Vijana ‘Wanaotumainia Yehova’
SI VIJANA pekee walio na uzuri, wala wazee-wazee pekee walio na hekima. (Linganisha Mithali 11:22; Mhubiri 10:1.) Badala ya hivyo, wale walio na uzuri udumuo na hekima ya kweli ni wale wanaomtumaini Yehova na ambao husema hivi kwa moyo wote juu yake: “Wewe ndiwe Mungu wangu.”—Zaburi 31:14; Mithali 9:10; 16:31.
Kotekote ulimwenguni kuna idadi yenye kuongezeka ya watu walio na uzuri, vijana na wazee pia, wanaoonyesha hekima yao kwa kumtumikia Mungu na kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. Kwa kielelezo fikiria Sabrina mwenye umri wa miaka minane.
Sabrina aishi Ujerumani na yuko katika darasa la pili. Yeye ni Shahidi wa Yehova wa kwanza kuhudhuria shule yake. Kwa kusikitisha, yeye alikuwa shabaha ya matukano ya wanashule wenzake mpaka ile siku ambayo mwalimu aliwaomba wanafunzi walete kitabu wapendacho zaidi darasani. Sabrina aliamua kuleta Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia. Usiku uliotangulia, alitayarisha vema kwa ajili ya somo hilo, ingawa alikuwa na wasiwasi. Kwa kuwa kulikuwa wanafunzi 26 darasani mwake, alijua kwamba huenda asiwe na wakati mwingi sana. Lakini alikuwa amepiga moyo konde kutoruhusu yeyote akatize utoaji wake na alikuwa na hakika kwamba Yehova angemsaidia. Kwenye siku iliyowekwa, mwalimu aliuliza ni nani aliyekuwa ameleta kitabu na angependa kuwa wa kwanza kukionyesha. Kwa kushangaza, ni Sabrina tu aliyekuwa ameleta kimoja. Alisimama mbele ya darasa akaanza kusema, kusoma, na kuonyesha picha kutoka kitabu hicho na kueleza kwamba kila jambo lilitegemea Biblia. Kwa kumalizia aliuliza hivi: “Ni nani angependezwa kuwa na kitabu hiki?” Alimpa mwalimu nakala moja, na katika siku chache zilizofuata, alitoa vitabu vingine kumi kwa baadhi ya wanadarasa wenzake. Elezo pekee la mwalimu juu ya utoaji wake lilikuwa: “Sijapata kamwe kuona jambo lolote kama hili.” Alimpa Sabrina maksi ya A kwa ajili ya kazi yake.
Kwa kweli, Mashahidi wengi wachanga ni wahubiri wenye furaha wa habari njema shuleni. Kielelezo kingine ni cha Erika, mhubiri mwenye umri wa miaka 11 katika Meksiko. Amefundishwa kumpenda Yehova tangu utotoni. Kazi yake ya shule ni yenye kutokeza. Mmojawapo migawo yake ulikuwa kutayarisha habari juu ya UKIMWI na uzoelevu wa tumbaku na kileo. Alitayarisha vema, akitumia gazeti Amkeni!, na alipokea maksi za juu kabisa. Mwalimu wake alimuuliza alikopata habari hiyo akapewa yale magazeti yaliyokuwa na makala juu ya habari hizo. Baadaye, mwalimu aliyatumia magazeti hayo ili kuzungumzia habari hizo na darasa nzima. Kwa sababu ya mwenendo wa Erika, staha yake kwa walimu wake, na maksi zake za juu, amestahili kupokea zawadi, diploma, na mitalaa anayogharimiwa nusu. Hata hivyo, yeye ahisi kwamba matimizo yake makubwa zaidi yamekuwa kwamba amejitambulisha mwenyewe kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, ameweza kuangusha fasihi ya Biblia, na amelitukuza jina la Mungu.
Kisha kuna Shannon, mvulana mwenye umri wa miaka kumi aishiye New Zealand. Ana jicho moja tu linaloona, lile jingine lilipatwa na kansa alipokuwa mtoto mchanga. Shannon alipokuwa na miaka saba, mama yake alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, muda mfupi tu baada ya yeye kuanza masomo yake ya Biblia, alianza kuishi pamoja na mwanamume bila kuolewa akaamua kukomesha mafunzo yake. Shannon alisihi kwamba funzo lake la Biblia liendelee. Aliruhusiwa. Mashahidi waliendelea kumtembelea, na hatimaye washiriki wote watatu wa nyumba hiyo walijifunza Biblia na kufanya maendeleo ya kiroho. Baada ya kuolewa kihalali, mamake Shannon na baba yake wa kambo walibatizwa.
Siku moja Shannon na mke wa mwangalizi wa mzunguko walikuwa katika utumishi wa shambani pamoja. Mwenye nyumba akamuuliza Shannon: “Ni nini kilichopata jicho lako?” “Lilipatwa na kansa, likalazimika liondolewe,” yeye akajibu. “Karibuni Yehova atanipa jipya katika Paradiso, na sisi tupo hapa kukuambia hivyo.”