Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 10/1 kur. 4-8
  • Mjue Yehova—Yule Mungu Mwenye Utu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mjue Yehova—Yule Mungu Mwenye Utu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Yehova na Musa “Uso kwa Uso”
  • Yehova—Mungu Mwenye Utu wa Eliya
  • Roho Takatifu Yamwelekeza Paulo
  • Uatheisti Hauzuii Kupendezwa Kibinafsi kwa Yehova
  • “Mpumbavu” na Mungu
  • Maonyo Kutoka kwa Mungu Wetu Mwenye Utu
  • Alifarijiwa na Mungu Wake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Je, Utakuwa Mwaminifu Kama Eliya?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Alifarijiwa na Mungu Wake
    Igeni Imani Yao
  • Je, wakati fulani unajihisi mpweke na kuogopa?
    Wafundishe Watoto Wako
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 10/1 kur. 4-8

Mjue Yehova—Yule Mungu Mwenye Utu

AKILINGANISHA dhana ya Wahindu juu ya Mungu na mifumo mingine ya dini, Dakt. Radhakrishnan wa India asema hivi: “Mungu wa Waebrania ni wa aina tofauti. Yeye ni mwenye utu na mtendaji katika historia na apendezwaye na mabadiliko na matukio yasiyotazamiwa ya ulimwengu huu wenye kusitawi. Yeye ni Aliye Hai ambaye huwasiliana nasi.”

Jina la Kiebrania la Mungu wa Biblia ni יהוה, ambalo kwa kawaida hutafsiriwa “Yehova.” Yeye hupita ile miungu mingine yote. Twajua nini kumhusu? Alishughulikaje na watu katika nyakati za Biblia?

Yehova na Musa “Uso kwa Uso”

Ukaribu wa “uso kwa uso” ulikuwako kati ya Yehova na mtumishi wake Musa, hata ingawa Musa hangeweza kumwona Mungu kihalisi. (Kumbukumbu la Torati 34:10; Kutoka 33:20) Ujanani mwake, moyo wa Musa ulikuwa pamoja na Waisraeli, ambao wakati huo walikuwa watumwa Misri. Yeye alikataa maisha yake akiwa mshiriki wa nyumba ya Farao, “akichagua kutendwa vibaya pamoja na watu wa Mungu.” (Waebrania 11:25) Tokeo ni kwamba, Yehova alimtolea Musa mapendeleo mengi ya pekee.

Akiwa mshiriki wa nyumba ya Farao, “Musa a[li]funzwa katika hekima yote ya Wamisri.” (Matendo 7:22) Lakini ili kuliongoza taifa la Israeli, alihitaji pia kukuza sifa ya unyenyekevu, ya subira, na ya usikivu. Hilo alifanya wakati wa miaka yake 40 akiwa mchungaji huko Midiani. (Kutoka 2:15-22; Hesabu 12:3) Ijapokuwa Yehova alibaki akiwa asiyeonekana, alijifunua mwenyewe na kusudi lake kwa Musa, na kupitia malaika Mungu akamkabidhi zile Amri Kumi. (Kutoka 3:1-10; 19:3–20:20; Matendo 7:53; Waebrania 11:27) Biblia hutuambia kwamba “BWANA akasema na Musa uso kwa uso, kama vile mtu asemavyo na rafiki yake.” (Kutoka 33:11) Kwa kweli, Yehova mwenyewe alisema hivi: “Kwake nitanena mdomo kwa mdomo.” Ni uhusiano wa kibinafsi wenye thamani kama nini ambao Musa alifurahia pamoja na Mungu wake mwenye utu asiyeonekana!—Hesabu 12:8.

Kwa kuongezea historia ya mapema ya taifa la Israeli, Musa alirekodi mfumo wa Sheria ukiwa na sehemu zake zote. Aliaminishwa pia pendeleo jingine lenye thamani kubwa—lile la kuandika kitabu cha Mwanzo. Sehemu ya mwisho-mwisho ya kitabu hicho ilikuwa historia iliyojulikana kwa usahihi miongoni mwa familia yake mwenyewe na kwa hiyo kuirekodi kulikuwa rahisi kwa kadiri. Lakini Musa alipata wapi habari ndogondogo juu ya historia ya mapema zaidi ya mwanadamu? Inawezekana kwamba Musa alikuwa na hati za kale zilizoandikwa, zilizohifadhiwa na baba zake wa zamani, za kutumia zikiwa chanzo cha habari ndogondogo. Kwa upande ule mwingine, angaliweza kupokea habari kupitia masimulizi ya mdomo au moja kwa moja kwa ufunuo wa kimungu kutoka kwa Yehova. Wanaume wenye staha wa enzi zote wamekubali kwa muda mrefu uhusiano wa kibinafsi ambao Musa alifurahia pamoja na Mungu wake kuhusiana na jambo hilo.

Yehova—Mungu Mwenye Utu wa Eliya

Nabii Eliya pia alimjua Yehova kuwa Mungu mwenye utu. Eliya alikuwa mwenye bidii kwa ajili ya ibada safi na alimtumikia Yehova ajapokuwa shabaha ya chuki na upinzani mkubwa kutoka kwa waabudu wa Baali, mungu mkuu wa hekalu la Wakanaani.—1 Wafalme 18:17-40.

Ahabu, Mfalme wa Israeli, na mkewe, Yezebeli, walitaka kumwua Eliya. Akihofia uhai wake, Eliya alikimbilia Beer-sheba, magharibi ya Bahari Iliyokufa. Huko alizurura nyikani na kusali afe. (1 Wafalme 19:1-4) Je, Yehova alikuwa amemwacha Eliya? Je, Yeye hakupendezwa tena na mtumishi wake mwaminifu? Huenda ikawa Eliya alifikiria hivyo, lakini alikuwa amekosea kama nini! Baadaye, Yehova alisema naye kimya-kimya, akimwuliza hivi: “Unafanya nini hapa, Eliya?” Baada ya wonyesho wenye kutazamisha wa nguvu zinazozidi zile za kibinadamu, “sauti ikamjia, kusema [tena], Unafanya nini hapa, Eliya?” Yehova alidhihirisha kupendezwa kwake kibinafsi na Eliya ili kumtia moyo mtumishi wake mwenye kutumainika. Mungu alikuwa na kazi zaidi aliyotaka Eliya afanye, naye Eliya aliitikia mwito huo kwa hamu! Eliya alitimiza migawo yake kwa uaminifu, akitakasa jina la Yehova, Mungu wake mwenye utu.—1 Wafalme 19:9-18.

Baada ya kukataa kwake taifa la Israeli, Yehova hakusema kibinafsi tena na watumishi wake duniani. Hilo halikumaanisha kwamba kupendezwa kwake kibinafsi nao kulikuwa kumefifia. Bado aliwaelekeza na kuwatia nguvu katika utumishi wake kupitia roho yake takatifu. Kwa kielelezo, fikiria mtume Paulo, aliyejulikana hapo zamani kuwa Sauli.

Roho Takatifu Yamwelekeza Paulo

Sauli alitoka Tarso, jiji mashuhuri la Kilikia. Wazazi wake walikuwa Waebrania, lakini alizaliwa akiwa raia wa Roma. Hata hivyo, Sauli alilelewa kulingana na itikadi kali za Mafarisayo. Baadaye, katika Yerusalemu, alikuwa na fursa ya kuelimishwa “penye miguu ya Gamalieli,” mwalimu mashuhuri wa Sheria.—Matendo 22:3, 26-28.

Kwa sababu ya bidii ya Sauli kwa ajili ya mapokeo ya Kiyahudi ambayo ilielekezwa vibaya, alishiriki katika kampeni kali dhidi ya wafuasi wa Yesu Kristo. Hata alikubali kuuawa kimakusudi kwa Stefano, Mkristo mfia-imani wa kwanza. (Matendo 7:58-60; 8:1, 3) Baadaye alikiri kwamba ijapokuwa alikuwa mkufuru na mnyanyasaji na mtu fidhuli hapo zamani, “[a]lionyeshwa rehema, kwa sababu [a]likuwa asiye na ujuzi na [a]litenda kwa ukosefu wa imani.”—1 Timotheo 1:13.

Sauli alichochewa na tamaa ya kweli ya kumtumikia Mungu. Baada ya Sauli kugeuzwa imani akiwa barabarani kwenda Damaski, Yehova alimtumia katika njia isiyo ya kawaida. Anania, mwanafunzi Mkristo wa mapema, alielekezwa na Kristo aliyekuwa amefufuliwa, amsaidie Paulo. Baada ya hapo Paulo (jina la Kiroma ambalo kwalo Sauli alijulikana akiwa Mkristo) aliongozwa na roho takatifu ya Yehova kutimiza huduma ndefu na yenye kuzaa matunda kotekote katika sehemu za Ulaya na Asia Ndogo.—Matendo 13:2-5; 16:9, 10.

Je, mwelekezo huohuo wa roho takatifu waweza kutambuliwa leo? Ndiyo, waweza.

Uatheisti Hauzuii Kupendezwa Kibinafsi kwa Yehova

Joseph F. Rutherford alikuwa msimamizi wa pili wa Watch Tower Society. Alibatizwa mwaka wa 1906 akiwa Mwanafunzi wa Biblia—jina la utambulisho ambalo kwa hilo Mashahidi wa Yehova walijulikana wakati huo—aliwekwa rasmi kuwa wakili wa Sosaiti mwaka uliofuata, akawa msimamizi wa hiyo Sosaiti Januari 1917. Lakini, wakati fulani mwanasheria huyu mchanga alikuwa mwatheisti. Alipataje kuwa mtumishi Mkristo wa Yehova mwenye kuchochewa?

Julai 1913, Rutherford alitumikia akiwa mwenyekiti wa mkusanyiko wa International Bible Students Association uliofanywa Springfield, Massachusetts, Marekani. Mwandishi wa habari wa gazeti la habari, The Homestead, la mahali hapo, alimhoji Rutherford, na hilo simulizi lilichapwa tena katika ripoti ya ukumbusho ya mkusanyiko huo.

Rutherford alieleza kwamba alipopanga kuoa, maoni yake ya kidini yalikuwa yale ya madhehebu ya Wabaptisti, lakini yale ya yule ambaye alitazamia awe mke wake yalikuwa ya Kipresbiteri. Pasta wa Rutherford aliposema kwamba “yeye (yule ambaye alitazamia awe Bi. Rutherford) alikuwa katika safari ya kwenda kwenye moto wa helo kwa sababu hakuwa amezamishwa na kwamba yeye (Rutherford) alikuwa katika safari ya kwenda mbinguni moja kwa moja kwa sababu alikuwa amezamishwa, akili yake yenye kuchanganua mambo ilichukizwa, akawa mwatheisti.”

Ilimchukua Rutherford miaka kadhaa ya utafiti wenye uangalifu kujenga upya imani yake katika Mungu mwenye utu. Alisema alisababu kutokana na dhana kwamba “lile ambalo haliwezi kutosheleza akili halina haki ya kutosheleza moyo.” Wakristo “lazima wawe na hakika kwamba Maandiko wanayoamini ni ya kweli,” Rutherford akaeleza, akiongeza hivi: “Lazima wajue msingi ambao juu yake wao husimama.”—Ona 2 Timotheo 3:16, 17.

Ndiyo, hata leo inawezekana mtu mwatheisti au mwagnosti achunguze Maandiko, ajenge imani, na kukuza uhusiano wa kibinafsi, wenye nguvu na Yehova Mungu. Baada ya kujifunza Biblia kwa uangalifu kwa msaada wa kichapo cha Watch Tower Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, mwanamume mmoja kijana, aliungama hivi: “Sikumwamini Mungu nilipoanza funzo hili, lakini sasa naona kwamba ujuzi wa Biblia umebadili kabisa kufikiri kwangu. Ninaanza kumjua Yehova na kuwa na itibari katika yeye.”

“Mpumbavu” na Mungu

“Mwandishi yeyote wa AK [Maandiko ya Kiebrania] hajapata kamwe kuwazia kuthibitisha au kubisha kuwako kwa Mungu,” asema Dakt. James Hastings katika kichapo A Dictionary of the Bible. “Kwa ujumla hailingani na mwelekeo wa ulimwengu wa kale kukana kuwako kwa Mungu, au kutumia majibizano ili kuthibitisha jambo hilo. Itikadi ilikuwa moja ambayo ilikuwa asilia ya akili ya kibinadamu na ya kawaida kwa wanadamu wote.” Bila shaka, hilo halimaanishi kwamba watu wote wakati huo walikuwa wenye kumhofu Mungu. Sivyo kabisa. Andiko la Zaburi 14:1 na 53:1 (NW) hutaja “asiye na akili,” au kama vile Biblia ya Union Version husema, “mpumbavu,” ambaye amesema moyoni mwake, “Hakuna Mungu.”

Huyu mpumbavu ni mtu wa aina gani, mtu ambaye hukana kuwako kwa Mungu? Si kwamba yeye hana ujuzi kiakili. Badala ya hivyo, neno la Kiebrania na·valʹ huonyesha kupungukiwa kiadili. Katika maandishi yake kwenye kichapo The Parallel Psalter, Profesa S. R. Driver husema kwamba huko kupungukiwa “si udhaifu wa kusababu, lakini ni ukosefu wa hisia kiadili na kidini, kukosa hisia, au ufahamu kabisa.”

Mtunga-zaburi aendelea kufafanua huo mvunjiko wa adili ulio tokeo la mtazamo kama huo hivi: “Wameharibu matendo yao na kuyafanya chukizo, hakuna atendaye mema.” (Zaburi 14:1) Kwa ufupi Dakt. Hastings alimalizia hivi: “Kwa kutegemea hali hiyo ya kutokuwako kwa Mungu ulimwenguni na kutokuwa na hofu ya kuadhibiwa, watu huwa wafisadi na hufanya vitendo vyenye kuchukiza.” Wao hukubali waziwazi kanuni zisizo za kimungu na hukosa kustahi Mungu mwenye utu ambaye hawataki kabisa awatoze hesabu. Lakini kufikiri huko ni kwa kipumbavu na kukosa akili leo kama vile kulivyokuwa mtunga-zaburi alipoandika maneno yake miaka zaidi ya 3,000 iliyopita.

