“Endelea na Kazi Mpaka Imalizike”
Imesimuliwa na Lois Dyer
Hilo ndilo lililokuwa azimio langu wakati nilipoanza utumishi wangu wa wakati wote miaka 49 iliyopita. Migawo imenipeleka kutoka Perth mpaka Tokyo, nikathawabishwa sana na mambo mengi ambayo nimeyaona wakati wote huo.
Nilizaliwa katika mwaka 1910 katika Northam, mji wa mashambani, sehemu ya magharibi ya Australia. Mojalapo la mambo ninayokumbuka ni vitabu vikubwa vilivyokuwa juu ya rafu ya chini kabisa kwenye kabati letu la kuwekea vitabu. Yalikuwa magazeti ya Mnara wa Mlinzi yaliyofungwa pamoja, yenye tarehe za kuanzia na mwaka 1904.
Wakati huo hakukuwa na kundi la Mashahidi wa Yehova mjini, lakini mara kwa mara makolporta (mapainia wa siku hizo) walikuwa wakitutembelea. Baba yangu aliamini aliyoyasoma katika vitabu vya Sosaiti, na, hata baada ya kupata ugonjwa, yeye aliendelea kusema na wengine juu ya kweli ya Biblia. Ndugu Robert Lazenby akaja kutoka Perth kuja kutoa hotuba ya mazishi ya baba yangu katika mwaka 1929. Nilipoisikia hotuba hiyo, mara moja nikaitambua kweli, na tangu wakati huo na kuendelea nikawa nikisoma kila kifaa kilichochapwa na Sosaiti kilichopatikana.
Nikiwa na tamaa yenye uharaka ya kumtumikia Yehova, niliiandikia Sosaiti katika mwezi wa Julai 1931, nikawaeleza juu ya tamaa yangu ya kushiriki katika kazi ya nyumba kwa nyumba. Katika kunijibu, walinitumia vibweta kadha vya vitabu pamoja na fomu ya maombi ya utumishi wa painia msaidizi. Ndiyo, jina la utumishi huu wa pekee lilikuwa lile lile kama lilivyo leo, na kwa hiyo nilitazamiwa nitumie saa 60 kila mwezi katika kutangaza “habari njema.” Nilikubali pendeleo hilo ijapokuwa wakati huo sikuwa nimebatizwa.
Barua yangu ya kwanza kutoka kwa Sosaiti baada ya hapo ilikuwa na nakala ya azimio lililokubali kulichukua jina “Mashahidi wa Yehova” katika kusanyiko la Columbus, Ohio, (U.S.A.) lililofanywa katika mwaka 1931. (Isa. 43:10-12) Kwa furaha mimi na mama yangu tukatia sahihi zetu kwenye barua hiyo. Bado tulikuwa peke yetu, lakini niliondoka nikatoe ushuhuda katika mji wa nyumbani kwetu. Kwa kuwa nilikuwa nimefundisha kwa muda wa miaka miwili katika shule ya msingi ya mahali hapo nikiwa kama mwalimu-mwanafunzi, nilijulikana sana katika ujamii huo. Halikuwa jambo rahisi kuanza kazi ya kushuhudia nyumba kwa nyumba nikiwa peke yangu, na zaidi kwa vile sikuwa nikishirikiana moja kwa moja na kundi lo lote. Nilipata kuhojiana mara nyingi na wapinzani wa kidini. Kasisi (padre) mmoja wa Kianglikana alisema hivi kwa dharau: “Usiniambie kwamba wewe unaamini ile hadithi ya Adamu na Hawa!” Watu wengine mmoja mmoja walisikiliza wakachukua vitabu na magazeti, lakini sikujua namna ya kufuatia wenye kupendezwa. Dada yangu na mume wake walikuwa wakisoma Mnara wa Mlinzi, ijapokuwa hatukuwa na funzo lililopangwa, nami nilitamani sana kushirikiana na kundi.
Januari 1, 1932, mimi na mama yangu tukahamia Perth. Lo! ilikuwa furaha kama nini kushirikiana na kundi la Kikristo kwa mara ya kwanza! Siku chache baadaye, Januari 4, 1932, tukabatizwa sote wawili katika Jumba la Ufalme la Subiaco. Siku ya pili yake, nikawa painia wa kawaida, nikawa nikifanya kazi pamoja na kikundi cha mapainia wenye juhudi, bila shaka nikiwa na furaha sana kwa kuwa na msaada wa watangazaji wa Ufalme wenye ujuzi. Wote wakanitia moyo ‘niendelee na kazi mpaka imalizike.’
Juma chache baadaye, wanne wetu tukaondoka kwa motokaa twende tukahubiri eneo la mashambani katika sehemu iliyo magharibi-kusini mwa magharibi ya Australia. Sehemu hii ilikuwa imetolewa ikaliwe na Waingereza wenyeji wa mashamba waliokuwa wameufyeka msitu na kuanzisha vikundi vya mashamba ya kufuga ng’ombe wa maziwa. Kila kikundi kilipewa namba yake, nao wenye mashamba waliitwa ‘wanavikundi.’ Kwa kuwa hawakuwa na fedha nyingi, mara nyingi tulibadilishana vitabu na maziwa, mayai na mboga. Pindi moja tulibadilisha vitabu kadha na sanduku la nyanya ambazo tulikula kwa juma nzima. Tulienda kikundi kwa kikundi, na kulala hemani po pote tulipomalizia kazi ya siku.
Mwaka huo, 1932, tuliadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo katika mji mdogo wa Donnybrook, katika nyumba ya Arthur Williams, Mkubwa, mmojawapo watu wa kwanza kukubali kweli katika Australia Magharibi. Dada yake, Vi Williams, alikuwa painia mwaminifu kwa muda wa miaka mingi naye alinisaidia sana kwa kunipa shauri jema. Sasa jamaa ya akina Williams wanajulikana sana kama Mashahidi wa Yehova katika sehemu yote hiyo.
KUTOA USHUHUDA CHINI YA MARUFUKU
Zamani sana, nilijifunza kutumia maneno haya ya Zaburi 55:22: “Umtwike [Yehova] mzigo wako naye atakutegemeza, hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele.” Zaidi sana jambo hilo lilipata kuwa kweli wakati serikali ilipopiga marufuku Mashahidi wa Yehova kuanzia Janauri 1941 mpaka Juni 1943.
Kipindi cha wakati huo, tuliendelea kuhubiri kwa siri, nalo lilikuwa jambo la lazima kuhifadhi vitabu vya kujifunza Biblia tulivyokuwa navyo. Niliweka vitabu vyangu kwenye sanduku la chuma ambalo nilichimbia chini ya ardhi katika shamba la dada yangu na mume wake. Tulitoa ushuhuda kwa kutumia Biblia, na wakati tulipompata mtu aliyependezwa kweli kweli, shamba lilichimbuliwa usiku kwa uangalifu sana! Kazi ya kutoa ushuhuda ilifanikiwa nayo hesabu ya wahubiri wa Ufalme katika Australia ikaongezeka maradufu katika wakati wa kipindi hicho.
UTUMISHI WA PAINIA WA PEKEE
Katika mwaka 1942, nikarudi Northam mji wa nyumbani kwetu nikiwa painia wa pekee. Kufikia wakati huo ndugu yangu Dan alikuwa amechukua msimamo wake katika upande wa kweli pamoja na mke wake na watoto. Jambo hilo likanifurahisha sana. Painia mwingine, Mary Ham (sasa aitwa Wallis), pamoja nami, mara nyingi tulitumia farasi pamoja na gari la kukokotwa na farasi mahali pa kutumia baisikeli zetu. Farasi huyo alikuwa mzee sana naye alitutatiza sana katika kumfanya aanze mwendo asubuhi. Watoto wa ndugu yangu wakawa wakisaidia kwa kutembea mbele yake wakiwa na fungu la nyasi au kisehemu cha tunda la tofaa ili kumtia moyo aanze mwendo.
