Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 10/15 kur. 8-12
  • Jinsi Biblia Ilivyotufikia—Sehemu ya Tatu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi Biblia Ilivyotufikia—Sehemu ya Tatu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Wamishonari na Sosaiti za Biblia
  • Majaribu ya Mtafsiri Mmoja
  • Ubishi Waizingira Biblia
  • Uvumbuzi Mbalimbali Wasaidia Kuthibitisha Maandishi ya Biblia
  • Watch Tower Society na Biblia
  • Tafsiri Moja, Lugha Nyingi
  • Habari Njema kwa Mataifa Yote
  • Kuchapa na Kugawanya Neno Takatifu la Mungu Mwenyewe
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Kitabu “Kisemacho” Lugha Zilizo Hai
    Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote
  • Kuiponyosha Codex Sinaiticus
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Hatua Muhimu kwa Wapendao Neno la Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 10/15 kur. 8-12

Jinsi Biblia Ilivyotufikia—Sehemu ya Tatu

BURMA, 1824—Maofisa wa mfalme wametoka tu kupekua makao ya mishonari ya Adoniram na Ann Judson, wakichukua kila kitu walichofikiri kuwa chenye thamani. Lakini wamekosa hazina yenye thamani zaidi—hati ya Biblia iliyotafsiriwa ambayo Ann alikuwa ameficha kisiri chini ya hiyo nyumba. Adoniram, mtafsiri, alala akiwa amefungwa kwa minyororo katika gereza lenye mbu wengi, akishtakiwa kupeleleza. Sasa unyevuanga watisha kuharibu hiyo hati. Yaweza kuokolewaje? Ann aishona ndani ya mto mgumu na kuupeleka kwa mume wake gerezani. Mto huo unahifadhiwa, na yaliyomo yawa sehemu ya Biblia ya kwanza ya Kiburma.

Biblia imepatwa na matukio mengi kama hayo katika historia. Katika matoleo yaliyotangulia, tulichunguza kutafsiriwa na kugawanywa kwa Biblia tangu kumalizika kwake hadi mapema miaka ya 1600. Biblia imekuwa na hali gani tangu wakati huo hadi wakati wa sasa? Je, ingepata kupatikana kwa watu wote? Watch Tower Society imekuwa na fungu gani?

Wamishonari na Sosaiti za Biblia

Katika nchi nyingi, miaka ya 1600 na ya 1700 ilitiwa alama na ongezeko kubwa la usomaji wa Biblia. Uingereza hasa iliathiriwa sana na Biblia wakati wa kipindi hicho. Kwa hakika, hadithi na mafundisho ya Biblia yalipenya mawazo ya karibu kila mtu katika hiyo nchi, toka mfalme hadi kijana mwongoza plau. Lakini uvutano wa Biblia ulienea mbali zaidi. Wakati huo Uingereza ilikuwa serikali yenye kufanya biashara baharini na ya kikoloni, na Waingereza fulani waliichukua Biblia katika safari zao. Hilo liliweka msingi wa kampeni ya Biblia iliyoenea.

Kuelekea mwisho wa miaka ya 1700, Biblia iliwachochea watu fulani Uingereza kufikiria mahitaji ya kiroho ya wenyeji wa nchi zilizotapakaa za Milki ya Uingereza. Hata hivyo, hangaiko hilo halikuwa la ulimwenguni pote kamwe. Watu wengi wa kanisa waliamini juu ya kuamuliwa kimbele yatakayompata mtu, na kwa hiyo waliyafikiria kuwa mapenzi ya Mungu kwamba watu fulani wasiokolewe. William Carey aliyetarajiwa kuwa mishonari alipotoa hotuba yenye idili ili kuchochea tegemezo kwa ajili ya kutuma misheni India, mtu fulani alipaaza sauti akimkemea: “Keti chini, mwanamume kijana; Mungu atakapo kugeuza makafiri, Atafanya hivyo bila msaada wako!” Hata hivyo, Carey alisafiri kupitia baharini kuelekea India mwaka wa 1793. Kwa kushangaza, hatimaye alitafsiri Biblia nzima au visehemu vyake katika lugha 35 za Kihindi.

Wamishonari waling’amua kwamba chombo chao cha msingi kabisa kilikuwa Biblia katika lugha ya kienyeji. Hata hivyo, ni nani angeandaa Biblia? Kwa kupendeza, Mary Jones, msichana kutoka Wales mwenye umri wa miaka 16, alianzisha bila kujua harakati ambayo ingeeneza Biblia ulimwenguni pote. Mwaka wa 1800, Mary alitembea kilometa 40 kwa miguu mitupu ili akanunue Biblia ya lugha ya Welsh kutoka kwa kasisi. Alikuwa ameweka akiba ya fedha zake kwa miaka sita, na alipopata kujua kwamba Biblia zote zilikuwa zimeuzwa, Mary alilia kwa huzuni, akatoa machozi ya uchungu wa kukatishwa tamaa. Akiwa amechochewa sana, huyo kasisi alimpa Mary mojawapo ya Biblia zake mwenyewe.

Baada ya hapo, huyo kasisi aliwafikiria wengine wengi waliohitaji Biblia, naye alijadiliana na marafiki juu ya tatizo hilo huko London. Tokeo lilikuwa kuundwa kwa British and Foreign Bible Society mwaka wa 1804. Kauli yake ilikuwa sahili: Kuandalia watu Biblia zenye kununulika katika lugha zao wenyewe, zilizochapishwa “bila marejezo wala maelezo.” Kwa kuondosha maelezo pambizoni, waanzilishi wa hiyo Sosaiti walitumainia kuepuka ubishi wa kimafundisho. Ingawa hivyo, mara nyingi Sosaiti ya Biblia ingegawanyika kuhusiana na Apokrifa, ubatizo kwa kuzamisha, na kuhusiana na fundisho la Utatu.

Idili ya mwanzoni ilienea upesi, na kufikia mwaka wa 1813 sosaiti zilizohusiana kwa ukaribu zilikuwa zimeundwa Ujerumani, Uholanzi, Denmark, na Urusi. Muda si muda, sosaiti za Biblia zikaongezwa katika nchi nyingine. Sosaiti za Biblia za mapema zilipounda miradi yake, zilifikiri kwamba sehemu kubwa ya ulimwengu ilitumia lugha chache tu kubwa-kubwa. Hazikuwazia kamwe kwamba kulikuwa na maelfu ya lugha! Watafsiri wachache kwa kulinganishwa walijua Kiebrania na Kigiriki ili kutafsiri moja kwa moja katika lugha za kienyeji. Kwa hiyo, British and Foreign Bible Society ilipofadhili tafsiri mbalimbali, mara nyingi watafsiri walitegemeza kazi yao juu ya tafsiri ya King James Version ya lugha ya Kiingereza.

Majaribu ya Mtafsiri Mmoja

Sehemu kubwa ya Biblia ni masimulizi na vielezi vitegemeavyo mambo yanayoonwa kila siku. Hilo hufanya iwe rahisi kutafsiri kuliko ikiwa ingeandikwa kwa kutumia mitajo dhahania ya falsafa. Hata hivyo, kama iwezavyo kutabiriwa, jitihada za mapema za wamishonari zilitokeza tafsiri zenye kutatanisha au zenye kuchekesha. Kwa kielelezo, tafsiri moja iliwapa watu katika sehemu fulani ya India wazo la kwamba Mungu ana rangi ya kibluu. Neno lililotumiwa kumaanisha “-a kimbingu” katika usemi “Baba wa kimbingu” lilimaanisha “kuwa na rangi ya anga”—mbingu halisi!

Kwa habari ya vizuizi vya mtafsiri, Adoniram Judson aliandika hivi mwaka wa 1819: Tunapojifunza lugha inayosemwa na watu sehemu ile nyingine ya dunia, ambao njia zao za kufikiri ni tofauti kabisa na zetu, na ambao kwa hiyo hatufahamu misemo yao, na herufi na maneno hayafanani hata kidogo na yale ya lugha yoyote ile ambayo tumeona; wakati ambapo hatuna kamusi wala mkalimani na ni lazima tuielewe lugha hiyo kidogo kabla hatujaweza kujipatia msaada wa mwalimu wa mahali hapo—hilo lamaanisha kazi!’ Nayo kazi ya watafsiri kama vile Judson iliongeza sana kupatikana kwa Biblia.—Ona chati kwenye ukurasa wa 12.

Ann Judson alimsaidia mumewe katika ile kazi ngumu ya kutafsiri. Lakini akina Judson walikabili zaidi ya majaribu ya kitaaluma. Maofisa wa mfalme walipomkokota Adoniram hadi jela, Ann alikuwa akitarajia kupata mtoto mchanga. Kwa muda wa miezi 21, akiwa na moyo mkuu, aliwaomba kwa bidii maofisa wenye uhasama wamwachilie mumewe. Masaibu hayo pamoja na ugonjwa ulidhuru afya yake. Muda mfupi baada ya Adoniram kuachiliwa, Ann wake mwenye ujasiri na binti yao mchanga walikufa kutokana na homa. Adoniram alivunjika moyo. Hata hivyo, alimtegemea Mungu ili kupata nguvu naye akaendelea kutafsiri, akikamilisha Biblia ya Kiburma mwaka wa 1835. Wakati huohuo, ubishi mwingine wenye hila juu ya Biblia ulikuwa ukikua.

Ubishi Waizingira Biblia

Miaka ya 1800 ilipatwa na ubishi mkubwa wa kijamii na kisiasa, nyakati nyingine Biblia ikiwa na fungu kuu. Mathalani, ijapokuwa Russian Bible Society ilianza ikiungwa mkono na zari na Kanisa Othodoksi la Urusi, muda si muda waliivunja na kuipiga marufuku hiyo Sosaiti. (Tayari wapinzani wa Sosaiti hiyo walikuwa wamechoma maelfu ya Biblia wapata mwaka mmoja mapema.) Sasa makasisi wa Othodoksi walijitahidi kwa bidii kukomesha kile ambacho Wakristo wa mapema walikuwa wameanzisha kwa idili—kuenezwa kwa Biblia katika ulimwengu wote mzima. Viongozi wa Othodoksi katika karne ya 19 walisisitiza kwamba Biblia ilihatarisha mamlaka ya Kanisa na ya Serikali. Kinyume cha hilo, harakati ya kimapinduzi ya kisiasa yenye kuibuka ilikuja kuiona Biblia kuwa silaha ya Kanisa na Serikali ya kutiisha matungamo ya watu, badala ya kuwa tisho kwa serikali. Biblia ilikuwa ikishambuliwa toka pande zote mbili!

Miaka iliyofuata pia ilikuwa na ongezeko la mashambulio ya “wenye akili” dhidi ya Biblia. Mwaka wa 1831, Charles Darwin alisafiri kwa merikebu katika safari ya uvumbuzi iliyoongoza kwenye nadharia yake ya mageuzi. Mwaka wa 1848, Marx na Engels walitoa hati iitwayo Communist Manifesto, ikionyesha Ukristo kuwa chombo cha uonevu. Pia katika kipindi hicho, wahakiki wa Biblia walisaili uasilia wa Maandiko na uhalisi wa kihistoria wa watu wanaotajwa na Biblia—hata wa Yesu mwenyewe! Lakini watu fulani wenye kufikiri walitambua kukosea kwa nadharia zilizokataa Mungu na Biblia, nao walitafuta njia za kisomi za kuthibitisha kutegemeka kwa Biblia. Mmojawapo wa hao alikuwa Konstantin von Tischendorf, Mjerumani aliyejua lugha kadhaa.

Uvumbuzi Mbalimbali Wasaidia Kuthibitisha Maandishi ya Biblia

Tischendorf alisafiri kupitia Mashariki ya Kati akitafuta hati za kale za Biblia, akitumainia kuimarisha maandishi ya awali ya Biblia pasipo shaka. Mwaka wa 1859, mwaka uleule ambao Darwin alichapisha kitabu The Origin of Species, Tischendorf alipata iliyokuwa nakala nzima ya zamani zaidi iliyojulikana ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika nyumba kubwa ya utawa chini ya Mlima Sinai. Yajulikana kuwa Codex Sinaiticus nayo yamkini ilitokezwa yapata miaka 50 kabla ya Jerome kukamilisha Vulgate ya Kilatini. Ingawa kufaa kwa kuiondoa kwake kodeksi kutoka katika hiyo nyumba kubwa ya utawa kungali kwajadiliwa, Tischendorf aliichapisha, hivyo akifanya wasomi waipate.a

Kwa kuwa Sinaiticus ilikuwa miongoni mwa hati za kale zaidi za lugha ya awali, ilifunua kwamba kimsingi Maandiko ya Kigiriki hayakuwa yamebadilika na pia iliwasaidia wasomi kufunua makosa yaliyokuwa yamepenya na kuingia katika hati za baadaye. Kwa kielelezo, rejezo kwa Yesu kwenye 1 Timotheo 3:16 katika Sinaiticus husomeka hivi: “Yeye alifanywa kuwa dhahiri katika mwili.” Mahali pa “yeye,” nyingi za hati zilizojulikana wakati huo zilionyesha ufupisho wa “Mungu,” uliofanywa kwa kufanya marekebisho madogo kwa neno la Kigiriki “yeye.” Hata hivyo, Sinaiticus ilifanyizwa miaka mingi kabla ya hati yoyote ya Kigiriki kusomeka “Mungu.” Hivyo, ilifunua kwamba maandishi yalikuwa yamefisidiwa baadaye, kwa wazi yakianzishwa ili kutegemeza fundisho la Utatu.

Tangu wakati wa Tischendorf, hati nyingi zaidi zimevumbuliwa. Leo, jumla ya hati zijulikanazo za Maandiko ya Kiebrania zapata 6,000, na za Maandiko ya Kigiriki, zaidi ya 13,000. Uchunguzi wa kulinganisha wa hizo umetokeza maandishi ya lugha ya awali yawezayo kutumainiwa kwa uhakika. Kama vile msomi F. F. Bruce aelezavyo: “Kusomeka kunakotofautiana . . . hakuathiri mambo hakika au mafundisho yoyote ya maana ya kihistoria au imani na desturi ya Kikristo.” Huku kutafsiriwa kwa Biblia katika lugha nyingi zaidi kulipoendelea, ujuzi huo ulioongezeka ungeweza kunufaishaje watu?

Watch Tower Society na Biblia

Mwaka wa 1881 walimu na wanafunzi wa Biblia waliokuwa kikundi kidogo lakini chenye bidii, waliunda iliyokuja kuwa Watch Tower Bible and Tract Society. Mwanzoni, waligawanya Biblia zilizotokezwa na sosaiti nyingine za Biblia, kutia na Maandiko ya Kigiriki ya Tischendorf. Hata hivyo, kufikia mwaka wa 1890 walikuwa wameingia moja kwa moja katika uchapishaji wa Biblia, wakifadhili chapa ya kwanza kati ya chapa kadha wa kadha za Biblia. Mwaka wa 1926 Sosaiti ilianza kuchapa Biblia kwa kutumia matbaa yake yenyewe. Lakini uhitaji wa tafsiri iliyofanywa iwe ya kisasa ya Biblia ulikuwa ukidhihirika zaidi. Je, ujuzi uliopatikana kupitia uvumbuzi mbalimbali na utaalamu wa karne zilizotangulia zingeweza kuunganishwa katika Biblia ielewekayo, yenye kununulika? Ikiwa na lengo hilo, mwaka wa 1946, washiriki wa Sosaiti walianza kutokeza tafsiri mpya ya Maandiko.

Tafsiri Moja, Lugha Nyingi

Halmashauri ya tafsiri ya Wakristo watiwa-mafuta wenye uzoefu ilipangwa ili kutokeza Biblia ya New World Translation of the Holy Scriptures katika Kiingereza. Ilichapishwa katika mabuku sita, yaliyotolewa kuanzia mwaka wa 1950 hadi 1960, ikianza na Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Tangu mwaka wa 1963 imetafsiriwa katika lugha 27 za ziada, nyingine zaidi zikiendelea kutafsiriwa. Miradi ya lugha nyingine imekuwa sawa na ile ya Kiingereza. Kwanza, tafsiri yapaswa kuwa sahihi, inayokaribia iwezekanavyo mawazo ya awali. Maana haipasi kupindwa ili ipatane na uelewevu fulani wa kimafundisho. Pili, upatano lazima udumishwe, hiyo tafsiri ikishikilia tafsiri moja kwa kila neno kuu maadamu muktadha waruhusu kwa kufaa. Mfikio huo husaidia wasomaji kuona jinsi waandikaji wa Biblia walivyotumia maneno hususa. Tatu, tafsiri yapaswa kuwa ya neno kwa neno kwa kadiri iwezekanavyo bila kuficha maana. Kutafsiri neno kwa neno humtolea msomaji fursa ya kukaribia zaidi ladha ya lugha za awali na ule utaratibu wa mawazo unaohusianishwa. Na nne, yapaswa kuwa rahisi kwa watu wa kawaida kuisoma na kuielewa.

Ule mtindo ulio wa neno kwa neno wa New World Translation ya Kiingereza hurahisisha kuitafsiri katika lugha nyingine. Kwa kusudi hilo vikundi vya kutafsiri vya Sosaiti sasa hutumia vyombo vya hali ya juu vinavyotumia kompyuta ili kuharakisha kazi yao na kuifanya iwe sahihi zaidi. Mfumo huo huwasaidia watafsiri kutunga orodha ya maneno ya kienyeji kwa ajili ya kila neno kuu. Pia huwawezesha kujifunza tafsiri ya Kiingereza ya kila neno la Kiebrania na Kigiriki katika Biblia.

Kutafsiri kutoka hicho Kiingereza, badala ya kutafsiri moja kwa moja kutoka Kiebrania na Kigiriki, hutoa faida za maana. Mbali na kufupisha wakati wa kutafsiri, hufanya iwezekane kuwe na muungano mkubwa zaidi wa usemi katika lugha zote. Kwa nini? Kwa sababu ni rahisi zaidi kutafsiri kwa usahihi kutoka lugha moja ya kisasa hadi lugha nyingine kuliko kutafsiri kutoka lugha ya kale hadi lugha mbalimbali za kisasa. Kwa vyovyote, watafsiri wanaweza kufanya shauri na wasemaji wenyeji wa lugha za kisasa lakini hawawezi kufanya hivyo kwa habari ya lugha zilizosemwa maelfu ya miaka iliyopita.

Habari Njema kwa Mataifa Yote

Mengi zaidi yangeweza kuandikwa kuhusu wanaume na wanawake walioazimia ambao wamesaidia kuifanya Biblia iwe kitabu kipatikanacho zaidi sana duniani. Kwa karne kadhaa, angalau Biblia na visehemu vya Biblia bilioni nne zimechapwa katika lugha zaidi ya elfu mbili, zisemwazo na zaidi ya asilimia 90 ya idadi ya watu wa dunia!

Biblia ilitabiri kupigwa mbiu kwa ulimwenguni pote juu ya Ufalme wa Mungu katika siku yetu. Kwa kusudi hilo, Yehova Mungu mwenyewe kwa wazi amewaongoza wanadamu katika kuifanya Biblia sasa ipatikane karibu katika ulimwengu wote mzima. (Mathayo 13:47, 48; 24:14) Watafsiri na wachapishaji wa Biblia wasio na hofu wa wakati uliopita walihatarisha kila kitu ili kutupatia Neno la Mungu—chanzo pekee cha nuru ya kiroho katika ulimwengu wenye giza kiadili. Kielelezo chao na kikusukume kulisoma, kuishi kupatana na hilo, na kulishiriki hilo Neno ukiwa na usadikisho uleule walioonyesha. Ndiyo, kila siku, tumia kwa faida kamili Biblia yenye kutegemeka uliyo nayo!—Isaya 40:6-8.

[Maelezo ya Chini]

a Ona makala “Kuiponyosha Codex Sinaiticus” katika Mnara wa Mlinzi la Oktoba 15, 1988.

[Chati katika ukurasa wa 12]

Ukuzi Katika Kutafsiriwa kwa Biblia

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Idadi ya

Lugha

1 Wayahudi waanza kutafsiri Maandiko ya Kiebrania katika

Kigiriki karibu 280 K.W.K.

12 Jerome akamilisha Vulgate ya Kilatini karibu 400 W.K.

35 Gutenberg akamilisha Biblia ya kwanza iliyochapwa karibu 1455

81 British and Foreign Bible Society iliyoanzishwa 1804

Idadi Zilizokadiriwa za Lugha Kulingana na Mwaka

522

1900

600

700

800

900

1,049

1950

1,100

1,200

1,300

1,471

1970

2,123

1996

2,200

2,300

2,400

[Hisani]

Vyanzo: Christianity Today, United Bible Society

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 9]

Mountain High Maps® Copyright © 1995 Digital Wisdom, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Judson alifungwa na kukokotwa

[Hisani]

Kutoka kitabu Judson the Hero of Burma, kilichoandikwa na Jesse Page

[Picha katika ukurasa wa 10]

Tischendorf aliokoa hati yenye thamani kwenye nyumba hii kubwa ya utawa chini ya Mlima Sinai

[Hisani]

Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki