Kuacha Ibada ya Maliki na Kuanza Ibada ya Kweli
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA ISAMU SUGIURA
Hata ingawa ilikuwa dhahiri katika 1945 kwamba Japani ilikuwa ikishindwa kwenye Vita ya Ulimwengu ya Pili, sisi tulikuwa na uhakika kwamba kamikaze (“upepo wa mungu”) ungevuma na kushinda adui. Kamikaze hurejezea zile dhoruba za 1274 na 1281 ambazo ziliharibu mara mbili nyingi za meli za Mongol zenye kuvamia karibu na pwani ya Japani, na hivyo kuzifanya ziondoke.
HIVYO, wakati Maliki Hirohito alipotangazia taifa katika Agosti 15, 1945 kwamba Japani ilikuwa imesalimu amri kwa Majeshi ya Muungano, matumaini ya watu milioni mia moja waliokuwa na ujitoaji kwake yalivunjwa. Wakati huo nilikuwa mvulana wa shule na matumaini yangu pia yalivunjwa. ‘Iwapo maliki siye Mungu aliye hai, nani ndiye?’ Nikajiuliza. ‘Nimtumaini nani?’
Ingawa hivyo, kwa kweli, kushindwa kwa Japani katika Vita ya Ulimwengu ya Pili, kulinifungulia njia, kutia na maelfu ya Wajapani wengine kujifunza juu ya Mungu wa kweli, Yehova. Kabla sijawaeleza mabadiliko niliyolazimika kufanya, acheni niwafahamishe malezi yangu ya kidini.
Mivutano ya Kidini ya Mapema
Nilizaliwa katika jiji la Nagoya Juni 16, 1932, nikiwa wa mwisho kati ya wavulana wanne. Baba alifanya kazi akiwa mkaguzi wa majengo ya jiji. Mama alikuwa mwamini mwenye kujitoa wa Tenrikyo, kidhehebu cha dini ya Shinto, na ndugu yangu mkubwa alikuwa amepata mazoezi ya kidini ili kuwa mwalimu wa kidhehebu hicho cha Tenrikyo. Mama nami tulikuwa na ukaribu hasa, naye aliandamana nami kwenda kwenye mahali tulipokutania kwa ajili ya ibada.
Nilifunzwa kuinamisha kichwa changu na kusali. Dini ya Tenrikyo ilinifundisha itikadi katika muumba aliyeitwa Tenri O no Mikoto, na pia katika miungu mingine midogo. Washiriki wake walizoea uponyaji wa imani na kukazia kutumikia wengine na kueneza itikadi zao.
Nilipokuwa kijana mdogo nilikuwa mwenye udadisi sana. Nilistaajabia mwezi na nyota zisizohesabika angani, nami nilijiuliza anga za juu zilienea umbali gani upande wa juu wa anga ya mawingu. Niliona kule kutazama ukuzi wa biringanya na matango ambayo nilipanda kwenye kisehemu kidogo nyuma ya nyumba, kuwa jambo lenye kuvutia. Kuchunguza kwa makini maumbile ya asili kulitia nguvu itikadi yangu katika Mungu.
Ile Miaka ya Vita
Miaka yangu kwenye shule ya msingi kuanzia 1939 hadi 1945 ililingana na kile kipindi cha Vita ya Ulimwengu ya Pili. Ibada ya Maliki, ambayo ni sehemu muhimu ya dini ya Shinto, ilikaziwa katika elimu ya shule zetu. Tulifundishwa shushin, ambayo ilihusisha mazoezi ya kimaadili yenye vidokezo vya kitaifa na kijeshi. Sherehe za kupandisha bendera, kuimba wimbo wa taifa, kujifunza kanuni za elimu za kimaliki, na kuipa heshima picha ya maliki, zote zilikuwa sehemu ya kawaida ya shule yetu.
Pia tulienda kwenye kihekalu cha dini ya Shinto cha mahali hapo ili kumwomba Mungu kwa bidii ili jeshi la kimaliki lishinde. Wawili wa ndugu zangu wa kimwili walitumikia katika jeshi. Kwa sababu ya mafundisho yangu ya utaifa na kidini, nilifurahia habari za ushindi wa jeshi la Japani.
Nagoya lilikuwa kitovu cha kiwanda cha ndege za Japani, hivyo, lilikuwa shabaha muhimu ya mashambulizi makubwa ya Majeshi ya Wana-Hewa wa Marekani. Wakati wa mchana, ndege aina ya B-29 za Kuangusha mabomu ziliruka juu ya mji uliokuwa ukikua, kutoka meta zipatazo 9,000, zikiangusha mamia ya tani ya mabomu juu ya wilaya zenye viwanda. Usiku kurunzi zingeweza kuangaza ndege hizo za kutupa mabomu zikiruka chini sana kufikia meta 1,300. Mashambulizi ya angani yenye kurudiwarudiwa kwa mabomu yenye kusababisha moto, yalifanyiza mioto mikubwa kwenye sehemu za makao ya watu. Nagoya peke yake ilipata mashambulizi 54 ya ndege wakati wa miezi tisa ya mwisho ya vita, ikitokeza kuteseka kwingi na vifo zaidi ya 7,700.
Kufikia wakati huu, kushambuliwa kwa mabomu kutoka kwenye meli za kivita, kulikuwa kumeanza dhidi ya majiji kumi ya pwani, na watu walikuwa wakizungumza juu ya uwezekano wa kutua kwa majeshi ya Marekani karibu na Tokyo. Wanawake na wavulana wachanga walizoezwa kupigana kwa mikuki iliyotengenezwa kwa mianzi ili kuilinda nchi. Shime yetu ilikuwa “Ichioku Sougyokusai” ikimaanisha “Afadhali kifo cha watu milioni 100 kuliko kusalimu amri.”
Katika Agosti 7, 1945, kichwa cha habari cha gazeti la habari fulani kiliripoti hivi: “Namna Mpya ya Bomu Yaangushwa Hiroshima.” Siku mbili baadaye, nyingine iliangushwa Nagasaki. Mabomu haya yalikuwa ya atomi, na baadaye tulielezwa kuwa yalikuwa yameua jumla ya watu zaidi ya 300,000 kwa pamoja. Kisha, katika Agosti 15, mwishoni mwa mazoezi ya kupiga hatua tukiwa na bunduki zetu za mbao, tulisikia hotuba ya maliki ambamo alitangaza kusalimu amri kwa Japani. Tulikuwa tumehakikishiwa kwamba tungeshinda, lakini sasa tulivunjika moyo sana!
Tumaini Jipya Latokea
Majeshi ya Marekani yalipoanza umilikaji, tulianza kukubali polepole uhakika wa kwamba Marekani ilikuwa imeshinda vita. Demokrasia ikaanzishwa Japani, kutia na katiba mpya ambayo ilitoa uhakikisho kamili wa uhuru wa ibada. Hali za maisha zikawa ngumu, chakula kikawa haba, na katika 1946 baba yangu akafa kutokana na utapiamlo.
Wakati uo huo, lugha ya Kiingereza ikaanza kufundishwa katika shule niliyokuwa nikisomea, na kituo cha radio cha NHK kikaanzisha kipindi cha mazungumzo ya Kiingereza. Kwa miaka mitano nilikisikiliza kipindi hiki chenye kupendwa na watu wengi nikiwa na vitabu vya mafundisho karibu. Jambo hili lilifanya niwaze juu ya kwenda Marekani siku moja. Kwa sababu ya kutamaushwa na dini za Shinto na Budha, nilianza kufikiri kwamba labda kweli juu ya Mungu ingeweza kupatikana katika dini za Magharibi.
Mapema katika Aprili, 1951, nilikutana na Grace Gregory, mishonari wa Watch Tower Society. Alikuwa amesimama mbele ya kituo cha garimoshi cha Nagoya akitolea watu nakala ya gazeti la Kiingereza la Mnara wa Mlinzi, na kijitabu katika lugha ya Kijapani chenye habari juu ya Biblia. Unyenyekevu wake katika kufanya kazi hii ulinivutia sana. Nilivichukua vichapo vyote viwili na mara moja nikakubali toleo lake la funzo la Biblia. Niliahidi kuja nyumbani kwake kwa ajili ya funzo la Biblia siku chache baadaye.
Nilipoketi kwenye garimoshi na kuanza kusoma Mnara wa Mlinzi, neno la kwanza nililoona kwenye makala ya kwanza, lilikuwa “Yehova.” Nilikuwa sijapata kuona jina hilo hapo awali. Sikutarajia kulipata kwenye kamusi ndogo ya Kiingereza na Kijapani niliyoibeba, lakini, kumbe lilikuwapo! “Yehova . . . , Mungu wa Biblia.” Sasa nilikuwa naanza kupata kujua juu ya Mungu wa Ukristo!
Kwenye ziara hiyo ya kwanza kwenye nyumba ya wamishonari, nilijifunza juu ya hotuba ya Biblia iliyokuwa itolewe majuma machache baadaye na Nathan H. Knorr, msimamizi wa wakati huo wa Watch Tower Bible and Tract Society. Alikuwa anazuru Japani pamoja na mwandishi wake Milton Henschel, na alikuwa aje Nagoya. Ijapokuwa ujuzi wangu wa Biblia ulikuwa mdogo, niliifurahia hotuba sana, kutia na ushirika pamoja na wamishonari na wengine waliohudhuria.
Kwa muda wa miezi miwili hivi, nilijua kutokana na kujifunza na Grace kweli za msingi juu ya Yehova, Yesu Kristo, fidia, Shetani Ibilisi, Harmagedoni, na dunia Paradiso. Habari njema za Ufalme ndiyo namna ya ujumbe hasa niliokuwa nikitafuta. Wakati uo huo, nilianza pia kuhudhuria mikutano ya kutaniko. Nilipenda hali yenye urafiki kwenye vikusanyiko hivi, ambapo wamishonari walichangamana kwa uhuru na Wajapani na kukalia tatami (mkeka uliofumwa kwa nyasi kavu) pamoja nasi.
Katika Oktoba 1951, mkusanyiko wa kwanza katika Japani ulifanywa kwenye Jumba la Umma la Nakanoshima katika jiji la Osaka. Kulikuwa na Mashahidi wasiozidi 300 katika Japani yote; na hata hivyo, watu karibu 300 walihudhuria mkusanyiko, kutia ndani wamishonari wapatao 50. Hata nilikuwa na sehemu ndogo kwenye programu. Niliyoona na kusikia yalinivutia sana hivi kwamba, siku iliyofuata niliazimia moyoni mwangu kumtumikia Yehova muda wote wa maisha yangu. Siku iliyofuata, nilibatizwa katika maji yaliyokuwa vuguvugu katika bafu moja ya umma iliyokuwa karibu na mahali hapo.
Shangwe ya Utumishi wa Painia
Nilitaka kuwa painia, kama waitwavyo wahudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova, lakini pia nilijihisi kuwa mwenye daraka la kusaidia kutegemeza jamaa yangu. Nilipojipa ujasiri wa kumwambia msimamizi wangu wa kazi tamaa yangu, nilishangazwa kumsikia akisema hivi: “Nitafurahi kushirikiana nawe ikiwa hilo litakufanya uwe mwenye furaha.” Niliweza kufanya kazi siku mbili pekee kwa juma, na bado niliweza kumsaidia mama yangu katika gharama za nyumbani. Kwa kweli, nilijihisi kama ndege aliyeachiliwa huru kutoka tunduni.
Hali zilipoendelea kuwa nafuu, nilianza kupainia Agosti 1, 1954, katika eneo fulani nyuma ya kituo cha Nagoya, hatua chache tu kutoka mahali nilipokutana na Grace kwa mara ya kwanza. Baada ya miezi kadhaa, nilipata mgawo wa kutumikia nikiwa painia wa kawaida katika Beppu, mji fulani katika kisiwa cha magharibi cha Kyushu. Tsutomu Miura alipewa mgawo wa kuwa mwenzi wangu.a Wakati huo, hakukuwa na makutaniko ya Mashahidi wa Yehova katika kisiwa chote, lakini sasa kuna mamia yayo, yaliyogawanywa katika mizunguko 22!
Mwonjo wa Kimbele wa Ulimwengu Mpya
Ndugu Knorr alipotembelea Japani tena katika Aprili 1956, aliniomba nisome kwa sauti mafungu machache kutoka gazeti la Mnara wa Mlinzi la Kiingereza. Sikuambiwa sababu, lakini miezi michache baadaye, nilipokea barua iliyonialika kuhudhuria darasa la 29 la shule ya mishonari ya Gileadi. Hivyo, katika Novemba mwaka huo, nilianza safari yenye kusisimua kuelekea Marekani ambayo ilitimiza ndoto yangu ya muda mrefu. Kuishi na kufanya kazi kwa miezi miwili pamoja na familia kubwa ya Betheli ya Brooklyn, kulitia imani yangu nguvu katika tengenezo la Yehova lionekanalo.
Katika Februari 1957, Ndugu Knorr alitupeleka kwa gari sisi wanafunzi watatu hadi kwenye majengo ya Shule ya Gileadi katika South Lansing, kaskazini mwa New York. Miezi mitano iliyofuata kwenye Shule ya Gileadi, nilipokuwa nikipokea maagizo kutoka kwa Neno la Yehova na kuishi katika mazingira yenye kupendeza pamoja na wanafunzi wenzangu, nilipata mwonjo wa kimbele wa dunia Paradiso. Kumi kati ya wanafunzi 103, mimi nikiwemo, tulipewa mgawo wa kwenda Japani.
Kuithamini Migawo Yangu
Kulikuwa na Mashahidi wapatao 860 katika Japani niliporudi katika Oktoba 1957. Nilipewa mgawo wa kazi ya kuzunguka nikiwa mwangalizi wa mzunguko, lakini kwanza nilipokea mazoezi ya siku chache ya kazi hiyo kutoka kwa Adrian Thompson katika Nagoya. Mzunguko wangu ulienea kutoka Shimizu, karibu na Mlima Fuji, hadi Kisiwa cha Shikoku na ulitia ndani miji mikubwa kama vile Kyoto, Osaka, Kobe, na Hiroshima.
Katika 1961, nilipewa mgawo wa kuwa mwangalizi wa wilaya. Mgawo huo ulihusisha kuzunguka kutoka kisiwa chenye theluji-theluji kaskazini mwa Hokkaido hadi kisiwa cha Okinawa ambacho kiko karibu na tropiki, na hata kufikia visiwa vya Ishigaki karibu na Taiwan, umbali wa karibu kilometa 3,000.
Kisha, katika 1963, nilialikwa kuhudhuria mtaala wa miezi kumi wa Shule ya Gileadi katika Betheli ya Brooklyn. Wakati wa mtaala huo, Ndugu Knorr alikazia umuhimu wa kuwa na mtazamo unaofaa kuelekea migawo. Alisema kwamba kusafisha vyoo ulikuwa mgawo muhimu, sawa tu na kufanya kazi ofisini. Alisema, ikiwa vyoo havingekuwa safi, familia nzima ya Betheli pamoja na kazi zao zingeathiriwa. Baadaye, sehemu ya kazi yangu katika Betheli ya Japani, ilikuwa kusafisha vyoo, nami nilikumbuka shauri hilo.
Baada ya kurudi Japani, nilipewa mgawo wa kazi ya kuzunguka. Miaka miwili hivi baadaye, katika 1966, nilimwoa Junko Iwasaki, painia wa pekee aliyetumikia katika mji wa Matsue. Lloyd Barry, msimamizi wa ofisi ya tawi katika Japani wakati huo, alitoa hotuba ya arusi yenye kuchangamsha moyo. Kisha Junko akajiunga nami katika kazi ya kuzunguka.
Migawo yetu ilibadilika katika 1968 nilipoitwa kwenye ofisi ya tawi katika Tokyo kufanya kazi ya utafsiri. Kwa sababu ya upungufu wa vyumba, nilisafiri kila siku kutoka eneo la Sumida, Tokyo, naye Junko alitumikia akiwa painia wa pekee pamoja na kutaniko la mahali hapo. Kufikia wakati huu, majengo ya ofisi ya tawi makubwa kidogo yalihitajiwa. Hivyo, katika 1970, uwanja ulinunuliwa katika Numazu karibu na Mlima Fuji. Hapo, kiwanda chenye orofa tatu pamoja na nyumba ya makazi zilijengwa. Kabla ya ujenzi kuanza, nyumba kadhaa kwenye uwanja huo zilitumiwa kufanyia Shule ya Huduma ya Ufalme, ambayo huandaa mazoezi kwa waangalizi wa kutaniko. Nilipata pendeleo la kufundisha shule hiyo, naye Junko alitayarisha milo kwa ajili ya wanafunzi. Ilisisimua kuona mamia ya wanaume Wakristo wakipewa mazoezi ya pekee kwa ajili ya huduma.
Alasiri moja, nilipokea telegramu ya dharura. Mama alikuwa amelazwa hospitalini na hakutazamiwa kuishi. Nilisafiri kwa garimoshi yenye mwendo wa kasi hadi Nagoya, na kuharakisha kwenda hospitalini. Hakuwa na fahamu, lakini nilikaa usiku kucha kando ya kitanda chake. Mama alikufa mapema asubuhi. Nikiwa garini kurudi Numazu, nilishindwa kujizuia kulia nilipokumbuka nyakati ngumu alizokuwa amekabili muda wa maisha yake, na shauku aliyokuwa nayo kwangu. Ikiwa ni mapenzi ya Yehova, nitamwona tena katika ufufuo.
Punde si punde, tuliongezeka tukawa wengi zaidi kuweza kutoshea majengo ya Betheli katika Numazu. Hivyo, ekari 18 za ardhi zilinunuliwa katika Jiji la Ebina, na ujenzi wa ofisi mpya ya tawi ukaanza katika 1978. Sasa nafasi yote iliyopo katika uwanja huu imefunikwa na majengo ya makazi na kiwanda, kutia na Jumba la Mkusanyiko linalotoshea watu zaidi ya 2,800. Nyongeza ya mwisho, inayotia ndani majengo mawili ya makazi yenye orofa 13 na jengo la utumishi na kuegeshea magari lenye sehemu 5, ilimalizika mwanzoni mwa mwaka huu. Familia yetu ya Betheli sasa imefikia washiriki 530, lakini majengo yaliyopanuliwa yataturuhusu kuwapa makao washiriki wapatao 900.
Sababu Nyingi za Kufurahi
Imesisimua kuona unabii wa Biblia ukitimizwa, ndiyo, kuona ‘mnyonge akikua kufikia taifa hodari.’ (Isaya 60:22) Nakumbuka mmoja wa ndugu zangu akiniuliza huko nyuma katika 1951, “Kuna Mashahidi wangapi Japani?”
“Karibu 260,” nikajibu.
“Je, ni hao tu?” akauliza kwa sauti yenye kudunisha.
Nakumbuka nikiwaza, ‘Kupita kwa wakati kutaonyesha ni watu wangapi Yehova atawaleta kwenye ibada yake katika nchi hii ya dini za Budha na Shinto.’ Naye Yehova ametoa jibu! Leo, hakuna maeneo yoyote ya kuhubiriwa katika Japani yasiyogawiwa mtu, na idadi ya waabudu wa kweli imeongezeka kufikia zaidi ya 222,000 katika makutaniko 3,800!
Miaka 44 iliyopita ya maisha yangu katika huduma ya wakati wote—32 pamoja na mke wangu mpendwa—imekuwa hasa yenye furaha. Kwa miaka 25 kati ya hiyo nimetumikia katika Idara ya Utafsiri katika Betheli. Katika Septemba 1979, nilialikwa pia kuwa mshiriki wa halmashauri ya ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika Japani.
Limekuwa pendeleo na baraka kushiriki fungu dogo katika kusaidia watu wenye mioyo myeupe, wapenda amani waje kwenye ibada ya Yehova. Wengi wamefanya sawa na nilivyofanya—kubadilika kuacha kumpa maliki ujitoaji, na kuanza kuabudu Mungu wa pekee wa kweli, Yehova. Ni tamaa yangu ya moyo mweupe kusaidia wengi zaidi waje upande wa Yehova wa ushindi, na kupata uhai usiokoma katika ulimwengu mpya wenye amani.—Ufunuo 22:17.
[Maelezo ya Chini]
a Baba yake alikuwa Shahidi mwaminifu aliyeokoka mlipuko wa bomu wa Hiroshima katika 1945 akiwa katika gereza la Japani. Ona Amkeni! ya Oktoba 8, 1994 ukurasa wa 11-15.
[Picha katika ukurasa wa 29]
Elimu ya shule ilikazia ibada ya maliki
[Hisani]
The Mainichi Newspapers
[Picha katika ukurasa wa 29]
Nikiwa New York na Ndugu Franz
[Picha katika ukurasa wa 29]
Nikiwa na mke wangu, Junko
[Picha katika ukurasa wa 31]
Nikiwa kazini katika Idara ya Utafsiri