Kwa Nini Wao Hufanya Hivyo?
KILA mwaka maelfu ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote hukusanyika kwenye mikusanyiko. Huko wao huonea shangwe ushirika na kusikiliza programu bora kabisa ya mafundisho ya Biblia. Baadhi yao hujitahidi sana kuhudhuria mikusanyiko hiyo. Kwa kielelezo, mwaka uliopita katika Malawi wenzi wa ndoa walio katika miaka yao ya 60, pamoja na mwana wao na mke wake na mtoto mchanga, walisafiri kilometa 80 kwa baiskeli ili kuhudhuria mkusanyiko. Waliondoka kijijini mwao saa 12 asubuhi na kufika kwenye uwanja wa mkusanyiko muda wa saa 15 baadaye.
Katika Msumbiji, kikundi fulani kilisafiri siku tatu kwa baiskeli ili kufika kwenye mkusanyiko. Usiku mmoja, walipopiga kambi nje, walisikia simba wakinguruma karibu. Ingawa walitupa kuni upande waliokuwa wanyama hao, hao simba walikaa karibu-karibu hadi mapambazuko. Shahidi mwingine aliyekuwa akisafiri kuelekea kusanyiko hilohilo alikutana uso kwa uso na simba barabarani. Alisimama kimya bila kujongea hadi huyo simba alipoenda zake. Kwenye huo mkusanyiko Mashahidi hao walisimulia kwa uchangamfu jinsi walivyokuwa “[wame]kombolewa kutoka katika kinywa cha simba.”—2 Timotheo 4:17.
Mashahidi wa Yehova walio wengi hujitahidi sana kuhudhuria mikusanyiko au hata mikutano ya kutaniko ya kila juma kwa ajili ya ibada. Kwa nini? Makala zinazofuata zitakusaidia uelewe kwa nini kukusanyika pamoja ni kwa maana sana.