Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w98 8/1 kur. 25-29
  • Kuthamini Sana Mapendeleo ya Utumishi Mtakatifu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuthamini Sana Mapendeleo ya Utumishi Mtakatifu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kunapokuwa na Mahitaji Muhimu ya Familia
  • Kuchukua Daraka Lao
  • Kukiwa na Ushirikiano wa Familia
  • Wazazi Wanaomtolea Yehova kwa Hiari
  • Makutaniko Yenye Kutegemeza
  • Kuzoea Bidii ya Kujitolea Mungu Kuhusiana na Wazazi Wazee-Wazee
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Wakumbuke Watumishi wa Wakati Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
  • Kutoa Utumishi Mtakatifu Kama Jamaa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • “Kutafuta Kwanza Ufalme”
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
w98 8/1 kur. 25-29

Kuthamini Sana Mapendeleo ya Utumishi Mtakatifu

MIGAWO ya utumishi mtakatifu haipasi kuchukuliwa kihivi-hivi. Makuhani wa Yuda la kale walipoonyesha mtazamo wa kutojali mapendeleo yao kuhusiana na hekalu la Yehova, yeye aliwakaripia vikali. (Malaki 1:6-14) Na wakati ambapo watu fulani katika Israeli waliwahimiza Wanadhiri wachukulie kihivi-hivi madaraka waliyokuwa wamekubali kuhusiana na utumishi mtakatifu, Yehova aliwakaripia Waisraeli hao wenye kutenda dhambi. (Amosi 2:11-16) Wakristo wa kweli pia hushiriki katika utumishi mtakatifu, na huuchukua kwa uzito. (Waroma 12:1) Utumishi huo mtakatifu ni wa aina nyingi na wote ni muhimu.

Wakati ambapo Yesu alikuwa bado duniani pamoja na wafuasi wake, aliwazoeza kuwa wahubiri wa Ufalme wa Mungu. Baada ya muda, ujumbe wao ungefika kwenye miisho ya dunia. (Mathayo 28:19, 20; Matendo 1:8) Kuhubiri huko kumekuwa na uharaka hata zaidi katika hizi siku za mwisho za mfumo wa mambo wa sasa.

Mashahidi wa Yehova wote hushiriki katika kazi hiyo. Mamia ya maelfu hufurahi kuweza kufanya hivyo wakiwa mapainia. Ili kutimiza mahitaji muhimu katika kazi ya ulimwenguni pote, maelfu wamejitoa kwa ajili ya utumishi wa pekee wa wakati wote kwenye Betheli, katika kazi ya kusafiri wakiwa waangalizi wa mzunguko na wa wilaya, au katika utumishi wa mishonari. Huenda kufanya hivyo kukahusisha nini kwa wale wanaotaka kuendelea katika utumishi huo wa pekee?

Kunapokuwa na Mahitaji Muhimu ya Familia

Kwa kawaida ni lazima mtu afanye marekebisho fulani katika hali zake kabla ya kuanza utumishi wa pekee wa wakati wote. Si kila mtu awezaye kufanya hivyo. Huenda wajibu mbalimbali wa Kimaandiko ambao mtu tayari anao, ukafanya utumishi huo usiwezekane. Ingawa hivyo, ni nini hutukia wakati ambapo wale walio katika utumishi wa pekee hukabili mahitaji ya haraka ya kifamilia, labda yanayohusisha wazazi wazee-wazee? Kanuni na shauri la Biblia kama hili linalofuata hutoa mwongozo unaohitajiwa.

Maisha yetu yote yapaswa kutegemea uhusiano wetu na Yehova. (Mhubiri 12:13; Marko 12:28-30) Ni lazima tuthamini sana mambo matakatifu tuliyoaminishwa kutunza. (Luka 1:74, 75; Waebrania 12:16) Katika pindi moja, mwanamume fulani aliyehitaji kubadili mambo aliyotanguliza aliambiwa na Yesu kwamba, angepaswa kujishughulisha kikamili na kutangaza Ufalme wa Mungu. Kwa wazi, mwanamume huyo alikuwa akinuia kuahirisha utendaji huo hadi baada ya kifo cha baba yake. (Luka 9:59, 60) Kwa upande mwingine, Yesu alifichua kufikiri kusikofaa kwa yeyote aliyedai kuwa ameweka kila kitu wakfu kwa Mungu kisha ‘kutofanya hata jambo moja kwa ajili ya baba yake au mama yake.’ (Marko 7:9-13) Mtume Paulo pia alionyesha daraka zito la kuwaandalia kitu ‘wale walio wa mtu mwenyewe,’ kutia ndani wazazi na, babu na nyanya.—1 Timotheo 5:3-8.

Je, hilo lamaanisha kwamba kunapokuwa na mahitaji ya haraka, ni lazima wale walio katika utumishi wa pekee waache migawo yao ili wapate kuwa watunzaji? Jibu la swali hilo linahusisha mambo mengi. Mtu binafsi ndiye awezaye kuamua. (Wagalatia 6:5) Ingawa walithamini migawo yao, wengi wameamua kwamba lingekuwa jambo la hekima kukaa na wazazi wao ili kuwapa msaada wenye kuhitajika. Kwa nini? Huenda ikawa uhitaji ulikuwa umekuwa mkubwa sana, huenda ikawa hakukuwa na mshiriki mwingine wa familia ambaye angeweza kusaidia, au huenda ikawa kutaniko la huko halingeweza kufanya jambo lililohitajika. Baadhi ya wengine wameweza kupainia huku wakitoa msaada huo. Wengine wameweza kuanza tena utumishi wa pekee wa wakati wote baada ya hali ya familia kushughulikiwa. Hata hivyo, katika visa vingi, imewezekana kushughulikia hali hiyo katika njia nyinginezo.

Kuchukua Daraka Lao

Wakati ambapo mahitaji muhimu yametokea, wengine walio katika utumishi wa pekee wa wakati wote wameweza kushughulikia mahitaji hayo bila kuacha migawo yao. Kati ya vielelezo vilivyo vingi, ebu fikiria vichache tu.

Wenzi wanaotumikia kwenye makao makuu ya Mashahidi wa Yehova waliingia katika utumishi wa Betheli mwaka wa 1978, baada ya kuwa wameshiriki katika kazi ya mzunguko na ya wilaya. Mgawo wa huyo ndugu wahusisha daraka kubwa sana katika tengenezo la kitheokrasi. Lakini wazazi wake pia wamehitaji msaada. Wenzi hao walio wana-betheli wamefanya ziara tatu au nne kila mwaka—wakisafiri umbali wa kilometa 3,500, kwenda na kurudi—ili kuwatunza wazazi wao. Walijenga nyumba wao wenyewe ili kutimiza mahitaji ya wazazi wao. Wamesafiri mara nyingi ili kushughulikia hali za dharura za kitiba. Kwa miaka ipatayo 20, wametumia likizo yao yote kushughulikia daraka hilo. Wanawapenda na kuwaheshimu hao wazazi, lakini wanathamini pia mapendeleo yao ya utumishi mtakatifu.

Ndugu mwingine alikuwa amekuwa katika kazi ya kusafiri kwa miaka 36 alipokabili ile aifafanuayo kuwa hali ngumu zaidi aliyowahi kukabili maishani mwake. Mama-mkwe wake mwenye umri wa miaka 85, ambaye ni mtumishi mwaminifu wa Yehova, alihitaji kuishi na mtu ambaye angeweza kumsaidia. Wakati huo, wengi wa watoto wake walihisi kwamba haingefaa waishi naye. Mtu mmoja wa jamaa alimwambia huyo mwangalizi asafiriye kwamba, iliwabidi yeye na mke wake waache utumishi huo na kumtunza mama kwa niaba ya familia. Lakini wenzi hao hawakuacha utumishi wao wenye thamani, wala hawakupuuza mahitaji ya mama. Katika miaka tisa iliyofuata, kwa wakati ulio mwingi, huyo mama alikuwa akiishi pamoja nao. Mwanzoni waliishi katika makao yawezayo kuhamishwa, kisha wakaishi katika vyumba mbalimbali walivyoandaliwa na mizunguko. Kwa vipindi virefu, huyo ndugu ambaye wakati huo alikuwa mwangalizi wa wilaya, aliendelea kusafiri ili kushughulikia migawo yake huku mke wake akikaa na mama yake ili aweze kutoa utunzaji wa wakati wote wenye upendo. Kila juma baada ya mikutano ya Jumapili, mume alisafiri mwendo mrefu kurudi ili akawasaidie. Wengi waliofahamu hali ya mambo walionyesha uthamini mkubwa kwa yale wenzi hao waliyokuwa wakifanya. Baada ya muda, washiriki wengine wa familia pia walisukumwa kutoa msaada. Maelfu ya watu wa Yehova huendelea kunufaika na utumishi wa kujidhabihu wa wenzi hao, kwa sababu hawakuacha pendeleo lao la utumishi wa pekee wa wakati wote.

Kukiwa na Ushirikiano wa Familia

Wakati washiriki mbalimbali wa familia wathaminipo utumishi wa pekee wa wakati wote, huenda wakashirikiana ili angalau baadhi yao waweze kushiriki katika utumishi huo.

Roho hiyo ya ushirikiano wa familia imesaidia wenzi kutoka Kanada ambao hutumikia wakiwa wamishonari katika Afrika Magharibi. Hawakungoja hadi wakati ambapo hali ya dharura ilitokea, wakitumaini tu kwamba hakuna lolote ambalo lingetukia. Katika kujitayarisha kwa ajili ya utumishi wa nchi za kigeni, kabla ya kwenda katika Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower, mume alizungumza na ndugu yake mwenye umri mdogo juu ya kumtunza mama yao kama angekuwa mgonjwa au asiyejiweza. Huyo ndugu mwenye umri mdogo alisema hivi kwa kuonyesha upendo kwa mama yao na vilevile uthamini kwa kazi ya mishonari: “Sasa nina familia na watoto. Siwezi kwenda mbali sana na kufanya mambo mwezayo kufanya. Kwa hiyo Mama akipatwa na jambo lolote, nitamtunza.”

Wenzi fulani wanaotumikia katika Amerika Kusini walipata ushirikiano mkubwa kutoka kwa familia ya mke katika kutunza mama yake aliyekuwa akizeeka. Mmoja wa dada za mke na mume wa huyo dada, walimtunza mama hadi dada huyo aliposhikwa na ugonjwa wa kufisha. Kisha kukawaje? Ili wasiwe na hangaiko lolote, ndugu-mkwe aliwaandikia hivi: “Maadamu mimi na watoto tuko hai, hamtalazimika kamwe kuacha utumishi wenu wa umishonari.” Msaada wa ziada wa familia ulipatikana wakati ambapo dada yao mwingine na mume wake waliacha makao yao na kuhamia alipoishi mama ili kumtunza, nao walifanya hivyo hadi alipokufa. Ni roho ya ushirikiano iliyoje! Wote walikuwa wakisaidia kutegemeza utumishi wa mishonari.

Wazazi Wanaomtolea Yehova kwa Hiari

Mara nyingi wazazi huonyesha uthamini wenye kutokeza kwa utumishi mtakatifu. Watoto wao wenyewe ni miongoni mwa mali zao zenye thamani zaidi ambazo kwazo wanaweza kumheshimu Yehova. (Mithali 3:9) Wazazi wengi Wakristo huwatia watoto wao moyo waingie katika utumishi wa wakati wote. Na baadhi yao huhisi kama alivyohisi Hana ambaye alimtoa mwana wake Samweli ili amtumikie Yehova “daima,” yaani, “wakati wote atakaokuwa hai.”—1 Samweli 1:22, 28.

Mzazi kama huyo alimwandikia binti yake akiwa Afrika barua iliyosema hivi: “Tunamshukuru Yehova kwa pendeleo lako la ajabu. Umetimiza matarajio yetu ya juu zaidi.” Na katika pindi nyingine alisema hivi: “Ni kweli kwamba twalazimika kujidhabihu kutengana nawe, lakini ni furaha iliyoje kuona jinsi Yehova anavyokutunza!”

Mishonari mmoja kutoka Ekuado, baada ya kuchunguza hali mbalimbali ambazo zilikuwa zimetokezwa na uhitaji wa kutunza wazazi wake walio wazee-wazee alisema hivi: “Ninafikiri kwamba sala za baba yangu zilikuwa msaada mkubwa zaidi ambao mimi na mke wangu tuliweza kupata. Baada ya kifo chake, mama yangu alituambia hivi: ‘Baba yako alisali kila siku ili Yehova awaruhusu nyinyi wawili mwendelee na mgawo wenu.’”

Wenzi walio wazee-wazee katika California, Marekani, walifurahi kuwa na mmoja kati ya wana wao katika utumishi wa wakati wote. Mwana huyo na mke wake walikuwa Hispania mama alipokufa. Washiriki wengine wa familia walionelea kwamba mipango ilihitajika kufanywa ili kumtunza baba. Kwa kuwa walikuwa na shughuli nyingi za kazi ya kimwili na kulea watoto, hawakuona kuwa ingewezekana kwao kuchukua daraka hilo. Badala yake, waliwahimiza sana wenzi waliokuwa katika utumishi wa pekee wa wakati wote warudi nyumbani kutunza baba. Hata hivyo, ingawa baba yao alikuwa na umri wa miaka 79, yeye alikuwa na afya nzuri, na pia maoni ya kiroho yaliyo hakika. Baada ya watu mbalimbali kuzungumza kwenye mkutano wa familia, huyo baba alisimama na kusema kwa uthabiti hivi: “Nataka warudi Hispania na kuendelea kuhubiri.” Walifanya hivyo, lakini walimsaidia pia kihalisi. Sasa wana mgawo wa kazi ya kuzunguka katika Hispania. Tangu walipofanya mkutano huo wa familia, washiriki wengine wa familia wameonyesha uthamini kwa yale ambayo hao wenzi wanaotumikia katika nchi za kigeni wanafanya. Baada ya miaka kadhaa, mmoja wa wale wana wengine alimpokea baba nyumbani mwake, akamtunza hadi alipokufa.

Huko Pennsylvania, Marekani, ndugu mtiwa-mafuta aliyekuwa amepainia kwa muda wa miaka 40, alikuwa mwenye umri wa miaka zaidi ya 90 mke wake alipopata kuwa mgonjwa sana na kufa. Mbali na kuwa na watoto wengi sana wa kiroho, alikuwa pia na mwana na binti watatu. Mmoja wa binti zake alikuwa amekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa miaka zaidi ya 40, akiwa ametumikia pamoja na mume wake akiwa mishonari, katika kazi ya kuzunguka, na kwenye Betheli. Alisaidia kufanya mipango ili utunzaji ufaao uweze kutolewa kwa baba yake. Ndugu wa huko pia walisaidia kumpeleka kwenye mikutano katika Jumba la Ufalme. Baadaye, baada ya mume wake kufa, alimwuliza baba yake kama alitaka aondoke Betheli ili kumtunza. Yeye huthamini sana mambo matakatifu, na alihisi kwamba mahitaji yake yangeweza kushughulikiwa katika njia nyinginezo. Kwa hiyo alijibu hivi: “Hilo ndilo jambo baya zaidi uwezalo kufanya, na lingekuwa jambo baya hata zaidi kama ningekuruhusu ulifanye.”

Makutaniko Yenye Kutegemeza

Makutaniko fulani yamekuwa yenye kusaidia sana katika kutunza wazazi wanaozeeka wa wale walio katika utumishi wa pekee wa wakati wote. Wao huwathamini hasa wale ambao wamejitoa kwa miaka mingi katika utumishi huo. Ingawa hayawezi kuwaondolea madaraka yao ya Kimaandiko, makutaniko hayo hufanya mengi kuwapunguzia mzigo vya kutosha ili watoto wasilazimike kuacha migawo yao ya pekee.

Wenzi fulani kutoka Ujerumani walikuwa katika mgawo wao wa nchi za kigeni kwa miaka 17 hivi, wakiutumia wakati huo mwingi katika kazi ya kuzunguka, mahitaji ya mama ya mume, aliyekuwa mzee-mzee, yalipoongezeka. Walitumia likizo yao kila mwaka kumsaidia. Pia majirani Mashahidi walitoa msaada wenye upendo. Kisha wakati fulani walipokuwa na mama ya mume akiwa katika hali mbaya, wazee wa kutaniko la huko walipanga kukutana na wenzi hao ambao ni watumishi wa wakati wote. Walifahamu vizuri yale ambayo wenzi hao walikuwa wakimfanyia mama yao kwa ukawaida. Walithamini pia utumishi wa pekee ambao wenzi hao walikuwa wakishiriki. Kwa hiyo wazee walieleza juu ya programu ya kumtunza mama iliyokuwa imependekezwa na kusema hivi: “Hamwezi kumtunza zaidi kuliko vile mnavyofanya; tutawasaidia ili kwamba mweze kuendelea katika mgawo wenu huko Hispania.” Wazee hao wameendelea kufanya hivyo kwa miaka saba iliyopita.

Vivyo hivyo, ndugu ambaye amekuwa akitumikia katika Senegal tangu mwaka wa 1967, alipokea utegemezo wenye upendo kutoka kwa kutaniko la mahali ambapo baba yake alikuwa. Kwa ushirikiano wa hiari wa mke wake mwenye upendo, huyo mume alisafiri peke yake kwenda Marekani kuwasaidia wazazi wake matatizo yalipozuka. Alilazimika kukaa huko kwa miezi kadhaa. Hali ilikuwa ngumu, lakini alipokuwa amefanya kadiri ya uwezo wake, kutaniko liliingilia na kumsaidia ili aweze kuendelea na utumishi wake wa mishonari. Kwa kipindi cha miaka 18, kutaniko liliandaa msaada wenye upendo katika njia nyingi, kwanza lilimsaidia baba (hata ingawa hakuwatambua kamwe wengi wao), kisha wakamsaidia mama. Je, kufanya hivyo kulimwondolea mwana huyo daraka? La; mara nyingi alisafiri kutoka Senegal na kutumia likizo yake kutoa msaada kadiri ambavyo angeweza. Lakini walio wengi katika kutaniko hilo walifurahi kujua kwamba walikuwa na fungu fulani katika kutegemeza wenzi waliofanya kazi kwa bidii huko Senegal wakiwa watumishi wa pekee wa wakati wote.

Yesu alisema kwamba wale walioacha vyote kwa ajili ya habari njema wangekuja kupata ndugu, dada, mama, na watoto mara mia. (Marko 10:29, 30) Jambo hilo ni kweli miongoni mwa watumishi wa Yehova. Wenzi ambao sasa wanatumikia katika Benin, Afrika Magharibi, walipata kuona jambo hilo katika njia ya pekee wakati ambapo Mashahidi wawili katika kutaniko la wazazi wao waliwaambia wasiwe na wasiwasi juu ya wazazi. Waliongeza kusema hivi: “Wazazi wenu ni wazazi wetu pia.”

Naam, tunaweza kuonyesha kwamba tunathamini sana mapendeleo ya utumishi mtakatifu katika njia nyingi. Je, kuna njia ambazo katika hizo unaweza kufanya hivyo kwa ukamili zaidi?

[Picha katika ukurasa wa 26]

Wamejitoa kwa utumishi wa pekee wa wakati wote

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki