Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w98 2/1 kur. 29-31
  • Je, Ni Kusifu au Ni Kurai?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Ni Kusifu au Ni Kurai?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kusifu na Kurai Kwafasiliwa
  • Maoni ya Kimaandiko
  • Kurai—Mtego
  • Ulinzi Dhidi ya Kurai
  • Kusifu Kustahilipo
  • Msifuni Yehova Mungu Wetu
    Mwimbieni Yehova
  • Msifuni Yehova Mungu Wetu!
    ‘Mwimbieni Yehova kwa Shangwe’
  • Jinsi ya Kuwapongeza Watoto
    Amkeni!—2015
  • Enyi Vijana, Msifuni Yehova!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
w98 2/1 kur. 29-31

Je, Ni Kusifu au Ni Kurai?

MTU fulani akuambia, “Mtindo wako mpya wa nywele wapendeza sana!” Je, ni kusifu au ni kurai? “Suti hiyo yakufaa kabisa!” Kusifu au kurai? “Huu ndio mlo wenye ladha zaidi ambao nimepata kuonja!” Je, ni kusifu au ni kurai? Tupokeapo pongezi za namna hiyo, huenda tukajiuliza ikiwa kwa kweli ni za moyo mweupe na za kweli au ikiwa zasemwa ili kutupendeza tu bila msemaji kuamini asemayo.

Twaweza kujuaje ikiwa mambo ambayo mtu atuambia ni kusifu au ni kurai? Je, ni jambo la maana? Je, hatuwezi kukubali tu yale yasemwayo na kuonea shangwe furaha yatupatiayo? Vipi wakati ambapo twawasifu wengine? Je, tumepata kuchunguza nia zetu? Kufikiria maswali hayo kwaweza kutusaidia kuwa wenye kufahamu na kutumia ulimi wetu katika njia imleteayo sifa Yehova Mungu.

Kusifu na Kurai Kwafasiliwa

Kamusi ya Webster’s Dictionary yafasili kusifu kuwa wonyesho wa kibali au pongezi, na neno hilo laweza pia kuonyesha ibada au kutukuza. Kwa wazi maana mbili za mwisho zarejezea tu kumsifu Yehova Mungu. Kusifu huko ni sehemu muhimu ya ibada ya kweli, kama vile mtunga-zaburi aliyepuliziwa ahimizavyo kwa bidii hivi: “Maana ni vema . . . , kwapendeza, kusifu ni kuzuri.” “Kila mwenye pumzi na amsifu BWANA.”—Zaburi 147:1; 150:6.

Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba wanadamu hawawezi kusifiwa. Wanaweza kusifiwa, katika maana ya kupongezwa, kukubaliwa, au kupendelewa. Katika mfano wenye somo uliotolewa na Yesu, bwana-mkubwa amwambia mtumishi wake hivi: “Vema, mtumwa mwema na mwaminifu!”—Mathayo 25:21.

Kwa upande mwingine, kurai kwafasiliwa kuwa kusifu kusiko kwa kweli, kusiko kwa moyo mweupe au kwa kupita kiasi, ambamo mwenye kurai kwa kawaida ana nia za kujipendeza. Pongezi ya ujanja au kuvisha kilemba cha ukoka kwafanywa ili kupata kibali au faida za kimwili kutoka kwa mtu mwingine au kutokeza hisia ya kuwa na wajibu kuelekea mwenye kurai. Kwa hiyo wenye kurai husukumwa na ubinafsi. Kulingana na Yuda 16, wako “tayari na maneno ya kurai watu wengine waonapo faida fulani katika kufanya hivyo.”—The Jerusalem Bible.

Maoni ya Kimaandiko

Maoni ya Kimaandiko juu ya kuwasifu binadamu wenzetu ni nini? Yehova hutuwekea kiolezo tufuate katika habari hii. Twaambiwa katika Biblia kwamba tutasifiwa tukifanya mapenzi ya Yehova. Mtume Paulo asema kwamba ‘kila mmoja atapata sifa yake ikimjia kutoka kwa Mungu.’ Petro atuambia kwamba ubora huu uliotahiniwa wa imani yetu “upatikane kuwa sababu ya sifa.” Kwa hiyo uhakika wa kwamba Yehova atawasifu wanadamu hutuonyesha kwamba kusifu kwa moyo mweupe ni tendo lenye fadhili, la upendo, na lenye manufaa, ambalo halipasi kupuuzwa.—1 Wakorintho 4:5; 1 Petro 1:7.

Kulingana na Biblia, chanzo kingine kiwezacho kutusifu, ni wenye mamlaka wa serikali ambao huangalia mwenendo wetu mwema na kutupongeza kwa kufuata haki. “Fuliza kufanya lililo jema,” twaambiwa, “nawe utakuwa na sifa kutoka kwayo.” (Waroma 13:3) Huenda pia tukasifiwa na watu ambao huamini kwa moyo mweupe mambo wasemayo na wasio na nia iliyofichika katika kutusifu. Maandiko yaliyopuliziwa yasema hivi kwenye Mithali 27:2: “Mwingine na akusifu wala si kinywa chako mwenyewe.” Hilo laonyesha kwamba kukubali kusifiwa na wanadamu kwafaa.

Sivyo ilivyo kwa habari ya kurai au kuraiwa. Kwa nini usemi wa kurai ni wenye kumchukiza Yehova sana? Jambo moja ni kwamba, si kwa moyo mweupe, na Yehova hulaumu kutokuwa na moyo mweupe. (Linganisha Mithali 23:6, 7.) Zaidi, hakufuatii haki. Akifafanua watu wastahilio kukataliwa na Mungu, mtunga-zaburi asema hivi: “Yote wafanyayo ni kudanganyana, midomo yenye kurai, husema kutoka katika mioyo miwili. Yahweh na akatilie mbali kila domo lenye kurai.”—Zaburi 12:2, 3, JB.

Zaidi ya yote, kurai ni kukosa upendo. Husukumwa na ubinafsi. Baada ya kusema juu ya wenye kurai, mtunga-zaburi Daudi awanukuu wakisema hivi: “Kwa ndimi zetu tutashinda; midomo yetu ni yetu wenyewe, ni nani aliye bwana juu yetu?” Yehova awafafanua wenye ubinafsi hao kuwa ‘waoneao wanyonge.’ Ndimi zao zenye kurai zimetumiwa kuwaonea na kuwataabisha wengine, wala si kuwajenga.—Zaburi 12:4, 5.

Kurai—Mtego

“Mwenye kujipendekeza kwa [“kumrai,” NW] jirani yake, hutandika wavu ili kuitega miguu yake.” Hivyo ndivyo asemavyo Mfalme Solomoni mwenye hekima, na jinsi hilo lilivyo kweli! (Mithali 29:5) Mafarisayo walijaribu kumtandikia Yesu mtego kwa kurai. Walisema hivi: “Mwalimu, twajua wewe ni mwenye ukweli nawe hufundisha njia ya Mungu katika kweli, nawe hujali yeyote, kwa maana wewe hutazami kuonekana kwa mtu kwa nje.” Hilo lilisikika kuwa lenye kupendeza kama nini! Lakini Yesu hakudanganywa na maneno yao laini. Alijua kwamba hawakuamini mafundisho yake ya kweli bali walikuwa wakijaribu tu kumnasa katika usemi wake juu ya suala la kumlipa Kaisari kodi.—Mathayo 22:15-22.

Mfalme Herode wa karne ya kwanza alikuwa tofauti kabisa na Yesu. Alipohutubu hadharani katika mji wa Kaisaria, watu waliitikia hivi: “Sauti ya mungu, na si ya binadamu!” Badala ya kuwakemea watu kwa sababu ya kusifu huko kubaya sana, kusiko kwa kweli, Herode alikubali kurai huko. Malaika wa Yehova alileta malipo ya papo hapo kwa kuwa Herode alipigwa kwa mabuu yaliyotokeza kifo chake.—Matendo 12:21-23.

Mkristo mkomavu atakuwa macho ili kutambua jinsi kurai kulivyo. Hasa wazee wa kutaniko wapaswa kuwa macho wakati ambapo mtu fulani ahusikaye katika jambo la kihukumu ni mwenye kupongeza-pongeza, labda hata kufikia kulinganisha mzee mmoja na mwingine na kusema jinsi mwenye kuzungumziwa alivyokuwa mwenye fadhili na mwenye hisia-mwenzi zaidi.

Biblia huonyesha waziwazi mtego mwingine ambao kurai kwaweza kutokeza wakati ifafanuapo jinsi mwanamume kijana ashawishiwavyo na mshawishi wa kike na kuingia katika ukosefu wa adili. (Mithali 7:5, 21) Onyo hilo lahusu hali ya leo. Miongoni mwa wale ambao hutengwa na ushirika kutoka katika kutaniko la Kikristo kila mwaka, wengi huondolewa kwa sababu ya mwenendo usio wa adili. Je, yawezekana kwamba kutumbukia huko katika dhambi nzito kulianzishwa na kurai? Kwa kuwa wanadamu hutamani sana kupongezwa na kusemwa vizuri, maneno laini kutoka katika midomo ya kurai yaweza kupunguza ukinzani wa Mkristo dhidi ya mwenendo usiofaa. Wakati ambapo mtu hajilindi dhidi ya hayo, yangeweza kuongoza kwenye matokeo mazito.

Ulinzi Dhidi ya Kurai

Kurai hutosheleza kujipenda au majivuno ya mwenye kuraiwa. Huelekea kumpa mtu maoni yaliyokuzwa ya ubora wake mwenyewe, kukimfanya ahisi kuwa bora zaidi kuliko wengine kwa njia fulani. Mwanafalsafa François de La Rochefoucauld alilinganisha kurai na fedha bandia, “ambako, isipokuwa kwa sababu ya kumfanya mtu ajivune, hakungekubalika hata kidogo.” Hivyo, njia ya kujilinda ni kutii onyo la upole la mtume Paulo lenye kutumika: “Naambia kila mtu huko miongoni mwenu asijifikirie mwenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri; bali afikiri ili awe na akili timamu, kila mmoja kama vile Mungu amemgawia kipimo cha imani.”—Waroma 12:3.

Ingawa sikuzote sisi huelekea kutaka kusikia lipendezalo masikioni petu, jambo ambalo kwa kweli twahitaji nyakati zilizo nyingi ni shauri na nidhamu yenye kutegemea Biblia. (Mithali 16:25) Mfalme Ahabu alitaka kusikia lililompendeza tu; watumishi wake hata walimwomba nabii Mikaya neno lake na liwe “kama neno la mmojawapo wao [manabii wa Ahabu wenye kurai], ukaseme mema.” (1 Wafalme 22:13) Ikiwa Ahabu angalikuwa na nia ya kusikiliza maongezi ya waziwazi na kubadili njia zake za uasi, angaliweza kuzuia hasara mbaya za pigano zilizopata Israeli na pia angaliepuka kifo chake mwenyewe. Kwa ajili ya hali njema yetu wenyewe ya kiroho, twapaswa kuwa wepesi wa kuitikia shauri thabiti, lakini lenye upendo, la wazee Wakristo waliowekwa rasmi, watakao kutusaidia tubaki tukiwa katika kijia kilichonyooka cha kweli, badala ya kutafuta watu ambao hufuliza kutuambia jinsi tulivyo wa ajabu sana, wakitekenya masikio yetu na usemi wenye kurai!—Linganisha 2 Timotheo 4:3.

Wakristo hawangetaka kamwe, kwa sababu yoyote ile, kugeukia kurai. Kama Elihu mwaminifu, wao husali hivi kwa kuazimia: “Na nisiwe mwenye ubaguzi kuelekea yeyote, wala kurai mtu yeyote; kwa kuwa sijui jinsi ya kurai, au sivyo Mfanyi wangu angeniondolea mbali upesi.” Kisha, kama Paulo, wangeweza kusema hivi: “Hakuna wakati wowote ambao sisi tumetokea ama na usemi wa kurai . . . ama na sura isiyo ya kweli kwa ajili ya tamaa.”—Ayubu 32:21, 22, An American Translation; 1 Wathesalonike 2:5, 6.

Kusifu Kustahilipo

Mithali iliyopuliziwa huonyesha kwamba kusifu kwaweza kutenda kukiwa kipimo, ikisema hivi: “Chungu cha kuyeyushia ni cha fedha na kiviga ni cha dhahabu, bali kusifu ni mtihani wa utu.” (Mithali 27:21, The New English Bible) Ndiyo, kusifu kwaweza kuendeleza hisia za ukubwa au majivuno, kukiongoza kwenye ushinde wa mtu. Kwa upande mwingine, kwaweza kufunua kiasi chake na unyenyekevu wake akikiri kuwiwa kwake na Yehova kwa lolote ambalo amefanya, ambalo limemletea sifa.

Kusifu kwa moyo mweupe kwa sababu ya mwenendo au mafikio yenye kustahili hujenga mwenye kusifu na mwenye kusifiwa. Huchangia kuthaminiana kwa njia yenye uchangamshi na yenye kujenga. Hutia moyo kujitahidi kufikia miradi yenye kustahili sifa. Huenda sifa istahiliyo wapewayo wachanga ikawafanya watake kufanya kazi kwa bidii zaidi. Huenda ikasaidia kufanyiza utu wao huku wakikusudia kuishi kulingana na viwango vitarajiwavyo kwao.

Kwa hiyo, na tuepuke kurai—tuwe twarai au twaraiwa. Na tuwe wanyenyekevu tusifiwapo. Na acheni tuwe wakarimu na wenye moyo wote tusifupo—tumsifupo Yehova kwa ukawaida katika ibada yetu na tuwasifupo wengine kwa moyo mweupe kwa pongezi na uthamini ujengao, tukikumbuka kwamba “neno linenwalo wakati wa kufaa ni jema kama nini!”—Mithali 15:23.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki