Kwa Nini Uwe Mwenye Shukrani?
UPASUAJI wa uti wa mgongo ulimlazimisha Harley abadilishe kazi-maisha yake kutoka kuwa mtengeneza-mashine na kuwa karani wa ofisi. Alipoulizwa alivyohisi kuhusu badiliko hilo, Harley alisema hivi: “Nahisi kukosa sana kufanya kazi kwa mashine. Lakini, kwa kusema kweli, ninafurahia zaidi kazi yangu ya sasa kuliko kazi yangu ya zamani.”
Akitoa sababu ya kuridhika kwake, Harley ataarifu hivi: “Ni mtazamo wa watu nifanyao kazi nao. Tofauti na wale wa mahali pangu pa kazi pa zamani, msimamizi wangu wa sasa na wafanyakazi wenzangu ni wenye kuthamini nifanyayo, na hutoa pongezi kwa utayari. Hilo limefanyiza tofauti kubwa.” Akihisi kuwa mwenye mafaa na mwenye kuhitajiwa, Harley sasa ni mfanyakazi mwenye furaha.
Maneno ya pongezi au ya shukrani, yastahilipo, kwa kweli ni yenye kuchangamsha moyo. Kwa upande mwingine, matokeo ya kukosa shukrani yaweza kuwa yenye kuvunja moyo kama vile Shakespeare alivyosema: “Vuma, vuma, ewe upepo wa majira ya baridi kali, wewe si mwenye kukosa fadhili sana kama vile kukosa shukrani kwa mwanadamu.” Kwa kusikitisha, watu wengi wamekosa kuonyeshwa fadhili hivyo.
Linda Dhidi ya Kukosa Shukrani
Katika ulimwengu wa leo semi za moyo mweupe za shukrani zinatoweka. Kwa mfano, mwandikaji fulani alizusha swali hili: “Ikiwa bibi-arusi alipata wakati wa kuandika anwani 200 za mialiko ya arusi, kwa nini hawezi kupata wakati wa kuandika barua fupi za kushukuru kwa ajili ya zawadi 163?” Mara nyingi hata lile neno sahili “asante” halisemwi. Mtazamo wa mimi-kwanza unazidi kuchukua mahali pa shukrani. Hali hiyo ni mojawapo ya alama zinazotambulisha siku za mwisho. Mtume Paulo alionya hivi: “Lazima mng’amue kwamba katika siku za mwisho nyakati zitakuwa zimejaa hatari. Wanadamu watakuwa wenye ubinafsi kabisa . . . Watakosa shukrani kabisa.”—2 Timotheo 3:1, 2, Phillips.
Katika visa vingine, kurai huchukua mahali pa shukrani. Semi za shukrani husemwa kutoka moyoni bila kufikiria pato la kibinafsi. Hata hivyo, kurai, ambako kwa kawaida hakutoki moyoni na kumetiwa chumvi, huenda kukatokana na nia iliyofichika ya kutafuta upandishwaji cheo au kujaribu kupata faida fulani za kibinafsi. (Yuda 16) Mbali na kumdanganya mpokeaji, maongezi hayo laini huelekea kuwa matunda ya majivuno na kiburi. Nani basi, ambaye angetaka kuwa mhasiriwa wa kurai kusikotoka moyoni? Lakini shukrani za kweli zinaburudisha kwelikweli.
Mtu mwenye kutoa shukrani hunufaika kutokana na kufanya hivyo. Ule uchangamshi ambao yeye hupata kwa sababu ya kuwa mwenye shukrani moyoni huchangia furaha yake na amani. (Linganisha Mithali 15:13, 15.) Na ikiwa sifa iliyo chanya, shukrani humlinda asiwe na hisia hasi kama hasira, wivu, na uchungu.
“Jionyesheni Wenyewe Kuwa Wenye Shukrani”
Biblia hutuhimiza tusitawishe roho ya shukrani. Paulo aliandika hivi: “Kuhusiana na kila jambo toeni shukrani. Kwa maana hayo ndiyo mapenzi ya Mungu katika muungano na Kristo Yesu kwa habari yenu nyinyi.” (1 Wathesalonike 5:18) Naye Paulo aliwashauri Wakolosai hivi: “Acheni amani ya Kristo idhibiti mioyoni mwenu . . . Na jionyesheni wenyewe kuwa wenye shukrani.” (Wakolosai 3:15) Zaburi nyingi sana zina semi za shukrani, zikionyesha kwamba shukrani zenye kuhisiwa moyoni ni wema wa adili wa kimungu. (Zaburi 27:4; 75:1) Kwa wazi, Yehova Mungu hupendezwa tudhihirishapo shukrani katika mambo ya kila siku ya maisha.
Lakini ni mambo gani katika ulimwengu huu usio na shukrani ambayo hufanya iwe vigumu kwetu kusitawisha roho ya shukrani? Twaweza kuonyeshaje mtazamo wenye shukrani katika maisha ya kila siku? Maswali hayo yatazungumziwa katika makala yenye kufuata.