Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 10/1 kur. 21-25
  • Kushukuru kwa Ajili ya Maisha Marefu Katika Utumishi wa Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kushukuru kwa Ajili ya Maisha Marefu Katika Utumishi wa Yehova
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kuathiriwa na Maoni ya Kidini
  • Msimamo Wangu kwa Ajili ya Kweli ya Biblia
  • Utumishi Kwenye Betheli
  • Kuwa na Uhakika Katika Tumaini la Ufalme
  • Utendaji Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili
  • Utendaji Uliofanywa Upya Baada ya Vita
  • Kufanya Niwezayo
  • Kudumisha Imani Mpaka Mwisho
  • Je, Hii Yaweza Kuwa Kazi-Maisha Inayokufaa Zaidi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Kusonga Mbele Pamoja na Tengenezo la Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Je, Waweza Kujitolea?
    Huduma Yetu ya Ufalme—2001
  • Maisha Yangu Katika Tengenezo la Yehova Lenye Kuelekezwa kwa Roho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 10/1 kur. 21-25

Kushukuru kwa Ajili ya Maisha Marefu Katika Utumishi wa Yehova

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA OTTILIE MYDLAND

Mwisho-mwisho wa karne ya 19, meli za kusafiri zilikuwa zimetia nanga sambamba bandarini Kopervik magharibi mwa Norway. Siku hizo watu na farasi walivuta mikokoteni barabarani. Watu walitumia taa za mafuta ili kupata mwangaza, na nyumba za mbao zilizopakwa rangi nyeupe zilipashwa moto kwa mbao na makaa-mawe zimwe. Nilizaliwa huko Juni 1898, nikiwa mtoto wa pili kati ya watoto watano.

BABA hakuwa ameajiriwa kazi mwaka wa 1905, hivyo akaenda Marekani. Alirudi miaka mitatu baadaye akiwa na sanduku lililojaa zawadi zenye kusisimua kwa ajili ya watoto na vitambaa vya hariri na vitu vingine kwa ajili ya mama. Lakini mali zake za thamani zaidi zilikuwa mabuku yaliyoandikwa na Charles Taze Russell yenye kichwa Studies in the Scriptures.

Baba alianza kuwaambia marafiki na jamaa mambo aliyojifunza kutoka katika vitabu hivyo. Kwenye mikutano ya kikanisa cha mahali hapo, alitumia Biblia kuonyesha kwamba hakuna helo yenye kuwaka moto. (Mhubiri 9:5, 10) Katika 1909, mwaka baada ya baba kurudi kutoka Marekani, Ndugu Russell alizuru Norway na kutoa hotuba Bergen na Kristiania, miji ambayo sasa yaitwa Oslo. Baba alienda Bergen kumsikiliza.

Watu walio wengi walimshtaki baba juu ya kuendeleza mafundisho yasiyo ya kweli. Nilimsikitikia na kumsaidia kuwapelekea majirani trakti za Biblia. Mwaka wa 1912, nilimpelekea binti ya kasisi fulani trakti juu ya helo. Alinitukana mimi na baba. Nilishtuka kwamba binti ya kasisi angeweza kutumia lugha chafu hivyo!

Wengine wa Wanafunzi wa Biblia, kama vile Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo, wakitia na Theodor Simonsen, msemaji mwenye uwezo, walituzuru Kopervik mara kwa mara. Nilikuwa nikialika watu kwenye hotuba alizotoa nyumbani kwetu. Kabla ya hotuba yake alicheza zeze na kuimba, na baada ya hotuba yake aliimba wimbo wa kututakia usiku mwema. Tulimstahi sana.

Mtu mwingine aliyezuru nyumbani kwetu alikuwa Anna Andersen, kolpota, au mhudumu wa wakati wote. Alisafiri kutoka mji hadi mji kotekote Norway, hasa kwa baiskeli, akiangushia watu fasihi za Biblia. Wakati mmoja alikuwa mhudumu aliyewekwa rasmi katika dini ya Jeshi la Wokovu na aliwajua wahudumu kadhaa waliowekwa rasmi wa dini ya Jeshi la Wokovu Kopervik. Walimruhusu atoe hotuba ya Biblia katika nyumba yao ya mikutano, nami nilialika watu waje na kumsikiliza.

