Msaada Halisi kwa Familia
“Ni sawa kusema kwamba kuna tatizo la familia Marekani. Huu ndio mkataa uwezao kufikiwa tu kutokana na viwango vya talaka, idadi ya watoto wanaozaliwa nje ya kifungo cha ndoa, [na] visa vya kuwatenda vibaya vijana na wenzi wa ndoa pia.”
MANENO hayo ya mtangazaji wa televisheni Tom Brokaw yanaweza kutumiwa kuhusu nchi karibu zote. Tatizo hilo lamaanisha nini?
Familia ni msingi wa kujengea jamii kwa njia nyingi. Familia ikiwa na taabu, jamii pia ina taabu. Zaidi ya hilo, familia ni chanzo cha tegemezo la kihisia-moyo na la kifedha kwa watoto. Ndipo wanapojifunza masomo ya kwanza ya maana zaidi maishani. Familia ikiwa na taabu, watoto wanajifunza nini? Usalama wao uko wapi? Watakuwa watu wazima wa aina gani?
Je, kuna msaada wowote kwa familia katika wakati huu mgumu? Ndiyo. Familia ni shirika ambalo Mungu mwenyewe alilianzisha. (Mwanzo 1:27, 28) Naye ametoa mwongozo ulio muhimu katika Neno lake, Biblia. (Wakolosai 3:18-21) Ni kweli, hatuwezi kubadili jamii yote nzima, lakini twaweza kutumia shauri la Biblia katika familia yetu wenyewe. Tungependa kukuambia juu ya watu fulani ambao walifanya hivyo na matokeo mazuri waliyopata.
Kuzuia Talaka
Katika nchi kadhaa karibu asilimia 50 ya ndoa zote huishia kwa talaka. Hicho ni kiwango kikubwa mno cha kushindwa kwa mahusiano ya kibinadamu! Kwa kweli, wengi ambao kwa sababu hii huishia kuwa mzazi aliye peke yake hufanya kazi kubwa katika kulea watoto wao. Lakini kwa kweli walio wengi wangekubali kwamba inakuwa afadhali zaidi wakati wenzi waliooana wanapoweza kutatua matatizo yao na kukaa pamoja.
Ndoa ya wenzi fulani katika Visiwa vya Solomon ilikuwa ikielekea kupatwa na msiba. Mume, aliye mwana wa chifu, alikuwa mwenye jeuri naye alikuwa na mazoea mengi mabaya. Maisha yalikuwa magumu sana kwa mke wake hata akajaribu kujiua. Kisha, mume akakubali kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Alijifunza kwamba mtu yeyote anayetaka kumpendeza Mungu lazima ajue lililo baya na pia ‘achukie lililo baya.’ (Zaburi 97:10) Hiyo yatia ndani kuchukia mambo kama vile kudanganya, kuiba, jeuri, na ulevi. Alitii shauri hili na upesi akashinda mazoea yake mabaya na hasira yake yenye jeuri. Mke wake alishangazwa na badiliko hilo, nayo ndoa yao ikafanya maendeleo makubwa, kwa sababu ya uvutano wa Neno la Mungu.
Katika Afrika Kusini mwanamke ambaye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova alisikia kwamba mwajiri wake na mume wa mwajiri wake walikuwa wakifikiria kutalikiana. Shahidi huyo aliongea na mkubwa wake kazini kuhusu maoni ya Mungu kuhusu ndoa na kumwonyesha kitabu chenye kichwa Siri ya Kupata Furaha ya Familia. Kitabu hiki, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova, hukazia kanuni za Biblia zinazohusu ndoa, zikitia mkazo hasa juu ya jinsi ambavyo Biblia yaweza kusaidia wenzi wa ndoa watatue matatizo yao. Mwajiri huyo na mume wake walikisoma kitabu hicho na kujaribu kutumia kwa unyoofu shauri la Biblia ambalo kitabu hicho kilitoa. Tokeo likawa kwamba, waliamua kutotalikiana—ndoa nyingine ikaokolewa kupitia kutumia kanuni za Biblia.
Dini Tofauti
Vipi ndoa ambazo wenzi wana dini tofauti? Biblia kwa kufaa hushauri Wakristo waoe “katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39) Ingawa hivyo, nyakati nyingine mwenzi wa ndoa hubadili dini. Je, hiyo yapasa kukomesha ndoa hiyo? Sivyo hata kidogo.
Katika Botswana, mwanamke aliyekuja kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova majuzi aliulizwa jinsi imani yake mpya ilivyombadili. Alimwomba mume wake amjibie, na hivi ndivyo alivyosema: “Tangu mke wangu awe mmoja wa Mashahidi wa Yehova, nimeona amefanya mabadiliko mengi yafaayo. Sasa yeye ana nguvu tulivu yenye hekima ambayo hakuwa nayo hapo awali. Alikuwa na nguvu na usadikisho wa kuacha kuvuta sigareti, tatizo ambalo bado sijaweza kulishinda. Mke wangu amekuwa mwenye upendo zaidi na mwenye shauku kwangu na kwa watoto wangu, na vilevile kwa wengine. Yeye ni mvumilivu zaidi, hasa kuelekea watoto. Naona akitumia wakati wake kwenye huduma, akijaribu kusaidia wengine waboreshe maisha zao. Nimeona mimi mwenyewe pia nimefanya mabadiliko yafaayo. Naamini kabisa kwamba ni kwa sababu ya kielelezo chake.” Hayo ni matokeo mazuri kama nini ambayo kanuni za Biblia zimekuwa nayo katika ndoa hii! Watu wengi wasio Mashahidi wametoa maelezo hayohayo kuhusu wenzi wao walio Mashahidi.
Baba Anapopuuza Madaraka Yake
Uhusiano kati ya baba na watoto wake ni ufunguo wa kujenga familia zilizo imara. Mtume Paulo alishauri hivi: “Nanyi, akina baba, msiwe mkiwasumbua watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4) Basi, ni jambo linaloeleweka kwamba, makala katika The Wilson Quarterly iliwalaumu kwa matatizo mengi ya kijamii akina baba ambao hawatimizi fungu lao. Makala hiyo ilisema: “Kati ya 1960 na 1990, asilimia ya watoto wanaoishi mbali na baba zao wa kiasili iliongezeka zaidi ya maradufu . . . Kushuka kwa utimizaji wa fungu la ubaba ndiko kisababishi kikuu zaidi cha matatizo mengi yenye kusumbua yanayoipata jamii ya Marekani.”
Je, hilo lamaanisha kwamba watoto ambao baba zao hawawaongozi wamekusudiwa kutofanikiwa? La. Mtunga-zaburi wa kale alisema hivi: “Baba yangu na mama yangu wameniacha, bali BWANA atanikaribisha kwake.” (Zaburi 27:10) Mvulana mmoja wa miaka tisa katika Thailand aliona andiko hilo kuwa kweli. Mama yake alikufa alipokuwa mtoto mchanga, naye baba yake alimkataa, akamwachia nyanya yake. Akihisi asiyetakwa na asiyependwa, mvulana huyo alikuwa mwasi na akawa mkatili. Hata alimtisha nyanya yake. Waeneza-evanjeli wawili wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova walipoona kwamba mara nyingi yeye alisimama nje ya Jumba la Ufalme la kwao, siku moja walimwalika nyumbani kwao.
Walizungumza naye kuhusu Mungu—kwamba Yeye, akiwa kama baba, hupenda watoto wake. Pia walizungumza juu ya Paradiso ya kidunia ambayo Mungu amewaahidi binadamu waaminifu. (Ufunuo 21:3, 4) Yote hayo yalimvutia mvulana huyo, naye alirudi kila siku kuja kujifunza mengi zaidi. Mashahidi hao walimwambia kwamba ingembidi aache kuwa mkatili ikiwa alitaka Mungu awe Baba yake. Hayo yalipatana na maneno ya Paulo kwa Waroma: “Ikiwezekana, kwa kadiri itegemeavyo nyinyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote.” (Waroma 12:18) Pia angehitajika kumtendea nyanya yake kwa fadhili. (1 Timotheo 5:1, 2) Punde si punde, akawa anatumia kanuni za Biblia—bila shaka akiboresha maisha ya familia yake na nyanya yake. (Wagalatia 5:22, 23) Majirani walivutiwa sana na mabadiliko waliyoona kwake hivi kwamba walitaka watoto wao wenyewe wajifunze Biblia na Mashahidi wa Yehova!
Roho Yenye Amani
Mtume Paulo aliwaandikia Wakolosai hivi: “Jivikeni wenyewe upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano. Pia, acheni amani ya Kristo idhibiti mioyoni mwenu.” (Wakolosai 3:14, 15) Roho yenye amani na upendo wa kutoka moyoni haviwezi kushindwa kuunganisha familia pamoja. Navyo vyaweza kurekebisha migawanyiko ya muda mrefu ya familia. Rukia, anayeishi Albania, hakumzungumzia ndugu yake kwa zaidi ya miaka 17 kwa sababu ya kutoelewana kwa kifamilia. Alipojifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, alipata kujua kwamba kila mtumishi wa Mungu anasihiwa kusitawisha amani pamoja na wengine. “Acheni atafute sana amani na kuifuatia.”—1 Petro 3:11.
Rukia alitambua kwamba ilimbidi atafute amani na ndugu yake. Alisali usiku mzima, na asubuhi iliyofuata, moyo wake ukipiga kwa nguvu, alienda hadi kwenye nyumba ya ndugu yake. Mpwa wa Rukia alifungua mlango na kuuliza kwa mshangao: “Unafanya nini hapa?” Kwa utulivu Rukia aliomba kumwona ndugu yake, akieleza kwamba alitaka kufanya amani pamoja naye. Kwa nini? Kwa sababu sasa alitambua kwamba hayo ndiyo yaliyokuwa mapenzi ya Mungu. Ndugu yake alikubali, na kuungana kwao tena kulionyeshwa kwa kukumbatiana na kutoa machozi ya shangwe—familia ikaunganishwa tena kwa sababu kanuni za Biblia zilifuatwa.
Mashirika Mabaya
“Leo, mtoto wa kawaida hutazama televisheni kwa muda wa saa saba kwa siku. Kufikia mwisho wa shule ya msingi yeye huwa ameona uuaji wa kimakusudi zaidi ya mara elfu nane na vitendo elfu mia moja vya jeuri.” Ndivyo kinavyosema kitabu The 7 Habits of Highly Effective Families. Mambo hayo yanaathirije mtoto? “Wataalamu” hawakubaliani miongoni mwao wenyewe juu ya jambo hilo, lakini Biblia huonya kwa mkazo dhidi ya mashirika mabaya. Kwa mfano, hiyo husema hivi: “Rafiki wa wapumbavu ataumia.” (Mithali 13:20) Pia hiyo husema hivi: “Mashirika mabaya huharibu mazoea yenye mafaa.” (1 Wakorintho 15:33) Maisha ya familia yanaweza kuboreka ikiwa twaiona kwa busara kanuni hii kuwa ya kweli iwe mashirika mabaya yanawakilishwa kibinafsi au kwenye kipindi cha televisheni.
Mama mmoja katika Luxembourg alikuwa anajifunza Biblia na mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Siku moja alimwambia Shahidi huyo kwamba nyakati za jioni binti zake wawili wenye umri wa miaka saba na nane walikuwa wagomvi na wachokozi sana. Shahidi huyo aliuliza kile ambacho wasichana hao walikuwa wakifanya nyakati za jioni. Mama huyo alisema kwamba walikuwa wakitazama televisheni alipokuwa akisafisha jikoni. Vipindi vipi? “Aah, katuni tu,” mama akajibu. Mgeni wake alipotaja kwamba vipindi kama hivyo mara nyingi huwa vyenye jeuri, mama ya wasichana hao aliahidi kutazama vipindi hivyo.
Siku iliyofuata, mama huyo aliripoti kwamba alishangazwa na katuni hizo ambazo binti zake walikuwa wakizitazama. Zilionyesha madubwana ya kuwaziwa kutoka anga la nje ambayo yalikuwa yakiharibu kwa ukatili kila kitu yanachokutana nacho. Aliwaeleza binti zake kwamba Yehova huchukia jeuri naye hafurahi wanapotazama ukatili huo. (Zaburi 11:5) Wasichana hao wakitaka kumpendeza Yehova, walikubali kuchora na kupaka rangi picha badala ya kutazama televisheni. Upesi mwenendo wao mchokozi ukabadilika, na hali ya familia ikaboreka.
Hivi ni vielelezo vichache tu vya kuonyesha kwamba kutumia kanuni za Biblia huboresha maisha ya familia. Shauri la Biblia hushughulikia hali za aina zote. Ni yenye uasili na ina matokeo yenye nguvu kwa yaliyo mema. (Waebrania 4:12) Watu wanapojifunza Biblia na kujaribu kwa unyoofu kutumia kile ambacho hiyo husema, familia huimarishwa, nyutu huboreshwa, na makosa huepukwa. Hata kama mshiriki mmoja tu wa familia ndiye anayefuata shauri la Biblia, mambo yanaboreka zaidi. Kwa kweli, katika sehemu zote za maisha, twapaswa kuliona Neno la Mungu kama alivyoliona mtunga-zaburi ambaye aliandika: “Neno lako ni taa ya miguu yangu, na mwanga wa njia yangu.”—Zaburi 119:105.
[Picha katika ukurasa wa 5]
Matatizo ya familia yametatuliwa kwa kutumia kanuni za Biblia