Ulimwenguni Lakini Si Sehemu Yake
“Kwa sababu nyinyi si sehemu ya ulimwengu, . . . ulimwengu huwachukia nyinyi.”—YOHANA 15:19.
1. Wakristo wana uhusiano gani na ulimwengu, hata hivyo ulimwengu huwaonaje?
USIKU wake wa mwisho akiwa na wanafunzi wake, Yesu aliwaambia hivi: “Nyinyi si sehemu ya ulimwengu.” Alikuwa akisema juu ya ulimwengu gani? Je, hakuwa amesema hivi pindi moja mapema: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akatoa Mwana mzaliwa-pekee wake, ili kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye asipate kuangamizwa bali awe na uhai udumuo milele”? (Yohana 3:16) Kwa wazi hao wanafunzi walikuwa sehemu ya ulimwengu huo kwa sababu ndio waliokuwa wa kwanza kudhihirisha imani katika Yesu ili wapate uhai udumuo milele. Kwa nini, basi, Yesu akasema sasa kwamba wanafunzi wake walikuwa wamejitenga na ulimwengu? Na kwa nini akasema hivi pia: “Kwa sababu nyinyi si sehemu ya ulimwengu, . . . kwa ajili ya hili ulimwengu huwachukia nyinyi”?—Yohana 15:19.
2, 3. (a) Wakristo walipaswa wasiwe sehemu ya “ulimwengu” gani? (b) Biblia husema nini juu ya “ulimwengu” ambao Wakristo si sehemu yake?
2 Jibu ni kwamba Biblia hutumia neno “ulimwengu” (Kigiriki, koʹsmos) katika njia tofauti-tofauti. Kama ilivyoelezwa katika makala iliyotangulia, nyakati nyingine katika Biblia “ulimwengu” hurejezea wanadamu kwa ujumla. Huo ndio ulimwengu ambao Mungu aliupenda na ambao Yesu alifia. Hata hivyo, kichapo The Oxford History of Christianity chataarifu hivi: “‘Ulimwengu’ pia ni neno katika matumizi ya Kikristo limaanishalo kitu fulani kilichotengwa na Mungu na chenye uhasama dhidi yake.” Hilo ni kweli namna gani? Mtungaji Mkatoliki Roland Minnerath, katika kitabu chake Les chrétiens et le monde (Wakristo na Ulimwengu), aeleza hivi: “Likichukuliwa katika maana hasi, hivyo ulimwengu huonekana kuwa . . . makao ambamo serikali zenye uhasama dhidi ya Mungu huendeleza utendaji wake na ambao kwa kupinga utawala wenye ushindi wa Kristo, hufanyiza milki ya adui chini ya uongozi wa Shetani.” “Ulimwengu” huo ni tungamo la jamii ya binadamu ambayo imetengwa na Mungu. Wakristo wa kweli si sehemu ya ulimwengu huo, nao ulimwengu huo huwachukia.
3 Kuelekea mwisho wa karne ya kwanza, Yohana alikuwa akifikiria ulimwengu huu alipoandika hivi: “Msiwe mkipenda ama ulimwengu ama vitu vilivyo katika ulimwengu. Ikiwa yeyote aupenda ulimwengu, kumpenda Baba hakumo katika yeye; kwa sababu kila kitu kilicho katika ulimwengu—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na wonyesho wa mtu wa kujivunia njia yake ya kutegemeza maisha—hakitokani na Baba, bali hutokana na ulimwengu.” (1 Yohana 2:15, 16) Pia aliandika hivi: “Sisi twajua twatokana na Mungu, lakini ulimwengu mzima unakaa katika nguvu ya mwovu.” (1 Yohana 5:19) Yesu mwenyewe alimwita Shetani “mtawala wa ulimwengu huu.”—Yohana 12:31; 16:11.
Ukuzi wa Serikali za Ulimwengu
4. Serikali za ulimwengu zilikujaje kuwapo?
4 Ulimwengu wa wanadamu uliopo sasa uliotengwa na Mungu ulianza kusitawi punde tu baada ya Furiko la siku ya Noa, wengi wa wazao wa Noa walipokoma kumwabudu Yehova Mungu. Siku za mapema, Nimrodi, mjenzi wa jiji na aliyekuwa “hodari kuwinda wanyama mbele za [“katika kupingana na,” NW] BWANA,” alikuwa mashuhuri. (Mwanzo 10:8-12) Miaka hiyo sehemu kubwa ya ulimwengu huo ilikuwa imepangwa katika falme ndogondogo za majiji, ambazo pindi kwa pindi ziliungana na kupigana vita. (Mwanzo 14:1-9) Baadhi ya falme za majiji zilipata kutawala nyingine na kuwa serikali za kimkoa. Hatimaye, baadhi ya serikali za kimkoa zilikua na kuwa serikali kubwa za ulimwengu.
5, 6. (a) Serikali saba za ulimwengu za historia ya Biblia ni zipi? (b) Serikali hizo za ulimwengu zinafananishwaje, na nguvu yake hutoka wapi?
5 Kufuatia kiolezo cha Nimrodi, watawala wa serikali za ulimwengu hawakumwabudu Yehova, jambo la hakika lililoonyeshwa katika matendo yao makatili ya jeuri. Katika Andiko serikali hizo za ulimwengu zinafananishwa na wanyama-mwitu, na kwa karne kadhaa, Biblia hutambulisha sita kati ya hizo ambazo zilikuwa na athari kubwa juu ya watu wa Yehova. Hizo zilikuwa, Misri, Ashuru, Babiloni, Umedi na Uajemi, Ugiriki, na Roma. Baada ya Roma, serikali ya saba ya ulimwengu ilitolewa unabii kuwa ingezuka. (Danieli 7:3-7; 8:3-7, 20, 21; Ufunuo 17:9, 10) Hiyo ilithibitika kuwa Serikali ya Ulimwengu ya Uingereza na Amerika, iliyofanyizwa na Milki ya Uingereza pamoja na rafiki yake Marekani, ambayo hatimaye iliipita Uingereza kwa nguvu. Milki ya Uingereza ilianza kusitawi baada ya sehemu ya mwisho ya Milki ya Roma kutoweka hatimaye.a
6 Katika kitabu cha Ufunuo, serikali saba za ulimwengu zilizoandamana zinafananishwa na vichwa vya hayawani-mwitu mwenye vichwa saba aibukaye kutoka katika bahari ya jamii ya binadamu isiyotulia. (Isaya 17:12, 13; 57:20, 21; Ufunuo 13:1) Ni nani humpa hayawani huyo anayetawala nguvu yake? Biblia yajibu hivi: “Joka kubwa li[li]mpa huyo hayawani nguvu yake na hicho kiti chake cha ufalme na mamlaka kubwa.” (Ufunuo 13:2) Hilo joka kubwa mno si mwingine ila Shetani Ibilisi.—Luka 4:5, 6; Ufunuo 12:9.
Utawala Unaokuja wa Ufalme wa Mungu
7. Wakristo hutumainia nini, na tumaini hilo huathirije uhusiano wao na serikali za ulimwengu?
7 Kwa karibu miaka 2,000, Wakristo wamesali hivi: “Acha ufalme wako uje. Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.” (Mathayo 6:10) Mashahidi wa Yehova wajua kwamba Ufalme wa Mungu pekee ndio uwezao kuleta amani halisi duniani. Kwa kuwa wao huchunguza kwa makini unabii wa Biblia, wanasadikishwa kwamba sala hii itajibiwa karibuni na kwamba punde tu, huo Ufalme utatwaa uongozi wa mambo ya dunia. (Danieli 2:44) Kushikamana kwao sana na Ufalme huo huwafanya wasiwemo katika mambo ya serikali za ulimwengu.
8. Serikali huitikiaje utawala wa Ufalme wa Mungu, kama ilivyotabiriwa katika Zaburi 2?
8 Mataifa fulani hudai kushikilia kanuni za kidini. Hata hivyo, kihalisi wao hupuuza uhakika wa kwamba Yehova ndiye Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote Mzima na kwamba amemtawaza Yesu kuwa Mfalme wa kimbingu mwenye mamlaka juu ya dunia. (Danieli 4:17; Ufunuo 11:15) Zaburi ya kiunabii yataarifu hivi: “Wafalme wa dunia wanajipanga, na wakuu wanafanya shauri pamoja, juu ya BWANA, na juu ya masihi wake, na tuvipasue vifungo vyao, na kuzitupia mbali nasi kamba zao.” (Zaburi 2:2, 3) Serikali hazikubali “vifungo” au “kamba” zozote ambazo zingewekea mipaka udhihirisho wao wa enzi kuu ya kitaifa. Kwa sababu hiyo, Yehova amwambia Yesu, Mfalme wake mteule: “Uniombe, nami nitakupa mataifa kuwa urithi wako, na miisho ya dunia kuwa milki yako. Utawaponda kwa fimbo ya chuma, na kuwavunja kama chombo cha mfinyanzi.” (Zaburi 2:8, 9) Hata hivyo, ulimwengu wa wanadamu aliofia Yesu ‘hautapondwa’ kikamili.—Yohana 3:17.
Kuepuka “Alama” ya “Hayawani”
9, 10. (a) Twaonywa dhidi ya nini katika kitabu cha Ufunuo? (b) Kuwa na ‘alama ya hayawani’ kwafananisha nini? (c) Watumishi wa Mungu hukubali alama zipi?
9 Ufunuo uliopokewa na mtume Yohana ulionya kwamba ulimwengu wa wanadamu ambao umetenganishwa na Mungu ungetoa madai zaidi na zaidi punde tu kabla ya mwisho wake, “[uki]washurutisha watu wote, walio wadogo na wakubwa, na matajiri na maskini, na walio huru na watumwa, ili wawape alama katika mkono wao wa kuume au juu ya kipaji cha uso wao, na ili mtu yeyote asiweze kununua au kuuza ila mtu aliye na alama.” (Ufunuo 13:16, 17) Hilo lamaanisha nini? Alama katika mkono wa kuume ni ishara ifaayo ya tegemezo lenye utendaji. Namna gani alama juu ya kipaji cha uso? Kichapo The Expositor’s Greek Testament chataarifu hivi: “Mtajo huo wa kitamathali sana, wadokeza zoea la kutia alama askari-jeshi na watumwa kwa kutumia chanjo au muhuri wenye kuonekana wazi . . . ; au, hata kwa njia iliyo bora zaidi, ladokeza ile desturi ya kidini ya kuvaa jina la mungu likiwa talasimu.” Wanadamu wengi huvaa alama hiyo kwa ufananisho kupitia kwa matendo na maneno yao, wakijitambulisha kuwa “watumwa” au “askari-jeshi” wa huyo “hayawani.” (Ufunuo 13:3, 4) Kwa habari ya wakati ujao wao, kamusi Theological Dictionary of the New Testament yasema hivi: “Adui wa Mungu hukubali [alama] ya hayawani, ile nambari ya kifumbo yenye jina lake, ipigwe muhuri juu ya vipaji vyao vya uso na katika mkono mmoja. Hilo huwapa fursa kubwa za kuendelea kiuchumi na kibiashara, lakini huwaleta chini ya ghadhabu ya Mungu na kuwatenga na ufalme wa mileani, Ufu. 13:16; 14:9; 20:4.”
10 Yahitaji moyo mkuu na uvumilivu zaidi na zaidi ili kukinza msongo wa kupokea “[hiyo] alama.” (Ufunuo 14:9-12) Hata hivyo, watumishi wa Mungu wana nguvu ya jinsi hiyo, na kwa sababu ya hiyo, mara nyingi huchukiwa na kudhuriwa. (Yohana 15:18-20; 17:14, 15) Badala ya kuwa na alama ya huyo hayawani, Isaya alisema kwamba wangeandika kwa ufananisho mkononi mwao, “Mimi ni wa Mwenyezi-Mungu [“Yehova,” NW].” (Isaya 44:5, Biblia Habari Njema) Isitoshe, kwa kuwa ‘wanaugua na kulia’ kwa sababu ya machukizo yafanywayo na dini ya uasi-imani, wao hupokea alama ya ufananisho juu ya vipaji vyao vya uso ikiwatambulisha kustahili kuepushwa hukumu za Yehova zitekelezwapo.—Ezekieli 9:1-7.
11. Ni nani ambaye hutoa ruhusa serikali za kibinadamu zitawale mpaka Ufalme wa Mungu uje kutwaa utawala wa dunia?
11 Mungu huruhusu serikali za kibinadamu zitawale hadi wakati wa Ufalme wa kimbingu wa Kristo kutwaa utawala wa dunia hii kikamili. Uvumilivu wa kimungu kuelekea serikali za kisiasa warejezewa na Profesa Oscar Cullmann katika kitabu chake The State in the New Testament. Aandika hivi: “Ile dhana tata ya serikali kuwa ‘ya muda’ ndiyo sababu ifanyayo mtazamo wa Wakristo wa kwanza kuelekea Serikali kuwa usiopatana, lakini badala yake waonekana kuwa wenye kupinga. Nakazia kwamba, waonekana kuwa hivyo. Twahitaji tu kutaja Waroma 13:1, ‘Acheni kila mtu ajitiishe kwa wenye mamlaka waliopo . . . ,’ pamoja na Ufunuo 13: Serikali ikiwa hayawani kutoka abiso.”
“Hayawani” na “Kaisari”
12. Mashahidi wa Yehova wana mtazamo gani wenye usawaziko kuelekea serikali za kibinadamu?
12 Lingekuwa kosa kukata kauli kwamba wanadamu wote katika mamlaka ya kiserikali ni vyombo vya Shetani. Wengi wamejithibitisha kuwa watu wenye kanuni, kama vile prokonso Sergio Paulo ambaye anafafanuliwa katika Biblia kuwa “mwanamume mwenye akili.” (Matendo 13:7) Watawala fulani wametetea kwa moyo mkuu haki za walio wachache, wakiongozwa na dhamiri zenye kupewa na Mungu hata ikiwa hawakumjua Yehova na makusudi yake. (Waroma 2:14, 15) Kumbuka kwamba, Biblia hutumia neno “ulimwengu” katika njia mbili zinazotofautiana: ulimwengu wa wanadamu, ambao Mungu hupenda na ambao twapaswa kuupenda, na ulimwengu wa jamii ya wanadamu ambayo imetengwa na Yehova, ambao Shetani ndiye mungu na ambao twapaswa kusimama kando nao. (Yohana 1:9, 10; 17:14; 2 Wakorintho 4:4; Yakobo 4:4) Hivyo, watumishi wa Yehova wana mtazamo wenye usawaziko kuelekea utawala wa kibinadamu. Sisi hatumo katika mambo ya kisiasa kwa kuwa twatumika tukiwa mabalozi au wajumbe wa Ufalme wa Mungu na maisha zetu zimewekwa wakfu kwa Mungu. (2 Wakorintho 5:20) Kwa upande ule mwingine, twajitiisha kwa kudhamiria chini ya wale walio mamlakani.
13. (a) Yehova huzionaje serikali za kibinadamu? (b) Ujitiisho wa Kikristo kwa serikali za kibinadamu ni wa kadiri gani?
13 Mfikio huu wenye usawaziko huonyesha maoni ya Yehova Mungu mwenyewe. Serikali za ulimwengu, au hata Serikali ndogo, zitumiapo vibaya mamlaka zilizo nayo, ziwaoneapo watu zinaotawala, au kuwanyanyasa wale wamwabuduo Mungu, bila shaka zastahili kufafanuliwa kiunabii kuwa mahayawani wakali. (Danieli 7:19-21; Ufunuo 11:7) Hata hivyo, serikali za kitaifa zitumikiapo kusudi la Mungu katika kudumisha sheria na utaratibu katika haki, yeye huziona kuwa ‘watumishi wa watu wote.’ (Waroma 13:6) Yehova hutarajia watu wake wastahi serikali za kibinadamu na kujitiisha kwazo, lakini ujitiisho wao una mipaka. Wanadamu watakapo mambo ambayo yamekatazwa na sheria ya Mungu kutoka kwa watumishi wa Mungu, au wawakatazapo kufanya mambo ambayo Mungu huwataka watumishi wake wafanye, watumishi hao hufuata msimamo uliotwaliwa na mitume, yaani: “Lazima sisi tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”—Matendo 5:29.
14. Ujitiisho wa Kikristo kwa serikali za kibinadamu waelezwaje na Yesu? na Paulo?
14 Yesu alisema kwamba wafuasi wake wangekuwa na wajibu kwa serikali na pia kwa Mungu alipotangaza hivi: “Basi, mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini mlipeni Mungu vitu vya Mungu.” (Mathayo 22:21) Akiwa chini ya upulizio mtume Paulo aliandika hivi: “Acheni kila nafsi iwe katika ujitiisho kwa mamlaka zilizo kubwa . . . Lakini ikiwa unafanya lililo baya, uwe katika hofu: kwa maana haichukui upanga bila kusudi; kwa maana hiyo ni mhudumu wa Mungu, mlipiza-kisasi ili kuonyesha hasira ya kisasi juu ya yeye anayezoea kufanya lililo baya. Kwa hiyo kuna sababu yenye kushurutisha nyinyi watu kuwa katika ujitiisho, si kwa sababu ya hasira hiyo ya kisasi tu, bali pia kwa sababu ya dhamiri yenu. Kwa maana hiyo ndiyo sababu mnalipa kodi pia.” (Waroma 13:1, 4-6) Tangu karne ya kwanza W.K. hadi leo, Wakristo wamelazimika kufikiria madai yenye kufanywa na Serikali. Wamehitaji kutambua ikiwa kujipatanisha na madai hayo kungeongoza kwenye kuridhiana ibada yao au ikiwa madai hayo yalikuwa halali nayo yalipasa kutimizwa kwa kudhamiria.
Raia Wenye Kudhamiria
15. Mashahidi wa Yehova humlipaje Kaisari kwa kudhamiria wawiwalo?
15 “Mamlaka zilizo kubwa” za kisiasa ni “mhudumu” wa Mungu zitimizapo fungu lake lenye kukubaliwa na Mungu, ambalo hutia ndani mamlaka ya “kupasisha adhabu juu ya watenda-maovu bali kusifu watenda-mema.” (1 Petro 2:13, 14) Watumishi wa Yehova humlipa Kaisari kwa kudhamiria yale ayadaiyo kihalali kwa njia ya kodi, nao huwa “watiifu kwa serikali na mamlaka zikiwa watawala, . . . tayari kwa ajili ya kila kazi njema,” kwa kadiri ambavyo dhamiri zao zilizozoezwa na Biblia zitawaruhusu. (Tito 3:1) “Kazi njema” hutia ndani kuwasaidia wengine, kama wakati msiba mkubwa utokeapo. Wengi wameshuhudia fadhili ionyeshwayo na Mashahidi wa Yehova kuelekea wanadamu wenzao katika hali hizo.—Wagalatia 6:10.
16. Mashahidi wa Yehova hufanyia serikali na wanadamu wenzao kazi gani njema kwa kudhamiria?
16 Mashahidi wa Yehova huwapenda wanadamu wenzao na huhisi kwamba kazi njema iliyo bora wawezayo kuwafanyia ni kuwasaidia wapate ujuzi sahihi juu ya kusudi la Mungu la kuleta “mbingu mpya na dunia mpya” zenye uadilifu. (2 Petro 3:13) Kwa kufundisha na kuzoea kufuata kanuni za juu za adili za Biblia, wao ni wenye manufaa kwa jamii ya kibinadamu, wakiwaokoa wengi dhidi ya ufasiki. Watumishi wa Yehova ni wenye kutii sheria na kustahi mawaziri wa serikali, maofisa, mahakimu, na wenye mamlaka ya majiji, wakiwapa heshima ‘watakao heshima.’ (Waroma 13:7) Wazazi Mashahidi hushirikiana kwa mteremo na walimu wa watoto wao na huwasaidia watoto wao wajifunze vema, ili baadaye waweze kujiruzuku na kutokuwa mzigo wenye kulemea jamii. (1 Wathesalonike 4:11, 12) Makutanikoni mwao, Mashahidi hupinga ubaguzi wa kijamii na tofauti za kitabaka, nao hutilia maanani sana kuimarisha maisha ya familia. (Matendo 10:34, 35; Wakolosai 3:18-21) Kwa hiyo, kwa matendo yao, wao huonyesha kwamba mashtaka ya kwamba wao hupinga familia au hawasaidii jumuiya si ya kweli. Hivyo, maneno haya ya mtume Petro huthibitika kuwa kweli: “Ndivyo mapenzi ya Mungu yalivyo, kwamba kwa kutenda mema mpate kufunga kinywa yale maongezi yasiyo na ujuzi ya watu wenye kukosa akili.”—1 Petro 2:15.
17. Wakristo waweza kuendeleaje “kutembea katika hekima kuelekea wale walio nje”?
17 Kwa hiyo ingawa wafuasi wa kweli wa Kristo “si sehemu ya ulimwengu,” wangali katika ulimwengu wa jamii ya kibinadamu na lazima waendelee “kutembea katika hekima kuelekea wale walio nje.” (Yohana 17:16; Wakolosai 4:5) Maadamu Yehova aruhusu mamlaka zilizo kubwa zitende zikiwa mhudumu wake, tutazionyesha heshima izifaayo. (Waroma 13:1-4) Huku tukidumisha kutokuwamo kwa habari ya siasa, twasali kuhusu “wafalme na wote wale walio katika cheo cha juu,” hasa hawa watakiwapo kufanya maamuzi yawezayo kuathiri uhuru wa ibada. Tutaendelea kufanya hilo “ili tupate kuendelea kuishi maisha yaliyo shwari na matulivu pamoja na ujitoaji-kimungu kamili na uchukuaji-mambo kwa uzito,” ili “watu wa namna zote waokolewe.”—1 Timotheo 2:1-4.
[Maelezo ya Chini]
a Ona kitabu Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!, sura ya 35, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
Maswali ya Kupitia
◻ Wakristo ni sehemu ya “ulimwengu” gani, lakini hawawezi kuwa sehemu ya “ulimwengu” gani?
◻ “Alama” ya “hayawani” katika mkono au juu ya kipaji cha uso wa mtu yafananisha nini, na ni alama zipi ambazo watumishi waaminifu wa Yehova wanazo?
◻ Wakristo wa kweli wana mtazamo gani wenye usawaziko kuelekea serikali za kibinadamu?
◻ Ni zipi baadhi ya njia ambazo Mashahidi wa Yehova huchangia hali njema ya jamii ya kibinadamu?
[Picha katika ukurasa wa 16]
Biblia hutambulisha serikali za kibinadamu kuwa mtumishi wa Mungu na vilevile kuwa hayawani-mwitu
[Picha katika ukurasa wa 17]
Kwa sababu ya kuwaonyesha wengine upendo wenye hangaiko, Mashahidi wa Yehova ni wenye manufaa kwa jumuiya zao