Wamejitolea Kufuata Njia ya Mungu ya Maisha
Mikusanyiko ya “Njia ya Mungu ya Maisha” ilikuwa na mengi sana ya kuwasaidia wale wanaotaka kumtumikia Mungu! Mjumbe mmoja aliufafanua mkusanyiko huo kuwa “kipindi kizuri ajabu cha maagizo, kutia moyo, na cha kuelimisha.”
MJUMBE mwingine alisema kwamba “kulikuwa na mengi ya kufurahia, kutafakari, na kujifunza.” Acheni tuchunguze programu yenyewe sasa.
Yesu Kristo—Ndiye Njia, Kweli, na Uhai
Hicho kilikuwa kichwa cha siku ya kwanza ya mkusanyiko. (Yohana 14:6) Hotuba ya kwanza ilifafanua kusudi la kukusanyika pamoja katika mkusanyiko huo: ili kufundishwa zaidi juu ya njia bora zaidi iwezekanayo ya maisha, njia ya Mungu ya maisha. Yehova huwafunza watu wake jinsi ya kutembea katika njia zake. Anawafundisha kupitia Biblia, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” na pia kupitia roho takatifu. (Mathayo 24:45-47; Luka 4:1; 2 Timotheo 3:16) Ni pendeleo lililoje kufundishwa na Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu!
Kwa kupatana na kichwa cha siku hiyo, hotuba ya msingi ilikuwa “Fidia ya Kristo—Njia ya Mungu ya Kuleta Wokovu.” Tunapojipatanisha na njia ya Mungu ya uhai, ni lazima tutambue fungu la Yesu Kristo katika kusudi la Yehova. Msemaji alisema: “Bila dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo, hakuna mtu yeyote, bila kujali itikadi na kazi zake, angeweza kupokea uhai wa milele kutoka kwa Mungu.” Ndipo akalinukuu andiko la Yohana 3:16, linalosema: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akatoa Mwana mzaliwa-pekee wake, ili kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye asipate kuangamizwa bali awe na uhai udumuo milele.” Ili kudhihirisha imani katika dhabihu ya fidia ya Kristo twahitaji kupata ujuzi sahihi wa ile kweli. Kudhihirisha imani kwatia ndani kuweka maisha yetu wakfu kwa Yehova, tukionyesha hilo kupitia ubatizo wa maji, na kuishi kupatana na kielelezo ambacho Yesu Kristo alituachia.—1 Petro 2:21.
Kipindi cha alasiri kilianza na hotuba yenye kichwa “Njia ya Upendo Haishindwi Kamwe.” Hotuba hiyo ilitia ndani mazungumzo ya mstari kwa mstari ya ufafanuzi wenye kusisimua wa Paulo juu ya upendo, uliorekodiwa katika 1 Wakorintho 13:4-8. Wasikilizaji walikumbushwa kuwa upendo wa kujidhabihu ni alama inayotambulisha Ukristo na kwamba kupenda Mungu na jirani ni sehemu muhimu za ibada inayokubaliwa na Yehova.
Kisha ikafuatia hotuba ya mfululizo yenye sehemu tatu yenye kichwa “Wazazi—Ikazieni Kikiki Njia ya Mungu Katika Watoto Wenu.” Wazazi wanaweza kuwasaidia watoto wao wamtumikie Mungu kwa kuweka kielelezo kizuri katika kusoma na kujifunza Neno lake. Wanaweza kuikazia kweli kikiki katika watoto wao kupitia funzo la familia la kawaida, wakilifanya liyafae mahitaji ya familia. Ni muhimu kuwasaidia watoto washiriki katika utendaji wa kutaniko na huduma ya shambani. Ingawa ni vigumu kulea watoto wenye kumhofu Mungu katika ulimwengu huu mwovu, kufanya hivyo kunatokeza thawabu nyingi.
