Kumwabudu Mungu Katika Kweli
Ili ibada ikubaliwe na Mungu, lazima itegemee kweli. (Yohana 4:23) Biblia hutambulisha waabudu wa kweli kuwa watu wa “kutaniko la Mungu aliye hai, nguzo na tegemezo la ile kweli.” (1 Timotheo 3:15) Wale wanaofanyiza kutaniko la Mungu hawaamini kweli ya Neno la Mungu tu bali pia wanaishi kupatana nayo na kuitetea, wakiijulisha kotekote duniani.—Mathayo 24:14; Waroma 10:9-15.
MASHAHIDI WA YEHOVA wanajulikana kwa kazi yao ya kufundisha Biblia, ambayo sasa yafanywa katika nchi zaidi ya 200. Wao hujifunza Biblia na kuifundisha kuwa kweli, bila kuiambatanisha na uvutano wa falsafa ya kibinadamu yenye kuidhoofisha. Je, wayafahamu mafundisho yao yenye kutegemea Biblia? Wengi husita kuwasikiliza Mashahidi wa Yehova kwa sababu ya habari zisizofaa ambazo huenezwa dhidi yao. Lakini watu wenye mioyo ya haki wanaalikwa wajiamulie wenyewe kama yale ambayo Mashahidi huhubiri ni kweli au si kweli. Uamuzi huo muhimu haupaswi kutegemea mambo ya kusikiwa tu. Wengi ambao wamefanya uchunguzi wao kibinafsi kuhusu mafundisho ya Mashahidi wa Yehova wamenufaika sana.
Ujuzi Kuhusu Kweli Huondoa Hofu
Kwa mfano, fikiria kisa cha Eugenia. Alilelewa katika nyumba iliyofuata Ukatoliki kwelikweli. Baba yake alikuwa mmoja wa wapangaji wa ziara ya kipapa katika Mexico mwaka wa 1979. Alipokuwa akitembelea marafiki, Eugenia alikutana na Mashahidi wa Yehova. Kwa msaada wao alianza kuchanganua kwa uangalifu yale ambayo Biblia husema. Yeye akumbuka hivi: “Mwanzoni, nilianza kupatwa na hofu nyingi. Nilikuwa nimeipata kweli! Lakini hiyo ilimaanisha kwamba itikadi zangu nyingi za awali zilikuwa zenye kosa. Familia yangu, marafiki wangu, watu niliowapenda—wote hao walikuwa wamekosea. Nilikuwa na wasiwasi. Niliendelea kujiuliza mwenyewe jinsi ambavyo familia yangu ingeitikia yale niliyokuwa nimetoka kuvumbua. Kadiri wakati ulivyopita na kwa msaada wa Yehova, nilianza kuzoea jambo hili lenye kulemea. Siku moja niliamua kufunua jambo hilo kwa rafiki wa familia, profesa wa theolojia. Nilimweleza tamaa yangu ya kupata kweli. Kisha akasema, ‘Ukitaka kujua kweli, tafuta Mashahidi wa Yehova.’”
Kama vile Eugenia alivyokuwa akihofu, familia yake ilimfukuza nyumbani. Hata hivyo, Mashahidi waliendelea kumpa msaada wa kiroho. Yeye aeleza hivi: “Niliimarishwa kuchukua msimamo kwa ajili ya kweli. Nilitambua kwamba ni jambo lililostahili kupiganiwa. Mwaliko niliopokea kutoka kwa Mashahidi wa Yehova ulikuwa wa maana sana. Nilihisi nimependwa katika kutaniko la Kikristo. Kuwa karibu na tengenezo la Mungu kulinisaidia kushinda hofu ya kuchukua msimamo kwa ajili ya kweli nikiwa peke yangu.”
Fikiria kielelezo kingine. Sabrina alikuwa amezoea kuwa na mazungumzo ya kawaida ya familia kuhusu Biblia. Kwa kweli, walikuwa wamesitawisha namna ya ‘dini ya familia.’ Alizoea kushirikiana na washiriki wa dini mbalimbali ili afichue makosa yao. Mmoja wa Mashahidi wa Yehova alipomtolea funzo la Biblia, alilikubali mara moja akiwa na kusudi la kukosoa itikadi zao. Yeye akumbuka: “Baada ya kujifunza kwa zaidi ya mwaka mmoja, nilihofu kupoteza ‘kweli yangu.’ Ilikuwa rahisi kwangu kufichua uwongo wa dini nyingi ambazo nilihusika nazo, lakini haikuwa rahisi wakati huu.”
Hofu ya Sabrina ilimfanya asiendelee kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Lakini akahisi akiwa mtupu kiroho. Aliamua kurudia funzo lake na hatimaye akakubali kweli hii mpya. Sabrina alifanya maendeleo hata kufikia hatua ya kutaka kushiriki na wengine yale aliyokuwa akijifunza. Hata aliomba kuandamana na Mashahidi katika huduma yao ya nyumba hadi nyumba. Sabrina aeleza: “Kabla ya kupokea kibali cha kuhubiri na Mashahidi wa Yehova, niliulizwa: ‘Je, kweli wataka kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova?’ ‘La!’ nikajibu. Hofu ilinijaa tena.” Mwishowe, baada ya kuendelea kuhudhuria mikutano yote na kuchunguza watu wa Mungu na jinsi walivyotumia kanuni za Biblia, Sabrina aliamua kwamba hiyo kwa kweli ilikuwa kweli. Alibatizwa na sasa yeye ni mweneza-evanjeli wa wakati wote.
Kwa Nini Ni Tofauti Hivyo?
Huenda mtu akauliza, ‘Kwa nini mafundisho ya Mashahidi wa Yehova ni tofauti sana na dini nyingine?’ Kutazama kifupi yale ambayo Mashahidi huitikadi kutakusaidia uone kwamba wao ni Wakristo wanyofu, wanafunzi wa Biblia wenye kudhamiria. Twakutia moyo utazame katika Biblia yako mwenyewe maandiko yaliyo katika muhtasari wa itikadi zao za msingi zilizoonyeshwa hapo juu.
Kwa kuchunguza kwa uangalifu yale ambayo Mashahidi wa Yehova huamini na jinsi wanavyoshikilia yale ambayo Biblia hufundisha, waweza kubarikiwa kuwa na uhuru ambao kweli hutoa. (Yohana 17:17) Hakuna sababu ya kuhofu kweli. Kumbuka ahadi ya Yesu: “Nanyi mtajua kweli, na kweli itawaweka nyinyi huru.”—Yohana 8:32.
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
BAADHI YA ITIKADI ZA MSINGI ZA MASHAHIDI WA YEHOVA
◯ Yehova ndiye Mungu mweza yote. Jina lake la kibinafsi lapatikana zaidi ya mara 7,000 katika hati-kunjo za awali zaidi za Biblia.—Zaburi 83:18.
◯ Yesu Kristo ni Mwana wa Mungu, aliyekuja duniani kutoa uhai wake kwa ajili ya wanadamu. (Yohana 3:16, 17) Mashahidi wa Yehova hufuata mafundisho ya Yesu Kristo kama yapatikanavyo katika zile Gospeli.
◯ Jina Mashahidi wa Yehova lategemea Isaya 43:10, ambalo husema: “Nyinyi ni Mashahidi wangu, asema BWANA [“Yehova,” NW].”
◯ Ufalme ambao watu husali juu yake katika ile sala “Baba yetu” ni serikali ya kimbingu ambayo hivi punde itaondoa kuteseka kote na maumivu katika ulimwengu na kuleta Paradiso ambayo Biblia huahidi.—Isaya 9:6, 7; Danieli 2:44; Mathayo 6:9, 10; Ufunuo 21:3, 4.
◯ Kila mtu afanyaye mapenzi ya Mungu ana fursa ya kufurahia baraka za Ufalme milele.—Yohana 17:3; 1 Yohana 2:17.
◯ Wakristo lazima warekebishe tabia yao kulingana na vile Biblia isemavyo. Lazima wajitahidi kuonyesha upendo kwa jirani zao.—Mathayo 22:39; Yohana 13:35; 1 Wakorintho 6:9, 10.
[Picha katika ukurasa wa 5]
Mashahidi wa Yehova hujulisha watu kweli ya Biblia katika nchi zaidi ya 200