Je, Waweza Kumwamini Mungu Mwenye Utu?
“HUHITAJI kumwamini Mungu ili uwe Mkristo . . . Sisi tu sehemu ya mapinduzi sasa, lakini katika karne ya 21 kanisa litakuwa bila Mungu katika maana ya kimapokeo,” akafafanua kasisi wa chuo kikuu cha Uingereza mwenye cheo cha juu. Alikuwa akizungumza kwa niaba ya harakati iitwayo Sea of Faith ambayo angalau makasisi Waingereza mia moja wamejiandikisha. “Wakristo [hawa] waatheisti” husisitiza kwamba dini ni ubuni wa wanadamu na kwamba, kama vile mshiriki mmoja alivyosema, Mungu ni “wazo” tu. Wazo la Mungu mwenye nguvu zizidizo zile za kibinadamu halipatani tena na kufikiri kwao.
“Mungu amekufa” ulikuwa wito uliopendwa na wengi miaka ya 1960. Ulidhihirisha maoni ya mwanafalsafa Mjerumani wa karne ya 19, Friedrich Nietzsche, na uliwapa vijana wengi udhuru waliotaka ili kufanya walivyotaka, kujiingiza katika ngono bila kuoana na utumizi mbaya wa dawa bila kizuizi cha kiadili. Lakini, je, uhuru huo uliwaongoza hao washabiki wa upendo na amani, kama vile walivyopata kujulikana, kwenye maisha ya furaha yenye kutosheleza zaidi?
Mwongo huohuo, askofu Mwanglikana, John A. T. Robinson alichapisha kitabu chake kiitwacho Honest to God chenye kuleta mabishano. Wengi wa makasisi wenzake walimchambua kwa sababu ya kumfikiria Mungu “kuwa sehemu fulani tu yenye kina ya mambo yaliyompata binadamu.” Profesa wa theolojia, Keith Ward, aliuliza hivi: “Je, kumwamini Mungu ni namna fulani ya mtindo wa ushirikina wa zamani, ambao sasa umetupwa na wenye hekima?” Kwa kulijibu swali lake mwenyewe, alisema hivi: “Hakuna kitu chochote kilicho muhimu zaidi katika dini leo kuliko kupata tena ujuzi wa wazo la kimapokeo juu ya Mungu.”
Kupatanisha Kuteseka na Mungu Mwenye Utu
Watu wengi ambao humwamini Mungu mwenye utu hulipata kuwa jambo gumu kupatanisha imani yao na mambo ya kuhuzunisha na ya kuteseka wayaonayo. Kwa kielelezo, Machi 1996, watoto wachanga 16, pamoja na mwalimu wao, walipigwa risasi na kuuawa katika Dunblane, Scotland. “Sielewi hata kidogo mapenzi ya Mungu,” akasema mwanamke mmoja aliyechanganyikiwa. Maumivu makali ya jambo hilo la kuhuzunisha yalionyeshwa katika kadi iliyoachwa pamoja na maua nje ya shule ya hao watoto. Ilikuwa na maneno, “KWA NINI?” Kwa kujibu mhudumu wa Dunblane Cathedral alisema hivi: “Hakuna ufafanuzi. Hatuwezi kujibu ni kwa sababu gani haya yalipata kutokea.”
Baadaye mwaka huohuo, kasisi kijana aliyependwa na wengi wa Kanisa la Uingereza aliuawa kinyama. Gazeti Church Times liliripoti kwamba kutaniko lenye fadhaiko lilisikia kasisi mkuu wa Liverpool akisema juu ya “kubisha kwa nguvu mlango wa Mungu akiuliza, kwa nini? kwa nini?” Kasisi huyo pia hakuwapa ujumbe wa kufariji kutoka kwa Mungu mwenye utu.
Basi, tuamini nini? Ni jambo la kiakili kumwamini Mungu mwenye utu. Kufanya hivyo ndio ufunguo wa kuyajibu maswali yanayohitaji uangalifu ambayo yameulizwa hapo juu. Twakualika ufikirie uthibitisho ambao umetolewa katika makala yenye kufuata.
[Picha katika ukurasa wa 3]
Kadi iliuliza “Kwa nini?”
[Hisani]
NEWSTEAM No. 278468/Sipa Press