919, chini ya makala “Mavuno Yamekwisha—Ni Nini Kitakachofuata?,” ukurasa 138, fungu 1. Walakini, badala ya kuwa kazi ya kuokota-okota tu mavuno, ilionekana kuwa ilikuwa kazi ya kuvuna kweli kweli.

22. Je! Waisraeli wa kiroho walitazamia kukaa katika paradiso ya duniani milele, nao wanajionaje katikati ya taratibu hii ya mambo?

22 Mabaki ya watiwa mafuta wavunaji walikuwa kana kwamba wanaishi katika “vibanda,” kwa kuwa hawakuwa wakiweka tamaa yao katika mambo ya kidunia. Wao hawakuwa wakitazamia kuishi katika paradiso ya kidunia katika wakati wote ujao. Walikuwa wakitazamia kuingia katika urithi wao wa kimbinguni pamoja na Bwana aliyetukuzwa, Yesu Kristo. Kwa hiyo waliyaona mambo kama vile ilivyoandikwa katika Waebrania 13:13, 14: “Basi na tutoke tumwendee nje ya kambi, tukichukua shutumu lake. Maana hapa hatuna mji udumuo, bali twautafuta ule ujao.” Kwa sababu hiyo, wao wanajiona kuwa “wapitaji na wasafiri” katikati ya taratibu hii ya mambo, kama vile walivyokuwa Ibrahimu, Isaka na Yakobo.​—1 Pet. 2:11; Mwa. 47:9; Kut. 6:4; Ebr. 11:13; Zab. 119:54.

23. (a) Je! mwangaza wa kiroho uliangaza sherehe ya mabaki ya sikukuu ya vibanda iliyofananishwa katika mwaka 1923? (b) Mfano wa Mathayo 25:31-46 ulionekana ukihusu nini?

23 Mwangaza wa kiroho ulianza kutokea kutoka katika hekalu la Yehova la kimbinguni na kuwaangazia wale mabaki watiwa mafuta waliokuwa wameanza kuingia sikukuu ya vibanda ya kisasa iliyofananishwa. Ulikuwa wakati wa kukusanywa kwa jamii ya kiroho iliyofananishwa na Ruthu na Esta kwamba mfano wa Yesu wa kondoo na mbuzi, kama vile ulivyoandikwa katika Mathayo 25:31-46, uliangazwa kipekee ili wapate nuru na kuufahamu. Wakati wa kusanyiko la watu wote la mwaka 1923 lililofanywa huko Los Angeles, California, U.S.A., msimamizi wa Sosaiti, ambaye sasa alikuwa amekuwa huru kwa miaka minne tangu atoke kifungoni huko Atlanta (Ga.), alizungumza juu ya mfano wa kondoo na mbuzi. Haukupaswa kungojea mpaka wakati wa utawala wa Yesu Kristo wa miaka elfu ili uanze kutimizwa. Jamii ya wale wa mfano wa kondoo ilikuwa tayari imeanza kufanyika. Washiriki wake walikuwa tayari wakionekana nao walikuwa wakifanyia mema mabaki ya “ndugu” wa kiroho wa Yesu Kristo aliyetukuzwa. Kichwa cha hotuba ya watu wote “Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Kamwe” kilikuwa kikitumiwa juu yao. Wao walikuwa wa “kondoo wengine” waliotajwa na Yesu katika Yohana 10:16.

24. Je! wakati huo jitihada zo zote zilifanywa katika kukusanya hao waliokuwa wakiwafanyia mema “ndugu” za kiroho za Kristo?

24 Katika wakati huo wa kutolewa maelezo hayo ya mfano wa Mathayo 25:31-46, hakuna jitihada za pekee zilizofanywa za kukusanya hao wa “kondoo wengine.” Walakini shukrani zilitolewa kwa ajili ya fadhili walizokuwa wakiwafanyia mabaki ya “ndugu” wa kiroho wa Kristo.

[Diagram/Picture katika ukurasa wa 17]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Lango

Matao

Lango

Lango

Tao la Kifalme

Tao la Sulemani

Lango

Tao la Kaskazini

Ua wa Mataifa

Ua wa Nje

Ukuta wa Mawe

Ua wa Wanawake

Ua wa Waisraeli

Ua wa Makuhani

Hekalu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki