Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w98 1/1 kur. 3-5
  • Kweli Hugeuza Maisha

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kweli Hugeuza Maisha
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kusudi Maishani
  • Familia Mpya
  • “Nilipambana Kama Simba”
    2015 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Kupata Faraja Baada ya Kukosa Tumaini Ujanani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Yehova Amwahidi Danieli Thawabu ya Ajabu
    Sikiliza Unabii wa Danieli!
  • “Mimi Ni Macho Yake Naye Hutumika Kama Miguu Yangu”
    Amkeni!—1992
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
w98 1/1 kur. 3-5

Kweli Hugeuza Maisha

YASIKITISHA lakini ni kweli kwamba maisha ya watu wengi leo ni magumu, hata yenye kukatisha tumaini. Je, yawezekana watu hao wapate furaha? Baadhi yao ni wahalifu na huvizia jirani zao. Je, wao waweza kamwe kuwa washiriki wa jamii wenye kufuatia haki? Jibu la maswali yote mawili ni ndiyo. Watu waweza kubadilika. Maisha zaweza kugeuzwa. Mtume Paulo alionyesha jinsi liwezekanavyo alipoandika hivi: “Mgeuzwe umbo kwa kufanya upya akili yenu, ili mpate kujithibitishia wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.”—Waroma 12:2.

Kutajwa kwa ‘mapenzi ya Mungu yaliyo makamilifu’ kwaweza kukumbusha jambo ambalo Yesu aliwaambia wanafunzi wake zaidi ya miaka 20 kabla Paulo hajaandika maneno yaliyo juu. Yesu alisema hivi: “Mtajua kweli, na kweli itawaweka nyinyi huru.” (Yohana 8:32) Alipotaja “kweli,” Yesu alimaanisha habari iliyopuliziwa kimungu—hasa habari kuhusu mapenzi ya Mungu— ambayo imehifadhiwa kwa ajili yetu katika Biblia. (Yohana 17:17) Je, kwa kweli, kweli ya Biblia huwaweka watu huru? Je, kwa kweli kuishi kupatana na mapenzi ya Mungu hugeuza maisha? Kwa kweli hufanya hivyo. Fikiria vielelezo vichache.

Kusudi Maishani

Muda mfupi uliopita, Moisés, katika Gibraltar, alikuwa mwanamume asiye na furaha hata kidogo. Asema hivi: “Nilikuwa mlevi na nililala barabarani. Nilihisi nimepotea. Kila usiku nilimwomba Mungu anihurumie na asiniwezeshe kuvumilia siku nyingine. Nilitoa machozi huku nikimwuliza Mungu kwa nini nilikuwa katika ulimwengu huu ikiwa nilikuwa kinyangarika, nisiye na kazi, bila familia, na bila mtu yeyote wa kunisaidia. Mbona niendelee kuishi?” Kisha, kitu fulani kikatokea.

Moisés aendelea kusema hivi: “Nilijua kwamba Mungu alikuwa amesikia sala yangu nilipokutana na Roberto, mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Roberto alinipa Biblia na nakala ya broshua Mungu Anataka Tufanye Nini?a ambayo ni msaada wa kujifunzia Biblia. Kila siku tulijifunza Biblia pamoja katika benchi niliyolalia usiku. Baada ya mwezi mmoja Roberto alinipeleka katika Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova la mahali hapo. Punde si punde, kweli ya Biblia ikawa imebadili kabisa mtazamo wangu. Silali nje tena kamwe; wala sinywi pombe au kuvuta sigareti. Maisha yangu yamebadilika, nami nina furaha. Natumaini kubatizwa karibuni na kumtumikia Yehova nikiwa mmoja wa Mashahidi wake.”

Mgeuzo ulioje! Watu wakosapo tumaini, mara nyingi sababu huwa ni kukosa ujuzi. Hawajui juu ya Mungu na makusudi yake ya ajabu. Katika kisa cha Moisés, alipopata ujuzi huo, ulimpa nguvu na moyo mkuu wa kugeuza kabisa maisha yake. Sala ya mtunga-zaburi kwa Mungu ilijibiwa katika kisa cha Moisés: “Niletewe nuru yako na kweli yako ziniongoze, zinifikishe kwenye mlima wako mtakatifu na hata maskani yako.”—Zaburi 43:3.

Katika Belize, Daniel alijionea jambo lifananalo na hilo. Daniel hakuwa akilala barabarani—alikuwa na kazi yenye fahari. Lakini kwa miaka 20 alishindana na uraibu wa dawa za kulevya na alkoholi na aliishi maisha yasiyo ya adili. Ingawa alilelewa akiwa Mkatoliki, Daniel hangeweza kuona maana yoyote maishani, naye alishuku kuwako kwa Mungu. Alikwenda makanisa tofauti-tofauti akitafuta msaada lakini alikuta kwamba wengi wa marafiki wake wenye kwenda kanisani na hata baadhi ya marafiki wake makasisi walitumia vibaya dawa za kulevya na alkoholi. Wakati huohuo, mke wake alikuwa karibu kumtaliki.

Kwa kukata tamaa Daniel alijiandikisha katika kituo cha kurekebisha tabia. Bado, alijua kwamba baada ya kuachiliwa kwake, angerudia dawa za kulevya ikiwa hangepokea msaada. Lakini msaada wa aina gani? Mei 1996, siku mbili baada ya kuondoka katika kituo cha kurekebisha tabia, Daniel alimfikia mmoja wa Mashahidi wa Yehova na kumshangaza kwa lile ombi, “Tafadhali jifunze Biblia nami.” Huyo Shahidi alipanga kujifunza Biblia na Daniel mara mbili kila juma, na upesi Daniel akaanza kupatanisha maisha yake na mapenzi ya Mungu na marafiki Wakristo ambao hawakutumia dawa za kulevya au alkoholi isivyofaa na ambao waliepuka kabisa ukosefu wa adili, walichukua mahali pa marafiki wake wa zamani. Hivyo Daniel aligundua kwamba maneno ambayo Biblia husema ni ya kweli: “Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima; bali rafiki wa wapumbavu ataumia.” (Mithali 13:20) Upesi, akasema hivi: “Hii ndiyo mara ya kwanza maishani mwangu ambayo nimepata kujua maana ya kuwa na dhamiri safi.” Maisha ya Daniel pia yaligeuzwa.

Katika Puerto Riko, mwanamume mwingine alipata mgeuzo wenye kutokeza. Alikuwa gerezani naye alionwa kuwa hatari sana, kwa kuwa alikuwa ameua watu kadhaa. Je, kweli ya Biblia ingeweza kumbadili? Ndiyo. Mmoja wa Mashahidi wa Yehova aliweza kumpa nakala kadhaa za gazeti la Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, naye akaomba mengine upesi. Funzo la Biblia lilianzishwa naye, na kweli ya Biblia ikaanza kuathiri moyo wake, mabadiliko aliyofanya yalionekana na wote. Mojawapo ya uthibitisho mbalimbali wa kwanza ulikuwa kwamba alikata nywele zake ndefu na kunyoa ndevu zake zilizotapakaa.

Biblia husema kwamba Mungu huwasamehe watenda-dhambi ambao hutubu kikweli na kubadili mtindo-maisha wao. Paulo aliandika hivi: “Je, hamjui kwamba watu wasio waadilifu hawatarithi ufalme wa Mungu? . . . Na hata hivyo baadhi yenu ndivyo mlivyokuwa. Lakini mmeoshwa mkawa safi.” (1 Wakorintho 6:9, 11) Bila shaka, maneno hayo yalimfariji mwanamume huyo, kama vile maneno ya Matendo 24:15: “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” Alisema hivi: “Nataka kuwa huko wakati ambapo ufufuo wa wafu utatukia ili niweze kuwaomba msamaha wale wote nilioua.”

Familia Mpya

Siku moja Luis, mweneza-evanjeli wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova katika Argentina, alijulishwa kwa mwanamume mchanga aliyekuwa na historia yenye kusikitisha. Akiwa ameachwa na wazazi wake alipozaliwa, alilelewa katika mashirika mbalimbali. Alipokuwa na umri wa miaka 20 hivi, alipata kujua alikokuwa mama yake, akaamua kuishi ujiranini. Alifanya kazi kwa bidii, akahifadhi fedha nyingi, na kusafiri kwenda jiji alikokuwa mama yake. Mama yake alimruhusu akae naye hadi fedha zake zilipoisha kisha akamtaka aondoke. Kukataliwa huko kulimfanya atake kujiua.

Hata hivyo, Luis aliweza kushiriki kweli ya Biblia na mwanamume huyo mchanga. Kweli hiyo yatia ndani ule uhakikishio: “Baba yangu na mama yangu wameniacha, bali BWANA atanikaribisha kwake.” (Zaburi 27:10) Mwanamume huyo mchanga alipata kujua kwamba alikuwa na Baba wa kimbingu ambaye hangeweza kumwacha kamwe. Sasa yu mwenye furaha kuwa sehemu ya familia mpya, familia ya Yehova.

Mwanamume mwingine katika nchi hiyohiyo alimwambia mmojawapo wa Mashahidi wa Yehova kwamba alipenda gazeti la Mnara wa Mlinzi. Kwa nini? Kwa sababu liliokoa ndoa yake. Yaonekana kwamba siku moja mwanamume huyo, alipokuwa akitoka kazini, aliona kwenye kapu la taka gazeti la Mnara wa Mlinzi lenye kichwa “Talaka” katika herufi kubwa. Kwa kuwa ndoa yake ilikuwa matatani naye na mke wake walikuwa wameanza harakati za kutengana kisheria, alichukua hilo gazeti na kuanza kulisoma. Alilipeleka nyumbani na kulisoma pamoja na mke wake. Wenzi hao walijaribu kutumia shauri lenye kutegemea Biblia katika hilo gazeti. (Waefeso 5:21–6:4) Punde si punde, uhusiano wao ukaboreka. Waliacha zile harakati za kutengana nao sasa wanajifunza Biblia wakiwa wenzi waliooana wenye muungano.

Katika Uruguay, mwanamume mwingine, aitwaye Luis hakuwa mwenye furaha hata kidogo. Uraibu wa dawa za kulevya, uwasiliani-roho, ibada ya sanamu, matumizi mabaya ya alkoholi—hayo yalikuwa baadhi ya mambo yaliyofanya maisha yake yachafuke. Hatimaye, Luis, akiwa amevunjwa moyo kabisa, akawa mwatheisti. Rafiki akampa kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation?b Hilo lilitokeza kuwasiliana kifupi na Mashahidi wa Yehova, lakini upesi Luis akarudia alkoholi na dawa za kulevya. Wakati ambapo, akiwa katika kipindi cha maumivu mengi makali, alijikuta akiketi katika shimo lililojaa takataka, alisali, akitoa sala yake kwa “baba ya Yesu Kristo,” kwa kuwa hakuwa na uhakika juu ya jina la Mungu.

Alimwomba Mungu amwonyeshe ikiwa kulikuwa na sababu ya kuwa kwake ulimwenguni. “Siku iliyofuata,” aripoti Luis, “mjuani alinipa kitabu ambacho hakukihitaji tena. Kichwa cha kitabu hicho kilikuwa nini? Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!”c Hicho kitabu kilimsaidia kujibu swali lake. Luis alisali tena ili apate msaada katika kupata dini ambayo ingemwonyesha jinsi ya kumtumikia Mungu. Mshangao ulioje! Kengele ya mlango ikalia, na Mashahidi wa Yehova wawili walikuwa wamesimama nje. Mara moja Luis akaanza kujifunza Biblia nao. Alifanya maendeleo ya haraka naye sasa ahisi kuwa amebarikiwa kuwa Shahidi aliyebatizwa. Anaishi maisha safi naye huwasaidia wengine pia kupata kusudi maishani mwao. Kwake yeye, maneno ya Zaburi 65:2 yametimia: “Wewe usikiaye kuomba, wote wenye mwili watakujia.”

Katika Filipino, Allan alikuwa mwanafunzi mhamasishaji mtendaji. Alikuwa mshiriki wa shirika ambalo kusudi lake lilikuwa “kupindua serikali ili vizazi vya wakati ujao viweze kuonea shangwe usawa.” Ingawa hivyo, siku moja alifikiwa na Mashahidi wa Yehova na kupata kujua kutoka katika Biblia kusudi la Mungu kwa ajili ya wanadamu. Kusudi hilo latia ndani ahadi hii iliyopuliziwa: “Bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo . . . Bali wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.” (Zaburi 37:10, 11) Allan alisema hivi: “Upesi niligundua kwamba kile ambacho harakati yetu ilikuwa ikipigania kilitabiriwa zamani za kale katika Biblia. Mambo yote tuliyotamani kwa shauku sana yatatolewa chini ya Ufalme wa Mungu.” Sasa Allan autegemeza Ufalme wa Mungu na husaidia wengine wawe na imani katika kweli ya Biblia.

Ndiyo, maisha yanageuzwa watu watiipo kweli ya Neno la Mungu, Biblia. Kwa kweli, wakati waja ambapo jamii ya kibinadamu yote iliyo hai itakuwa imepatanisha maisha yake na mapenzi ya Mungu. Huo utakuwa mgeuzo ulioje! Ndipo, unabii huu utakapotimizwa: “Hawatadhuru wala hawataharibu katika mlima wangu wote mtakatifu; maana dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.”—Isaya 11:9.

[Maelezo ya Chini]

a Iliyochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

b Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

c Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki