Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 7/1 kur. 5-8
  • Kwa Nini Utafute Kweli?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kwa Nini Utafute Kweli?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Gharama ya Uhusianifu
  • Kweli Ni Nini?
  • Kweli Katika Matendo
  • Hazina Inayostahili Gharama Yoyote
  • Wakristo Huabudu kwa Roho na Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • “Nitatembea Katika Kweli Yako”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2018
  • Kumwiga Mungu wa Ukweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • ‘Endelea Kutembea Katika Kweli’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 7/1 kur. 5-8

Kwa Nini Utafute Kweli?

VIKUNDI vingi vya kidini hudai kuwa na kweli, nao hutolea wengine kweli hiyo kwa shauku. Hata hivyo, miongoni mwa vikundi hivyo mna “kweli” za kushangaza ajabu. Je, huo ni uthibitisho mwingine tu kwamba kweli zote ni husianifu, kwamba hakuna kweli kamili? La.

Katika kitabu chake The Art of Thinking, Profesa V. R. Ruggiero aeleza mshangao wake kwamba hata watu wenye akili nyakati nyingine husema kwamba kweli ni husianifu. Atoa sababu hivi: “Ikiwa kila mtu anafanyiza kweli yake mwenyewe, basi hakuna wazo la mtu mmoja liwezalo kuwa bora kuliko la mwingine. Ni lazima zote ziwe sawa. Na ikiwa mawazo yote ni sawa, basi kuna haja gani ya kufanya utafiti wa jambo lolote? Kwa nini kuchimba ardhi kutafuta majibu ya maswali ya kiakiolojia? Kwa nini kuchunguza visababishi vya ugomvi katika Mashariki ya Kati? Kwa nini kutafuta tiba ya kansa? Kwa nini kuchunguza thurea ya nyota? Utendaji huo mbalimbali wapatana na akili iwapo tu kuna majibu yaliyo bora kuliko mengine, ikiwa kweli ni kitu kilicho mbali na maoni ya mtu binafsi na hata haiathiriwi nayo.”

Hakika, hakuna mtu aaminiye kabisa kwamba hakuna kweli. Tunapofikiria mambo halisi yanayoonekana, kama vile tiba, hesabu, au sheria za fizikia, hata mshupavu mkubwa wa kuamini uhusianifu ataamini kwamba vitu fulani ni kweli. Ni nani kati yetu angethubutu kupanda ndege kama hatukufikiri kwamba sheria za elimu-mwendo ya hewani hazikuwa kweli kamili? Kweli zinazoweza kuthibitishwa ziko; zimetuzingira, nasi hutumainisha uhai wetu kwa kweli hizo.

Gharama ya Uhusianifu

Lakini, ni katika hali za kawaida ambapo makosa ya wazo la uhusianifu huonekana wazi zaidi, kwa sababu ni hapa ndipo fikira hizo zimetokeza madhara zaidi. The Encyclopedia Americana yataja jambo hili: “Imetiliwa shaka kabisa kama wanadamu wanaweza kupata ujuzi, au kweli ijulikanayo . . . Hata hivyo, ni hakika kwamba wakati wowote mawazo haya mawili ya kweli na ujuzi yanapokataliwa kuwa ndoto tu au yenye kudhuru, jamii ya kibinadamu huzorota.”

Labda umeona mzoroto huo. Kwa kielelezo, mafundisho ya adili ya Biblia, yasemayo wazi kwamba ukosefu wa adili katika ngono ni mbaya, huonwa nadra sana kuwa kweli. Maadili ya kutegemea hali—“amua kilicho bora kwako”—ndiyo yameenea sana. Je, kuna mtu ambaye angeweza kudai kwamba kuzorota kwa hali ya kijamii hakujatokezwa na mtazamo huu wa uhusianifu? Kwa kweli mweneo mkubwa ulimwenguni pote wa maradhi ya kupitishwa kingono, familia zilizovunjika, na mimba za matineja ni uthibitisho wa kutosha.

Kweli Ni Nini?

Basi, tuacheni maji haya machafu ya uhusianifu na tuchunguze kifupi yale Biblia hufafanua kuwa maji safi ya kweli. (Yohana 4:14; Ufunuo 22:17) Katika Biblia, kamwe “kweli” si jambo la kuwaziwa tu, lisiloonekana ambalo wanafalsafa hujadili.

Yesu aliposema kwamba kusudi lake lote maishani lilikuwa kusema juu ya kweli, alikuwa akisema juu ya jambo ambalo Wayahudi waaminifu walikuwa wamethamini kwa karne nyingi. Katika maandiko yao matakatifu, kwa muda mrefu Wayahudi walikuwa wamesoma “kweli” kuwa halisi, isiyowaziwa tu. Katika Biblia, “kweli” ni tafsiri ya neno la Kiebrania “ʼemethʹ,” linaloonyesha kile kilicho thabiti, imara, na, labda muhimu zaidi, chenye kutegemeka.

Wayahudi walikuwa na sababu nzuri ya kuona kweli kwa njia hiyo. Wao walimwita Mungu wao, Yehova, “Mungu wa kweli.” (Zaburi 31:5) Hii ni kwa sababu kila kitu Yehova alisema angefanya, alikifanya. Alipotoa ahadi, alizitimiza. Alipopulizia unabii, ulitimia. Alipotangaza hukumu za mwisho, zilitekelezwa. Mamilioni ya Waisraeli walikuwa wamejionea mambo hayo halisi. Waandikaji waliopuliziwa wa Biblia waliyarekodi yakiwa mambo hakika ya historia yasiyoweza kukanwa. Kinyume cha vitabu vingine vinavyoonwa kuwa vitakatifu, Biblia haijaandikwa kwa kutegemea ngano au hekaya. Inategemezwa kabisa na mambo hakika yawezayo kuthibitishwa—mambo halisi ya kihistoria, kiakiolojia, kisayansi, na kisosholojia. Si ajabu kwamba mtunga-zaburi asema hivi juu ya Yehova: “Sheria yako ni kweli. . . . Maagizo yako yote ni kweli. . . . Jumla ya neno lako ni kweli”!—Zaburi 119:142, 151, 160.

Yesu Kristo alirudia maneno ya zaburi hiyo aliposema katika sala kwa Yehova: “Neno lako ndiyo kweli.” (Yohana 17:17) Yesu alijua kwamba kila kitu Baba yake alisema kilikuwa hakika na chenye kutegemeka kabisa. Vivyo hivyo, Yesu ‘alijaa kweli.’ (Yohana 1:14) Wafuasi wake walijifunza kutokana na mambo waliyojionea, na kurekodiwa kwa wote, kwamba kila kitu alichosema kilikuwa chenye kutegemeka kama mwamba, kweli.a

Hata hivyo, Yesu alipomwambia Pilato kwamba alikuwa amekuja duniani kusema kweli, alimaanisha kweli fulani hususa. Yesu alitoa taarifa hiyo akiitikia swali la Pilato: “Wewe u mfalme?” (Yohana 18:37) Ufalme wa Mungu, na fungu la Yesu mwenyewe akiwa Mfalme, vilikuwa kichwa hasa, kiini, cha mafundisho ya Yesu alipokuwa duniani. (Luka 4:43) Jambo la kwamba Ufalme huu utatakasa jina la Yehova, utatetea enzi yake kuu, na kurudisha wanadamu waaminifu kwa uhai wa milele wenye furaha ndiyo “kweli” ambayo Wakristo wote wa kweli hutumaini. Kwa kuwa fungu la Yesu katika kutimiza ahadi zote za Mungu ni muhimu sana, na kwa kuwa ahadi zote za Mungu zimekuwa “Amina,” au kweli, kwa sababu yake, Yesu angeweza kusema hivi: “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima.”—Yohana 14:6; 2 Wakorintho 1:20; Ufunuo 3:14.

Kutambua kweli hii kuwa yenye kutegemeka kabisa ni muhimu sana kwa Wakristo leo. Yamaanisha kwamba imani yao katika Mungu na tumaini lao katika ahadi zake zinategemea mambo ya hakika, mambo halisi.

Kweli Katika Matendo

Haishangazi kwamba Biblia yalinganisha kweli na matendo. (1 Samweli 12:24; 1 Yohana 3:18) Kwa Wayahudi wenye kumhofu Mungu, kweli haikuwa jambo la kujadiliwa tu kifalsafa; ilikuwa njia ya maisha. Neno la Kiebrania la “kweli” laweza pia kumaanisha “uaminifu” nalo lilitumiwa kufafanua mtu ambaye angetumainika kutenda kupatana na neno lake. Yesu alifundisha wafuasi wake kuona kweli kwa mtazamo huo. Alishutumu sana unafiki wa Mafarisayo, lile pengo kubwa lililokuwa kati ya maneno yao ya kujiona kuwa waadilifu na matendo yao yasiyo ya uadilifu. Naye aliweka kielelezo kwa kuishi kwa kupatana na kweli alizofundisha.

Ndivyo inavyotakiwa kwa wafuasi wote wa Kristo. Kwao, kweli ya Neno la Mungu, zile habari njema za kuburudisha za Ufalme wa Mungu chini ya utawala wa Yesu Kristo, inamaanisha zaidi, zaidi sana ya kuwa habari tu. Kweli hiyo huwasukuma watende, huwashurutisha kuishi kulingana nayo na kuishiriki na wengine. (Linganisha Yeremia 20:9.) Kwa kutaniko la karne ya kwanza la Kikristo, njia ya maisha waliyochukua wakiwa wafuasi wa Kristo nyakati nyingine iliitwa tu “kweli” au “njia ya kweli.”—2 Yohana 4; 3 Yohana 4, 8; 2 Petro 2:2.

Hazina Inayostahili Gharama Yoyote

Ni kweli kwamba kukubali kweli za Neno la Mungu hutoza gharama fulani. Kwanza, kujifunza tu kweli kwaweza kuwa ono lenye kutamausha sana. The Encyclopedia Americana yasema: “Mara nyingi kweli haikubaliki, kwa sababu haiungi mkono ubaguzi au ngano.” Kuona itikadi zetu zikifunuliwa kuwa za uwongo kwaweza kuvunja moyo, hasa kama tulifundishwa na viongozi wa kidini wenye kutumainika. Watu wengine waweza kulinganisha ono hilo na hali ya kugundua kwamba kumbe wazazi tunaowatumaini walikuwa, kwa kweli, wahalifu wa siri. Lakini, je, kupata kweli za kidini si bora kuliko kuishi katika hali ya kudanganywa? Je, si afadhali kujua mambo ya hakika kuliko kuongozwa na uwongo?b—Linganisha Yohana 8:32; Warumi 3:4.

Pili, kuishi kwa kupatana na kweli ya kidini kwaweza kutugharimu ukubalifu wetu kwa baadhi ya waliokuwa marafiki wetu. Katika ulimwengu ambao wengi ‘wameibadili kweli ya Mungu kuwa uongo,’ wale hushikilia kabisa kweli ya Neno la Mungu huonekana kuwa wa ajabu sana na nyakati nyingine huepukwa au hueleweka vibaya.—Warumi 1:25; 1 Petro 4:4.

Lakini kweli inastahili gharama hizi mbili. Kujua kweli hutuweka huru kwa uwongo, madanganyo, na ushirikina. Na tukiishi kwa kupatana nayo, kweli hutuimarisha kuvumilia magumu. Kweli ya Mungu hutegemeka na ina msingi mzuri sana, nayo hutujaza sana tumaini, hivi kwamba hiyo hutusaidia kusimama imara chini ya jaribu lolote. Si ajabu kwamba mtume Paulo alifananisha kweli kwa mshipi mpana wa ngozi wenye nguvu ambao askari walikuwa wakivaa wakienda vitani!—Waefeso 6:13, 14.

Mithali ya Biblia yasema: “Inunue kweli, wala usiiuze; naam, hekima, na mafundisho, na ufahamu.” (Mithali 23:23) Kuipuuza kweli kuwa hali ya husianifu au kitu kisichokuwapo ni kukosa utimizo wenye kusisimua zaidi na wenye uradhi zaidi ambao mtu aweza kupata maishani. Kuipata ni kupata tumaini; kuijua na kuipenda ni kujua na kumpenda Muumba wa ulimwengu wote mzima na Mwana wake mzaliwa-pekee; kuishi kupatana nayo ni kuishi kwa kusudi na amani ya akili, sasa na milele.—Mithali 2:1-5; Zekaria 8:19; Yohana 17:3.

[Maelezo ya chinis]

a Kuna zaidi ya mahali 70 katika masimulizi ya Gospeli ambapo Yesu arekodiwa akitumia usemi wa kipekee ili kukazia ukweli wa maneno yake. Mara nyingi angesema “Amina” (“Kwa kweli,” New World Translation) ili kutanguliza sentensi. Neno la Kiebrania linalolingana na hilo lilimaanisha “hakika, kweli.” Yasema The New International Dictionary of New Testament Theology: “Kwa kutanguliza maneno yake kwa amina Yesu aliyataja kuwa hakika na yenye kutegemeka. Alishikamana nayo na kuyafanya yashikamane naye mwenyewe na wasikilizaji wake. Hayo ni wonyesho wa utukufu na mamlaka yake.”

b Neno la Kigiriki la “kweli,” a·leʹthei·a, latokana na neno limaanishalo “isiyofichwa,” kwa hiyo mara nyingi kweli huhusisha kufunuliwa kwa kile ambacho awali kilikuwa kimefichwa.—Linganisha Luka 12:2.

[Sandukupage 6]

Je, Kweli Hubadilika Wakati Wowote?

SWALI hilo lilizushwa na V. R. Ruggiero katika kitabu chake The Art of Thinking. Jibu lake ni la. Afafanua hivi: “Nyakati nyingine kweli huenda ikaonekana kama hubadilika, lakini ikichunguzwa kwa ukaribu zaidi itapatikana kwamba haijabadilika.”

“Fikiria,” yeye asema, “hali ya utungaji wa kitabu cha kwanza cha Biblia, kitabu cha Mwanzo. Kwa karne nyingi Wakristo na Wayahudi vilevile waliamini kwamba kitabu hicho kiliandikwa na mtu mmoja. Baada ya muda, maoni hayo yalitiliwa shaka, na hatimaye yakabadilishwa na itikadi kwamba watunga-vitabu wapatao watano walichangia kutunga Mwanzo. Kisha, katika 1981, matokeo ya uchanganuzi wa kilugha wa Mwanzo uliochukua miaka mitano ulichapishwa, ukisema kwamba kuna uwezekano wa asilimia 82 wa utungaji wa mtu mmoja, kama ilivyofikiriwa awali.

“Je, kweli kuhusu utungaji wa Mwanzo imebadilika? La. Ni itikadi yetu tu ndiyo imebadilika. . . . Kweli haitabadilishwa na ujuzi wetu au hali yetu ya kutojua mambo.”

[Sandukupage 7]

Staha Kuelekea Kweli

“STAHA kuelekea kweli si tu uchambuzi usio halisi wa enzi yetu unaojaribu ‘kufunua’ kila kitu, kwa itikadi ya kwamba hakuna mtu, na chochote, awezaye kudai kwa hakika kwamba ana kweli. Staha kuelekea kweli ni mtazamo unaochangamana na uhakika wenye shangwe kwamba hakika kweli yaweza kupatikana, pamoja na unyenyekeo wenye unyenyekevu kuelekea kweli wakati wowote na mahali popote. Kuwa na akili iliyofunguka hivyo kuhusu kweli ni takwa kwa wale ambao huabudu Mungu wa kweli; huku staha ifaayo kuelekea kweli ikihakikisha kwamba mtu ni mwenye kufuata haki anaposhughulika na jirani yake, katika usemi na matendo. Ni mtazamo huu, ambao tumeona, ambao Testamenti ya Kale na Testamenti Mpya hutoa ushuhuda juu yao.”—The New International Dictionary of New Testament Theology, Buku la 3, ukurasa 901.

[Picha katika ukurasa wa7]

Maendeleo ya kisayansi hutegemea kufunuliwa kwa kweli za kisayansi

[Picha katika ukurasa wa8]

Kweli hukubali Ufalme na baraka zawo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki