Yehova Haachi Watumishi Wake
Kama ilivyosimuliwa na Matsue Ishii
KWA karibu mwaka mmoja, mimi nilikuwa nimekuwa katika uzuizi wa kufungiwa peke yangu katika kijumba kidogo sana cha gereza, kilicho kichafu na chenye viroboto, katika Sendai, Japani. Kwa muda wote huo, sikuruhusiwa kuoga kwa kujinyunyizia maji au kwa kuingia katika josho la kuogea. Mnofu wangu ulikuwa na vidonda, ukiwa umeliwa na kunguni. Nilisumbuliwa sana na baridi yabisi hivi kwamba sikuweza kuketi wala kusimama. Nikiwa nimebaki ngozi iliyoshikana na mifupa na mwenye kilogramu 30 tu, nilikuwa karibu kufa.
Lakini kwa sababu gani mimi nilikuwa huko? Kwa sababu gani wenye mamlaka walikuwa wamegonga mlango wangu kwa fujo saa kumi na moja ya alfajiri, Juni 21, 1939, na kunikamata? Nilikuwa nimefanya nini? Hizo zilikuwa nyakati zenye magumu katika Japani karibu miaka 50 iliyopita. Acha nikuambie juu yazo na juu ya hali zilizoniingiza katika gereza na jinsi nilivyookoka.
Maisha Yangu ya Mapema
Mimi nilizaliwa katika 1909 katika Jiji la Kure, Japani, kilometa 25 tu kutoka Hiroshima. Wazazi wangu waliendesha duka la kuuzia mchele na duka la mavazi ya kimono. Nilipokuwa na umri wa miaka tisa, yale mafua makali ya Kihispania yalikumba eneo letu, na baada ya muda mfupi majeneza yenye miili mifu yakarundikana kuzunguka jengo la kuchomea maiti. Dada yangu mkubwa na mimi tulipatwa na ugonjwa huo, na juma moja baadaye yeye akafa. Alipokufa kwa ghafula, mimi nilianza kushangaa nikitaka kujua: ‘Kwa nini watu hufa? Ni jambo gani huwapata wakifa?’
Baba alikuwa mfuasi mwenye juhudi wa Buddha, na ili nipate jibu, nilizuru mahekalu mbalimbali ya wafuasi wa Buddha. Nilikuwa nikiuliza watawa-waume wa huko: “Kwa nini watu wanakufa?”
“Si lazima ufikirie mambo kama hayo,” wao wakawa wakijibu. “Wewe ukiendelea kutegemea Buddha na kuimba-imba mantra (sala) zako, utakuwa na uhakika na kufikia Nirvana na kuingia paradiso.”
Nilipokuwa na umri wa miaka 17, nilipata habari juu ya kitabu kimoja kinachoitwa Biblia. Nilijipatia kimoja lakini sikuweza kukielewa. Baadaye nilianza kuhudhuria kanisa moja “la Kikristo” katika Jiji la Kure. Niliposikia kwamba kifo cha mwanadamu ni tokeo la dhambi ya Adamu, hilo lilisikika kuwa jambo la kiakili, nami nikawa mshiriki wa kanisa mwenye juhudi.
Wakati huo oni lililotajwa mara nyingi katika miji ya mashambani lilikuwa: “Dini ya Yaso [ya Kikristo] itaharibu nchi.” Kwa kuwa mimi ndimi niliyekuwa “Mkristo” wa kwanza mwenye juhudi katika eneo letu, wanamji walinishtakia kuleta aibu juu ya mji na karibu wanishurutishe niende zangu. Wazazi wangu walichukizwa sana nami.
Kujifunza Ukweli wa Biblia
Katika jitihada ya kunifanya niache imani yangu, Baba alinipangia kuolewa na mtu nisiyekuwa nimemjua hata kidogo,. Jizo Ishii, mfuasi wa Buddha mwenye juhudi. Ndugu yake mkubwa alikuwa mmoja wa wakuu wa makuhani wa hekalu moja la wafuasi wa Buddha. Mimi niliambiwa kwamba ingawa Jizo hakuwa Mkristo, yeye angeonyesha uelewevu juu ya imani yangu. Kwa hiyo nilihamia Osaka na nikiwa na umri wa miaka 19 nikaolewa na Jizo, aliyekuwa mshona-kwa-cherehani. Lakini tofauti na vile baba alivyokuwa amesema, Jizo hakutaka kuniruhusu nihudhurie kanisa.
Upande wa nyuma wa nyumba yetu katika Tojocho, Osaka, kulikuwa na nyumba iliyokuwa na ishara: “Tawi la Osaka la Shirika la Wanafunzi wa Biblia wa Kimataifa.” Kwa kujichukulia kwamba kilikuwa ni kikundi cha Kikristo, mimi nilizuru nyumba ile.
“Je! ninyi mnaitikadi katika kuja kwa pili kwa Bwana?” nikamuuliza mwanamume kijana aliyekuja mlangoni.
“Kuja kwa pili kwa Kristo kulitukia katika 1914,” yeye akajibu.
Kwa kugutuka, nikamwambia haiwezekani. “Inakupasa usome kitabu hiki,” yeye akasema, akinipokeza The Harp of God.
Ili kuzuia mume wangu asione kitabu hicho, nilikificha katika gunia lenye makaa lililotengenezwa kwa manyasi, nami nikakisoma wakati wote wote ambapo ningeweza. Kila uhakika uliotajwa ulinipiga kama radi—ni 144,000 peke yao watakaoenda mbinguni; Kristo si sehemu ya Utatu bali ndiye Mwana mzaliwa-pekee wa Yehova, yule Mungu mweza yote; sisi tunaishi katika wakati wa mwisho; na ile mafua kali ya Kihispania iliyoua dada yangu ilikuwa sehemu ya utimizo wa unabii wa Biblia. Nilisadiki kwamba huu ndio ukweli niliokuwa nimekuwa nikiutafuta.
Mwishowe, mume wangu aligundua kwamba nilikuwa nikisoma kitabu fulani cha Kikristo. Hata hivyo, nilipochukua msimamo thabiti kwa ajili ya imani yangu, yeye alianza kushangaa kama kuna jambo fulani la maana sana lililohusika na kwa hiyo akajisomea mwenyewe The Harp of God. Mimi nilibatizwa mwaka uliofuata, Machi 23, 1929, na mume wangu akabatizwa muda mfupi baada ya hapo.
Kutumikia Tukiwa Makolpota
Sisi tulifunga duka la ushonaji na tukawaondoa kazini waajiriwa. Tukiwa tumejawa na shangwe, tulijiondokea kwenda katika utendaji wa kuhubiri mlango kwa mlango katika Osaka. Katika Septemba 1929, mimi nikawa kolpota wa pili wa Japani, kama walivyoitwa wahudumu wa wakati wote wakati huo, na mume wangu akajiunga na hesabu za makolpota baadaye. Tukiwa pamoja tulifanya kazi robo tatu za Japani, kutia na Osaka, Kyoto, Nagoya Tokyo, Sendai, Sapporo, Okayama, na kisiwa cha Shikoku. Tulikaa kila mahali kwa miezi inayopata sita, tukikodi chumba fulani na kukaza fikira juu ya ugawaji vitabu.
Tulitumia vitabu vilivyopatikana katika Kijapani, kama The Harp of God, Deliverance Creation, Reconciliation, na Government, na pia The Golden Age (sasa Amkeni!) na Mnara wa Mlinzi. Tukiwa makolpota, tulitumia saa 180 kwa mwezi tukienda mlango kwa mlango. Ingawa sisi tulichoka sana kimwili, shangwe yetu katika kutumikia ilikuwa kubwa.
Siku hizo makolpota wa Japani hawakurudishiwa gharama zao lakini walipokea nusu ya pesa zilizotokana na maangusho ya vitabu ili wazitumie kwa gharama za maisha. Maisha hayakuwa rahisi. Kolpota mwenzetu aliuawa na ugonjwa wa kuhara damu. Nilipokuwa nikimuuguza mgonjwa huyo, mimi pia nilipatwa na ugonjwa huo na kulazwa hospitali. Tulipotumikia katika Nagoya, moto uliwaka kwenye nyumba jirani ya mahali tulipokuwa tukiishi. Sisi tulikimbia kwa kushuka vidato vya ngazi kutoka sakafu ya pili tukiwa na mavazi yale tu tuliyokuwa nayo, tukapona chupuchupu. Mali chache tulizokuwa nazo na vitabu vyetu vya ugawaji viliteketea vyote vikapaa juu vikiwa moshi mtupu, nasi tukabaki bila ndururu.
Tulipokuwa tukitumikia katika Okayama, joto la mwili wa mume wangu lilipanda sana kwa siku kadhaa, naye akapimwa na kusemwa kuwa mwenye kifua kikuu chenye kuathiri mapafu. Kwa kawaida kifua kikuu ulikuwa ugonjwa wa kufisha wakati huo. Ikiwa kifo kilikuwa kisichoepukika, sisi tulitaka kwenda Sapporo katika kisiwa cha kaskazini kabisa, Hokkaido, tukatoe ushuhuda mahali ambako kazi ya kuhubiri haikuwa imefanywa kamwe.
Katika Septemba 1930, tulihamia Hokkaido, ambako mimi nilitazamia mume wangu afe. Hapa hewa ilikuwa safi, maziwa na viazi havikuwa ghali, na afya ya mume wangu ikawa nafuu pole kwa pole. Yehova hakutuacha kamwe bali alitubariki kwa shangwe kubwa sana katika huduma yetu.
Sisi tulipofanya kazi katika Sendai kwa mara ya kwanza, Bw. Inoue, msimamizi wa Tohoku Imperial University, alinifanyia mahoji ya kibinafsi. Yeye alikubali vitabu nilivyokuwa navyo kisha akanisindikiza kwenye mwingilio. Nilipokuwa nikitoa ushuhuda mlango kwa mlango, nilimkuta pia Bansui Doi, mwanamume mwenye sifa ya fasihi, aliyetafsiri vitabu Iliad na Odyssey vya Homer katika Kijapani. Yeye alikubali kitabu Creation.
Miongoni mwa wapokeaji wenye uthamini wa ujumbe wetu ilikuwamo jamaa ya Miura kutoka Ishinomori. Hagino, yule mke, alikuwa na umri wa miaka 17 alipozuru maskani yetu katika Sendai. Baada ya kutumia usiku ule tukizungumzia Biblia, yeye alisadiki sisi ndio wenye ukweli. Baada ya muda mfupi jamaa nzima ilihamia Tokyo, ambako Hagino na mume wake, Katsuo, walitumikia wakiwa makolpota. Katsuo alikufa akiwa Shahidi mwaminifu, na Hagino angali anatumikia kwa uaminifu. Tsutomu, mwana wao, amekuwa mtafsiri kwenye tawi la Japani la Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi kwa miaka mingi.
Utumishi wa Muda wa Betheli
Katika miaka ya 1930 mume wangu na mimi tulikuwa tukitumikia miezi michache kila mwaka katika Betheli iliyokuwa katika Ogikubo, Tokyo. Wakati huo, kulikuwako wafanya kazi wapatao 20. Mashine mbili zenye makelele zilichapa The Golden Age. Jizo na mimi tulifanya kazi katika Idara ya Nguo. Wakati wa badiliko la majira, makolpota walikuwa wakipeleka Betheli nguo zilizoraruka. Sisi tulizifua, tukazishona, na kuzipiga pasi kisha tukazipeleka ziwarudie. Hata tuliwashonea makolpota nguo mpya. Kazi hiyo ilipomalizwa, sisi wenyewe tulikuwa tukirudia ukolpota wetu.
Moja la mambo ninayothamini sana kukumbuka juu ya Betheli lilihusiana na mkusanyiko ule wa kihistoria katika Columbus, Ohio, U.S.A., katika 1931. Ndugu mmoja alikuwa ameunganisha-unganisha redio moja ya shotiwevu ili kupokea matangazo ya nchi za nje. Kwa kuzungusha-zungusha kile kidude cha kunasa sauti mchana kuchwa na usiku kucha, sisi tulijaribu sana kuinasa programu ya mkusanyiko. Usiku wa manane, sauti ya msimamizi wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi, J. F. Rutherford ikatokea kwa kani zote. Mara hiyo ndugu mmoja akaanza kutafsiri. Hivyo sisi tulisikia lile azimio la kukubali lile jina jipya, “Mashahidi wa Yehova,” na ule ushangiliaji mwingi wa kulikubali. Tukiwa huko mbali katika Betheli ya Japani, sisi tukapaliza sauti ya shangwe kwa upatano na ndugu zetu katika Amerika. Dakika chache baadaye, mapokezi ya redio yalififia, na hakuna zaidi lililosikiwa. Lakini Yehova aliruhusu sisi tuwe sehemu ya kitambo hicho cha kihistoria.
Kutoa Ushuhuda Kujapokuwa na Upinzani
Wakati wa ule mshuko wa kiuchumi ulimwenguni pote baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, upepo wa kisulisuli cha utukuzo wa taifa na uanajeshi ulikumba Japani. Mmaliki alionwa kuwa ndiye mungu aliye hai aliyepasa kupewa ukamilifu wa raia wote. Lakini sisi tulikuwa tukiwaambia watu: “Kuna Mungu mmoja tu.”
“Ninyi mnasema kwamba mmaliki si Mungu?” wao wakawa wakijibu.
“Kuna wakati ujao ulio mzuri ajabu utakaoletwa na Ufalme wa Mungu,” sisi tukawa tukieleza.
“Ninyi mwataka utawala tofauti na ule wa mmaliki?” wao wakawa wakiuliza. Lo lote tulilosema, maneno yetu yalipindwa nasi tukaitwa wasaliti. Wenye mamlaka walizidisha sana jitihada zao za kuchunguza vitabu vyetu, na kufuatwa-kufuatwa kwetu na makachero kukaongezeka.
Kwa kawaida hotuba ya watu wote ilifanywa mara moja kwa mwaka. Hata ingawa tulikuwa na Mashahidi wapatao 20 katika Tokyo, watu wapatao 500 walihudhuria hotuba “Anguko la Mwerevuko wa Kikristo” katika Jumba la Watu Wote jijini Yodobashi. Polisi walimzunguka msemaji jukwaani, na ikiwa yeye alisema jambo lo lote ambalo wao waliliona kuwa lenye kukatalika, sauti ilikuwa ikivuma kusema, “We msemaji, wacha!” Hapo msemaji alikuwa akirejeza kwa nadhari kwenye andiko fulani na kulisoma. Kwa kuwa Biblia haikupigwa marufuku, aliruhusiwa kuendelea.
Kukamatwa na Kutiwa Gerezani
Takriban miaka kumi baada ya sisi kuanza ukolpota, ukamataji wa jumla wa Mashahidi wa Yehova ulitukia katika Japani. Asubuhi ile yenye balaa ya Juni 21, 1939, mimi nilipelekwa kituo cha polisi katika Ishinomaki na kutupwa ndani ya chumba cha uzuizi chenye giza, kilichokuwa na masizi yakining’inia kwenye dari. Baada ya muda mfupi nilihamishwa nikapelekwa Sendai na kutiwa katika uzuizi wa kufungiwa peke yangu. Mume wangu alikamatwa pia, nami nikapoteza mawasiliano yote pamoja naye mpaka baada ya vita.
Nililala katika kijumba hicho kichafu takriban mwaka mmoja na karibu nife. Baadaye nilipata habari kwamba wakati wa kipindi hicho wenye mamlaka walikuwa wakiendesha uchunguzi juu ya Junzo Akashi, mwangalizi wa tawi la Japani. Hatimaye, mimi nikaanza kuulizwa-ulizwa maswali. “Gongesha Biblia sakafuni na ukanyagishe mguu juu yayo,” akaagiza mchunguzi mwenye kutukana. Ndipo yeye akanionyesha kumbukumbu ya maandishi kuhusu kuchunguzwa kwa Akashi. Kwanza nilifikiri kilikuwa kiini-macho.
“Wewe unaitikadi katika Akashi?” akaniswali muulizaji yule.
“Akashi ni mwanadamu tu asiyekamilika,” nikajibu. “Kwa muda ambao Akashi alifuata kanuni za Biblia, Akashi alitumiwa akiwa mtumishi wa Mungu. Lakini kwa kuwa taarifa zake zimekengeuka kuacha Biblia, yeye si ndugu yangu tena.” Wee-we, Akashi alikuwa kweli ameuacha ukweli!
Mwishowe, hukumu ilitolewa, nami nikafungiwa katika Gereza la Wanawake la Sendai. Nilitiwa tena katika uzuizi wa kufungiwa peke yangu. Vyakula viliandaliwa, ingawa haba. Kwa dakika 30 kila asubuhi, niliruhusiwa kutembea kidogo nikiwa chini ya uchunguzi wa mlinzi mwanamke. Wakati mmoja mlinzi mmoja aliniambia: “Kama nyakati zingalikuwa nafuu, wewe ungaliweza kutufundisha. Kwa kuwa nyakati ni mbaya, tafadhali subiri.” Nilitiwa moyo na maneno yake.
Wakati huo, Japani ilijitumbukiza ndani ya vita pamoja na United States, na jambo hilo likawa ndilo tamasha ya ulimwengu. Kuelekea mwisho wa 1944, miaka mitano na nusu baada ya kukamatwa kwangu, mimi niliachiliwa. Katika Agosti 1945 makombora ya atomi yaliangushwa juu ya Hiroshima na Nagasaki, na Japani ikashindwa vita.
Kutoka Gizani Kuingia Nuruni
Mume wangu na mimi tulirudia Jiji la Kure na tulichakura-chakura riziki yetu katika machafuko hayo ya baada ya vita kwa kuendesha duka la ushonaji-cherehani. Waandamani wa zamani walikuwa wametawanyika, nasi tulipoteza takriban mawasiliano yote nao. Hata hivyo, yapata miaka minne baada ya vita, tulisikia kwamba wamisionari walikuwa wanakuja kutoka United States, na kazi ya Ufalme ingefunguliwa upya katika Japani.
Akiambatana na mwana wetu wa miaka sita tuliyekuwa tumemchukua baada ya vita ili awe wetu kimalezi, mume wangu alihudhuria kusanyiko la kwanza la baada ya vita, lililofanywa katika Tarumi, Kobe. Liliendelea kuanzia mwisho wa Desemba 1949 mpaka ndani ya mwaka mpya wa 1950. Tangu 1939 kazi ya Ufalme katika Japani ilikuwa imeona ‘muda wenye giza,’ lakini hatimaye sisi tukawa tunahamishwa kuingia nuruni!
Katika 1951 tulisikia kwamba Nathan H. Knorr, aliyekuwa wakati huo msimamizi wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi, aliratibiwa kuzuru Japani, lakini hatukujua tarehe. Siku ya Aprili 27, 1951, tulipokuwa tukishona nguo mpaka usiku wa manane, tulisikia habari za redio zilizo hatima ya siku. “Bw. N. H. Knorr, msimamizi wa Mnara wa Mlinzi, atazuru Japani na kutoa hotuba kwenye Jumba Kubwa la Kyoritsu,” mtangazaji akasema. Kesho yake nikapanda gari-moshi nikasafiri zile kilometa 900 kwenda Tokyo katikati ya umaskini wenye machafuko ya baada ya vita. Siku ya Aprili 29, nilikuwa nimeketi nikisikiliza Ndugu Knorr.
Mimi nilisisimuka kusikia tangazo la kuchapishwa kwa Mnara wa Mlinzi katika Kijapani kwa mara ya kwanza baada ya vita. Nilienda nyumbani nikiwa na toleo lililochapishwa upya-upya la Mei 1, 1951. Siwezi kukumbuka wakati wo wote katika maisha yangu mazima ambapo nilihisi nikiwa mwenye furaha hivyo. “Sasa kazi katika Japani imefunguliwa upya kirasmi,” nikawaza, “na sawa na unabii ulivyotolewa, kazi ya Yehova itaongezeka, mmoja atakuwa elfu.”
Tangu wakati huo sisi tumeshangilia mawasiliano kamili pamoja na tengenezo la Yehova. Katika Agosti 1951 Ndugu Adrian Thompson alituzuru kwa mara ya kwanza akiwa mwangalizi wa mzunguko. Mikutano ilianzwa, na ndugu wawili wa kwanza kuwa mapainia wa pekee katika Japani wakagawiwa kwenda Jiji la Kure. Kundi lilikua pole kwa pole, na mume wangu alitumikia akiwa mtumishi wa kundi.
Ni nini lililotukia kwa Mashahidi wapatao 130 katika Japani ya kabla ya vita? Kielelezo kibaya cha Junzo Akashi, yule mwangalizi wa tawi, kilikuwa na athari yenye kubumbuaza wengi. Wachache wakawa wafuasi wake, wengine walitawanyika, na inaonekana watu fulani kati yao walikufa katika ule mnyanyaso. Yapata dazani moja walibaki katika utumishi wa Yehova, na watu fulani kati yao wangali wamebarikiwa kwa kadiri fulani ya afya na wanatumikia kwa juhudi.
Afya yangu ilipokuwa nafuu, nilitumikia nikiwa painia wa kawaida kwa miaka michache. Mume wangu alipokuwa na umri wa miaka 71, yeye alitapika damu nyingi sana na kuharakishwa hospitalini. Jambo la kushukuria ni kwamba madaktari waliheshimu mkatao wake wa kutiwa damu mishipani. Ingawa alipona kwa kadiri kubwa, alikufa miezi sita baadaye. Kozo, mwana wetu wa kimalezi, alikuwa painia wa pekee kwa miaka mingi na sasa ni mzee Mkristo.
Ninapotazama ya nyuma, kwangu inaonekana kama kwamba wengi wa waliokuwako tangu wakati uliotangulia vita, ambao walikuwa na uwezo mwingi sana na ueledi mwingi wa kiakili, waliacha tengenezo la Yehova walipotiishwa chini ya mkazo mkubwa. Labda wao walitegemea uwezo wao wenyewe. Wale waliobaki waaminifu hawakuwa na uwezo wa pekee na walikuwa wasiotokeza sana. Kwa uhakika ni lazima sisi sote tuitibari katika Yehova sikuzote kwa moyo wetu wote.—Mithali 3:5.
Mwishowe “dhiki kubwa” itakuja hakika. (Mathayo 24:21) Huenda wakati huo tukaelekeana na majaribu yatakayofanya yale yaliyotangulia yaonekane madogo sana. Kuyavumilia huenda kusiwe rahisi kama vile sisi tunavyowazia. Lakini ikiwa sisi tunamtegemea Yehova kweli kweli, tunampenda kweli kweli na kupaliza kilio katika moyo wetu kuomba msaada wake, sawa na vile yeye hakuniacha mimi, yeye hataacha watumishi wake wanaojitahidi kumtumikia kwa uaminifu.—Zaburi 37:25.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Mimi niliolewa na Jizo Ishii, mtu nisiyekuwa nimemjua hata kidogo
[Picha katika ukurasa wa 25]
Ndugu Knorr alipozuru Japani katika 1951, yeye alitumikia wamisionari na mikusanyiko katika Tokyo, Nagoya, na Kobe (juu)