Nilimwona “Mnyonge” Akipata Kuwa “Taifa Hodari”
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA WILLIAM DINGMAN
Ulikuwa mwaka wa 1936; mahali palikuwa, Salemu, Oregon, Marekani. Nilikuwa nikihudhuria mkutano wa Mashahidi wa Yehova. Swali liliulizwa hivi: “Halaiki kubwa iko wapi?” (Ufunuo 7:9, King James Version) Ni mimi tu niliyekuwa mpya, hivyo wote wakanielekezea vidole na kusema, “Yupo pale!”
KWA kulinganishwa, katikati ya miaka ya 1930 kulikuwa na wachache miongoni mwa Mashahidi wa Yehova waliokuwa na tumaini la Biblia la kuishi milele katika Paradiso duniani. (Zaburi 37:29; Luka 23:43) Mambo yamebadilika kwa kutazamisha tangu wakati huo. Lakini acheni niwaambie juu ya matukio yaliyoongoza kwenye kuwako kwangu kwenye mkutano huo huko Salem, Oregon.
Baba yangu alikuwa mwandikishaji The Golden Age, jina la mapema zaidi la gazeti Amkeni! Nilipokuwa tineja, nilionea shangwe kulisoma, nikasadikishwa kwamba lilikuwa na kweli ya Biblia yenye maana. Kwa hiyo siku moja nikapeleka fomu ya kuagizia iliyokuwa nyuma ya Golden Age. Fomu hiyo ilitolea msomaji vijitabu 20, kitabu kimoja, na jina la kutaniko lililo karibu zaidi la Mashahidi wa Yehova. Nilipopokea hizo fasihi, nilienda kutoka nyumba hadi nyumba na kuangusha vijitabu vyote na hicho kitabu pia.
Wakati huo hakuna yeyote aliyekuwa amejifunza Biblia nami. Kwa kweli, sikuwa nimepata kamwe kuzungumza na mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Lakini sasa, nikiwa na anwani ya Jumba la Ufalme la karibu zaidi mikononi, niliendesha gari umbali upatao kilometa 40 hadi Salem, Oregon, ili kuhudhuria mkutano. Hapo ndipo nilipoteuliwa kuwa “halaiki kubwa,” nilipokuwa bado na umri wa miaka 18 tu.
Ijapokuwa sikuwa kwa vyovyote nimejitayarisha kwa ajili ya huduma, nilianza kuhubiri na Kutaniko la Salem. Nilitiwa moyo nitie ndani mambo matatu ya msingi katika kutoa kwangu ushahidi. Kwanza, kwamba Yehova ndiye Mungu; pili, kwamba Yesu Kristo ndiye Mfalme wake aliyewekwa; na tatu, kwamba Ufalme ndio tumaini la pekee kwa ulimwengu. Nilijaribu kushiriki ujumbe huo kwenye kila mlango.
Baada ya kushirikiana na Mashahidi wa Yehova huko Salem kwa miaka miwili, nilibatizwa Aprili 3, 1938. Marafiki huko Salem walipendezwa kuona kadhaa kati yetu wa “halaiki kubwa” tukibatizwa. Februari 1939, nikawa painia, au mhudumu wa wakati wote. Desemba mwaka huo, nilikubali mwaliko wa kuhamia Arizona, ambako kulikuwa na uhitaji mkubwa zaidi wa wapiga-mbiu wa Ufalme.
Kupainia Arizona
Kazi ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa mpya Arizona, na mara nyingi tulieleweka vibaya, kwa hiyo Marekani ilipoingia katika Vita ya Ulimwengu ya Pili, tulinyanyaswa sana. Kwa kielelezo, nilipokuwa nikitumikia huko Stafford, Arizona, mwaka wa 1942, kulikuwa na mazungumzo juu ya kufanyiwa ghasia na kikundi kimoja cha Wamormon. Mapainia wenzangu nami tulitukia kuishi karibu na nyumba ya askofu Mmormon aliyetustahi na kusema hivi: “Ikiwa wamishonari Wamormon wangekuwa watendaji kama Mashahidi, basi Kanisa la Mormon lingeongezeka.” Kwa hiyo kanisani aliongea kwa sauti kubwa na kusema hivi: “Nasikia kuna mazungumzo juu ya kufanya ghasia dhidi ya hao wavulana Mashahidi. Basi, naishi karibu na wavulana hao, na kukiwa na ufanyaji-ghasia, bunduki yangu ya marisau itakuwa imelengwa juu ya ua kati ya nyumba zetu. Bunduki hiyo ya marisau itatumiwa—lakini si dhidi ya hao Mashahidi. Itatumiwa dhidi ya wafanya-ghasia. Hivyo ikiwa mwataka kufanya ghasia, mwajua jambo la kutazamia.” Hicho kikundi cha wafanya-ghasia hakikuja kamwe.
Wakati wa miaka yangu mitatu katika Arizona, tulikamatwa na kutiwa jela mara kadhaa. Wakati mmoja nilitiwa jela kwa siku 30. Ili kupambana na usumbufu wa polisi katika huduma yetu, tulifanyiza tulichoita kikosi kirukacho. Shahidi aliyekisimamia alituambia hivi: “Kama vile jina letu lilivyo, ndivyo nasi tulivyo. Twaanza saa kumi na moja au kumi na mbili asubuhi, twaacha trakti au kijitabu kwenye kila mlango, na kisha twaruka.” “Kikosi [chetu] kirukacho” kilihubiri sehemu kubwa ya jimbo la Arizona. Hata hivyo, kilivunjwa hatimaye kwa sababu njia hiyo ya kuhubiri haikuturuhusu kuwaandalia msaada waliopendezwa.
Shule ya Gileadi na Utumishi wa Pekee
Desemba 1942, nilikuwa miongoni mwa mapainia kadhaa Arizona waliopokea barua ya kutualika kwenda shule mpya ya mishonari iliyokuwa ikianzishwa na Mashahidi wa Yehova. Mwanzoni hiyo shule iliitwa Chuo cha Biblia cha Gileadi cha Watchtower. Baadaye hilo jina lilibadilishwa kuwa Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower. Eneo la chuo hicho lilikuwa umbali wa karibu kilometa 4,800 karibu na jiji la Ithaca katika sehemu ya juu ya jimbo la New York.
Baada ya kuzuru Oregon kwa muda mfupi, kadhaa kati yetu mapainia tuliacha joto la Jangwa la Arizona ndani ya basi ya kampuni ya Greyhound, Januari 1943. Siku kadhaa baadaye tulifika mwisho wa safari yetu na kupata theluji ya majira ya baridi kali ya sehemu ya juu ya New York. Shule ilifunguliwa Februari 1, 1943, Nathan H. Knorr, msimamizi wa hiyo shule, aliposema hivi katika hotuba yake ya kuzindua kwa wanafunzi mia moja: “SI kusudi la chuo hiki kuwaandalia vifaa kuwa wahudumu walioagizwa rasmi. Nyinyi ni wahudumu tayari, na mmekuwa watendaji katika huduma kwa miaka kadhaa. . . . Mtaala huu wa kujifunza kwenye hiki chuo ni kwa kusudi la pekee la kuwatayarisha kuwa wahudumu wenye sifa ya kustahili zaidi katika maeneo ambayo mwaenda.”
Mwanzoni nilijihisi kuwa nisiyefaa kuwa Gileadi, kwa kuwa nilikuwa na elimu ndogo ya kilimwengu. Lakini wafunzi walikuwa wenye uelewevu sana kunielekea, nami nilikuja kuonea shangwe sana mafunzo yangu. Darasa letu lilihitimu baada ya miezi mitano ya mazoezi makali sana. Baadaye, wachache kati yetu walitumwa kwenda Brooklyn, New York, makao makuu ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova, tulikopokea mazoezi zaidi ili kututayarisha kutumikia katika kazi ya kusafiri tukiwa waangalizi wa mzunguko. Mgawo wangu wa kwanza ulikuwa Carolina Kaskazini na Kusini.
Siku hizo za mapema, mwangalizi wa mzunguko alikuwa mwendoni karibu sikuzote. Tungekaa siku moja na kutaniko ndogo au siku mbili ikiwa lilikuwa kubwa. Wakati huo makutaniko yaliyo mengi zaidi yalikuwa madogo. Hivyo baada ya kutumia siku nzima, na mara nyingi tukifuliza kukaa hadi karibu usiku wa manane tukizuru na kujibu maswali, niliamka karibu saa kumi na moja siku iliyofuata ili kusafiri kwenda kutaniko lililofuata. Nilitumikia katika kazi ya kuzunguka kwa karibu mwaka mmoja, na baadaye nikapainia kwa muda fulani Tennessee na New York.
Kwenda Kuba Kisha Puerto Riko
Mei 1945, nikiwa pamoja na wengine kadhaa, nilitumwa kwenda Kuba, mgawo wangu wa kwanza wa umishonari katika nchi ya kigeni! Tulienda kufanya kazi ya magazeti usiku tuliowasili Havana, mji mkuu wa Kuba. Tulikaa Havana hadi tulipoweza kupata makao Santa Clara. Rudishio letu la fedha la kila mwezi lilikuwa dola 25 tu kwa kila mmoja kwa ajili ya mahitaji yote, kutia na chakula na kodi ya nyumba. Tulitengeneza vitanda na fanicha kutokana na vifaa vilivyopatikana na kutumia masanduku ya matofaa kuwa almari yetu.
Mwaka uliofuata nilipewa mgawo wa kazi ya kuzunguka. Wakati huo Kuba yote ilikuwa mzunguko mmoja. Kwa sababu mwangalizi wa mzunguko aliyenitangulia alikuwa na miguu mirefu na alipenda kutembea, iliwabidi akina ndugu na dada wakimbie ili kutembea pamoja naye. Yaonekana kwamba walifikiri ningekuwa vivyo hivyo, kwa hiyo walipanga kila kitu kwa ajili ya ziara yangu. Wote hawakwenda katika huduma siku hiyohiyo lakini walijigawanya katika vikundi na kuhubiri kwa zamu pamoja nami. Siku ya kwanza kikundi kimoja kilinipeleka eneo la mbali; siku iliyofuata kikundi kingine kikanipeleka eneo jingine la mbali, na kadhalika. Nilikuwa nimechoka mwishoni mwa hiyo ziara, lakini nilikuwa nimeionea shangwe. Nina kumbukumbu nizipendazo za kutaniko hilo.
Kufikia mwaka wa 1950 tulikuwa na wahubiri wa Ufalme zaidi ya 7,000 Kuba, karibu idadi ileile ambayo Mexico ilikuwa nayo. Julai mwaka huo, nilihudhuria Ongezeko la Theokrasi mkusanyiko wa kimataifa Yankee Stadium katika New York City. Baadaye, nilipokea mgawo mpya wa umishonari, kwenda Puerto Riko. Miongoni mwa wamishonari wapya kutoka darasa la 12 la Gileadi walikuwa Estelle na Thelma Weakley, walioandamana nami kwenye safari ya ndege hadi Puerto Riko.
Miaka minane baadaye Estelle nami tulioana katika sherehe sahili huko Bayamón, Puerto Riko, sherehe iliyofanyiwa juu ya jukwaa wakati wa kipindi cha mapumziko cha kusanyiko la mzunguko letu. Kabla na baada ya ndoa yetu, nilitumika katika kazi ya kuzunguka. Wakati wa miaka yetu zaidi ya kumi Puerto Riko, Estelle nami tuliona ongezeko kubwa—kutoka wahubiri chini ya 500 hadi zaidi ya 2,000. Tuliweza kusaidia wengi kufikia hatua ya kujiweka wakfu na kubatizwa, nasi tulishiriki katika kuanzisha makutaniko kadhaa mapya.
Desemba 1960, Milton Henschel kutoka makao makuu ya Mashahidi wa Yehova yaliyo Brooklyn, New York, alizuru Puerto Riko na kuzungumza na wamishonari. Aliuliza ikiwa baadhi yao wangejitolea kwa ajili ya mgawo tofauti. Estelle nami tulikuwa miongoni mwa waliojitolea.
Makao Yetu Katika Jamhuri ya Dominika
Mgawo wetu mpya ulikuwa Jamhuri ya Dominika, na tuliweka Juni 1, 1961, kuwa tarehe yetu ya kuhama. Mei 30 dikteta wa Dominika Rafael Trujillo, aliuawa, na safari za ndege kuingia nchini zikafutwa. Ingawa hivyo, safari za ndege zilianzishwa tena upesi, na tuliweza kusafiri kwa ndege hadi Jamhuri ya Dominika Juni 1 kama tulivyopanga.
Hiyo nchi ilikuwa katika hali ya machafuko tulipofika, na kulikuwa na utendaji mwingi wa kijeshi. Kulikuwa na kuhofia mapinduzi, na askari-jeshi walikuwa wakichunguza kila mtu katika barabara kuu. Tulisimamishwa kwenye vituo kadhaa vya ukaguzi wa magari, na katika kila kimoja mizigo yetu ya safari ikachunguzwa. Kila kitu kilitolewa kutoka kwenye masanduku yetu, hata vitu vidogo zaidi. Huo ndio uliokuwa mwanzo wetu katika Jamhuri ya Dominika.
Tulikaa jiji kuu, Santo Domingo, kwa majuma kadhaa kabla ya kwenda katika mgawo wetu wa kwanza katika La Romana. Wakati wa udikteta wa Trujillo, watu wote walikuwa wameambiwa kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa Wakomunisti na walikuwa aina mbaya zaidi ya watu. Tokeo ni kwamba, Mashahidi walikuwa wamenyanyaswa vibaya. Ingawa hivyo, tuliweza kuvunja ubaguzi hatua kwa hatua.
Baada ya kuhubiri La Romana kwa wakati mfupi, tulianza kutumikia katika kazi ya kuzunguka kwa mara nyingine. Kisha, mwaka wa 1964, tulipewa mgawo wa kwenda jiji la Santiago tukiwa wamishonari. Mwaka uliofuata Jamhuri ya Dominika ilipatwa na mapinduzi, na kwa mara nyingine hiyo nchi ikawa katika hali ya mchafuko. Wakati wa mapambano hayo tulihamishwa hadi San Francisco de Macorís, jiji lililojulikana kwa vitendo vyake vya kisiasa. Hata hivyo, tulihubiri kwa uhuru bila kuingiliwa. Hata tulifanyiza kutaniko jipya ijapokuwako hali isiyo tulivu kisiasa. Katika miaka iliyofuata, tulipata mabadiliko zaidi ya mgawo wetu kabla ya kupewa mgawo tena kuja kwenye makao yetu ya sasa Santiago.
Hakika tumeona baraka za Yehova juu ya kazi hapa katika Jamhuri ya Dominika. Tulipowasili mwaka wa 1961, kulikuwa na Mashahidi wapatao 600 na makutaniko 20. Sasa kuna wahubiri karibu 20,000 wanaohubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu katika makutaniko zaidi ya 300. Matazamio ya ukuzi zaidi ni makubwa, kama ithibitishwavyo na hudhurio la watu 69,908 kwenye Ukumbusho wa kifo cha Kristo mwaka wa 1996. Idadi hiyo ni karibu mara tatu na nusu ya idadi ya wahubiri!
Taifa Hodari Sasa
Hata ingawa mandhari ya ulimwengu huendelea kubadilika, ujumbe wa Biblia ambao Mashahidi wa Yehova huhubiri hubaki vilevile. (1 Wakorintho 7:31) Yehova bado ndiye Mungu, Kristo bado ndiye Mfalme, na kwa wazi zaidi ya wakati mwingine wowote Ufalme ndio tumaini pekee la ulimwengu.
Wakati uleule, badiliko la kustaajabisha limetukia miongoni mwa watu wa Yehova tangu nilipohudhuria mkutano huo huko Salem, Oregon, miaka ipatayo 60 iliyopita. Kwa kweli, halaiki kubwa, au umati mkubwa, umekuwa mkubwa, hesabu yao ikiwa zaidi ya milioni tano. Ni kama tu vile Yehova alivyotabiri juu ya watu wake: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa hodari; mimi, BWANA, nitayatimiza hayo wakati wake.”—Isaya 60:22.
Baada ya karibu miaka 60 katika utumishi wa wakati wote, nafurahi kuwa na shangwe ya kuendelea kuhubiri na kufundisha katika mgawo wangu wa umishonari. Ni pendeleo kubwa kama nini kuwa na fungu katika kazi hiyo na kuwa nimeona “mnyonge” akipata kuwa “taifa hodari”!
[Picha katika ukurasa wa 21]
Nikiwa na mke wangu, katika Jamhuri ya Dominika