Mgawo wangu uliofuata ulikuwa tofauti sana. Ulikuwa eneo la biashara katika mji wa Perth. Mwanzoni, wazo la kutoa ushuhuda katika banki na afisini liliniogopesha, lakini nikawaza hivi: “Watu ni wale wale wawe nyumbani ama katika jengo la afisi. Kwa hiyo sababu gani niogope mazingira ya namna hiyo?” Nikimtegemea Yehova, niliendelea. Ijapokuwa lilikuwa jambo gumu kuanzisha mafunzo ya Biblia, nilipata watu niliokuwa nikipelekea magazeti kwa ukawaida, na kabla ya kuondoka katika eneo hilo, nikawa nimepata maandikisho 50 ya magazeti yetu.
Katika mwaka 1947, nilipewa mgawo wa kufanya kazi peke yangu katika mji mdogo wa Katanning, ambao katika wakati huo ulikuwa na idadi ya watu kama 3,000. Mji huo ni sehemu ya kati ya eneo ambalo watu hufuga kondoo na kulima ngano. Nikitumia baisikeli, nilikuwa nikienda mwendo wa kama maili 20 au 30 (kilometres 30 au 50) kila siku ili kuyafikia mashamba yaliyokuwa kandokando yake. Watu wa sehemu hiyo walikuwa wakaribishaji-wageni sana na mara nyingi walinikaribisha nile chakula pamoja nao. Katika wakati wa majira ya masika, wakati maua ya kondeni yalipotandaa kama mkeka wenye rangi nyingi nzuri sana katika pande zote mbili za barabara za mashambani, mara nyingi nilikuwa nikishuka kutoka juu ya baisikeli yangu na kutua huku nikifurahia uzuri wote huo.
MWALIKO KWENYE UTUMISHI WA MISIONARI
Baada ya kutumia muda wa miezi sita tu katika Katanning, pendeleo jipya zuri sana la utumishi likawekwa mbele yangu. Nilikubaliwa kuwa katika darasa la 11 la Shule ya Sosaiti ya Gileadi, nami nikawa mmoja wa kikundi cha watu 19 waliotoka Australia na New Zealand. Molly Heron ambaye amekuwa mwenzi wangu katika utumishi tangu wakati huo alikuwa katika kikundi hicho. Molly vilevile alikuwa ameanza upainia katika mwaka 1932, huko Brisbane. Kwa vile sote wawili tulikuwa tumekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa miaka inayolingana tulikuwa na mambo mengi yaliyofanana. Walakini, hali mimi nina maelekeo ya kufanya maamuzi kwa haraka, Molly hutenda kwa uangalifu zaidi. Kwa hiyo tumekuwa wenye kufaana sana nasi tumefurahia ushirika mzuri sana kwa muda wa miaka 31.
Baada ya kutumia muda wa miezi mitano yenye shughuli (kazi) nyingi na yenye furaha huko Gileadi, South Lansing, New York, (U.S.A.), tulipokea mgawo wetu. Kikundi chetu cha akina dada watano kilikuwa kiende New Caledonia. Walakini, Ndugu N. H. Knorr akasema baadaye kwamba alikuwa amesikia kwamba bado walikuwako wawindaji wa vichwa vya wanadamu katika kisiwa hicho! Kwa hiyo mgawo wetu ukabadilishwa ukawa Fiji. Tulipokuwa tukingojea hati zetu za kuingia Fiji, tulitumia muda wa miezi 16 huko San Francisco, California, (U.S.A.), tukawa tukifanya kazi pamoja na kundi la Daly City, tukafanya urafiki mzuri sana na watu wengi.
Katika mwezi wa Oktoba katika mwaka 1949, tukaona kikundi cha rafiki zetu wa darasa la 11 kikiondoka San Francisco kwa merikebu kuuendea mgawo wao huko Japan. Walikuwa Lloyd na Melba Barry, Percy na Ilma Iszlaub, na Adrian Thompson. “Tuonane baada ya Har–Magedoni,” tukawaambia wakati merikebu ilipokuwa ikiondoka ufuoni mwa bahari. (Ufu. 16:14, 16) Lakini wenye mamlaka walikataa kutupa hati za kuingia Fiji. Kwa hiyo Januari 1950 tukajikuta tukifuata rafiki zetu huko Japan, ambako tulijiunga nao katika nyumba ya misionari huko Tarumi, Kobe.
KAZI YA MISIONARI KATIKA JAPAN
Hivyo ikaanza sehemu yenye furaha zaidi ya miaka 49 ya utumishi wangu wa wakati wote. Mwanzoni, kwa kutojua lugha na desturi za watu wa Japan tulifanya makosa mengi sana. Kwa mfano, pindi moja niliwaambia watu kwamba nilikuwa ninakohoa (badala ya kutembelea) mlango kwa mlango. Lakini sikuzote nilikumbuka shauri la Ndugu Knorr: “Fanya yote uwezayo, na, ujapofanya kosa, FANYA JAMBO FULANI!” Kwa hiyo tulisonga mbele, tukifanya yote tuwezayo, na kwa msaada wa Yehova polepole tulifanya maendeleo.
Jambo moja jipya tulilopata kuona lilikuwa kukabiliana na ukali wa Dhoruba (upepo mkali) Jane. Tulikuwa tumetoka nje katika utumishi wa shambani wakati upepo huo ulipoanza, nao wahubiri wakatuhimiza turudi nyumbani. Kwa kuwa hatukujua hatari iliyokuwako, mimi na Molly tukaendelea tu kutoa ushuhuda kadiri ilivyowezekana. Walakini huu ulikuwa wakati mmoja ambapo tulilazimika kuacha. Huku nyuzi za umeme zikipindika na kukatika kwa sababu ya nguvu za upepo, tukakimbilia nyumba ya misionari ili tupone kuumizwa na vigae kutoka kwenye paa za nyumba pamoja na matawi ya miti yaliyokuwa yakiruka huku na huku hewani.
Mmisionari mmoja akawa anakosekana! Hata hivyo, akafika nyumbani usiku wa manane akiwa salama salimini, baada ya kukaa mchana kucha akiwa peke yake katika behewa la gari moshi. Upepo huo mkali ulipopungua, tuliona kwamba ni vioo vichache tu vya dirisha za nyumba ya misionari vilivyokuwa vimevunjika pamoja na sehemu ya maji. Sehemu nyinginezo, watu fulani walikuwa wamepoteza maisha zao, na katika bandari merikebu 500 zilikuwa zimezama.
Katika miaka hiyo ya mapema, kwa mara ya kwanza tulipata vilevile kuonana na matetemeko ya ardhi, ambayo yanaelekea kutukia mara nyingi huku Japan. Mojalapo la matetemeko hayo lilipata kuangusha kinara kirefu cha mawe cha taa kilichokuwa bustanini mwa nyumba ya misionari. Jambo zuri likawa, hakuna aliyekuwa karibu nacho wakati huo.
Vilevile kulikuwako mambo mengi mazuri sana tuliyoona. Katika muda wa miaka minne tuliyokaa Kobe, tulikuwa na pendeleo la kusaidia kuanzisha makundi ya Tarumi na Akashi. Baadhi ya wale tuliojifunza Biblia nao wakati huo wanatumikia sasa kama mapainia na wazee waliowekwa katika makundi.
Mgawo wetu uliofuata ulikuwa katika mji wa Kyoto, uliokuwa na maelfu ya mahekalu na sehemu takatifu za ibada. Ijapokuwa wingi wa watu walijishughulisha zaidi na sikukuu zao za kidini zenye sherehe, tulipata kuona kwamba watu wengi mmoja mmoja walikuwa na nia ya kujifunza Biblia pamoja nasi. Mmojawapo wa hao alikuwa Shozo Mima, mfuasi mnyofu wa dini ya Buddha. Moyoni mwake aliamini kwamba lazima kuweko na Muumba, akasema: “Nataka kujua juu ya Mungu wa kweli.” Kwa vile alivyokuwa na maulizo mengi naye sikuzote alikubali majibu ya Biblia, nilifurahia sana kujifunza pamoja naye. Upesi akawa Shahidi painia mwenye juhudi naye akawekwa awe akiangalia kundi baada ya wamisionari kuondoka Kyoto. Kulikuwako wahubiri 36 tu wa Ufalme wakati huo, walakini sasa kuna makundi 11 na Majumba ya Ufalme sita katika mji huo.
Mimi na Molly tukahamishwa tukapelekwa Kumamoto, katika kisiwa cha Kyushu. Tukapata kuona kwamba mji huo ulikuwa na watu wenye uadui wa ukabila, napo hapo mwanzoni ilikuwa vigumu kupata maendeleo katika kutangaza “habari njema” katika mji huo. Hana Mihara na Margaret Waterer (sasa aitwa Pastor) wakajiunga pamoja nasi, nasi akina dada wanne tukashindana na magumu yanayolipata kundi jipya. Lilikuwa jambo gumu sana. Lakini baada ya miaka sita yenye kazi ngumu, tuliweza kuliacha kundi likiwa na wahubiri 31 wenye juhudi, baadhi yao wamekuwa katika utumishi wa painia sasa kwa miaka mingi. Leo, kuna makundi matatu katika Kumamoto.
Baada ya hapo tukahamia Tokyo, ambapo tumetumikia pamoja na makundi ya Tamagawa na Setagaya kwa muda wa miaka 15. Watu wengi tunaojifunza Biblia pamoja nao wanatoka katika jamaa zenye kufuata dini ya Buddha, ijapokuwa baadhi yao wameshirikiana na makanisa ya Jumuiya ya Wakristo. Tulipopewa kwa mara ya kwanza mgawo kwenye kundi la Setagaya, nikakutana na Toshiko Nakamura, ambaye kwa muda wa miaka 20 amekuwa akitafuta kupata maelezo juu ya unabii wa Ufunuo na Mathayo 24. Alikuwa amehudhuria makanisa mbalimbali 13 naye alikuwa amepata kuwauliza makasisi mbalimbali. Walakini walimwambia kwamba hakuna mtu awezaye kueleza unabii huo. Mmojawapo wao alimwambia hivi, “Ukiisha kufa, utayafahamu mambo hayo.” Alipokuwa akijifunza Biblia alimwambia mwanawe kwa furaha hivi: “Mwishowe nimeipata kweli.” Kwa vile mama yake alikuwa amempeleka kwenye makanisa mbalimbali 13, yeye aliona shaka sana, walakini akakubali kujifunza naye akafanya maendeleo kwa haraka sana. Yeye amekuwa painia wa kawaida kwa miaka minane na sasa yeye anatumikia kama mzee katika kundi la Setagaya.
YEHOVA AMWAGA BARAKA
Nimekuwa na furaha kuu kushiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi hapa Japan. Ijapokuwa mwanzo ulikuwa mgumu, tunafurahi kwamba tulivumilia. Tumeona kazi ikisonga mbele kutoka wahubiri 12 kufikia zaidi ya 52,000 nasi tumepata maono mengi yenye kuchangamsha moyo. Kama vile ilivyo kwa watu wote, tumekuwa na magumu ya afya na kukatishwa tamaa nyakati nyingine. Lakini hatukufikiri kuacha hata kidogo kabla ya kazi kumalizika. Sasa tunajisikia kustarehe kabisa tukiwa pamoja na ndugu na dada zetu Wajapani. Kwa kweli, tunapokwenda kwenye makusanyiko katika nchi za ng’ambo, tunajisikia kuwa wageni huko.
Nikiangalia nyuma kwenye miaka ambayo imepita kwa haraka sana, naweza kusema kweli kweli kwamba Yehova amefungua madirisha ya mbinguni na kumwaga baraka. (Mal. 3:10) Utumishi wa wakati wote ni hazina. Kwa hakika ndivyo ulivyo utendaji wote wa moyo wote unaomletea sifa Baba wa kimbinguni. Na kwa kweli, tukijitahidi kuendelea na kazi mpaka imalizike, Yehova ataongeza baraka zake tele.