Kufahamu Kanuni Hudhihirisha Ukomavu
MASHIRIKA mabaya huharibu mazoea yenye mafaa. Unavuna unachopanda. (1 Wakorintho 15:33; Wagalatia 6:7) Kila taarifa ni kielelezo cha kweli ya msingi—kanuni—ama kimwili ama kiroho, na kila moja huandaa msingi kwa ajili ya sheria. Ingawa hivyo, huenda sheria zikawa za muda tu, na huelekea kuwa mahususi. Kanuni, kwa upande ule mwingine, ni pana, na zaweza kudumu milele. Hivyo, Neno la Mungu hututia moyo tufikiri kupatana na kanuni popote iwezekanapo.
Kichapo cha Webster’s Third New International Dictionary hufafanua kanuni kuwa “kweli ya ujumla au ya msingi: sheria, fundisho, au dhana iliyo pana na ya msingi ambayo juu yake nyingine hutegemezwa au kutolewa.” Kwa kielelezo, huenda mmoja akamtolea mtoto sheria, “Usiguse jiko kamwe.” Lakini kwa mtu mzima taarifa, “Jiko lina moto” ingetosha. Ona kwamba taarifa ya mwisho ni ya msingi zaidi. Kwa sababu yaongoza lile ambalo mmoja huenda akafanya—labda kupika, kuoka au kuzima jiko—kwa maana fulani inakuwa kanuni.
Bila shaka, kanuni za msingi za maisha ni za kiroho; hizo huongoza kumwabudu kwetu Mungu na furaha yetu. Ingawa hivyo, watu fulani huacha kufanya jitihada zitakwazo ili kusababu juu ya kanuni. Wao hupendelea ule urahisi wa sheria wakabiliwapo na uamuzi. Hilo si jambo la hekima na hutofautiana na kielelezo kilichotolewa na watu wa zamani katika nyakati za Biblia.—Waroma 15:4.
Watu wa Kanuni ya Kimungu
Miongoni mwa watu wasiokamilika, Abeli angeweza kuitwa mtu wa kwanza kabisa wa kanuni ya kimungu. Yaelekea alifikiria sana ile ahadi juu ya “mbegu” na kutambua kwamba ukombozi kutoka dhambi ungehusisha dhabihu ya damu. (Mwanzo 3:15) Hivyo alimtolea Mungu “wazao wa kwanza wa wanyama wake.” Fungu la maneno “na sehemu zilizonona za wanyama” huonyesha kwamba Abeli alimtolea Yehova kilichokuwa chema zaidi. Lakini, ingekuwa miaka zaidi ya elfu mbili baada ya kifo cha Abeli kwamba kwa mara ya kwanza Mungu angeeleza kinagaubaga matakwa yanayohusu dhabihu. Tofauti na Abeli, mtu wa kanuni na mwenye kumhofu Mungu, Kaini, ndugu yake alimtolea Mungu dhabihu ili tu kutimiza wajibu. Lakini mtazamo wake haukuwa wa kuridhisha, kulikuwa na jambo fulani kuhusiana na dhabihu yake lililoonyesha moyo wenye kukosa kanuni.—Mwanzo 4:3-5.
Noa pia alikuwa mtu wa kanuni ya kimungu. Ingawa rekodi ya Biblia huonyesha kwamba Mungu alimwamuru kihususa ajenge safina, hatusomi juu ya amri yoyote ya kumtaka awahubiri wengine. Hata hivyo, Noa huitwa “mhubiri wa uadilifu.” (2 Petro 2:5) Hata ingawa yaelekea Mungu alielekeza kwamba Noa ahubiri, hapana shaka kwamba hisi yake ya kanuni na kupenda kwake jirani pia kulimsukuma kufanya hivyo. Kwa kuwa twaishi katika nyakati kama za Noa, na tuige mtazamo na kielelezo chake bora.
Tofauti na makasisi wa siku yake, Yesu aliwafundisha watu kufikiri kupatana na kanuni. Mahubiri yake ya Mlimani ni kielelezo. Jambo kuu la mahubiri hayo ni ombi la kufuata kanuni. (Mathayo, sura ya 5-7) Yesu alifundisha hivyo kwa sababu, kama Abeli na Noa wa kabla yake, alimjua Mungu kikweli. Hata alipokuwa mvulana, alistahi hii kweli ya msingi: “Mwanadamu haishi kwa mkate tu, bali . . . kwa kila litokalo katika kinywa cha BWANA.” (Kumbukumbu la Torati 8:3; Luka 2:41-47) Ndiyo, ufunguo wa kuwa mtu wa kanuni ya kimungu kwa kweli ni kumjua Yehova, yampendezayo, yasiyompendeza, na makusudi yake. Kanuni hizi juu ya Mungu ziongozapo maisha zetu, huwa kwa kweli kanuni zenye uhai.—Yeremia 22:16; Waebrania 4:12.
Kanuni na Moyo
Yawezekana kutii sheria kwa kusitasita tu, labda kwa sababu ya hofu ya kuadhibiwa kwa kutotii. Hata hivyo, kutii kanuni huzuia mtazamo kama huo, kwa maana kiini hasa cha kanuni ni kwamba zinapoongoza mmoja linakuwa jambo la asili kuitikia kutoka moyoni. Fikiria Yosefu ambaye, kama Abeli na Noa, aliishi kabla ya kuanzishwa kwa agano la Sheria ya Kimusa. Mke wa Potifa alipojaribu kumshawishi, Yosefu aliitikia hivi: “Nifanyeje ubaya huu mkubwa nikamkose Mungu?” Ndiyo, Yosefu alijua ile kanuni kwamba mume na mke ni “mwili mmoja.”—Mwanzo 2:24; 39:9.
Leo ulimwengu unakosa kanuni zenye uadilifu. Wajilisha uhalifu na ukosefu wa adili kama mlafi. Hatari ni kwamba huenda Mkristo akashawishiwa kula kidogo-kidogo, labda kwa siri, chakula kilekile kisichofaa mwili—sinema, vidio, au vitabu. Basi, ni jambo lenye kustahili pongezi kama nini, tukataapo ubaya kwa kanuni kama Yosefu, tukikumbuka kwamba Mungu atahifadhi tu wale wenye uaminifu-mshikamanifu katika “dhiki kubwa” inayokuja. (Mathayo 24:21) Ndiyo, kimsingi ni jinsi tutendavyo faraghani, wala si jinsi tutendavyo hadharani, ndivyo hufunua vile tulivyo kindani.—Zaburi 11:4; Mithali 15:3.
Basi ikiwa twaongozwa na kanuni za Biblia, hatutatafuta idhaniwayo kuwa mianya katika sheria ya Mungu; wala hatutajaribu kuona ni kiwango gani twaweza kuvuka mipaka bila kuvunja sheria fulani. Kufikiri huko ni kujipinga; hutuumiza mwishowe.
Chunguza Kanuni Itegemezayo Sheria
Bila shaka, sheria hutekeleza fungu muhimu katika maisha ya Mkristo. Hizo ni kama walinzi ambao husaidia kutuhami, na kwenye msingi wa hizo sheria kuna kanuni nyingi za maana. Kukosa kufahamu kanuni hizo huenda kukapunguza kupenda kwetu sheria zenye kuhusiana na hizo kanuni. Taifa la kale la Israeli lilionyesha hivyo.
Mungu aliwapa Israeli zile Amri Kumi, ambazo za kwanza zilikataza ibada ya mungu mwingine yeyote ila Yehova. Kweli ya msingi ambayo hutegemeza sheria hiyo ni kwamba Yehova aliumba kila kitu. (Kutoka 20:3-5) Lakini je, hilo taifa liliishi kwa kanuni hiyo? Yehova mwenyewe ajibu hivi: “‘Wewe u baba yetu’ [Waisraeli wakaliambia] gogo la mti, [wakalia] ‘Mama’ kwa jiwe. Lakini mimi [Yehova] wamenipa visogo na kugeuza nyuso zao kutoka kwangu.” (Yeremia 2:27, The New English Bible) Ni upumbavu usio na hisia na ukosao kanuni kama nini! Na uliuumiza moyo wa Yehova kama nini!—Zaburi 78:40, 41; Isaya 63:9, 10.
Wakristo pia wana sheria kutoka kwa Mungu. Kwa kielelezo, wapaswa kuepuka ibada ya sanamu, ukosefu wa adili katika ngono, na utumizi mbaya wa damu. (Matendo 15:28, 29) Ufikiriapo hilo, twaweza kuona kanuni za msingi, kama vile: Mungu hustahili ujitoaji wetu usiohusisha mwingine; twapaswa kuwa waaminifu kwa mwenzi wetu; na Yehova ndiye Mpaji-Uhai wetu. (Mwanzo 2:24; Kutoka 20:5; Zaburi 36:9) Tukifahamu na kuthamini sana kanuni zitegemezazo mielekezo hiyo, twaona kwamba ni yenye manufaa kwetu. (Isaya 48:17) Kwetu sisi, “amri [za Mungu] si zenye kulemea.”—1 Yohana 5:3.
Ingawa wakati mmoja Waisraeli walipuuza amri za Mungu, kufikia wakati wa Yesu waandishi, “madaktari [wao] wa sheria,” walikuwa wamekuwa wakali mno. Walikuwa wamefanyiza sheria na mapokeo mengi sana yaliyozuia ibada safi na kusitiri kanuni za kimungu. (Mathayo 23:2, NEB) Watu walihisi kwamba wameshindwa, wamekosa tumaini, au unafiki. (Mathayo 15:3-9) Na nyingi za sheria zilizotengenezwa na watu zilikuwa hazina ubinadamu. Alipokuwa karibu kuponya mtu mwenye mkono uliokauka, Yesu aliwauliza Mafarisayo waliokuwapo hivi: “Je, yaruhusika kisheria siku ya sabato kutenda kitendo chema?” Kushindwa kwao kujibu kulifunua kabisa kwamba walihisi lilikuwa jambo lisiloruhusika kisheria, kukifanya Yesu ahisi “akiwa ametiwa kihoro kabisa kwa ukosefu-hisia wa mioyo yao.” (Marko 3:1-6) Mafarisayo wangemsaidia mnyama wa kufugwa (kitega uchumi kifedha) aliyeachwa au aliyejeruhiwa katika siku ya Sabato lakini hawangemsaidia kamwe mwanamume au mwanamke—isipokuwa liwe ni jambo la kufa na kupona. Kwa kweli, walishikilia sana sheria za kibinadamu na mambo madogo-madogo ya kisheria hivi kwamba kama mchwa wanaokimbia haraka juu ya mchoro, walishindwa kuona picha yote—kanuni za kimungu.—Mathayo 23:23, 24.
Hata hivyo, kwa kuthamini kwao kanuni za Biblia, hata wachanga waweza kumletea Yehova sifa, mioyo yao inapokuwa myeupe. Mwalimu wa Rebecca aliye na umri wa miaka 13, aliuliza darasa ni nani angecheza kamari. Walio wengi walisema hawangefanya hivyo. Lakini, hali za namna mbalimbali zilipotajwa, wote isipokuwa Rebecca walikubali kwamba wangecheza kamari katika njia moja au nyingine. Huyo mwalimu aliuliza Rebecca ikiwa angenunua tikiti ya bahati-nasibu yenye thamani ya hamusi moja ya dola ya Marekani kwa kusudi lifaalo. Rebecca alijibu kwa kusema la na kutoa sababu za Kimaandiko kuonyesha ni kwa nini kufanya hivyo kungekuwa namna fulani ya kucheza kamari. Ndipo mwalimu wake akaliambia darasa lote hivi: ‘Kwa maoni yangu, Rebecca ndiye peke yake hapa aliye na zile niitazo kikweli “kanuni.”’ Ndiyo, Rebecca angaliweza kujibu kwa usahili, “Jambo hilo ni kinyume cha dini yangu,” lakini alifikiria kwa kina zaidi kuliko hivyo; angeweza kujibu ni kwa nini kucheza kamari ni kosa na kwa nini alikataa kushiriki.
Vielelezo kama Abeli, Noa, Yosefu, na Yesu hutuonyesha jinsi tunufaikavyo kwa kutumia “uwezo wa kufikiri” na “nguvu [zetu] za kufikiri kuzuri” katika kumwabudu Mungu. (Mithali 2:11; Waroma 12:1) Wazee Wakristo hufanya vema kumwiga Yesu “[wachungapo] kundi la Mungu lililo katika utunzaji [wao].” (1 Petro 5:2) Kama vile Yesu alivyotoa kielelezo chema wakati mmoja, wapendao kanuni za kimungu ndio husitawi chini ya enzi kuu ya Yehova.—Isaya 65:14.