Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 6/1 kur. 28-31
  • Wafanyakazi Wenzi wa Paulo Wao Walikuwa Nani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wafanyakazi Wenzi wa Paulo Wao Walikuwa Nani?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Waandamani Wasafiri na Wakaribishaji
  • Rafiki Wengi Sana
  • Utegemezo Mwaminifu-Mshikamanifu Akiwa Gerezani
  • “Sisi Ni Wafanyakazi Wenzi wa Mungu”
  • “Kutoa Ushahidi Kamili”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
  • Uwe Jasiri​—Yehova Ni Msaidizi Wako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2020
  • “Mimi Sina Hatia ya Damu ya Mtu Yeyote”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
  • Paulo Katika Roma
    Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 6/1 kur. 28-31

Wafanyakazi Wenzi wa Paulo Wao Walikuwa Nani?

KITABU cha Biblia cha Matendo na barua za Paulo hutaja watu wapatao mia moja, washiriki wa kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza, ambao walishirikiana na “yule mtume kwa mataifa.” (Waroma 11:13) Mengi yanajulikana kuhusu baadhi yao. Yaelekea unajua shughuli za Apolo, Barnaba, na Sila. Kwa upande mwingine, yaelekea itakuwa vigumu zaidi kwako kusema mengi kuhusu Arkipo, Klaudia, Damarisi, Lino, Persisi, Pudensi, na Sopateri.

Katika pindi tofauti-tofauti na chini ya hali mbalimbali, watu wengi walitegemeza kwa bidii huduma ya Paulo. Wengine kama Aristarko, Luka, na Timotheo walitumikia pamoja na mtume huyo kwa miaka mingi. Baadhi yao walikuwa naye alipokuwa gerezani au alipokuwa safarini, ama wakiwa waandamani-wasafiri au wakaribishaji. Kwa kusikitisha, wengine kama vile Aleksanda, Demasi, Hermogenesi, na Figelo, hawakudumu katika imani ya Kikristo.

Kuhusu rafiki wengine kadhaa wa Paulo kama Asinkrito, Hermasi, Yulia, au Filologo kwa kutaja wachache tu, tunawajua kwa majina tu. Kuhusu dada ya Nereo au mama ya Rufo au wale wa nyumba ya Kloe, hatujui hata majina yao. (Waroma 16:13-15; 1 Wakorintho 1:11) Hata hivyo, kuchunguza habari chache tunazojua kuhusu watu hawa wapatao mia moja, hutufafanulia jinsi mtume Paulo alivyofanya kazi. Pia, hutufunza jambo fulani kuhusu manufaa za kuwa na idadi kubwa ya waamini wenzetu karibu nasi na kufanya kazi karibu-karibu nao.

Waandamani Wasafiri na Wakaribishaji

Mtume Paulo alisafiri sana katika huduma yake. Mwandikaji mmoja akadiria kwamba, kama inavyorekodiwa kwenye kitabu cha Matendo pekee, Paulo alisafiri umbali upatao kilometa 16,000 kwenye nchi kavu na baharini. Wakati huo, safari ilikuwa yenye kuchosha na hatari pia. Kati ya hatari mbalimbali alizokabili zilikuwa kuvunjikiwa na meli, hatari zilizotokana na mito na wanyang’anyi wa njia kuu, hatari za nyikani, na hatari za baharini. (2 Wakorintho 11:25, 26) Kwa kufaa, ni mara chache Paulo alisafiri kutoka sehemu moja kwenda nyingine akiwa peke yake.

Wale walioandamana na Paulo walikuwa chanzo cha ushirika, kitia-moyo, na msaada wenye kutumika katika huduma. Mara kwa mara, Paulo aliwaacha nyuma ili waweze kushughulikia mahitaji ya kiroho ya waamini wapya. (Matendo 17:14; Tito 1:5) Lakini, yaelekea kuwapo kwa waandamani kulikuwa muhimu kwa ajili ya usalama na utegemezo katika kushughulika na ugumu wa safari. Kwa hiyo, huenda watu kama Sopateri, Sekundo, Gayo, na Trofimo, ambao tunawajua kuwa walikuwa miongoni mwa waandamani wa Paulo, wakawa walitimiza fungu muhimu katika kufanikiwa kwa huduma yake.— Matendo 20:4.

Walifurahia pia msaada uliotolewa na wakaribishaji wao. Paulo alipowasili katika jiji ambako alikusudia kufanya kampeni ya kuhubiri au kupisha usiku tu, kutafuta makao ndiko kungekuwa shughuli ya kwanza. Mtu yeyote aliyesafiri sana kama Paulo angelazimika kihalisi kulala katika vitanda vingi tofauti-tofauti. Angeweza kukaa katika hoteli ndogo, lakini hoteli hizo zinafafanuliwa na wanahistoria kuwa “mahali hatari na pasipopendeza,” kwa hiyo, ilipowezekana, yaelekea Paulo alikaa na waamini wenzake.

Tunajua majina ya baadhi ya wakaribishaji wa Paulo—Akila na Priska, Gayo, Yasoni, Lidia, Mnasoni, Filemoni, na Filipo. (Matendo 16:14, 15; 17:7; 18:2, 3; 21:8, 16; Waroma 16:23; Filemoni 1, 22) Huko Filipi, Thesalonike, na Korintho, makao hayo yalimwandalia Paulo kituo ambapo angeweza kupangia shughuli zake za umishonari. Huko Korintho, Tito Yusto pia alimkaribisha nyumbani kwake na kumwandalia mtume huyo mahali ambapo angeweza kuendelea na kazi yake ya kuhubiri.—Matendo 18:7.

Rafiki Wengi Sana

Kama iwezavyo kutarajiwa, rafiki za Paulo walikumbukwa katika njia mbalimbali kwa sababu ya hali tofauti-tofauti ambazo alikutana nao. Kwa mfano, Maria, Persisi, Fibi, Trifaina, na Trifosa, wote walikuwa waamini wenzi wa kike, ambao walipongezwa kwa sababu ya kazi yao ngumu. (Waroma 16:1, 2, 6, 12) Paulo alibatiza Krispo, Gayo, na watu wa nyumbani mwa Stefanasi. Dionisio na Damarisi walikubali ujumbe wa ile kweli kutoka kwake akiwa Athene. (Matendo 17:34; 1 Wakorintho 1:14, 16) Androniko na Yuniasi, “watu maarufu miongoni mwa mitume” waliokuwa wameamini muda mrefu zaidi kabla ya Paulo, wanaitwa ‘mateka wenzake.’ Labda walikuwa gerezani pamoja naye wakati fulani. Paulo pia anawaita watu hawa wawili “jamaa” zake kama alivyowaita Herodioni, Yasoni, Lukio, na Sosipateri. (Waroma 16:7, 11, 21) Ingawa neno la Kigiriki linalotumiwa hapa laweza kumaanisha “wananchi wenzi,” maana yake ya msingi ni “jamaa wenye uhusiano wa damu wa kizazi kilekile.”

Wengi wa rafiki za Paulo walisafiri kwa ajili ya habari njema. Mbali na waandamani wake wanaojulikana vizuri zaidi, kuna Akaiko, Fortunato, na Stefanasi pia, ambao walisafiri kutoka Korintho kwenda Efeso ili kushauriana na Paulo juu ya hali ya kiroho ya kutaniko lao. Artemasi na Tikiko walikuwa tayari kusafiri kwenda kujiunga na Tito, aliyekuwa akitumikia katika kisiwa cha Krete, naye Zenasi alikuwa afunge safari pamoja na Apolo.—1 Wakorintho 16:17; Tito 3:12, 13.

Kuna wale ambao Paulo anatoa habari ndogo-ndogo na zenye kusisimua kuwahusu. Kwa mfano, tunafahamishwa kwamba, Epaineto alikuwa “matunda ya kwanza ya Asia,” kwamba Erasto alikuwa “mtumishi-nyumba wa jiji” huko Korintho, kwamba Luka alikuwa tabibu, kwamba Lidia alikuwa muuzaji wa rangi ya zambarau, na kwamba Tertio alikuwa mtu aliyetumiwa na Paulo kuandika barua yake kwa Waroma. (Waroma 16:5, 22, 23; Matendo 16:14; Wakolosai 4:14) Ufupi wa habari hizi ndogo-ndogo unatamanisha yeyote ambaye angetaka kufahamu mengi zaidi kuhusu watu hao.

Waandamani wengine wa Paulo walipokea ujumbe mbalimbali wa kibinafsi, ambao sasa umerekodiwa katika Biblia. Kwa mfano katika barua yake kwa Wakolosai, Paulo alimhimiza Arkipo hivi: “Fuliza kuangalia huduma ambayo ulikubali katika Bwana, ili uitimize.” (Wakolosai 4:17) Yaelekea Euodia na Sintike walikuwa na hitilafiano la kibinafsi la kutatua. Hivyo, Paulo aliwahimiza kupitia “mwenzi wa nira” asiyetajwa jina, aliyekuwa Filipi, lilikuwa kwamba “wawe wenye akili ileile katika Bwana.” (Wafilipi 4:2, 3) Bila shaka, hilo ni shauri zuri kwetu sote.

Utegemezo Mwaminifu-Mshikamanifu Akiwa Gerezani

Paulo alifungwa gerezani mara kadhaa. (2 Wakorintho 11:23) Kwenye pindi hizo lazima Wakristo wenyeji, ikiwa walikuwepo Wakristo wowote, wawe walijitahidi kufanya yote wawezayo ili kufanya kifungo chake kiwe chenye kuvumilika zaidi. Paulo alipofungwa mara ya kwanza huko Roma, aliruhusiwa kupanga nyumba yake mwenyewe kwa muda wa miaka miwili na angeweza kutembelewa na rafiki zake. (Matendo 28:30) Wakati huo, aliyaandikia barua makutaniko ya Efeso, Filipi, na Kolosai, na pia Filemoni. Vyanzo hivi vyatufahamisha mengi kuhusu wale waliokuwa na ukaribu na Paulo alipokuwa kizuizini.

Kwa mfano, tunapata habari kwamba Onesimo, mtumwa-mtoro wa Filemoni, alijiunga na Paulo huko Roma, kama alivyofanya Tikiko, ambaye angeandamana na Onesimo katika safari yake ya kurudi kwa bwana-mkubwa wake. (Wakolosai 4:7-9) Pia kulikuwa na Epafrodito, aliyefunga safari ndefu kutoka Filipi akiwa na zawadi kutoka kwa kutaniko lake, na ambaye wakati huo alipatwa na ugonjwa. (Wafilipi 2:25; 4:18) Waliohubiri karibu-karibu na Paulo huko Roma walikuwa Aristarko, Marko, na Yesu aitwaye Yusto, ambao Paulo alisema hivi kuwahusu: “Ni hawa tu walio wafanyakazi wenzangu kwa ajili ya ufalme wa Mungu, na hawahawa wamekuwa kwangu msaada wenye kutia nguvu.” (Wakolosai 4:10, 11) Timotheo na Luka pia, ambao wanajulikana vema zaidi, walikuwa miongoni mwa waaminifu hawa wote, kutia ndani na Demasi, ambaye baadaye, kwa sababu ya kupenda ulimwengu, alimwacha Paulo.—Wakolosai 1:1; 4:14; 2 Timotheo 4:10; Filemoni 24.

Yaonekana, hakuna yeyote kati ya watu hao aliyetoka Roma, hata hivyo, walikuwepo kumsaidia Paulo. Labda wengine walienda hasa kumsaidia wakati wa kifungo chake gerezani. Yaelekea wengine walitumwa naye, wengine wakapewa utume wa kwenda sehemu za mbali, na bado wengine wakaandika barua za Paulo za imla. Ni ushuhuda ulio dhahiri kama nini wa ufungamano na uaminifu-mshikamanifu ambao wote hawa walikuwa nao kwa Paulo na kwa kazi ya Mungu!

Tunatambua kutokana na umalizio wa baadhi ya barua za Paulo kwamba, inaelekea alizungukwa na ushirika wa ndugu na dada Wakristo waliokuwa wengi zaidi kuliko wale wachache tunaowajua kwa majina. Katika pindi tofauti-tofauti, yeye aliandika hivi: “Watakatifu wote wawapelekea nyinyi salamu zao” na “Wale wote walio pamoja nami wakupelekea wewe salamu zao.”—2 Wakorintho 13:13; Tito 3:15; Wafilipi 4:22.

Wakati wa kifungo chake cha pili huko Roma, kilichokuwa hatari, Paulo aliwafikiria sana wafanyakazi wenzake wakati ambapo alikuwa anakaribia kufia imani. Alikuwa bado anasimamia na kuratibu shughuli za angalau wengine kati yao. Tito na Tikiko walikuwa wamepewa utume wa kwenda sehemu za mbali, Kresensi alikuwa ameenda Galatia, Erasto akabaki Korintho, Trofimo akaachwa huko Mileto akiwa mgonjwa, lakini Marko na Timotheo wakawa waje kwake. Hata hivyo, Luka alikuwa pamoja na Paulo, naye mtume alipomwandikia Timotheo barua yake ya pili, waamini wengine kadhaa, kutia ndani Eubulo, Pudensi, Lino, na Klaudia, walikuwepo kupeleka salamu zao. Bila shaka, walikuwa wakifanya kile wawezacho kumsaidia Paulo. Wakati huohuo, Paulo mwenyewe aliwapelekea salamu Priska na Akila na watu wa nyumbani mwa Onesiforo. Hata hivyo, kwa kusikitisha, Demasi alimwacha wakati huo wa taabu, naye Aleksanda akamtenda mabaya mengi.—2 Timotheo 4:9-21.

“Sisi Ni Wafanyakazi Wenzi wa Mungu”

Ni mara chache Paulo alishughulika na kazi yake ya kuhubiri akiwa peke yake. “Taswira inayojitokeza,” mwelezaji E. Earle Ellis asema, “ni ya mishonari mwenye wenzi wengi sana. Kwa kweli, ni mara chache Paulo anakuwa bila waandamani.” Akiongozwa na roho takatifu ya Mungu, Paulo aliweza kuhamasisha watu wengi na kupanga kampeni za umishonari zenye matokeo. Alizungukwa na wenzi wa karibu, wasaidizi wa muda, watu kadhaa mashuhuri, na watumishi wengi sana wanyenyekevu. Hata hivyo, hawa hawakuwa wafanyakazi wenzi tu. Hata wawe walifanya kazi au kushirikiana na Paulo kadiri gani, kifungo cha upendo wa Kikristo na urafiki wa kibinafsi ni dhahiri.

Mtume Paulo alikuwa na kile ambacho kimeitwa “kipaji cha kupata rafiki.” Alifanya mengi kupeleka habari njema kwa mataifa, lakini hakuthubutu kufanya hivyo peke yake. Alishirikiana na kutumia kikamili kutaniko la Kikristo lililopangwa kitengenezo. Paulo hakujisifu kwa sababu ya matokeo aliyopata, bali alikiri kwa unyenyekevu kwamba alikuwa mtumwa na kwamba heshima yote ilipaswa imwendee Mungu, aliyetokeza ukuzi huo.—1 Wakorintho 3:5-7; 9:16; Wafilipi 1:1.

Hali za Paulo zilikuwa tofauti na zetu, hata hivyo, hakuna mtu yeyote katika kutaniko la Kikristo leo anayepaswa kufikiri kwamba anaweza au anahitaji kujitegemea. Badala yake, yatupasa sikuzote kufanya kazi pamoja na tengenezo la Mungu, kutaniko la kwetu, na waamini wenzetu. Tunahitaji msaada wao, utegemezo, na faraja nyakati zifaazo na nyakati zenye taabu. Tuna pendeleo lenye thamani la kuwa sehemu ya ‘ushirika mzima wa ndugu katika ulimwengu.’ (1 Petro 5:9) Ikiwa kwa uaminifu na kwa upendo tunafanya kazi bega kwa bega na kwa kushirikiana pamoja nao wote, basi kama Paulo, sisi pia tunaweza kusema kwamba “sisi ni wafanyakazi wenzi wa Mungu.”—1 Wakorintho 3:9.

[Picha katika ukurasa wa 31]

APOLO

ARISTARKO

BARNABA

LIDIA

ONESIFORO

TERTIO

TIKIKO

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki