“Kweli Itawaweka Nyinyi Huru”
“Nanyi mtajua kweli, na kweli itawaweka nyinyi huru.” Ndivyo alivyotangaza Yesu alipokuwa akifundisha umati katika hekalu huko Yerusalemu. (Yohana 8:32) Mitume wa Yesu wangeweza kutambua mara moja mafundisho ya Yesu kuwa kweli. Walikuwa wameona uthibitisho mwingi wa asili ya kimungu ya mwalimu wao.
HATA hivyo, leo huenda watu fulani wakaona ikiwa vigumu kuitambua kweli aliyosema Yesu. Kama ilivyokuwa katika siku za nabii Isaya, leo kuna wale “wasemao kwamba uovu ni wema, na kwamba wema ni uovu; watiao giza badala ya nuru, na nuru badala ya giza; watiao uchungu badala ya utamu, na utamu badala ya uchungu!” (Isaya 5:20) Kukiwa na kauli nyingi, falsafa, na mitindo-maisha yenye kuendelezwa siku hizi, watu wengi huhisi kwamba kila kitu hakitegemeki na kwamba hakuna kweli.
Yesu alipowaambia wasikilizaji wake kwamba kweli ingewaweka huru, waliitikia kwa kusema: “Sisi ni uzao wa Abrahamu nasi hatujapata kamwe kuwa watumwa wa yeyote. Ni jinsi gani wewe wasema, ‘Nyinyi mtakuwa huru’?” (Yohana 8:33) Hawakuhisi uhitaji wa yeyote kuwa huru au chochote kiwaweke huru. Kisha Yesu alielezea: “Kwa kweli kabisa mimi nawaambia, Kila mtendaji wa dhambi ni mtumwa wa dhambi.” (Yohana 8:34) Kweli ambayo Yesu alikuwa akizungumzia yaweza kufungua njia ya kupata uhuru kutoka katika dhambi. Yesu alisema hivi: “Mwana akiwaweka nyinyi huru, mtakuwa huru kikweli.” (Yohana 8:36) Kwa hiyo, kweli ambayo huweka watu huru ni kweli kuhusu Yesu Kristo, Mwana wa Mungu. Ni kwa imani katika dhabihu ya Yesu ya uhai mkamilifu wa kibinadamu ndipo yeyote anaweza kuwekwa huru kutoka katika dhambi na kifo.
Katika pindi nyingine Yesu alisema hivi: “Watakase kwa njia ya ile kweli; neno lako ni kweli.” (Yohana 17:17) Neno la Mungu laelezwa katika Biblia kuwa ile kweli iwezayo kuleta uhuru kutoka katika ushirikina na ibada isiyo ya kweli. Biblia inayo kweli kuhusu Yesu Kristo ambayo huongoza watu wawe na imani katika yeye na kufungua njia ya kupata tumaini la wakati ujao. Ni jambo zuri kama nini kuijua kweli ya Neno la Mungu!
Kujua kweli ni kwa maana kadiri gani? Dini nyingi leo, ijapokuwa zinadai kufuata Biblia, zimeathiriwa sana na falsafa na mapokeo. Mara nyingi, viongozi wa kidini huonekana wakihangaikia kukubaliwa kwao na watu kuliko kuhangaikia usahihi wa ujumbe wao. Wengine huhisi kwamba Mungu hutosheka na aina yoyote ya ibada, maadamu ni nyofu. Lakini Yesu Kristo alieleza hivi: “Saa inakuja, nayo ipo sasa, wakati waabudu wa kweli watakapomwabudu Baba kwa roho na kweli, kwa maana, kwa kweli, Baba anawatafuta wa namna hiyo wamwabudu yeye.”—Yohana 4:23.
Tukitaka kumwabudu Mungu kwa kukubalika, lazima tuijue kweli. Hilo ni suala la maana. Furaha yetu ya milele yaitegemea. Kwa hivyo, kila mtu apaswa kujiuliza: ‘Njia yangu ya ibada yakubalika kwa Mungu? Je, napendezwa kikweli na kujifunza kweli ya Neno la Mungu? Au naogopa kile ambacho uchunguzi wenye uangalifu waweza kufunua?’