Nilitegemezwa na Mungu Asiyeweza Kusema Uwongo
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA MARY WILLIS
Matokeo ya mshuko wa kiuchumi wa ulimwengu ulikuwa umefikia sehemu za mashambani za Australia Magharibi kufikia 1932. Mwaka huo, nilipokuwa na miaka 19 tu, Ellen Davies nami tulipokea mgawo wa kuhubiri eneo lenye kuenea kilometa za mraba 100,000. Tungeanzia mji mdogo wa Wiluna, uliokuwa kilometa zipatazo 950 kaskazini-mashariki mwa makao yetu jijini Perth, ambalo ni jiji kuu la Australia Magharibi.
TULIPOKUWA njiani kuelekea huko, Ellen nami tulikuwa katika behewa moja la gari-moshi pamoja na mlinzi mmoja wa reli aliyekuwa mwenye urafiki. Gari-moshi liliposimama katika kila stesheni, kwa fadhili mlinzi huyo alikuwa akituambia muda ambao tungesimama hapo. Jambo hilo lilitupa fursa ya kushuka na kutolea ushahidi watu waliokuwa wakiishi katika vijiji hivyo vya mbali vya stesheni za reli. Hatimaye tulifikia mji wa mgodi wa Wiluna wakati wa dhoruba ya upepo wenye vumbi.
Hata hivyo, stesheni ya Wiluna ilikuwa karibu kilometa tatu kutoka mjini. Sisi sote hatukuwa wenye nguvu sana, na tulikuwa na katoni tatu nzito za fasihi pamoja na masanduku mawili. Tungefanyaje? Tulibeba katoni kwenye ufito, na kila mmoja akashika upande mmoja wa ufito huo. Kwa njia hiyo tulibeba katoni hizo moja-moja. Tulienda na kurudi mara saba kabla ya kuweza kupeleka katoni hizo tatu na masanduku yetu mawili hizo kilometa tatu hadi mjini. Tulipumzika mara kwa mara kwa sababu ya uchungu mwingi wa mikono yetu.
Kujapokuwa mavumbi, uchungu wa mikono, na uchovu wa miguu yetu, tulifurahia sana magumu hayo na ujasiri huo. Sote tulihisi kwamba Yehova alikuwa nasi, kwamba alikuwa akitutegemeza tukabiliane na magumu hayo ya kwanza katika mahubiri ya sehemu za mbali. Upesi tuliona pia baraka zake juu ya kazi yetu, kwa sababu jitihada zetu katika safari hiyo zilitokeza kijana mmoja aitwaye Bob Horn akubali kweli ya Biblia. Twafurahi kwamba Bob aliweza kutumia miaka fulani katika utumishi wa Betheli na kwamba aliendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu kwa karibu miaka 50 mpaka kifo chake katika 1982.
Kutoka Wiluna tulihubiri katika vijiji tulivyopata kwenye safari yetu ya zaidi ya kilometa 725 kuelekea Geraldton uliokuwa pwani. Kutoka huko tulisafiri tukirudi Perth. Usiku kadhaa tulikuwa tukilala sakafuni mwa vyumba vitupu vya kungojea gari-moshi na mara moja tulilala katika majani ya kuliwa na ng’ombe kando ya reli.
Tulibeba mfuko wa mto wa kulalia uliojazwa mikate ya unga wa ngano tuliyojipikia wenyewe. Hicho kilikuwa chakula chetu kuu kwa nusu ya kwanza ya safari yetu. Katika pindi nyingine tulipata mlo kwa kuosha vyombo na kuosha sakafu katika makao ya wasafiri kulala na vyumba vya mlo. Nyakati nyingine tulikuwa tukifanya kazi kwenye jua kali tukivuna njegere au maharagwe. Michango kutoka kwa watu wenye kupendezwa waliokubali fasihi za Biblia ilisaidia gharama zetu.
Jambo lililonitia nguvu nidumishe imani yangu kwa Yehova na kukabiliana kwa furaha na hali nyingi zilizo ngumu katika siku hizo lilikuwa ni kielelezo na mazoezi ya mapema niliyopokea kutoka kwa mama yangu.
Urithi wa Kikristo
Mama yangu alikuwa na imani yenye nguvu kwa Muumbaji, na kwa kadiri niwezavyo kukumbuka, alikuwa akisema na sisi watoto juu yake. Hata hivyo, imani yake ilitahiniwa sana na kifo cha ndugu yetu mwenye umri wa miaka saba katika aksidenti yenye msiba akiwa shuleni. Lakini badala ya kumkasirikia Mungu, mama alianza kujifunza Biblia kwa bidii. Kama ingewezekana, alitaka kujifunza sababu zinazotokeza misiba. Utafutaji wake wa kweli ya Biblia ulithawabishwa, naye akafananisha wakfu wake kwa Mungu wa kweli, Yehova, kwa ubatizo wa maji katika miaka ya mapema ya 1920.
Kutokea wakati huo na kuendelea, mazungumzo yake pamoja nasi mara nyingi yalikazia jinsi ahadi za Mungu zilivyo hakika kutimizwa. Nyakati zote alikuwa akituhimiza tukumbuke kwamba hata jambo gani litendeke, ‘Mungu hawezi kusema uwongo.’ (Tito 1:2) Basi, dada yangu nami na ndugu zetu wawili, pamoja na familia zetu na wajukuu, twamsifu Yehova Mungu leo. Wapwa wangu wawili, Alan na Paul Mason, wanatumika wakiwa waangalizi wasafirio.
Tamaa ya Mapema ya Kuwa Mweneza-Evanjeli
Sikuwa mwanafunzi mzuri nami nikaacha shule mwaka wa 1926, nilipokuwa na umri wa miaka 13. Lakini, nilikuwa nimesitawisha tamaa kubwa ya kueleza wengine yale ambayo nilikuwa nimejifunza juu ya Biblia. Baba alifikiri kwamba sikuwa nimesoma vya kutosha kuweza kusaidia mtu yeyote, lakini mama alisema: “Hata kama anaeleza watu tu juu ya vita ya Har–Magedoni inayokaribia na kwamba watu wapole watairithi dunia, hayo yatatosha kutangaza Ufalme wa Mungu.” Kwa hiyo nilianza kushiriki katika kazi ya nyumba kwa nyumba nikiwa katika umri wa mapema wa utineja, ingawa sikubatizwa mpaka mwaka wa 1930. Upesi baada ya kubatizwa, nilianza kazi ya kueneza evanjeli wakati wote katika eneo la Perth.
Mwaka uliofuata, 1931, tulianza kutumia jina letu jipya Mashahidi wa Yehova. Lakini, wenye nyumba walio wengi walipinga kutumia kwetu jina hilo takatifu la Mungu nao wakaitikia kwa ukali sana. Hata hivyo niliendelea katika huduma yajapokuwa matukio hayo yasiyofurahisha. Nilikuwa na hakika kwamba Mungu hasemi uwongo anapoahidi kwamba watumishi wake waweza kutegemea ‘nguvu wanazojaliwa na Mungu.’—1 Petro 4:11; Wafilipi 4:13.
Kutambulisha “Mkutano Mkubwa”
Katika 1935, nilipokea mgawo wa kwenda upande ule mwingine wa bara hili kubwa la Australia. Hivyo, kwa miaka mingi baadaye nilitumikia nikiwa mhudumu painia kotekote katika wilaya ya New England katika jimbo la New South Wales, kilometa zipatazo 4,000 kutoka nyumbani ya awali Perth.
Kufikia wakati huo nilikuwa nikishiriki mifano ya mkate usiotiwa chachu na divai nyekundu katika Ukumbusho wa kila mwaka wa kifo cha Yesu. Ingawa ilionwa kuwa sawa kufanya hivyo, hasa kwa wahudumu wa wakati wote wenye bidii, sikusadiki kamwe kwamba nilikuwa na tumaini la kimbingu. Kisha, katika 1935, tulielezwa wazi kwamba mkutano mkubwa wenye tumaini la kuishi milele duniani ulikuwa ukikusanywa. Wengi wetu tulifurahi kujua kwamba tulikuwa sehemu ya huo mkutano mkubwa, nasi tukaacha kushiriki mifano. (Yohana 10:16; Ufunuo 7:9) Kweli ya Biblia ilikuwa iking’aa zaidi na zaidi, kama vile tu Yehova alikuwa ameahidi.—Mithali 4:18.
Njia Mpya za Kuhubiri
Katika miaka ya katikati ya 1930, tulianza kutumia kinanda katika huduma yetu. Hivyo, ilikuwa lazima tuweke katika baiskeli zetu zenye nguvu vibebaji vya mbele na vya nyuma kwa ajili ya mifuko ya fasihi zetu na vilevile kwa ajili ya vinanda vyetu vizito pamoja na santuri. Ilikuwa lazima nijihadhari wakati baiskeli yangu ilipojaa kabisa kwa sababu ilikuwa nzito sana hivi kwamba kama ingalianguka, nisingaliweza kuiinua tena!
Karibu na wakati huo tulianza pia yale tuliyoita maandamano ya kutoa habari. Tulivaa mabango, au kwenye ishara upande wa mbele na wa nyuma, zenye shime fulani za kuvutia watu tulipotembea katika barabara kuu za miji. Nilipata kazi hii hasa kuwa yenye kutahini imani sana, hasa nilipokamatwa na kutiwa mbaroni kwa usiku kucha katika seli ndogo mjini Lismore. Ilikuwa aibu sana kuletwa mahakamani siku iliyofuata bila hata kukubaliwa kuchana nywele zangu! Lakini kwa mara nyingine tena Yehova alinitegemeza jinsi alivyoahidi. Kesi hiyo ilitupiliwa mbali kwa sababu mashtaka pekee ya yule polisi aliyenikamata yalikuwa kwamba maandishi ya bango langu yaliudhi dini yake.
Narudi Magharibi
Katika miaka ya mapema ya 1940, kazi yangu ya upainia ilinirudisha kwenye miji ya mashambani katika Australia Magharibi. Niliendelea kufurahia maono mengi mazuri na baraka nyingi za kiroho huko. Nikiwa katika mgawo wangu katika mji wa Northam, nilikutana na mke mmoja wa nyumbani mwenye shughuli mno, Flo Timmins, kilometa zipatazo 11 kutoka mjini. Alikubali kitabu Reconciliation, na upesi akawa Shahidi aliyejiweka wakfu kwa Yehova Mungu. Angali mwenye bidii katika utumishi wa Ufalme, na binti yake ambaye wakati huo alikuwa na miaka minne tu, alikua akawa mhudumu painia wa pekee.
Lakini kulikuwa na maono mengine ambayo siwezi kuyasahau. Pindi moja, mwenzangu nami tulikuwa tukivuka daraja fulani kule Northam katika kigari chetu cha kukokotwa na farasi, wakati ambapo kwa ghafula yule farasi akaanza kukimbia kwa kasi sana, akituogofya sana tukiwa juu ya yale maji yenye kwenda kasi ya Mto Avon kule chini. Baada ya mwendo unaozidi kilometa moja, farasi huyo alipunguza mwendo.
Ndoa na Familia
Katika 1950, niliolewa na Arthur Willis, ambaye pia alikuwa amekuwa painia kwa miaka mingi. Tulikaa katika mji wa mashambani wa Pingelly katika Australia Magharibi, tulikobarikiwa kupata mwana, Bentley, na binti, Eunice. Watoto hao walipokaribia kumaliza shule, Arthur aliamua kuwa painia tena. Kielelezo chema cha baba kilitia moyo watoto wetu wawili waanze upainia wa kawaida mara tu walipohitimu.
Mara nyingi Arthur aliwachukua watoto hao kwenda sehemu za mbali mashambani ili kuhubiri. Mara moja-moja, angekaa nao mbali na nyumbani kwa muda wa juma moja au zaidi kwa kipindi kimoja, akipiga kambi kila usiku. Katika pindi hizo nilipokuwa peke yangu, nilibaki nyumbani kuendesha biashara ya familia yetu ya fanicha, iliyowezesha watatu waendelee na upainia.
Huduma Miongoni mwa Wenyeji
Asubuhi moja baada tu ya familia yetu kurudi kutoka mojapo ziara za mashambani, tulipokea mgeni asiyetazamiwa. Mgeni huyo alikuwa mwenyeji, aliyeuliza hivi: “Nifanye nini ili nirudishwe?” Kwanza tulipigwa bumbuazi. Kisha Arthur akamtambua kuwa mtu ambaye miaka mingi mapema alitengwa na ushirika wa kutaniko la Kikristo kwa sababu ya ulevi. Tangu wakati huo alikuwa amesitawisha sifa mbaya ya kunywa kwa kupindukia na kuwa na madeni ya watu.
Arthur alimweleza jambo alilohitaji kufanya ili arudishwe katika tengenezo safi la Yehova. Aliondoka kwa ukimya bila kusema mengi, na sisi sote tukajiuliza jambo atakalofanya. Hakuna yeyote kati yetu aliyetarajia yale mambo yaliyotokea katika miezi michache iliyofuata. Mtu huyo alifanya mabadiliko makubwa zaidi! Alianza kuzuru watu katika wilaya aliyoishi akiwakumbusha juu ya madeni yake, na kuwalipa madeni hayo na vilevile alianza kushinda tatizo lake la unywaji wa kupindukia! Leo, kwa mara nyingine tena, leo yeye ni ndugu wa Kikristo, na ametumika kwa muda fulani akiwa mhudumu painia.
Kulikuwa na wenyeji wengi wanaoishi Pingelly, na tulifurahia huduma yenye kuridhisha sana, tukisaidia watu hao wanyenyekevu wajifunze na kukubali kweli ya Neno la Mungu. Imani yangu imeimarishwa sana kama nini kuweza kushiriki katika kusaidia wenyeji wengi wa Australia kujifunza kweli!
Kutaniko lilianzishwa mjini Pingelly, na mwanzoni washiriki walo wengi zaidi walikuwa wenyeji. Ilikuwa lazima tufundishe wengi wao kusoma na kuandika. Walibaguliwa sana katika miaka hiyo ya mapema, lakini wakazi wa mijini wakaanza polepole kustahi Mashahidi wenyeji kwa sababu ya njia yao safi ya maisha na pia kwa sababu ya kuwa wenye kutumainika.
Msaada wa Yehova Usiokosa
Mume wangu mpendwa, Arthur, aliyekuwa amemtumikia Mungu kwa uaminifu kwa miaka 57, alikufa mapema katika mwaka wa 1986. Aliheshimiwa sana na wafanyabiashara wote katika Pingelly na wakazi wa wilaya hiyo. Kwa mara nyingine tena, Yehova alinitegemeza, akinipa nguvu ya kuvumilia potezo hilo la ghafula.
Mwana wangu, Bentley, anatumikia akiwa mzee katika sehemu ya kaskazini mwa Australia Magharibi, ambako yeye na mke wake, Lorna, wamelea familia yao katika kweli. Chanzo kingine cha shangwe kwangu ni kwamba binti yangu, Eunice, ameendelea na utumishi wa wakati wote kufikia wakati huu. Yeye na mumewe, Jeff, wanatumikia wakiwa mapainia. Ninaishi nao wakati huu na nimebarikiwa kuweza kufanya upainia msaidizi kwa kuendelea.
Kwa zaidi ya miaka 60, nimeona utimizo wa ahadi ya Yehova yenye upendo ya kuwaimarisha watumishi wake na kuwasaidia kukabiliana na hali zozote zile wawezazo kukabili. Yeye ataandaa mahitaji yetu yote tusipomtilia shaka wala kumpuuza. Imani yangu imeimarishwa kwa kuwa nimehisi mkono wa Mungu ukifanya kazi, na nimeona jinsi Mungu anavyobariki watu kwa kadiri tusiyoweza kuelewa. (Malaki 3:10) Kwa kweli, Mungu hawezi kusema uwongo!
[Picha katika ukurasa wa 27]
Mary katika 1933
[Picha katika ukurasa wa 29]
Mary na Arthur katika miaka ya baadaye