Kolpota mwingine aliyetuzuru Kopervik alikuwa Karl Gunberg. Mwanamume huyu mwenye kiasi, mtulivu, lakini mwenye ucheshi, pia pindi kwa pindi alitumikia akiwa mtafsiri kwenye ofisi ya tawi katika Oslo. Miaka mingi baadaye tulifanya kazi pamoja huko.

Kuathiriwa na Maoni ya Kidini

Wakati huo watu walio wengi zaidi walikuwa na imani yenye nguvu si katika Mungu na Biblia tu bali pia katika itikadi za kimapokeo zilizo imara, kama vile moto wa helo na Utatu. Kwa hiyo ilisababisha mshtuko mkubwa Wanafunzi wa Biblia walipofundisha kwamba mafundisho hayo hayakupatana na Biblia. Niliathiriwa na mashtaka makali ya jirani zetu kwamba baba alikuwa mzushi. Wakati mmoja hata nilimwambia hivi: “Uyafundishayo si kweli. Ni uzushi!”

“Njoo hapa, Ottilie,” akanitia moyo, “na uone yale ambayo Biblia husema.” Ndipo akanisomea Maandiko. Tokeo ni kwamba, uhakika wangu katika yeye na yale aliyofundisha ulikua. Alinitia moyo nisome vichapo Studies in the Scriptures, kwa hiyo wakati wa kiangazi cha mwaka wa 1914, mara nyingi nilisoma nikiwa nimeketi juu ya kilima chenye kuelekea mjini.

Agosti 1914 umati ulikusanyika nje ya jengo la magazeti ya habari la mahali hapo wakisoma juu ya kuzuka kwa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Baba alikuja na kuona yaliyokuwa yakitukia. “Asante Mungu!” akasema kwa mkazo. Alitambua katika kuzuka kwa hiyo vita utimizo wa unabii mbalimbali wa Biblia ambao alikuwa amehubiri juu yake. (Mathayo 24:7) Wakati huo Wanafunzi wa Biblia wengi waliamini kwamba wangechukuliwa mbinguni upesi. Hilo lilipokosa kutukia, baadhi yao walitamauka.

Msimamo Wangu kwa Ajili ya Kweli ya Biblia

Mwaka wa 1915, nikiwa mwenye umri wa miaka 17, nilimaliza shule ya kati na kuanza kufanya kazi ya kimwili ofisini. Kisha nikaanza kusoma Mnara wa Mlinzi kwa ukawaida. Lakini mikutano ya kawaida haikufanywa Kopervik hadi mwaka wa 1918. Mwanzoni, tulihudhuria tukiwa watano. Tulisoma vichapo vya Watch Tower Society, kama vile Studies in the Scriptures, na kuzungumzia habari hiyo kwa njia ya maswali na majibu. Ijapokuwa mama aliwasifu Wanafunzi wa Biblia kwa watu wengine, hakupata kamwe kuwa mmoja wetu.

Ofisini nilikofanyia kazi, kuanzia mwaka wa 1918, nilipata kujuana na Anton Saltnes, niliyeweza kumsaidia kuwa Mwanafunzi wa Biblia. Wakati huo nilipata kuwa mhubiri wa kawaida na kubatizwa kwenye kusanyiko fulani Bergen mwaka wa 1921.

Mei 1925 kulikuwa na kusanyiko Örebro, Sweden, kwa ajili ya nchi zote za Skandinavia. Watu zaidi ya 500 walihudhuria, kutia na Joseph F. Rutherford, msimamizi wa Watch Tower Society. Sisi tukiwa watu karibu 30 tulisafiri kutoka Oslo kwa gari-moshi ndani ya kochi iliyohifadhiwa kwa ajili ya Wanafunzi wa Biblia.

Kwenye kusanyiko hilo kulitangazwa kwamba ofisi ya tawi iliyoitwa Northern European Office ingeanzishwa Copenhagen, Denmark, ili kushughulikia kazi ya kuhubiri kotekote katika Skandinavia na nchi za Baltiki. William Dey kutoka Scotland alipewa mgawo wa kusimamia kazi ya kuhubiri. Alipendwa sana, na upesi akaja kuitwa Big Scotsman (Mskochi Mkubwa). Mwanzoni Ndugu Dey hakuwa na ujuzi wa lugha yoyote ya Kiskandinavia, hivyo alikuwa akiketi nyuma wakati wa mikutano na makusanyiko na kutunza watoto ili kwamba wazazi wao waweze kukazia fikira yale yaliyokuwa yakisemwa jukwaani.

Gazeti The Watch Tower la Machi 1, 1925, lilizungumzia Ufunuo sura ya 12 na kueleza kwamba sura hii yahusiana na kuzaliwa kwa Ufalme wa Mungu na kwamba kuzaliwa huko kulitukia mbinguni mwaka wa 1914. Nililipata kuwa jambo gumu kuelewa, hivyo nikasoma hiyo makala tena na tena. Hatimaye nilipoelewa, nilifurahi sana.

Wakati ambapo marekebisho yamefanywa katika uelewevu wetu wa habari za Biblia, watu fulani wamekwazika na wamejiondoa kutoka kwa watu wa Mungu. Lakini wakati ambapo rekebisho kama hilo limekuwa gumu kueleweka, sikuzote nimesoma hiyo habari tena na tena ili kujaribu kuelewa njia ya kusababu. Ikiwa bado sijaelewa ufafanuzi mpya, mimi hungojea kueleweshwa. Subira hiyo imenithawabisha tena na tena.

Utumishi Kwenye Betheli

Kwa miaka kadhaa nilifanya kazi nikiwa mweka-hesabu, sekretari, na mhasibu wa mkoa. Mwaka wa 1928 mtu aliyekuwa ametunza hesabu za kifedha za Sosaiti akawa mgonjwa na kulazimika kuondoka Betheli. Kwa kuwa nilikuwa na uzoefu katika kazi hiyo, niliombwa kuifanya. Nilianza utumishi wa Betheli Juni 1928. Mara kwa mara, Ndugu Dey alituzuru na kukagua hesabu zangu. Familia yetu ya Betheli pia iliongoza katika kazi ya kuhubiri waziwazi Oslo, ambako wakati huo tulikuwa na kutaniko moja tu.

Baadhi yetu tulisaidia ndugu aliyesimamia upakizi wa fasihi kwenye Betheli, Ndugu Sakshammer, kufunga na kutuma gazeti The Golden Age (liitwalo sasa Amkeni!). Ndugu Simonsen na Gunberg walikuwa miongoni mwa waliotusaidia. Tulikuwa wenye furaha, mara nyingi tukiimba nyimbo tulipokuwa tukifanya kazi.

Kuwa na Uhakika Katika Tumaini la Ufalme

Mwaka wa 1935 tulikuja kuelewa kwamba “umati mkubwa” haukuwa jamii ya pili ya kimbingu. Tulijifunza kwamba badala ya hivyo huo huwakilisha jamii itakayookoka dhiki kubwa na yenye fursa ya kuishi milele katika Paradiso duniani. (Ufunuo 7:9-14) Wakiwa na uelewevu huo mpya, baadhi ya wale waliokuwa wameshiriki mifano ya Ukumbusho waling’amua kwamba tumaini lao lilikuwa la kidunia, wakaacha kushiriki.

Ijapokuwa sikuwa na shaka kamwe juu ya tumaini langu la kimbingu, mara nyingi niliwaza, ‘Mbona Mungu anitaka mimi?’ Nilijihisi sistahili pendeleo kubwa kama hilo. Nikiwa mwanamke mdogo, mwenye haya, nilipata jambo la kujifikiria kuwa mfalme nikitawala pamoja na Kristo mbinguni kuwa jambo lisilo la kawaida. (2 Timotheo 2:11, 12; Ufunuo 5:10) Hata hivyo, nilifikiria kwa uzito maneno ya mtume Paulo kwamba “si wengi wenye nguvu” walioitwa, bali “Mungu alivichagua vitu dhaifu vya ulimwengu, ili apate kuaibisha vitu vyenye nguvu.”—1 Wakorintho 1:26, 27.

Utendaji Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili

Aprili 9, 1940, Norway ilivamiwa na askari wa Ujerumani, na punde si punde hiyo nchi ikakaliwa. Likiwa tokeo la vita, wengi waliitikia ujumbe wa Ufalme. Kuanzia Oktoba 1940 hadi Juni 1941, tuliangusha vitabu na vijitabu zaidi ya 272,000. Hilo lamaanisha kwamba kila mmoja wa Mashahidi zaidi ya 470 waliokuwa Norway wakati huo, aliangusha kwa wastani, vitabu na vijitabu zaidi ya 570 wakati wa miezi hiyo tisa!

Julai 8, 1941, Gestapo waliwazuru waangalizi-wasimamizi wote na kuwaambia kwamba ikiwa kazi ya kuhubiri haikukoma, wangetumwa kwenye kambi za mateso. Maofisa wa polisi Wajerumani watano walikuja Betheli na kutwaa nyingi ya mali za Watch Tower Society. Familia ya Betheli ilichukuliwa na kuhojiwa, lakini hakuna hata mmoja wetu aliyetiwa gerezani. Hatimaye, Julai 21, 1941, jengo la Sosaiti, Inkognitogaten 28 B, lilitwaliwa, na kazi yetu ya kuhubiri ikapigwa marufuku. Nilihamia Kopervik tena na kupata kazi ya kimwili ili kujitegemeza.

Wakati huo, baba alikuwa akitumikia akiwa painia. Siku moja Wanazi walikuja na kupekua nyumba ya baba. Walitwaa fasihi zake zote, kutia na Biblia na konkodansi zake za Biblia. Tulipokea kiasi kidogo tu cha ugavi wa chakula cha kiroho wakati huo. Ili kubaki wenye nguvu kiroho, tulijifunza vitabu vya zamani tena na tena, kama vile kitabu Government, na tuliendelea kuhubiri.

Kwa kusikitisha, katika mahali pengi ndugu waligawanyika. Baadhi yao walishikilia kauli kwamba ilitupasa kuhubiri waziwazi na kwenda kutoka nyumba hadi nyumba huku wengine wakihisi kwamba ilitupasa kuhubiri kwa siri zaidi, tukiwasiliana na watu katika njia nyingine. Hivyo ndugu mashuhuri, ambao hapo awali walikuwa wameshirikiana vizuri sana na ambao tuliwapenda sana, wakawa hawasemezani. Huo mgawanyiko kati yao uliniumiza moyo zaidi ya hali nyingine yoyote maishani mwangu nikiwa Shahidi.

Utendaji Uliofanywa Upya Baada ya Vita

Baada ya vita, Ndugu Dey alizuru Norway na kufanya mikutano Oslo, Skien, na Bergen, katika kiangazi cha 1945. Aliwaomba ndugu kusameheana na kuomba wote waliotaka kufanya hivyo wasimame. Wote wakasimama! Huko kubishana kulisuluhishwa kabisa Desemba 1945, baada ya ziara ya Nathan H. Knorr, aliyekuwa msimamizi wa Watch Tower Society wakati huo.

Wakati huohuo, Julai 17, 1945, nilipokea telegramu kutoka kwa mtumishi wa ofisi ya tawi, Ndugu Enok Öman, akiniuliza hivi: ‘Lini waweza kurudi Betheli?’ Mashahidi fulani walisema kwamba ilinipasa kukaa nyumbani na kumtunza baba yangu, aliyekuwa mwenye umri wa miaka zaidi ya 70 wakati huo. Lakini baba alinitia moyo kurudia tena utumishi wa Betheli, jambo ambalo nilifanya. Mwaka wa 1946, Marvin F. Anderson, ndugu kutoka Marekani alipata kuwa mwangalizi wetu wa ofisi ya tawi, na kazi ya kuhubiri ikapangwa tena.

Wakati wa likizo za kiangazi nilikuwa nikirudi Kopervik kuona familia yangu. Ndugu zangu wawili na dada zangu wawili hawakupata kuwa Mashahidi, lakini walikuwa wenye urafiki sikuzote kwa baba nami. Mmoja wa ndugu zangu alipata kuwa mkuu wa bandari na msimamizi wa meli, na yule mwingine alikuwa mwalimu. Ijapokuwa nilikuwa na vichache kimwili, baba alikuwa akiwaambia hivi: “Ottilie ni tajiri zaidi kuliko nyinyi.” Na hilo lilikuwa kweli! Waliyokuwa wamejipatia hayangeweza kulinganishwa na utajiri wa kiroho niliokuwa nikifurahia! Baba alikufa mwaka wa 1951 akiwa mwenye umri wa miaka 78. Mama alikuwa amekufa mwaka 1928.

Jambo kuu maishani mwangu lilikuwa kuhudhuria mkusanyiko wa kimataifa wa watu wa Yehova katika Jiji la New York mwaka wa 1953. Mwaka huo shamba la ulimwengu lilipita alama ya wahubiri 500,000 na watu zaidi ya 165,000 walihudhuria huo mkusanyiko! Kabla ya mkusanyiko wa mwaka wa 1953, nilifanya kazi kwa muda wa juma moja kwenye Betheli ya Brooklyn, makao makuu ya tengenezo la Yehova duniani.

Kufanya Niwezayo

Katika miaka ya juzijuzi uwezo wangu wa kuona umedhoofika kwa sababu ya ugonjwa wa mtoto wa jicho. Nikiwa na miwani yenye nguvu na kiookuzi, naweza bado kusoma chapa kubwa kwa kiasi kidogo. Na dada Wakristo hunizuru na kunisomea mara mbili kwa juma, na ninashukuru sana kwa jambo hilo.

Utendaji wangu wa kuhubiri ni mdogo pia. Wakati wa kiangazi, dada Wakristo wamenitoa nje pindi kwa pindi katika kiti changu chenye magurudumu hadi mahali ambapo naweza kuhubiri kwa kiasi fulani. Pia mimi huzipelekea shule katika Kopervik magazeti na broshua kwa ukawaida, kama ile shule ya msingi ambako nilikuwa mwanafunzi karibu miaka 100 iliyopita. Ninaterema kwamba bado yawezekana kwangu kuwa mhubiri wa kawaida.

Kwa uzuri chumba cha kulia na Jumba la Ufalme viko kwenye orofa moja na chumba changu Betheli, ambayo tangu mwaka wa 1983 imekuwa katika mji wa Ytre Enebakk nje ya Oslo. Hivyo ninaweza kufika kwenye ibada ya asubuhi, milo, na mikutano yetu kwa kutumia kifaa cha kunisaidia kutembea. Na ninafurahi kwamba bado naweza kufika kwenye mikusanyiko na makusanyiko. Mimi hufurahia kukutana na marafiki ambao nimewajua kwa miaka mingi, na vilevile ndugu na dada wapya na watoto wengi wazuri.

Kudumisha Imani Mpaka Mwisho

Ni baraka kuzingirwa hapa Betheli na watu wenye bidii, wenye kupendeza, na wa kiroho. Nilipoanza utumishi wangu wa Betheli, familia nzima ilifanyizwa na wale waliokuwa na tumaini la kimbingu. (Wafilipi 3:14) Sasa kila mtu Betheli isipokuwa mimi hutazamia kuishi milele duniani.

Ni kweli, tulitarajia kwamba Yehova angalikuwa amechukua hatua mapema zaidi. Lakini, nashangilia kuona umati mkubwa ukiendelea kuwa mkubwa zaidi na zaidi. Nimeona maongezeko kama nini! Niliposhiriki katika huduma kwa mara ya kwanza, kulikuwa na wahubiri wapatao 5,000 ulimwenguni pote. Sasa kuna wahubiri zaidi ya 5,400,000! Kwa kweli, nimeona ‘mdogo akiwa elfu, na mnyonge akiwa taifa hodari.’ (Isaya 60:22) Twahitaji kufuliza kumtarajia Yehova, kama vile nabii Habakuki alivyoandika: “Ijapokawia, ingojee; kwa kuwa haina budi kuja.”—Habakuki 2:3.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki