‘Fadhili-Upendo Zako ni Njema Kuliko Uhai’
Kama ilivyosimuliwa na Calvin H. Holmes
Ilikuwa Desemba 1930, na nilikuwa tu nimemaliza kukamua ng’ombe Baba alipokuja nyumbani kutoka kumzuru jirani wa karibu. “Hiki ni kitabu alichoniazima Wyman,” akasema huku akitoa mfukoni mwake kichapo cha bluu. Kilikuwa na kichwa Deliverance, kilichochapishwa na Watch Tower Bible and Tract Society. Baba, ambaye ilikuwa nadra kwake kusoma kitu chochote, alisoma kitabu hicho hadi usiku sana.
BAADAYE, Baba aliazima vitabu vingine, vyenye vichwa kama vile Light na Reconciliation, vilivyochapishwa na wachapishaji walewale. Alipata Biblia ya Mama ya zamani na kukaa hadi usiku sana ili kuvisoma kwa mwangaza wa taa ya mafuta. Badiliko kubwa lilimpata Baba. Katika majira ya baridi kali ya mwaka huo alizungumza kwa muda wa saa nyingi nasi—mamangu, dada zangu watatu, nami—huku tukisongamana kulizunguka jiko letu la zamani lenye kuwaka moto wa kuni.
Baba alisema kwamba waliokuwa wakichapisha vitabu hivyo waliitwa Wanafunzi wa Biblia na kwamba, kulingana nao, tulikuwa tukiishi katika “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1-5) Alieleza kwamba dunia haingeharibiwa kwenye mwisho wa ulimwengu bali chini ya Ufalme wa Mungu ingegeuzwa kuwa paradiso. (2 Petro 3:5-7, 13; Ufunuo 21:3, 4) Jambo hilo kwa kweli lilisikika kwangu kuwa lenye kupendeza.
Baba alianza kuzungumza nami tulipofanya kazi pamoja. Nakumbuka kwamba tulikuwa tukiambua mahindi alipoeleza kwamba jina la Mungu ni Yehova. (Zaburi 83:18) Hivyo, katika masika ya 1931, nilipokuwa na umri wa miaka 14 tu, nilichukua msimamo wangu kwa ajili ya Yehova na Ufalme wake. Nilisali kwa Yehova katika shamba la zamani la matofaa lililokuwa nyuma ya nyumba na kuahidi rasmi kwamba ningemtumikia milele. Moyo wangu ulikuwa tayari umevutwa na fadhili-upendo za Mungu wetu wa ajabu.—Zaburi 63:3.
Tuliishi katika shamba lililokuwa karibu kilometa 30 kutoka St. Joseph, Missouri, Marekani, na kilometa zilizopungua 65 kutoka Jiji la Kansas. Baba alizaliwa katika kibanda cha magogo ambacho baba mzazi wa babu yangu alikuwa amekijenga katika hilo shamba mapema katika karne ya 19.
Mazoezi kwa Ajili ya Huduma
Katika kiangazi cha 1931, familia yetu ilisikia katika redio hotuba ya watu wote “Ufalme, Tumaini la Ulimwengu,” ambayo Joseph Rutherford, aliyekuwa msimamizi wa Watch Tower Society wakati huo, alitoa kwenye mkusanyiko katika Columbus, Ohio. Ilichochea moyo wangu, nami niliterema kushiriki na Baba katika kugawanya miongoni mwa wajuani wetu kijitabu kilichokuwa na hotuba hiyo ya maana ya watu wote.
Katika masika ya 1932, nilihudhuria mkutano wangu wa kwanza wa Mashahidi wa Yehova. Jirani yetu alimwalika Baba nami ili kusikia hotuba katika St. Joseph iliyotolewa na George Draper, mwangalizi asafiriye wa Mashahidi wa Yehova. Tulipowasili, mkutano ulikuwa katikati, na nilipata mahali pa kuketi nyuma ya mgongo imara na mpana wa J. D. Dreyer, ambaye angetimiza fungu la maana maishani mwangu.
Septemba 1933, nilihudhuria kusanyiko nikiwa na Babangu katika Jiji la Kansas, ambako kwa mara ya kwanza nilishiriki katika kuhubiri hadharani. Baba alinipa vijitabu vitatu na kuniagiza niseme hivi: “Mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova ninayehubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu. Hapana shaka umemsikia Jaji Rutherford katika redio. Hotuba zake husambazwa na vituo zaidi ya 300 kila juma.” Kisha nilitoa kijitabu. Jioni hiyo, nilipokuwa nikikamua ng’ombe huko shambani, niliona kwamba hiyo ilikuwa siku ya kukumbukwa zaidi maishani mwangu.
Punde si punde majira ya baridi kali yalianza, na tulisafiri mara chache. Lakini wakati huo Ndugu Dreyer na mkewe walituzuru na kuniuliza ikiwa ningependa kwenda nyumbani kwao Jumamosi jioni na kukaa usiku kucha. Kule kutembea kilometa 10 hadi nyumbani kwa Dreyer kulistahili jitihada niliyofanya kwa sababu niliweza kuandamana nao katika huduma siku iliyofuata na kuhudhuria Funzo la Mnara wa Mlinzi katika St. Joseph. Tangu wakati huo, nimekosa mara chache kushiriki katika huduma kila Jumapili. Mazoezi na shauri la Ndugu Dreyer lilithibitika kuwa lenye thamani sana.
Mwishowe, katika Septemba 2, 1935, niliweza kufananisha wakfu wangu kwa Yehova kwa ubatizo wa maji kwenye kusanyiko katika Jiji la Kansas.
Kuanza kwa Kazi-Maisha
Mapema mwaka wa 1936, nilipeleka ombi ili kutumikia nikiwa painia, au mhudumu wa wakati wote, na niliwekwa katika orodha ya wale waliokuwa wakitafuta painia-mwenzi. Upesi baada ya hapo nilipokea barua kutoka kwa Edward Stead wa Arvada, Wyoming. Alieleza kwamba alitumia kiti chenye magurudumu na alihitaji msaada ili apainie. Nilikubali toleo lake mara moja, nikawekwa rasmi kuwa painia katika Aprili 18, 1936.
Kabla ya kuondoka ili kujiunga na Ndugu Stead, mamangu alisema nami nikiwa peke yangu. “Mwanangu, je, una hakika hilo ndilo utakalo kufanya?” akauliza.
“Maisha hayangekuwa na maana yoyote nikifanya jambo tofauti,” nikajibu. Nilikuwa nimepata kufahamu kwamba fadhili-upendo za Yehova ni za maana zaidi kuliko kitu kingine chochote.
Kupainia pamoja na Ted, kama tulivyomwita Ndugu Stead, kulikuwa mazoezi bora kabisa. Alijawa na bidii na alikuwa na njia yenye kuvutia sana ya kutoa ujumbe wa Ufalme. Lakini kile tu ambacho Ted angeweza kufanya ni kuandika na kuzungumza; viungo vyake vyote vilikuwa vimekwamishwa na yabisi-kavu. Nilikuwa nikiamka mapema na kumwosha na kumnyoa, kutayarisha kifungua-kinywa, na kumlisha. Kisha nilikuwa nikimvalisha na kumtayarisha kwa ajili ya utumishi. Kiangazi cha mwaka huo tulipainia katika Wyoming na Montana, tukipiga kambi usiku. Ted alilala katika chumba cha pekee kilichojengwa juu ya gari lake aina ya pickup, nami nililala chini. Baadaye mwaka huo nilihamia kusini ili kupainia katika Tennessee, Arkansas, na Mississippi.
Septemba 1937, nilihudhuria mkusanyiko wangu mkubwa wa kwanza katika Columbus, Ohio. Huko mipango ilifanywa ili kuongoza kazi ya kuhubiri kwa kutumia kinanda cha gramafoni. Kila tulipotumia hicho kinanda cha gramafoni tuliuita huo wakati setup (utumizi wa gramafoni). Mwezi mmoja nilikuwa na setup 500, na watu zaidi ya 800 walisikiliza. Baada ya kutoa ushahidi katika miji mingi ya mashariki mwa Tennessee, Virginia, na West Virginia, nilialikwa kutumikia nikiwa painia wa pekee katika cheo kipya, nikifanya kazi pamoja na mtumishi wa kanda ya dunia, kama vile waangalizi wasafirio walivyoitwa wakati huo.
Nilizuru makutaniko na vikundi vilivyokuwa pekee katika West Virginia—nikitumia majuma mawili hadi majuma manne pamoja na kila kikundi—na niliongoza katika huduma ya shambani. Kisha, katika Januari 1941, niliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa kanda ya dunia. Kufikia wakati huo Mama na dada zangu watatu—Clara, Lois, na Ruth—walikuwa wamechukua msimamo wao kwa ajili ya Ufalme. Kwa hiyo kiangazi cha mwaka huo familia yetu ilihudhuria pamoja mkusanyiko mkubwa katika St. Louis.
Upesi baada ya huo mkusanyiko, watumishi wa kanda ya dunia walijulishwa kwamba kazi ya kanda ya dunia ingeisha mwishoni mwa Novemba 1941. Mwezi uliofuata Marekani iliingia katika Vita ya Ulimwengu ya Pili. Nilipewa mgawo wa kuwa painia wa pekee, uliotaka nitumie saa 175 kwa mwezi katika huduma.
Mapendeleo ya Pekee ya Utumishi
Julai 1942, nilipokea barua iliyouliza kama ningekuwa tayari kutumikia katika nchi za nje. Baada ya kukubali, nilialikwa kwenda Betheli, makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova, katika Brooklyn, New York. Ndugu waseja wapatao 20 walialikwa kwa ajili ya mazoezi ya pekee wakati huohuo.
Nathan H. Knorr, aliyekuwa msimamizi wa Watch Tower Society wakati huo, alieleza kwamba utendaji wa kuhubiri ulikuwa umepungua na kwamba tungezoezwa ili tuyatie makutaniko nguvu kiroho. “Hatutaki kujua matatizo ya makutaniko tu,” akasema, “lakini yale mliyofanya juu yake.”
Tulipokuwa Betheli, Fred Franz, aliyechukua nafasi ya Ndugu Knorr kuwa msimamizi mwaka wa 1977, alitoa hotuba ambayo katika hiyo alisema hivi: “Vita ya Ulimwengu ya Pili itaisha, na kazi kubwa ya kuhubiri itatokea. Hapana shaka mamilioni ya watu bado watakusanywa kuingia katika tengenezo la Yehova!” Hotuba hiyo ilibadili mtazamo wangu kabisa. Migawo ilipofanywa, nilipata habari kwamba nilipaswa kuyazuru makutaniko yote katika majimbo ya Tennessee na Kentucky. Tuliitwa watumishi wa ndugu, utambulisho ambao tangu wakati huo ulibadilishwa kuwa mwangalizi wa mzunguko.
Nilianza kutumikia makutaniko katika Oktoba 1, 1942, nilipokuwa bado na umri wa miaka 25 tu. Wakati huo njia ya pekee ya kuyafikia baadhi ya makutaniko ilikuwa kwa kutembea kwa miguu au kwa kupanda farasi. Nyakati nyingine nililala katika chumba kilekile pamoja na familia iliyonipa malazi.
Nilipokuwa nikitumikia Kutaniko la Greeneville huko Tennessee katika Julai 1943, nilipokea mwaliko wa kuhudhuria darasa la pili la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower. Huko Gileadi, nilijifunza kile kimaanishwacho kwa kweli na “kukazia uangalifu zaidi kuliko ilivyo kawaida mambo yaliyosikiwa” na sikuzote kuwa na “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.” (Waebrania 2:1; 1 Wakorintho 15:58) Ile miezi mitano ya mtaala wa shule ilipita upesi, na kuhitimu kukafika katika Januari 31, 1944.
Kanada na Kuendelea Hadi Ubelgiji
Idadi fulani kati yetu ilipewa mgawo wa kwenda Kanada, ambako marufuku ya utendaji wa Mashahidi wa Yehova yalikuwa yameondolewa majuzi. Nilipewa mgawo wa kazi ya kusafiri, uliotaka nisafiri umbali mkubwa kati ya makutaniko fulani. Niliposafiri, ilikuwa ni shangwe kusikia mambo yaliyoonwa juu ya jinsi ambavyo kazi yetu ya kuhubiri ilikuwa imeendelezwa katika Kanada wakati wa marufuku. (Matendo 5:29) Wengi walizungumzia kile kilichoitwa kwa kawaida blitz (kampeni isiyo ya kijeshi) wakati ambapo katika usiku mmoja, kijitabu kiliwekwa katika karibu kila nyumba kutoka upande mmoja wa Kanada hadi upande ule mwingine. Ilikuwa ni habari njema kama nini kupata kujua katika Mei 1945 kwamba vita katika Ulaya ilikuwa imekwisha!
Kiangazi cha mwaka huo, nilipokuwa nikitumikia kutaniko fulani katika mji mdogo wa Osage, Saskatchewan, nilipokea barua kutoka kwa Ndugu Knorr, iliyosomeka hivi: “Ninakutolea pendeleo la kwenda Ubelgiji. . . . Kuna kazi nyingi ya kufanywa katika nchi hiyo. Ni nchi iliyoharibiwa na vita, na ndugu zetu wahitaji msaada, na yaonekana yafaa kutuma mtu fulani kutoka Marekani ili awape msaada ufaao na faraja wahitajiyo.” Nilijibu mara moja, nikikubali huo mgawo.
Novemba 1945, nilikuwa katika Betheli ya Brooklyn nikijifunza Kifaransa pamoja na Charles Eicher, ndugu mzee-mzee kutoka Alsatia. Nilipokea pia mazoezi ya haraka katika kushughulikia utaratibu wa ofisi ya tawi. Kabla ya kuondoka kwenda Ulaya, nilitembelea familia yangu na marafiki zangu kwa muda mfupi huko St. Joseph, Missouri.
Desemba 11, niliondoka New York katika meli iitwayo Queen Elizabeth, na siku nne baadaye nikawasili Southampton, Uingereza. Nilikaa mwezi mmoja katika ofisi ya tawi ya Uingereza, ambako nilipokea mazoezi ya ziada. Baada ya mazoezi hayo, katika Januari 15, 1946, nilivuka Mlango-Bahari wa Uingereza na kushuka huko Ostend, Ubelgiji. Kutoka hapo nilisafiri kwa garimoshi hadi Brussels, ambako familia nzima ya Betheli ilinilaki kwenye stesheni ya garimoshi.
Utendaji wa Baada ya Vita Ulioongezeka
Mgawo wangu ulikuwa kusimamia kazi ya Ufalme katika Ubelgiji, lakini singeweza hata kusema lugha ya nchi hiyo. Katika miezi ipatayo sita, nilijua Kifaransa kiasi cha kutosha. Ilikuwa ni pendeleo kufanya kazi pamoja na watu waliokuwa wamehatarisha uhai wao ili kuendelea na kazi ya kuhubiri wakati wa miaka mitano ya utekaji wa Nazi. Baadhi yao walikuwa wameachiliwa majuzi kutoka katika kambi za mateso.
Ndugu walikuwa wenye hamu ya kupanga kazi kitengenezo na kulisha waliokuwa na njaa ya kupata kweli ya Biblia. Kwa hiyo mipango ilifanywa ili kufanya makusanyiko na ili waangalizi wasafirio wazuru makutaniko. Tulikuwa pia na ziara zenye kutia moyo kutoka kwa Nathan Knorr, Milton Henschel, Fred Franz, Grant Suiter, na John Booth—wote wakiwa wawakilishi kutoka makao makuu ya Brooklyn. Katika siku hizo za mapema, nilitumikia nikiwa mwangalizi wa mzunguko, mwangalizi wa wilaya, na mwangalizi wa ofisi ya tawi. Desemba 6, 1952, baada ya miaka ipatayo saba ya utumishi katika Ubelgiji, nilimwoa Emilia Vanopslaugh, ambaye pia alifanya kazi katika ofisi ya tawi ya Ubelgiji.
Miezi kadhaa baadaye, katika Aprili 11, 1953, niliitwa kwenda kwenye kituo cha polisi na kujulishwa kwamba kuwapo kwangu kulikuwa hatari kwa usalama wa Ubelgiji. Nilikwenda Luxembourg kungoja huku rufani ya kesi yangu ikikatwa kwa Baraza la Taifa.
Februari 1954 Baraza la Taifa la Ubelgiji lilitegemeza lile agizo kwamba kuwapo kwangu kulikuwa hatari kwa hiyo nchi. Uthibitisho uliotolewa ulikuwa kwamba tangu kuwasili kwangu katika Ubelgiji, idadi ya Mashahidi katika hiyo nchi ilikuwa imeongezeka kwa njia ya kutazamisha—toka Mashahidi 804 mwaka wa 1946 hadi Mashahidi 3,304 mwaka wa 1953—na kwamba, tokeo ni kwamba, usalama wa Ubelgiji ulihatarishwa kwa sababu Mashahidi wengi vijana walikuwa wakichukua msimamo imara kwa ajili ya kutokuwamo kwa Kikristo. Hivyo, Emilia nami tukapewa mgawo wa kwenda Uswisi, ambako tulianza kutumikia katika kazi ya kuzunguka katika eneo la watu wenye kusema Kifaransa.
Shule ya Huduma ya Ufalme—shule ya kuandaa mazoezi ya hali ya juu kwa ajili ya wazee Wakristo—ilianzishwa mwaka wa 1959 katika South Lansing, New York. Nilialikwa kwenda huko ili kupokea mazoezi ya kufundisha madarasa ya shule hiyo katika Ulaya. Nilipokuwa Marekani, nilizuru familia yangu katika St. Joseph, Missouri. Huko nilimwona mamangu mpendwa kwa mara ya mwisho. Alikufa katika Januari 1962; Baba alikuwa amekufa katika Juni 1955.
Shule ya Huduma ya Ufalme katika Paris, Ufaransa, ilianza katika Machi 1961, naye Emilia aliandamana nami. Waangalizi wa wilaya, waangalizi wa mzunguko, waangalizi wa makutaniko, na mapainia wa pekee walikuja kuhudhuria hiyo shule kutoka Ufaransa, Ubelgiji, na Uswisi. Katika miezi 14 iliyofuata, nilifundisha madarasa 12 ya mtaala huo wa majuma manne. Baadaye, katika Aprili 1962, tulipata kujua kwamba Emilia alikuwa na mimba.
Kujipatanisha na Hali
Tulirudi Geneva, Uswisi, ambako tulikuwa na vibali vya kuwa wakazi wa kudumu. Hata hivyo, haikuwa rahisi kupata mahali pa kuishi, kwa sababu kulikuwa na upungufu mkubwa wa nyumba. Hali kadhalika kupata kazi ya kuajiriwa hakukuwa rahisi. Mwishowe niliajiriwa katika duka kubwa katikati ya Geneva.
Nilikuwa nimetumia miaka 26 katika huduma ya wakati wote, kwa hiyo hali zetu zilizobadilika zilitaka kujipatanisha kukubwa. Katika miaka 22 ambayo nilifanya kazi katika hilo duka na kusaidia kuwalea binti zetu wawili, Lois na Eunice, familia yetu sikuzote iliweka masilahi ya Ufalme kwanza. (Mathayo 6:33) Baada ya kustaafu kwangu kutoka katika kazi ya kimwili mwaka wa 1985, nilianza kutumikia nikiwa mwangalizi wa mzunguko wa badala.
Afya ya Emilia imekuwa mbaya sana, lakini yeye hufanya awezavyo katika huduma. Lois alitumikia akiwa painia kwa miaka ipatayo kumi. Lilikuwa jambo kuu la kiroho kama nini kuweza kuonea shangwe pamoja naye ule mkusanyiko wa kimataifa wa ajabu zaidi katika Moscow wakati wa kiangazi cha 1993! Upesi baadaye, akiwa katika safari ya likizo huko Senegal, Afrika, Lois alipoteza uhai wake alipokuwa akiogelea baharini. Upendo na fadhili za ndugu zetu Waafrika na za wamishonari zilikuwa faraja kubwa kwangu niliposafiri kwenda Senegal kushughulikia maziko. Jinsi ambavyo natamani kumwona Lois katika ufufuo!—Yohana 5:28, 29.
Ninashukuru kuwa nimeonea shangwe kwa zaidi ya miongo minne tegemezo lenye uaminifu-mshikaminifu la mwandamani mwenye upendo. Kwa kweli, kujapokuwa na huzuni na usumbufu wangu mbalimbali, fadhili-upendo za Yehova zimekuwa zenye kupendeza na zimefanya maisha yawe yenye maana. Moyo wangu wasukumwa kutangaza kuhusu Mungu wetu, Yehova, katika maneno haya ya mtunga-zaburi: “Maana fadhili [“fadhili-upendo,” NW] zako ni njema kuliko uhai; midomo yangu itakusifu.”—Zaburi 63:3.
[Picha katika ukurasa wa 26]
Tuliongoza kazi ya kuhubiri kwa kinanda cha gramafoni
[Picha katika ukurasa wa 26]
Wazazi wangu mwaka wa 1936
[Picha katika ukurasa wa 26]
Kutoa ushahidi wa barabarani katika Ubelgiji mwaka wa 1948