Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w98 11/1 kur. 30-31
  • Yesu Alitumia Wakati Pamoja na Watoto

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yesu Alitumia Wakati Pamoja na Watoto
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Yesu Awakaribisha Watoto
  • Somo Kwetu
  • Je, Una “Akili ya Kristo”?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Watoto Wetu Ni Urithi Wenye Thamani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Je! Wewe Una Akili ya Kristo?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Wale Ambao Wakawa Wanafunzi wa Yesu
    Kumsikiliza Mwalimu Mkuu
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
w98 11/1 kur. 30-31

Walifanya Mapenzi ya Yehova

Yesu Alitumia Wakati Pamoja na Watoto

HUDUMA ya Yesu ya miaka mitatu na nusu ilikuwa ikikaribia kumalizika. Karibuni angeingia Yerusalemu na kufa kifo chenye maumivu makali. Alijua vizuri yale aliyotazamia, kwa kuwa alikuwa amewaambia wanafunzi wake hivi: “Mwana wa binadamu atapaswa kukabidhiwa mikononi mwa watu, nao watamuua, lakini, ijapokuwa atauawa, yeye atafufuliwa siku tatu baadaye.”—Marko 9:31.

Bila shaka, Yesu angependa kutumia vizuri iwezekanavyo kila siku, saa, na wakati uliobaki. Wanafunzi wake pia walihitaji kupewa uangalifu. Yesu alitambua kwamba bado walihitaji onyo kali kuhusu uhitaji wa kuwa wanyenyekevu na kuhusu ile hatari ya kujikwaa ambayo ipo sikuzote. (Marko 9:35-37, 42-48) Walihitaji pia maagizo kuhusu ndoa, talaka, na useja. (Mathayo 19:3-12) Akijua kwamba alikuwa afe karibuni, hapana shaka kwamba Yesu alizungumza na wanafunzi wake kihususa, akiwa na hisi ya uharaka. Wakati ulikuwa muhimu—jambo ambalo lilifanya kile Yesu alichofuata kufanya kiwe cha kutokeza hata zaidi.

Yesu Awakaribisha Watoto

Simulizi la Biblia lasema: “Watu wakaanza kumletea watoto wachanga ili awaguse.” Wanafunzi walipoona hilo, walilalamika mara moja. Labda walisababu kwamba Yesu alikuwa mtu wa maana sana au mwenye shughuli sana kuweza kujishughulisha na watoto. Basi wazia mshangao wa wanafunzi hao, Yesu alipowaghadhibikia! “Waacheni watoto wachanga waje kwangu,” akawaambia. “Msijaribu kuwakomesha, kwa maana ufalme wa Mungu ni wa walio kama hao.” Kisha Yesu akaongeza kusema: “Kwa kweli nawaambia nyinyi, Yeyote yule asiyeupokea ufalme wa Mungu kama mtoto mchanga hataingia kwa vyovyote ndani ya huo.”—Marko 10:13-15.

Yesu aliona sifa zenye kupendeza katika watoto. Kwa kawaida wao ni wadadisi na wenye kutumaini. Watakubali yale waambiwayo na wazazi wao na hata kuwatetea mbele ya watoto wengine. Hali yao ya kuwa tayari kusikiliza na kufundishwa yastahili kuigwa na wote wanaotaka kuingia katika Ufalme wa Mungu. Kama vile Yesu alivyosema, “ufalme wa Mungu ni wa walio kama hao.”—Linganisha Mathayo 18:1-5.

Lakini Yesu hakuwa akitumia watoto hao kwa ajili ya kutoa kielezi tu. Simulizi hilo ladhihirisha kwamba Yesu alipenda kikweli kuwa karibu nao. Marko aripoti kwamba Yesu “a[li]chukua watoto akawakumbatia na kuanza kuwabariki, akiweka mikono yake juu yao.” (Marko 10:16) Simulizi la Marko pekee ndilo hutia ndani ile habari changamfu kwamba Yesu “a[li]chukua watoto akawakumbatia.”a Hivyo, Yesu alifanya zaidi ya matarajio ya hao watu wazima, ambao waliwaleta watoto hao kwa Yesu ili aweze ‘kuwagusa’ tu.

Ilimaanisha nini kwa Yesu ‘kuweka mikono yake’ juu ya hao watoto? Hapa hakuna dokezo la sherehe ya kidini, kama vile ubatizo. Ingawa pindi fulani, kuwekelea mikono kulimaanisha kuteua katika wadhifa fulani, katika pindi nyinginezo kulimaanisha tu kubariki. (Mwanzo 48:14; Matendo 6:6) Kwa hiyo, huenda ikawa Yesu alikuwa tu akiwabariki watoto.

Kwa vyovyote, Marko atumia neno lenye nguvu zaidi kwa neno “baraka” (ka·teu·lo·geʹo), linalomaanisha nguvu nyingi. Hilo ladokeza kwamba Yesu aliwabariki watoto kwa hisia nyingi, kwa wororo, na uchangamshi. Kwa wazi, yeye hakuwaona watoto kuwa mzigo wenye kumpotezea wakati.

Somo Kwetu

Njia ya Yesu ya kushughulika na watoto na pia watu wazima haikuwa yenye kuogopesha wala kutweza. “Ni lazima awe alitabasamu kwa urahisi na kucheka kwa furaha,” chasema kitabu kimoja cha marejezo. Si ajabu kwamba watu wa umri wote walistarehe karibu naye. Tukifikiria kielelezo cha Yesu, twaweza kujiuliza, ‘Je, wengine huniona kuwa mtu mwenye kufikika?’ ‘Je, mimi huonekana kuwa mwenye shughuli mno nisiweze kujisumbua na shughuli na mahangaiko ya wengine?’ Kusitawisha upendezi wa moyo mweupe katika watu kutatusukuma tujitoe, kama vile Yesu alivyofanya. Wengine wataona upendezi wetu wa kweli nao watavutiwa nasi.—Mithali 11:25.

Kama vile simulizi la Marko lionyeshavyo, Yesu alifurahia kuwa pamoja na watoto. Kwa wazi, alichukua wakati kuwachunguza walipokuwa wakicheza, kwa maana alirejezea michezo yao katika kimojawapo cha vielezi vyake. (Mathayo 11:16-19) Labda baadhi ya watoto waliobarikiwa na Yesu walikuwa wachanga mno wasiweze kufahamu yeye alikuwa nani wala alifundisha nini. Lakini hilo halikumfanya ajihisi kwamba alikuwa akipoteza wakati wake. Alitumia wakati pamoja na watoto kwa sababu aliwapenda. Yaelekea, wengi wa watoto ambao Yesu alikutana nao wakati wa huduma yake, baadaye walisukumwa kuitikia upendo wake kwa kuwa wanafunzi wake.

Ikiwa Yesu alitumia wakati pamoja na watoto katika majuma ya mwisho muhimu ya uhai wake, bila shaka, tunaweza kutafuta wakati kwa ajili yao katika ratiba yetu yenye shughuli nyingi. Yatupasa hasa tuwafikirie wale walio na mahitaji ya pekee, kama vile wavulana na wasichana wasio na baba. Kwa kweli, watoto wote husitawi uangalifu unapotolewa kwao, naye Yehova hutamani kwamba tuwapende na kuwasaidia kadiri tuwezavyo.—Zaburi 10:14.

[Maelezo ya Chini]

a Tafsiri moja yasema kwamba Yesu “aliwapiga pambaja.” Nyingine yasema kwamba “aliwatia katika sehemu ya ndani ya mkono wake.”y

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki