Aristarko—Mwandamani Mwenye Uaminifu-Mshikamanifu
MIONGONI mwa wafanyakazi wenzi wengi walioitibariwa wa mtume Paulo alikuwa Aristarko. Unafikiria nini usikiapo jina lake? Je, jambo lolote linakuja katika akili yako? Ungeweza kusema ni sehemu gani aliyotimiza katika historia ya Wakristo wa mapema? Ingawa huenda Aristarko asiwe mmoja kati ya watu mashuhuri katika Biblia ambao tunawafahamu sana, hata hivyo alihusika katika matukio mengi yanayosimuliwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.
Hivyo, basi, Aristarko alikuwa nani? Alikuwa na uhusiano gani na Paulo? Kwa nini inaweza kusemwa kwamba Aristarko alikuwa mwandamani mwenye uaminifu-mshikamanifu? Na tunaweza kujifunza masomo gani kutokana na kuchunguza kielelezo chake?
Aristarko aingia kwa kutazamisha katika simulizi la kitabu cha Matendo wakati wa kelele nyingi na mvurugo wa kikundi cha wafanya-ghasia chenye hamaki katika jiji la Efeso. (Matendo 19:23-41) Kazi ya kutengeneza vihekalu vya fedha vya mungu asiye wa kweli Artemi ilikuwa ya faida kubwa kwa Demetrio na Waefeso wengine wafua-fedha. Hivyo basi, wakati kampeni ya kuhubiri ya Paulo katika jiji hilo ilipofanya idadi kubwa ya watu kuacha ibada isiyo safi ya huyu mungu-mke, Demetrio aliwachochea wasanii wengine. Aliwaambia kwamba kazi ya kuhubiri ya Paulo haikuwa tisho tu kwa usalama wao wa kifedha bali pia ilitokeza uwezekano wa kukoma kwa ibada ya Artemi.
Baada ya kushindwa kumpata Paulo, hicho kikundi cha wafanya-ghasia chenye hasira kiliwakokota kwa nguvu waandamani wa Paulo, Aristarko na Gayo hadi ndani ya mahali pa michezo. Kwa vile hao wawili walikuwa katika hatari kubwa, rafiki za Paulo walimwomba “asijihatarishe mwenyewe mahali pa michezo.”
Jifikirie ukiwa katika hali hiyo. Kwa muda wa karibu saa mbili, hicho kikundi cha wafanya-ghasia chenye hamaki kiliendelea kupiga kelele, “Ni Mkubwa Artemi wa Waefeso!” Wakijikuta chini ya udhibiti kamili wa umati huo wenye ushupavu bila hata kuweza kujitetea ni lazima kuliwaogopesha sana Aristarko na Gayo. Lazima wawe walijiuliza ikiwa wangeweza kuokoka. Kwa uzuri, waliokoka. Kwa kweli, udhahiri wa simulizi la Luka umewaongoza baadhi ya wasomi kufikiri kwamba alipata ushuhuda kutoka kwa watu waliojionea kwa macho, labda kutoka kwa Aristarko na Gayo wenyewe.
Hatimaye, karani wa jiji alituliza ghasia. Ni lazima kiwe kilikuwa kitulizo sana kwa Aristarko na Gayo kumsikia akitangaza bila upendeleo kuwa hawana hatia kisha kuona fujo iliyowazunguka ikiisha.
Ungehisije baada ya tukio kama hilo? Je, ungekata kauli kwamba kuwa mwandamani mishonari wa Paulo si jambo ambalo lingekufaa, kwamba lilikuwa hatari sana, na kwamba ingekuwa bora ikiwa ungetafuta maisha ya utulivu zaidi? Aristarko hakufikiria hivyo! Kwa vile alikuwa ametoka Thesalonike, bila shaka alijua wazi hatari za kutangaza habari njema. Paulo alipohubiri katika jiji lake miaka michache tu iliyopita, fujo zilitokea hapo pia. (Matendo 17:1-9; 20:4) Aristarko alishikamana kwa uaminifu-mshikamanifu na Paulo.
Kutoka Ugiriki Hadi Yerusalemu
Miezi fulani baada ya fujo za wafua-fedha, Paulo alikuwa Ugiriki na alikuwa karibu kusafiri kwa mashua kwenda Siria akiwa njiani kuelekea Yerusalemu wakati ambapo “njama ilitungwa dhidi yake na Wayahudi.” (Matendo 20:2, 3) Tunampata nani akiwa pamoja na Paulo katika hali hizo zenye hatari? Aristarko!
Tisho hili jipya lilisababisha Paulo, Aristarko, na waandamani wao kubadili mipango yao, kwanza wasafiri kupitia Makedonia, kisha wasafiri hatua kwa hatua kando ya pwani ya Asia Ndogo kabla ya kuanza mwishowe safari ya kwenda Foinike katika Patara. (Matendo 20:4, 5, 13-15; 21:1-3) Kwa wazi kusudi la safari hiyo lilikuwa kukabidhi michango ya Wakristo katika Makedonia na Akaya kwa ndugu zao wenye uhitaji katika Yerusalemu. (Matendo 24:17; Waroma 15:25, 26) Watu wengi walisafiri pamoja, labda kwa sababu walikuwa wamekabidhiwa daraka hilo na makutaniko mbalimbali. Bila shaka, kikundi kikubwa kama hicho pia kingehakikisha usalama zaidi.
Aristarko alikuwa na pendeleo kubwa la kuandamana na Paulo kutoka Ugiriki hadi Yerusalemu. Hata hivyo, safari yao iliyofuata ilikuwa kutoka Yudea hadi Roma iliyo mbali.
Safari ya Kwenda Roma
Wakati huu hali zilikuwa tofauti kabisa. Paulo alikuwa amekuwa kizuizini huko Kaisaria kwa miaka miwili, alikuwa amekata rufani kwa Kaisari, na alipasa kupelekwa Roma akiwa amefungwa minyororo. (Matendo 24:27; 25:11, 12) Jaribu kufikiri jinsi waandamani wa Paulo walivyohisi. Safari ya kutoka Kaisaria kwenda Roma ingekuwa ndefu na yenye kuleta mkazo wa kihisia-moyo, kukiwa na matokeo yasiyo na hakika. Ni nani angeenda naye ili kumtolea tegemezo na msaada? Wanaume wawili walichaguliwa au walijitolea. Walikuwa Aristarko na Luka, mwandishi wa kitabu cha Matendo.—Matendo 27:1, 2.
Luka na Aristarko waliwezaje kupanda meli ileile katika sehemu ya kwanza ya safari hiyo ya kwenda Roma? Mwanahistoria Giuseppe Ricciotti adokeza hivi: “Hawa wawili walipanda wakiwa wasafiri wa kujilipia wenyewe . . . au, kama inavyoelekea, waliruhusiwa kwa fadhili za ofisa mwenye amri wa Roma aliyefanya ionekane kwamba walikuwa watumwa wa Paulo, kwani sheria iliruhusu raia wa Roma kusaidiwa na watumwa wawili.” Lazima Paulo awe alitiwa moyo kama nini na kuwapo kwao na kitia-moyo chao!
Luka na Aristarko walionyesha upendo wao kwa Paulo kwa gharama kubwa na kwa kujihatarisha. Kwa kweli, walikabili hali yenye kutishia uhai wakati, wakiwa na mwandamani wao mfungwa, walipovunjikiwa meli katika kisiwa cha Malta.—Matendo 27:13–28:1.
‘Mateka Mwenzi’ wa Paulo
Paulo alipoandika barua zake kwa Wakolosai na kwa Filemoni katika 60-61 W.K., Aristarko na Luka walikuwa bado wako naye Roma. Aristarko na Epafrasi wanarejezewa kuwa ‘mateka wenzi’ wa Paulo. (Wakolosai 4:10, 14; Filemoni 23, 24) Kwa hiyo, kwa muda fulani, kwa wazi, Aristarko alishiriki vifungo vya gereza vya Paulo.
Ingawa Paulo alikuwa mfungwa katika Roma kwa angalau miaka miwili, aliruhusiwa kuishi chini ya ulinzi katika nyumba aliyokodi, ambapo angeweza kutangaza habari njema kwa waliomtembelea. (Matendo 28:16, 30) Aristarko, Epafrasi, Luka, na wengine walimhudumia Paulo wakati huo, wakimsaidia na wakimtegemeza.
“Msaada Wenye Kutia Nguvu”
Baada ya kuchunguza matukio mbalimbali ambayo Aristarko alihusika katika rekodi ya Biblia iliyopuliziwa, Aristarko alikuwa mtu wa aina gani? Kulingana na mwandishi W. D. Thomas, Aristarko “atofautishwa kabisa kuwa mtu ambaye angeweza kukabili upinzani na kuupita huku imani yake ikiwa imara kabisa na azimio lake la kutumikia likiwa imara. Atofautishwa kuwa mtu aliyempenda Mungu si katika nyakati nzuri tu, bali hata katika nyakati mbaya sana.”
Paulo asema kwamba Aristarko na wengine walikuwa “msaada wenye kutia nguvu” (Kigiriki, pa·re·go·riʹa) kwake, yaani, chanzo cha faraja. (Wakolosai 4:10, 11) Hivyo kwa kumfariji na kumtia moyo Paulo, Aristarko alikuwa mwandamani halisi katika nyakati zenye uhitaji. Kuwa na uandamani na urafiki wa mtume kwa kipindi cha miaka kadhaa lazima lilikuwa jambo lenye kuridhisha na kujenga sana kiroho.
Huenda tusipatwe na hali zinazofanana kabisa na zile zenye kutazamisha zilizoonwa na Aristarko. Hata hivyo, uaminifu-mshikamanifu kama huo kwa ndugu wa kiroho wa Kristo na kwa tengenezo la Yehova ni wa lazima kwa wote walio katika kutaniko la Kikristo leo. (Linganisha Mathayo 25:34-40.) Yaelekea waamini wenzi ambao tunawajua hatimaye watapatwa na janga au msononeko, labda kwa sababu ya kufiwa, ugonjwa, au majaribu mengine. Kwa kushikamana nao na kuwasaidia, kuwafariji, na kuwatia moyo, twaweza kupata shangwe na kujithibitisha kuwa waandamani wenye uaminifu-mshikamanifu.—Linganisha Mithali 17:17; Matendo 20:35.