Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 10/15 kur. 5-7
  • Furaha Halisi—Ufunguo Ni Nini?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Furaha Halisi—Ufunguo Ni Nini?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ukiroho Huongoza Kwenye Furaha
  • Uwezo Wetu wa Kuchagua
  • Hekima na Utii wa Kimungu —Ule Ufunguo
  • Kupata Furaha ya Kweli kunategemea Wewe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Jinsi ya Kupata Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Furaha ya Kweli Katika Kumtumikia Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Wenye Furaha Ni Watu Wanaomtumikia “Mungu Mwenye Furaha”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2018
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 10/15 kur. 5-7

Furaha Halisi—Ufunguo Ni Nini?

WANADAMU walitakiwa wawe wenye furaha. Kwa nini twaweza kuwa na hakika juu ya jambo hilo? Fikiria mwanzo wa mwanadamu.

Yehova Mungu aliumba wenzi wa kwanza wa kibinadamu wakiwa na uwezo wa kuwa na furaha. Adamu na Hawa waliwekwa katika paradiso, bustani ya raha iliyoitwa Edeni. Muumba aliwaandalia vitu vyote vya kimwili vya lazima maishani. Hiyo bustani ilikuwa na “kila mti unaotamanika kwa macho na kufaa kwa kuliwa.” (Mwanzo 2:9) Adamu na Hawa walikuwa wenye afya, wenye nguvu, na wazuri—walikuwa wakamilifu na wenye furaha kikweli.

Ingawa hivyo, ni nini uliokuwa ufunguo wa furaha yao? Je, ulikuwa makao yao ya kiparadiso au labda ukamilifu wao wa kimwili? Zawadi hizi kutoka kwa Mungu zilichangia kufurahia kwao maisha. Lakini furaha yao haikutegemea vitu hivyo vyenye kugusika. Bustani ya Edeni haikuwa tu shamba zuri. Ilikuwa mahali patakatifu, mahali pa kumwabudu Mungu. Ufunguo wa kupata kwao furaha ya milele ulikuwa uwezo wao wa kuimarisha na kudumisha uhusiano wenye upendo na Muumba. Ili kuwa wenye furaha, iliwapasa kwanza kuwa wa kiroho.—Linganisha Mathayo 5:3.

Ukiroho Huongoza Kwenye Furaha

Mwanzoni Adamu alikuwa na uhusiano wa kiroho na Mungu. Ulikuwa uhusiano wenye upendo na mwororo kama ule wa mwana na baba. (Luka 3:38) Katika bustani ya Edeni, Adamu na Hawa walikuwa na hali zifaazo zilizowaruhusu kutosheleza tamaa yao ya kutoa ibada. Kupitia utii wao kwa Yehova wenye upendo, usio wa kulazimishwa, wangemletea Mungu heshima na utukufu mkubwa zaidi ya ule ambao uumbaji wa wanyama ungeweza kumletea. Kwa kutumia akili wangeweza kumsifu Mungu kwa sababu ya sifa zake za ajabu na wangeweza kutegemeza enzi kuu yake. Pia wangeweza kuendelea kupokea utunzaji wa Yehova wenye upendo na mwororo.

Ushirika huo pamoja na Muumba na kutii amri zake ziliwaletea wazazi wetu wa kwanza furaha ya kweli. (Luka 11:28) Adamu na Hawa hawakutarajiwa waishi miaka mingi ya kujaribu-jaribu mambo kabla ya kugundua ufunguo wa kupata furaha. Walikuwa wenye furaha tangu walipoumbwa. Kuwa wenye amani na Mungu na wenye kunyenyekea mamlaka yake kuliwafurahisha.

Hata hivyo, furaha hiyo iliisha, mara walipokosa kumtii Mungu. Kwa kuasi, Adamu na Hawa walivunja uhusiano wao wa kiroho na Yehova. Hawakuwa tena rafiki za Mungu. (Mwanzo 3:17-19) Yaonekana kwamba tangu ile siku walipofukuzwa bustanini, Yehova alikatiza uwasiliano wote pamoja nao. Walipoteza ukamilifu wao, tazamio la kuishi milele, na makao yao ya bustani. (Mwanzo 3:23) Lakini lililo la maana zaidi, kwa kuwa walipoteza uhusiano wao na Mungu, walipoteza ufunguo wa kupata furaha.

Uwezo Wetu wa Kuchagua

Kabla ya kufa, Adamu na Hawa waliwapitishia wazao wao tabia zao za kibinadamu, dhamiri yao ya kiasili, na uwezo wa ukiroho. Familia ya kibinadamu haikushushwa kufikia kiwango cha wanyama. Twaweza kupatanishwa na Muumba. (2 Wakorintho 5:18) Wakiwa viumbe wenye akili, wanadamu huendelea kuwa na uwezo wa kuchagua ikiwa watamtii Mungu au la. Jambo hili lilitolewa kielezi karne nyingi baadaye Yehova alipolitolea taifa la Israeli lililotoka tu kufanyizwa, chaguo la uhai au kifo. Kupitia msemaji wake Musa, Mungu alisema hivi: “Nimekuwekea leo mbele yako uzima [“uhai,” NW] na mema, na mauti [“kifo,” NW] na mabaya.”—Kumbukumbu la Torati 30:15-18.

Hata sasa, maelfu ya miaka baada ya Paradiso ya awali kupotea, sisi wanadamu bado tuna uwezo wa kufanya chaguo lifaalo. Tuna dhamiri yenye kutenda na uwezo wa msingi wa kutii sheria za Mungu. Biblia husema juu ya “mtu tuliye kwa ndani” na yule mtu “kwa ndani.” (2 Wakorintho 4:16; Waroma 7:22) Semi hizo zahusiana na ule uwezekano tuliozaliwa nao wa kudhihirisha utu wa Mungu, kufikiri kwa njia ambayo Mungu hufikiri, kuwa wa kiroho.

Kwa habari ya asili yetu ya kiadili na dhamiri yetu, mtume Paulo aliandika hivi: “Wakati wowote ule watu wa mataifa wasio na sheria wafanyapo kwa asili mambo ya sheria, watu hawa, ijapokuwa hawana sheria, wao ni sheria kwao wenyewe. Wao ndio walewale waonyeshao kiini cha sheria kuwa imeandikwa katika mioyo yao, huku dhamiri yao ikitoa ushahidi pamoja nao na, kati ya fikira zao wenyewe, wanashtakiwa au hata wanatetewa.”—Waroma 2:14, 15.

Hekima na Utii wa Kimungu —Ule Ufunguo

Ingawa hivyo, huenda mtu akauliza, ‘Ikiwa sisi sote tuna mwelekeo wa kiasili wa kuabudu Mungu na, hivyo kuonea shangwe furaha ya kweli, kwa nini hali ya kukosa furaha imeenea sana hivyo?’ Ni kwa sababu kila mmoja wetu lazima akuze ukiroho ili awe mwenye furaha. Ijapokuwa awali tuliumbwa kwa mfano wa Mungu, mwanadamu amefarakana na Muumba wake. (Waefeso 4:17, 18) Kwa sababu hiyo, kila mmoja wetu lazima achukue hatua dhahiri kuanzisha na kudumisha uhusiano wa kiroho na Mungu. Uhusiano huo hautakua bila kufanya jitihada yoyote.

Yesu alionyesha kanuni mbili za maana katika kukuza ukiroho. Kanuni moja ni kujipatia ujuzi juu ya Mungu, na ile nyingine ni kuyanyenyekea kwa utiifu mapenzi yake. (Yohana 17:3) Akinukuu Neno la Mungu, Yesu alisema hivi: “Imeandikwa, ‘Binadamu lazima aishi, si kwa mkate pekee, bali kwa kila tamko linalokuja kupitia kinywa cha Yehova.’” (Mathayo 4:4) Wakati mwingine, Yesu alitaarifu hivi: “Chakula changu ni kwamba mimi nifanye mapenzi yake aliyenituma na kumaliza kazi yake.” (Yohana 4:34) Si lazima tutumie miaka mingi tukitafuta furaha kwa kujaribu-jaribu mambo. Kupatwa na jambo si ufunguo wa kupata furaha. Badala ya hivyo, ni hekima na utii wa kimungu kwa Muumba wetu uwezao kutuongoza kwenye shangwe ya kweli maishani.—Zaburi 19:7, 8; Mhubiri 12:13.

Kwa wazi, furaha ambayo hutokana na kudhihirisha hekima ya kimungu na kuwa na msimamo mzuri mbele ya Mungu haiko mbali nasi. (Matendo 17:26, 27) Ujuzi juu ya Yehova na kusudi lake linapatikana kwa kila mmoja. Ikiwa na bilioni za nakala katika lugha nyingi, Biblia yaendelea kuwa kitabu kilichogawanywa kwa wingi zaidi. Biblia yaweza kukusaidia uwe rafiki ya Mungu na uonee shangwe furaha ya kweli, kwa sababu Maandiko hutuambia kwamba ‘heri watu wenye BWANA kuwa Mungu wao!’—Zaburi 144:15.

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

Hatua Kuelekea Furaha

1. Ng’amua na kusitawisha ukiroho. Yesu alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika!”—Luka 11:28.

2. Tambua kwamba kibali cha Mungu ni cha maana zaidi kuliko mali au anasa. Paulo aliandika hivi: “Kwa hakika, huo ni njia ya kupata faida kubwa, ujitoaji-kimungu huu pamoja na ujitoshelevu. . . . Tukiwa na riziki na cha kujifunika, tutakuwa wenye kuridhika na vitu hivi.”—1 Timotheo 6:6-8.

3. Jitahidi kusitawisha na kuitikia dhamiri iliyozoezwa na Biblia.—Waroma 2:14, 15.

4. Azimia kumtii Yehova Mungu, hivyo ukistahili kuwa mmoja wa watu wake. Daudi wa zamani aliandika hivi: “Heri watu wenye BWANA [“Yehova,” NW] kuwa Mungu wao.”—Zaburi 144:15.

[Picha katika ukurasa wa 7]

“Wenye furaha ni wale wenye kuona uhitaji wao wa kiroho.”—Mathayo 5:3

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki