Misherehekeo ya Matukio Muhimu Katika Historia ya Israeli
“Mara tatu kwa mwaka na watokee wanaume wako wote mbele za BWANA, Mungu wako, mahali atakapochagua . . . , wala wasitokee mbele za BWANA mikono mitupu.”—KUMBUKUMBU LA TORATI 16:16.
1. Ni nini liwezalo kusemwa juu ya pindi za msherehekeo nyakati za Biblia?
NI NINI huja akilini ufikiriapo msherehekeo? Misherehekeo fulani katika nyakati za kale ilitiwa alama na ujitiaji kupita kiasi na ukosefu wa adili. Hivyo ndivyo ilivyo kuhusu misherehekeo fulani ya siku ya kisasa. Lakini misherehekeo ambayo imeonyeshwa katika Sheria ya Mungu kwa Israeli ilikuwa tofauti. Ingawa zilikuwa pindi zenye shangwe, zingeweza pia kufafanuliwa kuwa “makusanyiko matakatifu.”—Mambo ya Walawi 23:2.
2. (a) Wanaume Waisraeli walitakwa wafanye nini mara tatu kwa mwaka? (b) Kama vile litumiwavyo kwenye Kumbukumbu la Torati 16:16, NW, neno “msherehekeo” ni nini?
2 Wanaume Waisraeli waaminifu—mara nyingi wakiandamana na familia zao—walipata raha yenye kuburudisha katika kusafiri kwenda Yerusalemu, ‘mahali BWANA alipochagua,’ nao walichangia kwa ukarimu misherehekeo mikubwa mitatu. (Kumbukumbu la Torati 16:16) Kitabu Old Testament Word Studies hufasili neno la Kiebrania litafsiriwalo “msherehekeo” kwenye Kumbukumbu la Torati 16:16, NW, kuwa “pindi ya shangwe kuu . . . ambayo katika hiyo nyakati mashuhuri zenye upendeleo wa Mungu zilisherehekewa kwa dhabihu na karamu.”a
Thamani ya Misherehekeo Mikubwa
3. Misherehekeo mitatu ya kila mwaka yakumbusha baraka zipi?
3 Kwa kuwa jamii yao ilikuwa ya wakulima, Waisraeli walitegemea baraka ya Mungu katika namna ya mvua. Hiyo misherehekeo mikubwa mitatu katika Sheria ya Kimusa ilisadifiana na kukusanywa kwa mavuno ya shayiri mwanzoni mwa masika, mavuno ya ngano mwishoni-mwishoni mwa masika, na yale mavuno mengine mwishoni-mwishoni mwa kiangazi. Hizo zilikuwa pindi za kushangilia kukubwa na za shukrani kwa Mtegemezaji wa duru ya mvua na Mfanyi wa nchi yenye kuzaa. Lakini hiyo misherehekeo ilihusisha mengi zaidi.—Kumbukumbu la Torati 11:11-14.
4. Msherehekeo wa kwanza ulikuwa wa kusherehekea tukio gani la kihistoria?
4 Msherehekeo wa kwanza ulifanyika katika mwezi wa kwanza wa kalenda ya kale ya Biblia, kutoka Nisani 15 hadi Nisani 21, wakati ulinganao na mwisho-mwisho wa mwezi wetu wa Machi au mwanzoni mwa mwezi wetu wa Aprili. Uliitwa Msherehekeo wa Keki Zisizotiwa Chachu, na kwa sababu ulifuata mara tu baada ya Sikukuu ya Kupitwa ya Nisani 14, uliitwa pia “msherehekeo wa sikukuu ya kupitwa.” (Luka 2:41; Mambo ya Walawi 23:5, 6) Msherehekeo huo ulikumbusha Israeli kukombolewa kwao kutoka kwenye taabu kubwa huko Misri, keki zisizotiwa chachu zikiitwa “mikate ya mateso.” (Kumbukumbu la Torati 16:3) Uliwakumbusha kwamba kukimbia kwao kutoka Misri kulikuwa kwa hima hivi kwamba hakukuwa na wakati wa kuongeza chachu kwenye kinyunya chao na kukingojea kifure. (Kutoka 12:34) Wakati huo wa msherehekeo hakuna mkate uliotiwa chachu uliopaswa kupatikana nyumbani mwa Mwisraeli. Msherehekeaji yeyote, kutia na mkazi kutoka nchi nyingine, aliyekula mkate uliotiwa chachu alipaswa kuadhibiwa kwa kifo.—Kutoka 12:19.
5. Huenda msherehekeo wa pili ukawa ulikumbusha pendeleo gani, na nani ambao walipaswa kutiwa ndani katika huko kushangilia?
5 Msherehekeo wa pili ulifanyika majuma saba (siku 49) baada ya Nisani 16 na uliangukia siku ya 6 ya mwezi wa tatu, uitwao Sivani, unaolingana na mwisho-mwisho wa mwezi wetu wa Mei. (Mambo ya Walawi 23:15, 16) Uliitwa Msherehekeo wa Majuma (katika siku ya Yesu, uliitwa Pentekoste, neno lililomaanisha “-a Hamsini” katika Kigiriki), nao ulifanyika karibu na wakati uleule wa mwaka ambapo Waisraeli waliingia katika agano la Sheria kwenye Mlima Sinai. (Kutoka 19:1, 2) Huenda ikawa wakati wa msherehekeo huo Waisraeli waaminifu walitafakari juu ya pendeleo lao la kuwekwa kando wakiwa taifa takatifu la Mungu. Kuwa kwao watu wa pekee wa Mungu kulitaka utii kwa Sheria ya Mungu, kama vile ile amri ya kuwajali waliokuwa katika hali ngumu ili wao pia waweze kuonea shangwe huo msherehekeo.—Mambo ya Walawi 23:22; Kumbukumbu la Torati 16:10-12.
6. Msherehekeo wa tatu uliwakumbusha watu wa Mungu jambo gani lililoonwa?
6 Wa mwisho katika hiyo misherehekeo mikubwa mitatu uliitwa Msherehekeo wa Kukusanya, au Msherehekeo wa Vibanda. Ulifanyika mwezi wa saba, uitwao Tishri, au Ethanimu, kuanzia siku ya 15 hadi siku ya 21, wakati unaolingana na mwanzo wa mwezi wetu wa Oktoba. (Mambo ya Walawi 23:34) Wakati huo, watu wa Mungu walikaa nje ya nyumba zao au juu ya paa zao katika vibanda vya muda vilivyotengenezwa kutokana na matawi na majani ya miti. Hilo liliwakumbusha safari yao ya miaka 40 kutoka Misri kwenda Bara Lililoahidiwa, wakati ambapo taifa lilipaswa kujifunza kumtegemea Mungu kwa mahitaji yao ya kila siku.—Mambo ya Walawi 23:42, 43; Kumbukumbu la Torati 8:15, 16.
7. Twanufaikaje na kupitia sherehe za misherehekeo katika Israeli la kale?
7 Acheni tupitie misherehekeo fulani iliyothibitika kuwa matukio muhimu katika historia ya watu wa kale wa Mungu. Hilo lapaswa kututia moyo leo, kwa kuwa sisi pia twaalikwa kukusanyika pamoja kwa ukawaida kila juma na mara tatu kwa mwaka katika makusanyiko na mikusanyiko mikubwa.—Waebrania 10:24, 25.
Wakati wa Wafalme wa Kidaudi
8. (a) Ni sherehe ipi ya kihistoria iliyofanywa katika siku za Mfalme Solomoni? (b) Ni upeo upi mtukufu wa ufananisho halisi wa Msherehekeo wa Vibanda ambao twaweza kutazamia kwa hamu?
8 Sherehe ya kihistoria wakati wa Msherehekeo wa Vibanda ilifanyika wakati wa utawala wa Mfalme Solomoni, mwana wa Daudi. “Kusanyiko kubwa sana” lilikusanyika kutoka ncha za Bara Lililoahidiwa kwa ajili ya Msherehekeo wa Vibanda na kwa ajili ya kuwekwa wakfu kwa hekalu. (2 Mambo ya Nyakati 7:8) Ulipokamilika, Mfalme Solomoni aliwaaga washerehekeaji, ambao ‘walimbarikia mfalme wakaenda hemani kwao, wakifurahi na kuchangamka moyoni kwa wema wote BWANA aliomfanyia Daudi mtumishi wake, na Israeli watu wake.’ (1 Wafalme 8:66) Kwa kweli huo ulikuwa msherehekeo wa tukio muhimu. Leo, watumishi wa Mungu watazamia kwa hamu upeo mtukufu wa ufananisho halisi wa Msherehekeo wa Vibanda mwishoni mwa Utawala wa Miaka Elfu wa Solomoni Mkubwa Zaidi, Yesu Kristo. (Ufunuo 20:3, 7-10, 14, 15) Wakati huo, watu wanaoishi katika kila pembe ya dunia, kutia na wenye kufufuliwa na waokokaji wa Har–Magedoni, wataungana katika kumwabudu Yehova Mungu kwa shangwe.—Zekaria 14:16.
9-11. (a) Ni nini kilichoongoza kwenye msherehekeo wa tukio muhimu katika utawala wa Mfalme Hezekia? (b) Ni kielelezo gani kilichowekwa na wengi kutoka katika ufalme wa kaskazini wa makabila kumi, nacho chatukumbusha nini leo?
9 Msherehekeo mwingine wenye kutokeza ambao umeripotiwa katika Biblia ulifanyika baada ya utawala wa Mfalme mwovu Ahazi, aliyekuwa amelifunga hekalu na kuuongoza ufalme wa Yuda kuingia katika uasi-imani. Mwandamizi wa Ahazi alikuwa Mfalme mzuri Hezekia. Mwaka wa kwanza wa utawala wake, akiwa na umri wa miaka 25, Hezekia alianza programu kubwa ya urudisho na rekebisho. Alifungua hekalu mara moja na kufanya mpango lirekebishwe. Kisha mfalme akawapelekea barua Waisraeli waliokuwa wakiishi katika ufalme wa Israeli wa makabila kumi wa kaskazini uliokuwa wenye uhasama, akiwaalika waje kusherehekea Sikukuu ya Kupitwa na Msherehekeo wa Keki Zisizotiwa Chachu. Wengi walikuja, wajapodhihakiwa na binadamu wenzao.—2 Mambo ya Nyakati 30:1, 10, 11, 18.
10 Je, huo msherehekeo ulifanikiwa? Biblia yaripoti hivi: “Nao wana wa Israeli waliohudhuria Yerusalemu wakafanya sikukuu ya mikate isiyochachawa [“isiyotiwa chachu,” NW] siku saba kwa furaha kubwa; Walawi na makuhani wakamsifu BWANA siku kwa siku, wakimwimbia BWANA kwa vinanda vyenye sauti kuu.” (2 Mambo ya Nyakati 30:21) Waisraeli hao waliweka kielelezo kizuri kama nini kwa watu wa Mungu leo, ambao wengi wao huvumilia upinzani na husafiri mwendo mrefu ili kuhudhuria mikusanyiko!
11 Kwa kielelezo, fikiria “Ujitoaji Kimungu” Mikusanyiko ya Wilaya mitatu iliyofanywa Poland mwaka wa 1989. Miongoni mwa wahudhuriaji 166,518 kulikuwa na vikundi vikubwa kutoka ule uliokuwa Muungano wa Sovieti na nchi nyingine za Ulaya Mashariki ambako wakati huo kazi ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa imepigwa marufuku. “Kwa baadhi ya watu waliohudhuria mikusanyiko hiyo,” charipoti kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu,b “ilikuwa mara ya kwanza ambayo walipata wakati wowote kuwa kwenye mkusanyiko mkubwa wa watu wa Yehova zaidi ya 15 au 20. Mioyo yao ilijaa uthamini walipokuwa wakitazama makumi ya maelfu katika stediamu hizo, wakijiunga katika sala, na kuunganisha sauti zao katika nyimbo za sifa kwa Yehova.”—Ukurasa wa 279.
12. Ni nini kilichoongoza kwenye msherehekeo wa tukio muhimu katika utawala wa Mfalme Yosia?
12 Baada ya kifo cha Hezekia, Wayudea waliangukia tena ibada isiyo ya kweli chini ya Mfalme Manase na Mfalme Amoni. Kisha ukaja utawala wa mfalme mwingine mzuri, Yosia mchanga, aliyetenda kwa ujasiri katika kurudisha ibada ya kweli. Akiwa na umri wa miaka 25, Yosia aliamuru kwamba hekalu lirekebishwe. (2 Mambo ya Nyakati 34:8) Huko kurekebishwa kulipokuwa kukiendelea, Sheria iliyoandikwa na Musa ilipatikana ndani ya hilo hekalu. Mfalme Yosia alichochewa sana na yale aliyosoma katika Sheria ya Mungu, akapanga isomewe watu wote. (2 Mambo ya Nyakati 34:14, 30) Kisha, kulingana na yaliyoandikwa, alipanga sherehe ya Sikukuu ya Kupitwa. Mfalme pia aliweka kielelezo chema kwa kuchangia kwa ukarimu hiyo pindi. Tokeo ni kwamba, Biblia yaripoti hivi: “Wala haikufanyika pasaka kama ile katika Israeli tangu siku za nabii Samweli.”—2 Mambo ya Nyakati 35:7, 17, 18.
13. Sherehe za misherehekeo ya Hezekia na Yosia zatukumbusha nini leo?
13 Marekebisho ya Hezekia na ya Yosia yalingana na urudisho wenye kustaajabisha wa ibada ya kweli ambao umetokea miongoni mwa Wakristo wa kweli tangu kutawazwa kwa Yesu Kristo mwaka wa 1914. Kama ilivyokuwa kweli hasa kwa marekebisho ya Yosia, urudisho huo wa siku ya kisasa umetegemezwa juu ya yale ambayo yameandikwa katika Neno la Mungu. Na, kwa kulingana na siku za Hezekia na za Yosia, urudisho wa siku ya kisasa umetiwa alama na makusanyiko na mikusanyiko ambako maelezo yenye kusisimua juu ya unabii wa Biblia na juu ya matumizi ya kanuni za Biblia ya wakati ufaao yamekaziwa. Yenye kuongezea shangwe ya pindi hizi za mafundisho ni idadi kubwa ya waliobatizwa. Kama Waisraeli wenye kutubu katika siku za Hezekia na za Yosia, watu waliobatizwa karibuni wameyaacha mazoea maovu ya Jumuiya ya Wakristo na sehemu nyinginezo za ulimwengu wa Shetani. Mwaka wa 1997 zaidi ya watu 375,000 walibatizwa wakionyesha wakfu wao kwa yule Mungu mtakatifu, Yehova—wastani wa watu zaidi ya 1,000 kwa siku.
Baada ya Uhamisho
14. Ni nini kilichoongoza kwenye msherehekeo wa tukio muhimu katika mwaka wa 537 K.W.K.?
14 Baada ya kifo cha Yosia, hilo taifa liligeukia tena ibada isiyo ya kweli, yenye kushusha. Mwishowe, mwaka wa 607 K.W.K., Yehova aliadhibu watu wake kwa kuyaleta majeshi ya Babiloni dhidi ya Yerusalemu. Hilo jiji na hekalu lake liliharibiwa na nchi ikaachwa ukiwa. Ilifuata miaka 70 ya utekwa wa Wayahudi katika Babiloni. Kisha Mungu akahuisha mabaki ya Wayahudi wenye kutubu, waliorudi kwenye Bara Lililoahidiwa ili kurudisha upya ibada ya kweli. Waliwasili kwenye jiji lililoangamizwa la Yerusalemu mwezi wa saba wa mwaka wa 537 K.W.K. Jambo la kwanza walilofanya lilikuwa kujenga madhabahu ili kutoa dhabihu za kila siku kama ilivyoonyeshwa katika agano la Sheria. Jambo hilo lilifanywa wakati uliofaa kabisa kwa ajili ya msherehekeo mwingine wa kihistoria. “Wakaishika Sikukuu ya Vibanda, kama ilivyoandikwa.”—Ezra 3:1-4.
15. Ni kazi gani iliyokuwa mbele ya mabaki waliorudishwa mwaka wa 537 K.W.K., na ni jinsi gani hali yenye kulingana nayo ilikuwako mwaka wa 1919?
15 Kazi kubwa ilikuwa mbele ya wahamishwa hao waliorudishwa—kujengwa upya kwa hekalu la Mungu na kwa Yerusalemu pamoja na kuta zake. Kulikuwa na upinzani mwingi kutoka kwa majirani wenye wivu. Hekalu lilipokuwa likijengwa, ilikuwa “siku ya mambo madogo.” (Zekaria 4:10) Hiyo hali ililingana na hali ya Wakristo watiwa-mafuta waaminifu mwaka wa 1919. Mwaka huo ulio wa kukumbukwa, waliachiliwa kutoka katika utekwa wa kiroho wa Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli. Idadi yao ilikuwa elfu chache tu na walikabili ulimwengu wenye uhasama. Je, adui za Mungu wangeweza kuzuia kusonga mbele kwa ibada ya kweli? Jibu la swali hilo lakumbusha ile misherehekeo miwili iliyorekodiwa katika Maandiko ya Kiebrania.
16. Ni nini kilichokuwa cha maana juu ya msherehekeo fulani mwaka wa 515 K.W.K.?
16 Mwishowe hekalu lilijengwa upya mwezi wa Adari wa mwaka wa 515 K.W.K., wakati uliofaa kabisa kwa ajili ya msherehekeo wa Nisani ya wakati wa masika. Biblia yaripoti hivi: “Wakaifanya sikukuu ya mikate isiyotiwa chachu kwa furaha, kwa muda wa siku saba; kwa kuwa BWANA amewafurahisha, na kumgeuza moyo mfalme wa Ashuru, awaelekee, ili awatie nguvu mikono yao katika kazi hiyo ya nyumba ya Mungu, Mungu wa Israeli.”—Ezra 6:22.
17, 18. (a) Ni msherehekeo gani wa tukio muhimu uliofikiwa mwaka wa 455 K.W.K.? (b) Tukoje katika hali kama hiyo leo?
17 Miaka 60 baadaye, mwaka wa 455 K.W.K., tukio jingine muhimu lilifikiwa. Mwaka huo Msherehekeo wa Vibanda ulitia alama ukamilisho wa kujengwa upya kwa kuta za Yerusalemu. Biblia yaripoti hivi: “Mkutano wote wa watu, waliorudi kutoka nchi ya uhamisho wao, wakafanyiza vibanda, wakakaa katika vibanda hivyo; maana tokea siku za Yoshua, mwana wa Nuni, hata siku ile, wana wa Israeli hawakufanya hivyo. Pakawa na furaha kubwa sana.”—Nehemia 8:17.
18 Ni urudisho wa kukumbukwa wa ibada ya kweli ya Mungu ulioje kujapokuwa na upinzani mkali! Hali leo iko vivyo hivyo. Kujapokuwa ongezeko la mnyanyaso na upinzani, ile kazi tukufu ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu imefika hadi miisho ya dunia, na ujumbe mbalimbali wa hukumu ya Mungu umevumishwa kotekote. (Mathayo 24:14) Kutiwa muhuri kwa mwisho kwa wanaobaki wa wale watiwa-mafuta 144,000 kwakaribia. “Kondoo wengine” zaidi ya milioni tano walio waandamani wao wamekusanywa kutoka mataifa yote kuwa “kundi moja” pamoja nao. (Yohana 10:16; Ufunuo 7:3, 9, 10) Ni utimizo ulioje wa huo ufananisho halisi wa kiunabii wa Msherehekeo wa Vibanda! Nayo kazi hiyo tukufu ya kukusanya itaendelea hadi ulimwengu mpya wakati ambapo mabilioni ya wenye kufufuliwa yataalikwa kujiunga katika kusherehekea ufananisho halisi wa Msherehekeo wa Vibanda.—Zekaria 14:16-19.
Karne ya Kwanza W.K.
19. Ni nini kilichofanya Msherehekeo wa Vibanda mwaka wa 32 W.K. uwe wenye kutokeza?
19 Bila shaka miongoni mwa sherehe za misherehekeo zenye kutokeza zilizorekodiwa katika Biblia zilikuwa zile ambazo Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, alihudhuria. Kwa kielelezo, fikiria kuhudhuria kwa Yesu Msherehekeo wa Vibanda (au, Tabenakulo) mwaka wa 32 W.K. Alitumia pindi hiyo kufundisha kweli zenye maana na kutegemeza mafundisho yake kwa kunukuu kutoka Maandiko ya Kiebrania. (Yohana 7:2, 14, 37-39) Sehemu ya kawaida ya msherehekeo huo ilikuwa ile desturi ya kuwasha vinara vikubwa vyenye mishumaa mingi katika ua wa ndani wa hekalu. Hilo lilichangia kule kufurahia utendaji mbalimbali wa msherehekeo ulioendelea mpaka usiku. Yaonekana, Yesu alirejezea taa hizo kubwa aliposema hivi: “Mimi ni nuru ya ulimwengu. Yeye anifuataye mimi hatatembea kwa vyovyote katika giza, bali atakuwa na nuru ya uhai.”—Yohana 8:12.
20. Kwa nini Sikukuu ya Kupitwa ya mwaka wa 33 W.K. ilikuwa yenye kutokeza?
20 Kisha ikafika Sikukuu ya Kupitwa na Msherehekeo wa Keki Zisizotiwa Chachu wa mwaka wenye maana wa 33 W.K. Siku ya Sikukuu hiyo ya Kupitwa, Yesu alifishwa na maadui wake, akafananisha kihalisi Mwana-Kondoo wa Sikukuu ya Kupitwa, aliyekufa ili aondolee mbali “dhambi ya ulimwengu.” (Yohana 1:29; 1 Wakorintho 5:7) Siku tatu baadaye, katika Nisani 16, Mungu alimfufua Yesu akiwa na mwili wa roho usioweza kufa. Jambo hilo lilisadifiana na kutolewa kwa matunda ya kwanza ya mavuno ya shayiri kama ilivyoagizwa na Sheria. Hivyo, Bwana Yesu Kristo aliyefufuliwa akawa “matunda ya kwanza kati ya wale ambao wamelala usingizi katika kifo.”—1 Wakorintho 15:20.
21. Ni nini kilichotukia kwenye Pentekoste mwaka wa 33 W.K.?
21 Msherehekeo wenye kutokeza kikweli ulikuwa Pentekoste 33 W.K. Siku hiyo Wayahudi na wageuzwa-imani wengi, kutia na wanafunzi wa Yesu wapatao 120 walikusanyika Yerusalemu. Huo msherehekeo ulipokuwa ukiendelea, Bwana Yesu Kristo aliyekuwa amefufuliwa alimwaga roho takatifu ya Mungu juu ya hao 120. (Matendo 1:15; 2:1-4, 33) Kwa hiyo walitiwa-mafuta, wakawa taifa jipya la Mungu lililochaguliwa kupitia agano jipya ambalo lilipatanishwa na Yesu Kristo. Wakati wa msherehekeo huo kuhani wa cheo cha juu wa Kiyahudi alitolea Mungu mikate miwili iliyotiwa chachu ambayo ilitengenezwa kutokana na matunda ya kwanza ya mavuno ya ngano. (Mambo ya Walawi 23:15-17) Mikate hiyo iliyotiwa chachu yafananisha wale wanadamu wasio wakamilifu 144,000 ambao Yesu ‘aliwanunua kwa ajili ya Mungu’ ili watumikie wakiwa ‘ufalme na makuhani, watawale wakiwa wafalme juu ya dunia.’ (Ufunuo 5:9, 10; 14:1, 3) Uhakika wa kwamba watawala hao wa kimbingu hutokana na matawi mawili ya wanadamu wenye dhambi, Wayahudi na Wasio Wayahudi, huenda ukafananishwa na ile mikate miwili iliyotiwa chachu.
22. (a) Kwa nini Wakristo hawasherehekei misherehekeo ya agano la Sheria? (b) Tutachunguza nini katika makala inayofuata?
22 Agano jipya lilipoanza kutenda kazi kwenye Pentekoste ya 33 W.K., hilo lilimaanisha kwamba agano la zamani la Sheria lilikuwa limeacha kuwa na thamani machoni pa Mungu. (2 Wakorintho 3:14; Waebrania 9:15; 10:16) Jambo hilo halimaanishi kwamba Wakristo watiwa-mafuta hawana sheria. Wao huja chini ya sheria ya kimungu iliyofundishwa na Yesu Kristo na kuandikwa mioyoni mwao. (Wagalatia 6:2) Kwa hiyo, ile misherehekeo mitatu ya kila mwaka, ikiwa sehemu ya Sheria ya agano la zamani, haisherehekewi na Wakristo. (Wakolosai 2:16, 17) Hata hivyo, twaweza kujifunza mengi kutokana na mtazamo wa watumishi wa Mungu wa kabla ya Ukristo kuelekea misherehekeo yao na mikutano yao mingine kwa ajili ya ibada. Katika makala yetu inayofuata, tutachunguza vielelezo ambavyo bila shaka vitachochea wote wafahamu uhitaji wa kuwa wa kawaida katika kuhudhuria makusanyiko ya Kikristo.
[Maelezo ya Chini]
a Ona pia kichapo Insight on the Scriptures, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc., Buku la 1, ukurasa wa 820, safu ya 1, fungu la 1 na la 3, chini ya “Festival” (Msherehekeo).
b Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
Maswali ya Kupitia
◻ Misherehekeo mikubwa mitatu ya Waisraeli ilitimiza kusudi gani?
◻ Misherehekeo ya Hezekia na ya Yosia ilitia ndani nini?
◻ Ni tukio gani muhimu lililosherehekewa mwaka wa 455 K.W.K., na ni kwa nini hilo latutia moyo?
◻ Ni nini kilichokuwa cha maana juu ya Sikukuu ya Kupitwa na Pentekoste mwaka wa 33 W.K.?
[Sanduku katika ukurasa wa 12]
Somo la Msherehekeo Kwetu Leo
Wale wote ambao wangenufaika kwa umilele na dhabihu ya Yesu ya kufunika dhambi lazima waishi kwa kupatana na kilichofananishwa na Msherehekeo wa Keki Zisizotiwa Chachu. Msherehekeo huo wa ufananisho halisi ulikuwa sherehe yenye shangwe ya Wakristo watiwa-mafuta iliyohusu kukombolewa kwao kutoka ulimwengu huu mwovu na kuachiliwa kutoka hatia ya dhambi kupitia fidia ya Yesu. (Wagalatia 1:4; Wakolosai 1:13, 14) Ule msherehekeo halisi ulidumu kwa siku saba—nambari itumiwayo katika Biblia kufananisha ukamili wa kiroho. Msherehekeo wa ufananisho halisi hudumu kwa wakati kamili ambapo kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta linakuwa duniani na lazima usherehekewe kwa “weupe wa moyo na kweli.” Hilo lamaanisha kuwa wenye kulinda daima dhidi ya chachu ya kitamathali. Chachu hutumiwa katika Biblia kufananisha mafundisho yenye ufisadi, unafiki, na ubaya. Waabudu wa kweli wa Yehova lazima wachukie chachu hiyo, bila kuiruhusu ifisidi maisha yao na bila kuiruhusu iharibu utakato wa kutaniko la Kikristo.—1 Wakorintho 5:6-8; Mathayo 16:6, 12.
[Picha katika ukurasa wa 9]
Mganda wa mavuno mapya ya shayiri ulitolewa kila mwaka katika Nisani 16, siku aliyofufuliwa Yesu
[Picha katika ukurasa wa 10]
Huenda Yesu akawa alirejezea taa za msherehekeo alipojiita “nuru ya ulimwengu”