“Kila Siku Mahali pa Soko”
Wapiga-mbiu wa Ufalme Waripoti
MTUME Paulo alitumia kila fursa ili kueneza ujumbe wa Ufalme. Ili kutafuta wenye kupendezwa, alijadiliana kwa kutoa sababu “katika sinagogi pamoja na Wayahudi . . . na kila siku mahali pa soko pamoja na wale waliotukia kuwa hapo.”—Matendo 17:17.
Bidii hiyo imekuwa alama ya waabudu wa kweli wa Yehova tangu karne ya kwanza W.K. (Mathayo 28:19, 20) Leo, Mashahidi wa Yehova hali kadhalika hutumia njia tofauti-tofauti wawasaidiapo kwa bidii watu wenye mioyo ya haki wapate ujuzi sahihi wa kweli. (1 Timotheo 2:3, 4) Jambo lililoonwa lifuatalo kutoka Australia latolea hilo kielezi.
Siku tano kila juma, Sid na Harold hupokezana zamu kutunza kimeza kidogo cha kuonyeshea watu fasihi za Biblia kando ya kituo cha reli huko Sydney. Wamekuwa wakiwahubiria watu habari njema ya Ufalme wa Mungu kwa njia hiyo kwa miaka mitano kufikia sasa. Sid, mwenye umri wa miaka 95, aeleza hivi: “Nilipotimia miaka 87, sikuweza kuendesha gari tena. Hilo lilinivunja moyo sana kwa sababu nilifurahia utendaji wa kutoa ushahidi hadharani. Siku moja nilipokuwa karibu na eneo linalopendwa na watalii liitwalo Echo Point huko Katoomba, nilimwona mchoraji akiuza picha za mandhari. Nilizichunguza picha hizo na kufikiri, ‘Nina picha bora zaidi kuliko hizo kwenye mkoba wangu wa vitabu—na kwa kiasi kidogo zaidi cha fedha!’ Kwa hiyo nikaamua kutengeneza kimeza kidogo cha kuonyeshea vichapo, nikiweke mahali penye watalii wengi, na kuwatolea wapita-njia fasihi za Biblia, zenye picha nzuri, ambazo hugawanywa na Mashahidi wa Yehova.
“Miaka minne iliyopita, nilihamisha kimeza hicho hadi Sydney, naye Harold akajiunga nami. Sisi hupokezana zamu kutunza kimeza hicho na kuhubiri na makutaniko yetu.” Harold, mwenye umri wa miaka 83 sasa, asema hivi: “Watu wachache sana huwa nyumbani Jumatatu hadi Ijumaa. Kwa hiyo kuhubiri ujumbe wa Ufalme kwa njia hii hutuweka mahali ambapo watu wako. Bila shaka, sisi hupata matokeo bora zaidi. Sisi huangusha fasihi nyingi kwa kulinganisha na kiwango cha nchi.”
“Ingawa tumeweka kimeza chetu katika sehemu nne au tano kwa miaka kadhaa,” asema Sid, “punde watu hujua sisi ni akina nani na twapatikana wapi. Watu fulani hutujia ili kupata fasihi. Wengine huwa na maswali wanayotaka yajibiwe. Na wengine hutaka tu kuongea kwa dakika chache. Huu ndio wakati pekee ambao marudio yangu hunijia,” asema akicheka.
“Watu wengi kwa kweli wanapendezwa na Biblia,” Harold aongeza. “Katika mwezi mmoja tu watu wanne walianza kujifunza Biblia na Mashahidi kwa sababu ya fasihi walizokuwa wamepokea kutoka kwetu na kwa sababu ya maswali tuliyoweza kuwajibu kutoka katika Biblia. Mambo yaliyoonwa kama hayo hututia moyo sana.”
Kama Sid na Harold—na kama mtume Paulo, Mashahidi wa Yehova kotekote hutumia kila njia iwezekanayo ili kueneza ujumbe wao muhimu. Hivyo, “habari njema” yaendelea kuhubiriwa “katika dunia yote inayokaliwa.”—Mathayo 24:14.y