Hotuba iliyofuata baada ya mfululizo huo ilikuwa yenye kichwa “Yehova na Akufinyange kwa Ajili ya Matumizi Yenye Kuheshimika.” Kama vile mfinyanzi hufinyanga chombo cha udongo, ndivyo Mungu hufinyanga wale wanaotaka kumtumikia. (Waroma 9:20, 21) Yeye hufanya hivyo kwa kuandaa shauri kupitia Neno lake na pia kupitia tengenezo lake. Yehova atatusaidia kuutumia uwezo wetu kwa ukamili ikiwa sisi tunajitoa, tunatumia fursa mbalimbali, na kuwa tayari kuongozwa naye.
Sehemu yenye kusisimua ya programu sasa ilifuata—“Utumishi Katika Shamba la Kimishonari.” Wakati huu kuna wahudumu wa Kikristo 2,390 katika nchi 148 wanaoonwa kuwa wamishonari. Wanaweka kielelezo kizuri ajabu cha uaminifu-mshikamanifu na bidii, nao wanashukuru sana kwa ajili ya pendeleo la kutumikia katika shamba la nchi za kigeni. Sehemu hiyo ya programu ilipokuwa ikiendelea katika mikusanyiko ya kimataifa, wamishonari walisimulia magumu na shangwe za maisha ya umishonari.
Hotuba ya mwisho siku ya kwanza ilikuwa yenye kichwa “Je, Kuna Uhai Baada ya Kifo?” Swali hilo limewahangaisha wanadamu kwa maelfu ya miaka. Watu katika kila jamii wametafakari juu ya suala hilo. Na kuna majibu mengi ya kudhaniwa tu. Nayo yatofautiana kama vile desturi na dini za wale wanaotoa majibu hayo hutofautiana. Ingawa hivyo, watu wahitaji kujifunza kweli.
Basi, msemaji akatangaza kutolewa kwa broshua Ni Nini Hutupata Tunapokufa? yenye kupendeza yenye kurasa 32. Broshua hii yaeleza chanzo cha lile fundisho la kutokufa kwa nafsi na huonyesha jinsi dhana hiyo ilivyopata kuwa kiini cha karibu dini zote za ulimwengu leo. Yaeleza waziwazi na kwa njia yenye kuvutia mambo ambayo Biblia husema juu ya nafsi, kwa nini tunakufa, na ni nini hutupata tunapokufa. Pia broshua hiyo yaeleza kuna tumaini gani kwa wafu na kwa walio hai. Kichapo hicho kitakuwa baraka iliyoje kwa wote wanaotafuta kweli!
Angalieni Sana Jinsi Mnavyotembea
Hicho kilikuwa kichwa chenye kufaa kama nini siku ya pili ya mkusanyiko huo! (Waefeso 5:15) Programu ya asubuhi ilikazia kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Baada ya kuchunguza andiko la siku, hotuba iliyofuata kwenye programu ilikuwa yenye kichwa “Kuwasaidia Watu Waingie Katika Njia Iendayo Kwenye Uhai.” Tunapoifanya kazi hii yenye uharaka, ni muhimu tuwe na mtazamo unaofaa, tukijua kwamba kushiriki kweli na wengine ni pendeleo na wajibu pia. Katika karne ya kwanza W.K., watu wengi walilikataa Neno la Mungu. Hata hivyo, kujapokuwa upinzani, kulikuweko ‘waliokuwa na mwelekeo ufaao kwa ajili ya uhai udumuo milele na wakawa waamini.’ (Matendo 13:48, 50; 14:1-5) Hali iko hivyo leo. Ingawa walio wengi leo huikataa kweli ya Biblia, sisi twaendelea kutafuta-tafuta wale walio na mwelekeo unaofaa.—Mathayo 10:11-13.
Hotuba iliyofuata ilizungumzia ugumu wa kuwafikia wengine kwa ujumbe wa uhai. Kwa kuwa siku hizi ni vigumu kupata watu nyumbani, twahitaji kuwa wenye kubuni njia mbalimbali na kutimiza kikamili mgawo wetu ili kuwafikia watu wengi iwezekanavyo kwa ujumbe wa Ufalme. Katika nchi nyingi, wahubiri wa habari njema hupata matokeo mazuri kwa kutoa ushahidi kupitia simu, kwa kuhubiri katika eneo la kibiashara, hivyo wakiwafikia wale ambao ni vigumu kuwafikia kupitia njia nyingine.
Hotuba yenye kichwa “Kufundisha Wanafunzi Yote Ambayo Kristo Aliamuru” ilikazia umuhimu wa kuwa stadi katika huduma yetu. Stadi zetu za kufundisha huimarishwa tunapojifunza kutoka kwa wengine na kutumia mazoezi bora kabisa tunayopokea kwenye mikutano ya kutaniko. Tunapoendeleza stadi zetu za kufundisha, twapata shangwe nyingi na uradhi katika kazi yetu ya kuwasaidia watu wajifunze kweli ya Biblia.
Hotuba ya mwisho kwenye kipindi cha asubuhi ilizungumzia maana ya wakfu na ubatizo. Moja ya hoja zilizofafanuliwa na msemaji ilionyesha kwamba tukimtumaini Mungu kabisa na kujaribu kwa bidii kufanya mapenzi yake, yeye atatubariki na kututegemeza. Mtu mwenye hekima aliandika: ‘Katika njia zako zote mkiri Mungu, naye atayanyosha mapito yako.’ (Mithali 3:6) Ubatizo wenyewe, ambao ulitokeza shangwe, ulikuwa jambo kuu kwenye mkusanyiko na ulithibitisha kuwa wengi wameanza kujipatanisha na njia ya Mungu ya maisha.
Baada ya pumziko la adhuhuri, kipindi cha alasiri kilianza na hotuba yenye kichwa “Kutumikia Tukitazamia Uhai Usio na Mwisho.” Kusudi la Mungu la kutaka wanadamu watiifu wamtumikie duniani milele litatimizwa. Basi, yafaa kama nini kwamba tukazie fikira, mipango na matumaini yetu juu ya kumtumikia Yehova tukitazamia umilele! Ingawa twataka kuweka “siku ya Yehova” karibu akilini, ni muhimu kukumbuka kwamba mradi wetu ni kutumikia milele. (2 Petro 3:12) Kutojua wakati barabara ambapo Yesu atatekeleza kisasi cha Mungu hutuweka chonjo na hutupa fursa kila siku ya kuthibitisha kwamba sisi twamtumikia Yehova kwa makusudi yasiyo na ubinafsi.
Hotuba mbili zilizofuata zilifafanua sura ya 4 ya barua ya Paulo kwa Waefeso. Baadhi ya mambo yaliyozungumziwa ni ile baraka ya kuwa na “zawadi zikiwa wanadamu,” wanaume wakomavu kiroho ambao wamewekwa rasmi na roho takatifu. Wazee hawa huandaa shauri na mwongozo kwa faida yetu ya kiroho. Pia, barua ya Paulo iliyopuliziwa yawahimiza Wakristo wavae “utu mpya.” (Waefeso 4:8, 24) Utu wa kimungu watia ndani sifa kama vile huruma, fadhili, hali ya akili ya kujishusha chini, upole, ustahimilivu, na upendo.—Wakolosai 3:12-14.
Kuangalia sana jinsi tunavyotembea kwatia ndani kufuliza kujitunza wenyewe bila doa kutokana na ulimwengu—hii ikiwa habari iliyozungumziwa katika hotuba iliyofuata. Kuna uhitaji wa kuwa na usawaziko katika kuchagua vitumbuizo, shughuli za kijamii, na ufuatiaji wa vitu vya kimwili. Kwa kutumia shauri linalopatikana katika Yakobo 1:27 la kujitunza wenyewe bila doa kutokana na ulimwengu, twafurahia msimamo safi na pia dhamiri njema pamoja na Mungu. Twaweza pia kuishi maisha yenye kusudi nasi tutabarikiwa kwa amani, ufanisi wa kiroho, na washirika wazuri ajabu.
Ndipo hotuba ya mfululizo iliyo na sehemu tatu yenye kichwa “Vijana—Fuateni Njia ya Mungu” ikafuata. Wakijua kuwa Mungu anawapenda na anathamini juhudi zao za kutetea ibada safi, vijana wapaswa kuzoeza nguvu zao za ufahamu ili wamtumikie kwa uaminifu. Njia moja ya kukuza nguvu za ufahamu ni kusoma na kutafakari Neno la Mungu kila siku. Tukifanya hivyo, twaweza kuzijua njia za Yehova. (Zaburi 119:9-11) Pia, nguvu za ufahamu zaweza kukuzwa kwa kukubali shauri la ukomavu kutoka kwa wazazi waliokomaa, wazee, na vichapo vya Sosaiti. Kwa kutumia nguvu zao za ufahamu katika njia ifaayo, vijana hukinza kujishughulisha mno na vitu vya kimwili, usemi mchafu, na tafrija ya kupita kiasi ambazo huutambulisha ulimwengu huu uliojitenga na Mungu. Kwa kufuata njia ya Mungu ya maisha, vijana kwa wazee vilevile wanaweza kufurahia ufanisi wa kweli.
Hotuba ya mwisho siku hiyo ilikuwa na kichwa “Utu wa Muumba na Njia Zake.” Baada ya kutaja kwamba mabilioni ya watu hawamjui Muumba, msemaji alisema: “Kusudi halisi maishani lahusu kumjua Muumba, Mungu wetu halisi; kutambua utu wake; na kushirikiana na njia zake. . . . Kuna mambo yanayohusu ulimwengu wetu na yanayotuhusu ambayo unaweza kutumia kusaidia watu wamkubali Muumba na kupata umaana kuhusiana naye.” Ndipo msemaji akazungumzia uthibitisho wa kuwepo kwa Muumba mwenye hekima na upendo. Kilele cha hotuba hiyo kilikuwa kutolewa kwa kitabu kipya—Je, Kuna Muumba Anayekujali?
“Njia Ni Hii, Ifuateni”
Hicho kilikuwa kichwa cha siku ya tatu ya mkusanyiko huo. (Isaya 30:21) Programu ilianza kwa mfululizo wenye kusisimua wa hotuba tatu, zikikazia ono la Ezekieli la hekalu. Ono hilo lina umaana mkubwa sana kwa watu wa Mungu leo, kwa kuwa linahusu ibada safi wakati wetu. Ufunguo wa kulielewa ono hilo ni huu: Hekalu kubwa la kiroho la Yehova huwakilisha mpango wake wa ibada safi. Mambo makuu ya ono hilo yalipokuwa yakizungumzwa, wasikilizaji walitafakari kwa uzito juu ya wanayotenda ili kuunga mkono kazi inayofanywa na waangalizi wenye upendo wa jamii ya mabaki watiwa-mafuta na, vilevile, wanayofanya kuunga mkono wale wanaotazamia kuwa washiriki wa jamii ya mkuu.
Baadaye asubuhi, kulikuwa na drama yenye kuchangamsha ya Biblia iliyokuwa na washiriki wenye mavazi ya kuigiza. Kichwa cha drama hiyo kilikuwa “Familia—Fanyeni Usomaji wa Biblia Kila Siku Uwe Njia Yenu ya Maisha!” Ilionyesha imani na ujasiri wa Waebrania watatu waliokataa kuiinamia sanamu ya dhahabu iliyosimamishwa na Mfalme Nebukadneza wa Babiloni. Lengo la drama hiyo lilikuwa kuonyesha kuwa Biblia si kitabu cha historia ya kale tu bali shauri lake lina manufaa kwelikweli kwa vijana na watu wazima leo.
Alasiri ilikuwa wakati wa hotuba ya watu wote yenye kichwa “Njia Pekee Iendayo Kwenye Uhai Udumuo Milele.” Baada ya kurudia historia ya jinsi mwanadamu alivyotumbukia kwenye dhambi na kifo, msemaji alimalizia kwa kusema maneno haya yenye kuamsha fikira: “Andiko la msingi la Biblia la siku hii ya mkusanyiko limekuwa Isaya sura ya 30, mstari wa 21, lisemalo hivi: ‘Masikio yako yatasikia neno nyuma yako, likisema, Njia ni hii, ifuateni; mgeukapo kwenda mkono wa kulia, na mgeukapo kwenda mkono wa kushoto.’ Sisi huisikiaje sauti hii? Ni kwa kusikiliza Neno la Mungu, Biblia Takatifu, na kwa kufuata mwongozo ambao Mfundishaji wetu Mkuu, Yehova Mungu, huandaa kupitia kwayo na kupitia kwa tengenezo lake la kisiku hizi la Kikristo. Kwa kweli, kufanya hivi ndiyo njia pekee ya kupata uhai udumuo milele.”
Baada ya muhtasari wa makala ya funzo la Mnara wa Mlinzi la juma hilo ikafuatia hotuba ya mwisho, yenye kichwa “Endeleeni Kutembea Katika Njia ya Yehova.” Kwa sehemu, hotuba hii ilirudia mambo makuu ya programu. Ndipo msemaji akasoma azimio linaloonyesha kujitolea kuendelea kuishi katika njia ya Mungu.
Azimio hilo lilimalizia kwa maneno haya yenye kuchochea: “Twasadiki kwamba kuishi kwa kanuni, shauri, na onyo la upole la Kimaandiko kwatokeza njia bora ya maisha leo na huweka msingi bora kwa ajili ya wakati ujao, ili tupate kushika imara uhai ulio halisi. Zaidi ya yote, twafanya azimio hili kwa sababu sisi twampenda Yehova Mungu kwa moyo wetu wote, nafsi yetu yote, akili yetu yote, na nguvu zetu zote!” Wahudhuriaji wote walionyesha kibali chao kwa kusema ndiyo kwa sauti kubwa!
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8]
Je, Kuna Muumba Anayekujali?
Kitabu kipya chenye kichwa hicho hutoa uthibitisho wenye kusadikisha wa kuwepo kwa Muumba, Yehova, na chazungumzia sifa zake. Kimekusudiwa hasa wale wenye elimu nzuri ya kilimwengu lakini hawamwamini Mungu. Pia, kitabu hiki chenye kurasa 192 kitakuza imani ya watu mmoja-mmoja ambao tayari wanamwamini Mungu, kikijenga uthamini kwa utu na njia zake.
Kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali? hakiamui kimbele kuwa msomaji ana imani katika Mungu. Badala ya hivyo, kinachunguza namna mawazo na mavumbuzi ya hivi majuzi ya kisayansi hushuhudia kuwepo kwa Muumba. Baadhi ya sura ni zile zenye vichwa “Ni Nini Kinachoweza Kufanya Maisha Yako Yawe na Maana Zaidi?,” “Ulimwengu Wetu Ulitokeaje?—Ubishi Uliopo,” na “Jinsi Ulivyo Kiumbe cha Kipekee!” Sura nyingine zazungumza juu ya kwa nini twaweza kuwa na uhakika kwamba Biblia imepuliziwa kimungu. Kitabu hicho kipya pia chatupatia maoni ya jumla kuhusu Biblia, ambayo hufunua utu na njia za Muumba. Kitabu hicho hakielezei tu kwa nini Mungu ameruhusu kuteseka bali pia chaeleza jinsi ambavyo atakomesha kuteseka milele.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Wengi walibatizwa
[Picha katika ukurasa wa 7]
A. D. Schroeder, mmoja wa washiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, akitangaza kutolewa kwa ile broshua mpya
[Picha katika ukurasa wa 8, 9]
Drama yenye kusisimua ilitia moyo usomaji wa Biblia kila siku