Maonyo Kutoka kwa Mungu Wetu Mwenye Utu

Acheni sasa turudie maswali yaliyoulizwa katika makala yetu ya kufungua. Ni kwa nini watu wengi hushindwa kupatanisha Mungu mwenye utu na kuteseka ambako kumeenea katika ulimwengu wa leo?

Biblia ina habari iliyoandikwa kutoka kwa wanaume ambao “walisema kutoka kwa Mungu walipokuwa wakichukuliwa na roho takatifu.” (2 Petro 1:21) Hiyo pekee ndiyo hutufunulia yule Mungu mwenye utu, Yehova. Pia hutuonya juu ya kiumbe mwovu, asiyeonekana kwa wanadamu, ambaye ni mwenye nguvu katika kuelekeza na kuongoza kufikiri kwa kibinadamu—Shetani Ibilisi. Kiakili, ikiwa hatumwamini Mungu mwenye utu, twawezaje kuamini kwamba kuna Ibilisi, au Shetani mwenye utu pia?

Chini ya upulizio mtume Yohana aliandika hivi: “Yeye aitwaye Ibilisi na Shetani, [ana]iongoza vibaya dunia nzima inayokaliwa.” (Ufunuo 12:9) Baadaye Yohana alisema hivi: “Sisi twajua twatokana na Mungu, lakini ulimwengu mzima unakaa katika nguvu ya mwovu.” (1 Yohana 5:19) Taarifa hizi zadhihirisha maneno ya Yesu, maneno ambayo Yohana mwenyewe aliyarekodi katika Gospeli yake hivi: “Mtawala wa ulimwengu anakuja. Naye hana mshiko juu yangu.”—Yohana 14:30.

Fundisho hilo la Kimaandiko liko tofauti kama nini na yale ambayo watu huamini sasa! “Kuzungumza juu ya Ibilisi ni jambo ambalo kwa udhahiri halipendelewi leo. Enzi yetu yenye kutilia shaka na ya kisayansi, imemstaafisha Shetani,” lasema gazeti Catholic Herald. Lakini, Yesu aliwaambia kwa nguvu hivi wale wanaume waliokusudia kumwua kimakusudi: “Nyinyi mwatoka kwa baba yenu Ibilisi, nanyi mwataka kufanya tamaa za baba yenu.”—Yohana 8:44.

Ufafanuzi wa Biblia juu ya nguvu za Shetani ni jambo la kiakili na lenye kueleweka. Huelewesha wazi ni kwa nini, ijapokuwa tamaa ya watu walio wengi ya kuishi kwa amani na upatano, ulimwengu unasumbuliwa na chuki, vita, na jeuri isiyo na maana, kama ilivyoonyeshwa huko Dunblane (mji uliotajwa kwenye ukurasa wa 3 na wa 4). Zaidi ya hayo, hatulazimiki kushindana na Shetani pekee. Biblia hutoa maonyo zaidi kuhusu maibilisi, au roho waovu—viumbe-roho waovu ambao zamani sana walijiunga na Shetani ili kuwaongoza na kuwatumia wanadamu vibaya. (Yuda 6) Yesu Kristo alikabili nguvu za hawa roho waovu mara nyingi, na aliweza kuwashinda.—Mathayo 12:22-24; Luka 9:37-43.

Mungu wa kweli, Yehova, amekusudia kusafisha dunia hii uovu na hatimaye aondoshe utendaji mbalimbali wa Shetani na roho waovu wake. Kwa kutegemea ujuzi wetu juu ya Yehova, twaweza kuwa na imani na itibari imara katika ahadi zake. Yeye husema hivi: “Kabla yangu hakuumbwa Mungu awaye yote, wala baada yangu mimi hatakuwapo mwingine. Mimi, naam, mimi, ni BWANA, zaidi yangu mimi hapana mwokozi.” Yehova kwa kweli ni Mungu mwenye utu kwa wote wamjuao, kumwabudu, na kumtumikia. Twaweza kumtegemea yeye, na yeye peke yake, ili kupata wokovu wetu.—Isaya 43:10, 11.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Mchoro wa karne ya 18 ambao waonyesha Musa akiandika Mwanzo 1:1 chini ya upulizio

[Hisani]

Kutoka Biblia ya The Holy Bible ya J. Baskett, Oxford

[Picha katika ukurasa wa 8]

Yesu Kristo alishinda roho waovu mara nyingi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki